Nav bar

Jumatano, 13 Desemba 2023

PROF. SHEMDOE CHUONI NDC

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe  akiwasili na kupokelewa na Maafisa wa Chuo Cha Taifa Cha Ulinzi – Tanzania (NDC) kwa ajili ya kutoa Mhadhara kuhusu" Livestock and Fisheries Sector's Development in Tanzania"kwa Washiriki wa Kozi ya Kumi na Mbili jana tarehe  12 Disemba 2023.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe akisaini kitabu cha Wageni mara tu baada ya kuwasili katika Ukumbi wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) Jana  tarehe 12 Disemba2023 jijini Dar es salaam.

 

Jumanne, 31 Oktoba 2023

WADAU WAHIMIZWA KUFUGA SAMAKI KUKUZA SEKTA YA UVUVI NCHINI


Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe amewahimiza wadau wa sekta ya uvuvi kujikita katika ufugaji wa viumbe maji ili kusaidia kukuza mchango wa sekta ya uvuvi katika Pato la Taifa kutoka asilimia 1.7 walau kufika mpaka asilimia 5 ifikapo mwaka 2025.

Prof. Shemdoe alitoa rai hiyo wakati akifungua kikao kazi cha wadau wa Ukuzaji  Viumbe maji kilichofanyika jijini Dodoma Oktoba 31, 2023.

Alisema kuwa hivi sasa wanaandaa kanuni zitakazosaidia kuwa na usimamizi madhubuti wa tasnia ya uvuvi kwa lengo la kuimarisha ukuzaji wa viumbe maji ili kuchangia vyema katika Pato la Taifa.

"Tunaandaa kanuni kwa ajili ya ufugaji viumbe maji , kwenye ufugaji wa samaki na mavuvi ya samaki ili kuona  namna tutaweza ndani ya miaka hii miwili  kuchangia  asilimia 5 kwenye pato la taifa," alisema Prof. Shemdoe

Aliongeza kuwa kanuni hizo zitakwenda kuboresha namna tasnia ya ukuzaji viumbe maji inasimamiwa na kuwezesha kile kinachozalishwa kiweze kufika kwenye masoko makubwa ya kikanda na kimataifa

Naye Naibu Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi Bi. Agness Meena amesema kupitia kikao hicho wadau watapata fursa ya kubainisha changamoto zinazoikabili tasnia ya ukuzaji viumbe maji na kuweka mikakati ya pamoja ya kukabiliana na changamoto hizo na kuongeza uelewa kuhusu usimamizi shirikishi na kuwa na tasnia endelevu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji, Dkt. Nazael Madala amesema tasnia ya ukuzaji viumbe maji itakuja kuwa na mchango mkubwa sana kwenye  Sekta ya Uvuvi kwa vile bado ni ndogo na inakuwa kwa haraka.

"Tanzania tuna bahati ya kuwa na rasilimali nyingi za maji kwa maana ya maziwa, mabwawa makubwa, maji ya chini ya ardhi, ambayo yanaweza kuchimbwa na sehemu yoyote ikafanyika ufugaji wa samaki katika mabwawa na tukiweza kufanya hivi tunaweza tukaongeza fursa zaidi za ajira, na kuongeza kipato cha mwananchi mmoja mmoja na jamii kwa ujumla" Alisema Dkt. Madala

Kikao hicho, kimefanyika kwa ushirikiano wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Shirika la Chakula na kilimo Duniani (FAO) Tamisemi pamoja na wafugaji wa samaki na mwani, lengo likiwa ni kujenga uelewa wa pamoja kuhusu changamoto zilizopo na kubaini mikakati ya kuzitatua.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe akiongea na washiriki wakati akifungua kikao kazi cha wadau wa ukuzaji viumbe maji kilichofanyika kwenye ukumbi wa Rafiki hotel jijini Dodoma,  Oktoba 31,2023

Naibu Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi Bi. Agness Meena akitoa neno fupi wakati wa kufungua kikao kazi cha wadau wa ukuzaji viumbe maji kilichofanyika kwenye ukumbi wa Rafiki hotel jijini Dodoma,  Oktoba 31,2023

Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Nazael Madala  akiwasilisha mada wakati wa kikao kazi cha wadau wa ukuzaji viumbe maji kilichofanyika kwenye ukumbi wa Rafiki hotel jijini Dodoma,  Oktoba 31,2023

Afisa Uvuvi anayeshughulikia minyororo ya thamani ya uvuvi na ufugaji wa viumbe maji kutoka Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) Bw. Hashim Muumin akitoa neno wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha wadau wa ukuzaji viumbe maji kilichofanyika kwenye ukumbi wa Rafiki hotel jijini Dodoma Oktoba 31,2023


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya wadau walioshiriki kikao kazi cha  ukuzaji viumbe maji  mara baada ya kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa Rafiki hotel jijini Dodoma Oktoba 31,2023


Jumamosi, 28 Oktoba 2023

WATAALAMU WATAKIWA KUKUSANYA TAKWIMU SAHIHI ZA KITAFITI

Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, maliasili na Mifugo Mhe. Shamata Saame amewataka wataalamwa Sekta ya Mifugo na Uvuvi kuhakikisha wanachukua  takwimu sahihi wakati wa kukusanyataarifa za kitafiti   ili ziweze kuisaidia Serikali katika kupanga mipango yake.

Waziri  Shaame ameyasema hayo wakati akifunga Kongamano la 46 la Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Mkutano  Mkuu wa 47 wa Mwaka wa Chama cha Wataalamu wa Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Uvuvi (TSAP) lililofanyika kwenye Ukumbi wa Olasit Garden, Arusha  Oktoba 27, 2023.

"Takwimu sahihi kuhusu taarifa za mifugo na uvuvi zitasaidia kutunga sera,  kunyoosha maono, fikra na miongozo ya ilani ya chama cha mapinduzi kuweza kufikia  malengo ya kuwainua wananchi  kupata mafanikio kwa haraka," alisema

Aliongeza kwa kusema kuwa Serikali inawategemea sana wataam na hivyo watumie vizuri teknolojia walizonazo ili zikaboreshe tasnia nzima ya ufugaji ili kupata maendeleo.

“Wizara na Wadau wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa pamoja lazima tutambue kuwa huu ni wakati mwafaka wa kufanya mapinduzi makubwa katika minyororo ya thamani ya mifugo na samaki ili kukidhi mahitaji ya chakula na lishe bora kwa Wananchi na masoko yanayotuzunguka” Alisema Mhe. Shaame

Aliendelea kwa kuwahimiza Wafugaji na wazalishaji kuwekeza katika teknolojia za kisasa na vitendea kazi sahihi vitakavyoongeza uzalishaji katika kilimo, mifugo na sekta ya Uvuvi na hivyo Wizara, itaendelea kuhakikisha kuwa mazingira bora ya kufuga, kusindika na kufanya biashara ya mifugo na uvuvi yanazidi kuwa bora kwa watengenezaji wa vyakula vya mifugo na samaki.

Aliongeza kuwa Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo  inaunga mkono jitihada za vyama vya hiari vya kitaaluma , hivyo TSAP iendelee kujitangaza ili kuongeza mashirikiano na wataalamu walioko Zanzibar ili kuendelea kupata wanachama wengi.

Naye Naibu Katibu Mkuu amewataka wataalam kuweka bidii katika kujiendeleza kutaaluma ili kuongeza ujuzi na ufanisi zaidi katika kazi zao na kuweza kutengeneza mfumo utakaohifadhi taarifa za wataalam wote wa mifugo nchini ili kujua umma uliopo ni asilimia ngapi ya wataalam walioko huko nje.

Pia amewataka wataalam kuwa chachu ya kuhamasisha wafugaji kulima, kuhifadhi malisho na kutengeneza vyanzo mbadala vya maji kwa mwaka mzima ili kupunguza idadi kubwa ya vifo vya wanyama vinavyotokea kipindi cha kiangazi.


Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo  Mhe.  Shamata Saame akiongea na Washiriki (hawapo pichani) wakati akifunga Kongamano la 46 la Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Mkutano Mkuu wa 47 wa Mwaka wa Chama cha Wataalamu wa Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Uvuvi (TSAP) lililofanyika katika Ukumbi wa Olasit Garden, Arusha  Oktoba 27, 2023.
Naibu Katibu Mkuu Sekta ya Mifugo Dkt.  Daniel Mushi akiongea wakati wa kufunga Kongamano la 46 la Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Mkutano Mkuu wa 47 wa Mwaka wa Chama cha Wataalamu wa Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Uvuvi (TSAP) lililofanyika kwenye Ukumbi wa Olasit Garden, Arusha Oktoba 27, 2023.
Mwenyekiti wa TSAP, Dkt. Jonas Kizima akitoa neno katika Kongamano la 46 la Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Mkutano Mkuu wa  47 wa Mwaka wa Chama cha Wataalamu wa Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Uvuvi (TSAP) lilifanyika katika Ukumbi wa Olasit Garden, Arusha Oktoba 27, 2023.
Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Mhe. Shamata Saame (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Washiriki muda mfupi baada ya  kufunga Kongamano la 46 la Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Mkutano Mkuu wa 47 wa Mwaka wa Chama cha Wataalamu wa Uzalishaji na Uendelezaji wa Mifugo na Uvuvi (TSAP) lililofanyika kwenye Ukumbi wa Olasit Garden, Arusha Oktoba 27, 2023.



 

 

 

Ijumaa, 27 Oktoba 2023

WADAU WAKUTANA KUWEKA MIKAKATI KUENDELEZA SEKTA YA MIFUGO NA UVUVI


Wataalam na wadau wa  sekta ya Mifugo Nchini, wamekutana jijini  Arusha kwa lengo la kujadili namna ya kuongeza uzalishaji katika sekta hizo ambayo italeta tija  kwa wananchi.

Hayo yamesemwa na  Mwenyekiti wa chama cha wataalamu wazalishaji mifugo na Uvuvi ,Dkt. Jonas  Kizima katika ziara ya kutembelea mbuga ya  Tarangire, ikiwa ni sehemu ya kongamano la siku tatu la kisayansi liloanza Oktoba  26 jijini  Arusha

Alisema kuwa  lengo kubwa ni  kupitia machapisho ya kisayansi yaliyoletwa na wadau  ili angalau waweze kutoa matokeo ya tafiti, na kutatua changamoto  katika sekta ya Mifugo na Uvuvi

"Katika hizi siku tatu, tumetenga siku moja ya kuja kutembelea mbuga za wanyama nchini, na mwaka huu tumechagua  Tarangire   ili kupata muda wa kufurahi na kujifunza zaidi, Pia tunaunga juhudi za Rais katika kuongeza watalii nchini kupitia Royal  tour na kuongeza pato kupitia utali,"alisema Dkt. Kizima

Naye Dkt Zablon Nziku, alisema  kuwa katika  kongamano hilo pia wameweza kujadili kwa kina Teknolojia   bora zilizotumika au zinazotumika katika kuwasaidia wadau wetu kuongeza uzalishaji.

"Pamoja na kujifunza mambo mbalimbali ya kisayansi katika uendelezaji wa Mifugo na Uvuvi nchini, bado tunaona ipo haja  ya kufanya ziara kwenye vivutio vyetu vya utalii ili kuwaonyesha  wageni kutoka nje, nasi tunaweza kufanya utalii, hii itasaidia ongezeko la watali wa ndani,"alisema

Aidha baadhi ya washiriki    akiwemo Bi. Neema Urassa alisema  kufanyika kwa ziara hiyo kutawasaidia watumishi na wadau wa sekta hiyo kutambua vivutio vya hapa nchini.

"Pia itamjengea mtumishi anaporudi katika eneo lake la kazi kufanya kazi kwa jitihada na inaongeza ufanisi wa kazi, kwa kufanya hivi kwa sekta zote kutaongeza utalii wa ndani na kuongeza pato la nchi,"alisema Bi. Neema


Sehemu ya wataalam wazalishaji mifugo na Uvuvi wakiwa kwenye picha za pamoja  katika ziara ya kutembelea mbuga ya  Tarangire, ikiwa ni sehemu ya kongamano la siku tatu la kisayansi liloanza Oktoba  26 jijini  Arusha

Sehemu ya wataalam wazalishaji mifugo na Uvuvi wakiwa kwenye picha za pamoja  katika ziara ya kutembelea mbuga ya  Tarangire, ikiwa ni sehemu ya kongamano la siku tatu la kisayansi liloanza Oktoba  26 jijini  Arusha

Sehemu ya wanyama wanaopatikana kwenye mbuga ya Tarangire.


Jumatatu, 9 Oktoba 2023

MIFUGO NA UVUVI YATINGA NUSU FAINALI KIBABE!

◾ Kukutana na Katiba na Sheria Oktoba 10 


Timu ya soka ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetinga hatua ya nusu fainali ya Michuano ya SHIMIWI inayoendelea mkoani Iringa baada ya kuifumua timu ya bunge kwa magoli 2-1 kwenye mchezo uliochezwa leo Oktoba 08, 2023 uwanja wa Samora mkoani humo.


Katika mchezo huo uliokuwa wa kasi kwa pande zote mbili timu ya Wizara ya Mifugo iliweka kimiani magoli yake kupitia kwa mlinzi wa pembeni Ignatus Mwasa aliyefunga kwa shuti kali la  mpira wa adhabu dakika ya 06 ya mchezo kabla ya timu ya bunge kusawazisha kupitia kwa mshambuliaji wao Mnubi Kajobi dakika ya 37 na kufanya timu hizo kwenda mapumziko wakiwa wametoshana nguvu.


Timu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ilianza kipindi cha pili kwa kasi kubwa huku ikielekeza mashambulizi ya nguvu upande wa Bunge hali iliyoilazimu timu yote kurudi nyuma kwa ajili ya kuzuia mashambulizi hayo.


Mashambulizi hayo makali ya timu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi yalizaa matunda katika dakika ya 71 baada ya kupata goli la ushindi kupitia kwa kiungo wao Hema Mughenyi aliyekuwa nyota wa mchezo wa leo na mwiba kwa timu ya Bunge ambapo alipachika bao hilo kwa mpira wa kona uliozama moja kwa moja wavuni.


Timu ya soka ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi inatinga hatua ya nusu fainali kwa mara ya kwanza tangu ilipoanza kushiriki michuano hiyo ambapo msimu uliopita iliondolewa kwa matuta na timu ya Ujenzi katika hatua ya robo fainali.


Timu hiyo sasa itacheza na timu ya SHERIA kwenye hatua ya nusu fainali mchezo utakaopigwa Oktoba 10 kwenye uwanja wa Samora.



MIFUGO NA UVUVI NAFASI YA 3 BAISKELI WANAUME

Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia mshiriki wake Siraji Mohammed imefanikiwa kushika nafasi ya 3 kwenye mashindano ya mbio za baiskeli umbali wa Km.40 yaliyofanyika leo Oktoba 08, 2023 kwenye michuano ya SHIMIWI inayoendelea mkoani Iringa.


Siraji ambaye alionesha upinzani wa hali ya juu na kuwa miongoni mwa washiriki 3 wa kwanza walioanza mzunguko wa pili kukamilisha umbali huo huku akitetea nafasi ya 3 aliyoibeba kwenye mashindano ya mwaka jana yaliyofanyika mkoani Tanga.


Wizara ya Mifugo na Uvuvi itakuwa kibaruani tena leo mchana kwenye hatua ya robo fainali ambapo timu yake ya mpira ya miguu itapepetana na timu ya Bunge huku upande wa mchezo wa kamba wanaume watachuana vikali na timu ya Ikulu.



ULEGA AZITAKA LITA, NARCO KUANDAA VIJANA KUWA WAFANYABIASHARA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amezitaka Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) na Bodi ya Ushauri ya Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo (LITA) kuwa na mkakati wa pamoja wa kuwaandaa vijana kuwa wafanyabiashara katika sekta ya mifugo kupitia programu kielelezo ya BBT Mifugo.


Waziri Ulega ametoa maelekezo hayo wakati akizindua Bodi ya Nne ya Ushauri ya Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo (LITA) na Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) katika tukio lililofanyika jijini Dar es Salaam leo Oktoba 7, 2023.


"Huu ndio uwe mtazamano wetu, kijana anapofundishwa na kumaliza Mafunzo yake pale LITA nyie NARCO muweke utaratibu wa kutenga maeneo kwa ajili ya kuwapa vijana hao ili wajifunze kwa vitendo ufugaji wa kisasa, hatutaki kufundisha watu ili waende kuangaika bali waingie katika biashara ya mifugo na mazao yake," alisema Waziri Ulega 


Aidha, aliwataka  LITA kuhakikisha wanakuwa na mkakati wa kuwaunganisha vijana hao na taasisi za kifedha kwa ajili ya kuwajengea uwezo wa kuwapa mbinu za kutekeleza mkakati wa kibiashara na kupata mitaji.




Halikadhalika, ameielekeza  NARCO kuhakikisha wanaweka mikakati ya kuvutia wawekezaji na kuhakikisha wanakuwa kinara wa biashara ya nyama nchini.

SERIKALI YADHAMIRIA KUWAINUA VIJANA WA BBT-LIFE KWA KUWATAFUTIA MASOKO YA MIFUGO

SERIKALI kupitia  Wizara ya Mifugo na Uvuvi imesema kuwa inaendelea na majadiliano  na Wadau wa sekta ya Mifugo nchini  ili kuona namna bora ya kushirikiana na vijana waliopo kwenye Programu ya  BBT  -LIFE katika kunenepesha Mifugo na kuisafirisha kwenye masoko ya nje ya nchi.


Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, (Mifugo) Dkt. Daniel Mushi wakati wa  kikao kati ya menejimenti ya sekta mifugo na wadau kuhusu kuwaunga mkono vijana waliopo kwenye programu ya BBT- LIFE , jijini Dodoma, tarehe 06.10.2023.


Dkt.Mushi amebainisha kuwa wamekutana na Kampuni za ELIA FOOD na TANCHOICE  Limited za uchakataji nyama  kwa ajili ya  kutengeneza muunganiko wa BBT -LIFE na Soko kubwa la nje ya nchi la uuzaji wa mazao ya Mifugo ili kukabiliana na changamoto ya masoko ya mifugo kwa vijana wa BBT-LIFE.


"Tumefikiria kuwa tukiwapata  wanunuzi wakubwa wa Mifugo programu yetu ya BBT - LIFE itakuwa imefanikiwa katika kuwawezesha vijana kujiajiri kupitia fursa hii ya wadau “, Amesema Dk. Mushi.


 Pia alisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha Mifugo haisafirishwi nje ya nchi ikiwa hai bali ichakatwe ndani ya nchi ili kuleta ajira kwa vijana hapa nchini na hatimaye kunufaika na rasilimali zilizopo na kuongeza pato la taifa.


Katika hatua nyingine Naibu Katibu Mkuu huyo,amefafanua kuwa,Wizara ya Mifugo na Uvuvi inatarajia kuanzisha Vituo vingine zaidi vya BBT -LIFE  kwa ajili ya Vijana ambao watakuwa wanashirikiana na wadau mbalimbali katika biashara hiyo ya mifugo.


Naye mmoja wa wadau hao Dkt.Sele Luwongo kutoka  kampuni ya TANCHOICE Limited ambayo ni  machinjio na kiwanda cha kuchakata  nyama amesema wao kama sekta binafsi wako tayari kushirikiana na Serikali katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto za masoko kwa mifugo ya vijana waliopo kwenye prigramu ya BBT -LIFE .



MIFUGO NA UVUVI YATAKATA MBELE YA MAMBO YA NDANI NA KUTINGA ROBO FAINALI

Timu ya soka kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetinga hatua ya robo fainali ya michuno ya SHIMIWI 2023 inayoendelea mkoani Iringa baada ya kuishindilia timu ya Wizara ya Mambo ya Ndani goli 1-0 leo Oktoba 06, 2023 kwenye mchezo uliochezwa uwanja wa Samora.


Goli hilo limefungwa na mshambuliaji hatari wa timu hiyo Joseph Buhigwe dakika ya 35 ya mchezo baada ya vuta nikuvute iliyotokea kwenye lango la timu ya timu ya Wizara ya Mambo ya Ndani kabla ya mpira kufika kwa Buhigwe aliyeachia shuti kali lililozama wavuni moja kwa moja.


Timu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ilionekana kuutawala mchezo huo wakati wote na kama si uimara wa mabeki na golikipa wa timu ya Wizara ya  Mambo ya Ndani huenda wangefungwa magoli mengi zaidi.


Baada ya ushindi huo Wizara ya Mifugo na Uvuvi sasa imeingiza timu 2 kwenye hatua ya robo fainali baada ya kutanguliwa na timu ya kamba wanaume waliofuzu hatua hiyo mapema leo asubuhi.



 MIKOPO NA MAFUNZO YATAJWA KUWA NA TIJA KWA WALENGWA 


 

Na. Edward Kondela

 


Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema Mkoani Mwanza, umesema mikopo itakayotolewa na serikali kwa kushirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) kwa wanawake wanaojihusisha na uvuvi itakuwa na tija kwa kuwa imezingatia utoaji wa mafunzo ya namna ya kutumia mikopo hiyo.


Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo Bw. Binuru Shekideli amebainisha hayo (05.10.2023) wakati alipotembelewa ofisini kwake na wataalamu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na wakufunzi wa vikundi vya kuweka na kukopa ili kumuarifu juu ya mradi wa kusimamia na kuendeleza uvuvi mdogo nchini ambao unatekelezwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na FAO kwa vikundi vya FARAJA na TEGA ZIFE vilivyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema.


Bw. Shekideli amesema mikopo hiyo ni dhahiri itavifanya vikundi hivyo hususan vya wanawake wanaojihusha na masuala ya uvuvi kuwa na tija kwa kuwa licha ya kupatiwa mikopo wanapatiwa pia mafunzo na kwamba wapo pia ambao wana mitaji lakini hawana mafunzo, hivyo itakuwa fursa kwao kujifunza zaidi.


Aidha, amesema halmashauri itasimamia maelekezo yatakayotolewa na wataalamu huku akiwapongeza kwa kuweza kuwafikia na kuchagua vikundi viwili vya wanawake vinavyojihusisha na masuala ya uvuvi katika halmashauri hiyo ambavyo vimekuwa sehemu ya vikundi vya mwanzo katika mradi huo kabla ya kufikiwa kwa vikundi vingine nchini.


Nao baadhi ya wanawake kutoka vikundi vya FARAJA na TEGA ZIFE ambavyo vimepatiwa vitendea kazi vya kuendesha shughuli za kuweka na kukopa pamoja na majiko maalum yanayotumia gesi kwa ajili ya kuandalia mazao ya uvuvi wakiwemo dagaa ambao ndiyo wanashughulika nao zaidi, wamesema mafunzo hayo yamekuwa na tija kwao kwa kuwa sasa wamefahamu namna bora ya kutumia vikundi hivyo ili viwe na manufaa kwenye shughuli zao na hatimaye waweze kujiinua kiuchumi, hivyo watakuwa makini zaidi mara watakapopatiwa fedha.


Wizara ya Mifugo na Uvuvi inashirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO katika mradi wa kusimamia na kuendeleza uvuvi mdogo nchini wa namna ya upatikanaji wa mikopo kwa vikundi vya wanawake wanaojihusisha na uvuvi, ambapo kwa sasa mradi huo unaanza kwa kufanyiwa majaribio kwa baadhi ya vikundi vya Wilaya ya Sengerema Mkoani Mwanza, Muleba Mkoani Kagera, Mtera Mkoani Iringa na Mkuranga Mkoani Pwani.



KAMBA WANAUME YATINGA ROBO FAINALI KIBABE!

◾ Wanawake watolewa na Mahakama 


Timu ya kamba ya wanaume ya  Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefuzu hatua ya robo fainali ya michuano ya SHIMIWI inayoendelea mkoani Iringa mara baada ya kufanikiwa kupata ushindi wa mivuto yote miwili kwenye mchezo wao dhidi ya Wizara ya Afya uliochezwa leo Oktoba 06, 2023 kwenye uwanja wa Mkwawa.


Dalili ya ushindi katika mchezo huo ilianza kuonekana mapema ambapo Wizara ya Mifugo na Uvuvi iliuanza kwa kasi na kuthibitisha namna ilivyojipanga kubeba pointi kwenye mivuto yote.


Wakati huo huo timu ya kamba ya wanawake kutoka Wizarani hapo leo imeaga rasmi mashindano hayo baada ya kupoteza mchezo wao dhidi ya timu ngumu ya Mahakama kwenye mivuto yote miwili.


Wawakilishi wengine wa Wizara hiyo timu ya Mpira wa Miguu wanatarajia kutupa karata yao dhidi ya timu ya Wizara ya Mambo ya Ndani leo Oktoba 06, 2023 mchana kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa.



KAHAMA FRESH WAUNGA MKONO BBT MIFUGO

Kampuni ya Kahama Fresh inayomiliki Kiwanda cha kusindika maziwa na Shamba la mifugo imeunga mkono Programu ya BBT kwa kutoa ng'ombe wa maziwa (mitamba) watano (5) kwa kikundi cha vijana 17 ili kuwawezesha kujishughulisha na uzalishaji wa maziwa na  kujiongezea kipato.


Tukio hilo limefanyika katika shamba la mifugo la kampuni hiyo lililopo wilayani Karagwe, Mkoani Kagera leo Oktoba 5, 2023.


Akizungumza wakati wa kukabidhi ng'ombe hao kwa vijana, Waziri Ulega alimpongeza Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Bw. Josam Ntangeki kwa kuunga mkono Programu ya BBT kwa vitendo.


"Nampongeza Ndugu Josam kwa kuunga mkono Programu hii ya BBT kwa kuwakopesha ng'ombe wa maziwa vijana wetu kupitia mpango wa Kopa Ng'ombe Lipa Maziwa ili kuwawezesha vijana wetu kuzalisha maziwa kwa wingi na kuyapeleka katika viwanda vya uchakataji wa maziwa kikiwemocha Kahama Fresh", alisema Mhe. Ulega


Aliongeza kwa kusema kuwa programu hiyo ya BBT haiwezi kuendeshwa na Serikali peke yake bila ya wadau wa maendeleo, hivyo  Kampuni ya Kahama Fresh wameunga mkono Programu hiyo kwa vitendo huku akisema kitendo hicho kitatoa hamasa kwa wadau wengine kujitokeza.


Aidha, Waziri Ulega aliwakikishia wadau wote kuwa wataendelea kushirikiana nao ili programu hiyo ya kielelezo ya  BBT ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan iweze kushamiri na vijana wengi waweze kupata fursa za kujiajiri.


Halikadhalika,  Waziri Ulega amewahimiza  wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kuunga mkono Programu hiyo ili kwa pamoja waweze kushirikiana katika kuleta mabadiliko ya kweli katika sekta za uzalishaji.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Bw. Josam Ntangeki ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwapa fursa ya kuendesha shughuli zao huku akisema kuwa wametoa mitamba hiyo ili kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuwawezesha vijana kupata fursa mbalimbali za kujiajiri kupitia sekta za uzalishaji.


Kahama imetoa ng'ombe hao kupitia programu Kopa Ng'ombe Lipa Maziwa unaotekelezwa na Shirika la kimataifa la Heifer International kupitia  mradi wa kuboresha sekta ya maziwa (TI3P) kwa Kanda ya Ziwa na Zanzibar ambao unaofadhiliwa na Taasisi ya Bill and Melinda Gates (BMGF) kupitia Benki ya Maendeleo ya kilimo nchini (TADB).


Tukio hilo la utoaji ng'ombe watano kwa vijana ni sehemu ya uzinduzi wa  mpango wa  ukopeshaji ng'ombe Mia Sita (600) watakaotolewa na TADB kupitia programu ya Kopa Ng'ombe Lipa Maziwa.



MIFUGO NA UVUVI YATINGA FAINALI RIADHA MITA 100

◾ Yafikia rekodi yake ya mwaka jana kupitia kwa mwanariadha yule yule. 


Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia kwa mwanariadha wake William Valentino imefanikiwa kutinga hatua ya fainali ya riadha umbali wa mita 100 baada ya kukamilisha hatua ya nusu fainali akiwa mshindi wa 2.


Kwa hatua hiyo William anaifikia rekodi aliyoiweka kwenye michuano ya SHIMIWI msimu uliopita ambapo pia alifanikiwa kutinga hatua ya fainali.


Mpaka sasa Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefanikiwa kushika nafasi ya 3 kwenye riadha upande wa mita 3000, imeingia fainali upande wa mita 100 na nusu fainali upande wa mita 200.


Michuano ya SHIMIWI itaendelea tena kesho Oktoba 06, 2023  kwa hatua ya 16 bora ambapo kwa upande wa mpira wa miguu timu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi itamenyana na timu ya Mashitaka kwenye uwanja wa Samora majira ya saa 8 kamili mchana, timu ya kamba wanawake itachuana na timu ya Mahakama saa 12:30 asubuhi kwenye uwanja wa Mkwawa huku timu ya kamba wanaume ikitoana jasho na timu ya Wizara ya Afya.



SALEMA AIPA WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI NAFASI YA 3 TUFE

◾ Kufutiwa kwa matokeo yake ya ushindi kwazua utata na kushangaza wengi. 


Mchezaji Theodata Salema kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi amefanikiwa kuipa Wizara ya Mifugo na Uvuvi ushindi wa nafasi ya 3 kwenye mchezo wa kurusha tufe uliofanyika leo Oktoba 05, 2023 uwanja wa Samora mkoani Iringa.


Mchezaji huo alirusha mitupo yote mitatu na kupata ushindi wa mita 10. 05 kwenye mtupo wa kwanza na 7.45 kwenye mtupo wa pili huku mtupo wake wa 3 ukifutwa baada ya kurusha tufe nje ya mstari.


Hata hivyo katika hali iliyowashangaza wengi waliokuwa wakishuhudia mashindano hayo matokeo ya mtupo wa mita 10.5  yaliyopaswa kumpa ushindi kwenye mitupo yote mitatu ambayo yalikubaliwa hapo awali na waamuzi wote yalifutwa baadae ambapo ilibainika kuwa  alilalamikiwa na mmoja wa viongozi wa timu zilizokuwa zikishiriki wakidai hakuweka mkono wake mahala sahihi wakati akirusha tufe jambo lililolalamikiwa na wengi kuwa ameonewa.


Mshindi wa kwanza katika mashindano hayo upande wa wanawake ni Tume ya walimu na wa pili ni Mawasiliano.




MIFUGO NA UVUVI RIADHA WASHIKA NAFASI YA 3 RIADHA MITA 3000.

◾ Yatinga nusu fainali mita 100 na 200. 


Mkimbiaji Deonatus Magendelo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi amefanikiwa kushika nafasi ya 3 kwenye mashindano ya riadha umbali wa mita 3000 mbio zilizofanyika kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa leo Oktoba 05, 2025.


Magendelo amefanikiwa kushika nafasi hiyo mara baada ya kuwapiku wanariadha wenzake 54 waliokuwa nyuma yake ambao kwa muda mrefu walionekana kuwa na ushindani wakati wote wa mbio hizo.


Kwa upande wa wanawake umbali huo huo mkimbiaji Beatrice Ilomo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi licha ya kushindwa kushika nafasi za juu amefanikiwa kumaliza mbio hizo jambo ambalo limewashinda baadhi ya wanariadha wenzake.


Katika hatua nyingine Mwanariadha Fihiri Mbawala amefanikiwa kufuzu hatua ya nusu fainali ya mbio za mita 200 mara baada ya kufanikiwa kushika nafasi ya 2 kwenye kundi lake.


Kwa upande wa mbio za mita 100 wakimbiaji William Valentino na Nuru Musa nao wamefanikiwa kutinga hatua ya  nusu fainali ya mbio hizo ambapo William Valentino amefuzu hatua hiyo  baada ya kukamilisha raundi ya kwanza akiwa kinara wa kundi lake huku Nuru Musa akishika nafasi ya 3 kwenye kundi lake.



KAMPENI YA TUTUNZANE MVOMERO DAWA YA MIGOGORO YA ARDHI

Kampeni ya upandaji wa Malisho ya mifugo, uchimbaji wa visima na malambo katika mashamba binafsi ya wafugaji, hamasa ya kilimo biashara na rafiki kwa mazingira imelenga kutatua migogoro ya ardhi wilayani Mvomero.

 

Kampeni hii inayokwenda na kauli mbiu, “Mfugaji Mtunze Mkulima, Mkulima Mtunze Mfugaji ili Kulinda Mazingira Yetu” inalenga kuwaelimisha kwanza kuanza kumiliki ardhi kwa ajili ya kupanda malisho ya mifugo yao na kuanza kufuga mifugo inayoendana nae neo la ardhi wanalomiliki ili kuondokana na migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara kutokana na wafugaji kuhamahama.

 

Akizungumza wakati wa kuhitimisha jukwaa la maandalizi ya kampeni hiyo ijulikanayo kama Tutunzane Mvomero, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti amesema kuwa utekelezaji wa kampeni hiyo unakwenda kutatua tatizo la migogoro ya ardhi iliyopo kati ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi hasa wakulima.

 

Naibu Waziri Mnyeti amesema kumekuwa na migogoro mingi ya ardhi imekuwa ikijitokeza kutokana na kutokuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi katika vijiji na kwenye maeneo ambayo tayari mipango hiyo usimamizi wake unakuwa hafifu. Hivyo amewasihi viongozi wa Mvomero kuhakikisha vijiji vinakuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi na kuusimamia.

 

Wafugaji wameendelea kuhimizwa kumiliki maeneo kwa ajili ya shughuli za ufugaji na kufuata sheria na taratibu zilizopo ili wasiingie kwenye migogoro ambayo inaweza kusababisha uvuvnjifu wa amani. Naibu Waziri Mnyeti amewaeleza wafugaji kuwa Wizara kwa sasa imejipanga kuhakikisha haki inatendeka kwa kila mwananchi hivyo ikiwa kosa linakuwa kwa mfugaji au mkulima basi kila mmoja atachukuliwa hatua kulingana na sheria na taratibu zilizopo.

 

Jukwaa hilo la maandalizi ya kampeni ya tutunzane Mvomero limefanyika likilenga kumaliza migogoro ya ardhi kati ya wafugaji na wakulima na watumiaji wengine wa ardhi inamalizika na kuwafanya wananchi wote kuishi kwa amani na utulivu.



VIONGOZI WATEMBELEA KAMBI YA TIMU YA WIZARA IRINGA

◾ Meneja SAO-HILL atoa motisha ya Maji na Maziwa kwa wachezaji 


Wakurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu  kwa upande wa sekta za Mifugo na Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Charles Mhina na  Bw. Emmanuel Kayuni wametembelea kambi ya timu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi inayoshiriki michuano ya SHIMIWI iliyopo kwenye viunga vya chuo kikuu cha Mkwawa mkoani Iringa leo Oktoba 04, 2023 ambapo mbali na kutoa pongezi kwa timu hiyo kufanya vizuri kwenye michezo mbalimbali wamewasilisha salamu kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Prof. Riziki Shemdoe.


Akizungumza wakati wa ziara hiyo Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu kwa upande wa sekta ya Uvuvi Bw. Emmanuel Kayuni amevitaka vikosi vyote vya Wizara hiyo kuhakikisha vinashinda kwenye michezo yake yote iliyosalia na kupunguza matokeo ya sare ambayo timu ya mpira wa miguu imeyapata kwenye baadhi ya mechi zake.


“Lakini jambo la pili naomba tusiendekeze sana haya mambo ya kupewa ushindi wa mezani, tunataka kucheza na yoyote tuliyepangiwa naye na tumfunge ili afahamu umahiri tulionao kwenye upande wa michezo” Ameongeza Bw. Kayuni


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu kutoka sekta ya Mifugo Dkt. Charles Mhina ameupongeza uongozi wa kamati ya michezo wa Wizara hiyo kwa kutafuta kambi tulivu yenye madhari ya kuwawezesha wanamichezo kujiandaa vema na mechi mbalimbali za michuano hiyo.


“Katibu Mkuu alipanga kuja ili kuungana nasi leo kwenye sherehe za ufunguzi wa michuano hii lakini kutokana na kukabiliwa na majukumu mengine ya kikazi ametuagiza mimi na mwenzangu kufika kwenye ufunguzi na kuja kuungana na nyie hapa kambini ili kufahamu kama mna changamoto zozote tuweze kuziwasilisha kwao” Amebainisha Dkt. Mhina.


Akielezea hali ya kambi na ushiriki wa Wizara kwa ujumla kwenye michuano hiyo Mwenyekiti wa kamati ya Michezo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Ally Suru aliwaeleza viongozi hao kuwa wachezaji wote wapo salama kambini na kuwahakikishia  kuendelea kufanya vizuri kwenye michezo inayofuata kutokana na maandalizi yanayoendelea kwa upande wa timu zote.


Aidha Bw. Suru aliushukuru uongozi wa Wizara kwa ujumla kwa mchango mkubwa wanaoendelea kuutoa kwa timu zake ambapo aliwaahidi kuendelea kudumisha nidhamu wakati wote wa michuano hiyo kama ambavyo timu hizo zimekuwa zikifanya tangu alipochaguliwa kushika wadhifa huo.


“Lakini pia nitumie fursa hii kutoa shukrani za dhati kwa wakuu wa Taasisi za TVLA ambao wametupa wachezaji 7 na kuwagharamia 6, Deep Sea kutoka Zanzibar ambao tuliwaomba wachezaji 3 walikubali na wote waliwagharamia, LITA ambao tuliwaomba wachezaji 4 wametupa wote na kuwagharamia 2, Bodi ya Nyama ambao tuliwaomba mchezaji mmoja walitupa na kumgharamia na Bodi ya Maziwa ambao  tuliwaomba wachezaji  3, wametupa wawili na kumgharamia mmoja” Amesisitiza Bw. Suru.


Naye Meneja wa Shamba la Mifugo la SAO-HILL lililopo Mafinga mkoani Iringa Bw. Noel Byamungu ambaye amewapelekea wachezaji hao katoni za maziwa na maji amebainisha kuwa hatua hiyo imetokana na kuguswa kwake na matokeo mazuri ambayo vikosi mbalimbali vya timu hiyo vimekuwa vikipata na hivyo kuwapa motisha ili wafanye vizuri zaidi.


“Mmekuja kwenye mkoa ambao mimi ni mwenyeji hivyo nikaona ni vizuri nije kuwapa sapoti kidogo na ninatumai mtaendelea kufanya vizuri zaidi kwenye michezo inayofuata.” Amehitimisha Bw. Byamungu.


Michuano hiyo ya SHIMIWI inatarajiwa kuendelea kesho kwa mchezo wa riadha ambapo Wizara ya Mifugo na Uvuvi inatarajia kuwa na wawakilishi katika mchezo huo.



WADAU WAHIMIZWA KUWEKEZA KWENYE SEKTA YA MIFUGO NA UVUVI WILAYANI PANGANI

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti amewasihi wadau kuwekeza kupitia Sekta za Mifugo na Uvuvi wilayani pangani ili kuongeza uzalishaji na tija.

 

Naibu Waziri Mnyeti ameyasema hay oleo (03.10.2023) wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Wilaya ya Pangani Mkoani Tanga ambapo aliwaeleza washiriki kuwa zipo fursa nyingi kupitia sekta za mifugo na uvuvi.

 

Wadau wamehimizwa kutumia fursa zilizopo katika ufugaji wa mifugo na samaki kwa kuhakikisha wanaongeza uzalishaji na uongezaji wa thamani wa mazao ya mifugo na uvuvi ili kuongeza ajira, kipato na mchango wa sekta hizo kwenye pato la taifa.

 

“Niwaombe wadau kuja kuwekeza hapa pangani kupitia sekta hizi za mifugo na uvuvi kwa kuwa fursa zipo kuanzia kwenye kuongeza uzalishaji na uongezaji wa thamani wa mazao ya mifugo na uvuvi, hivyo kupitia kongamano hili ni vema tukazitumia fursa hizi kwa ajili ya kuleta maendeleo yetu, ya wanapangani na taifa kwa ujumla,’ alisema

 

Naibu Waziri Mnyeti pia amewasihi wafugaji kufuga mifugo iliyobora ambayo inakuwa na thamani kubwa badala ya kuwa na ng’ombe wengi ambao tija yake ni ndogo na hivyo kusababisha migogoro ya ardhi. Amewashauri wafugaji kuanza kubadilisha mifugo yao kwa kutumia njia ya uhimilishaji pamoja na kupunguza ng’ombe wengi ambao tija yake ni ndogo na kununua ng’ombe ambao ni wakubwa na wanauwezo wa kutoa maziwa mengi.

 

Aidha, amewasihi wadau kutumia fursa ya uwepo wa bandari wilayani Pangani kwa shughuli za uvuvi kwa kuzingatia sheria kwani bila hivyo serikali itaendelea kuchukua hatua kwa wale wanaokiuka. Naibu Waziri Mnyeti amesema kwa sasa serikali imejipanga kuwashughulikia wauzaji wa nyavu zisizokidhi vigezo kwa kuwa wao ndio wanaowauzia wavuvi.

 

Naye Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kihale amesema serikali imeweka mazingira wezeshi ya kuhakikisha wadau hawakwamishwi pale wanapokuwa na lengo la kuwekeza hapa nchini. Hivyo amewasihi wadau kupitia kongamano hilo kwenda kuwekeza wilayani pangani kwa kuwa fursa zilizopo ni nyingi kupitia sekta mbalimbali.

 

Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Mhe. Zainab Issa amesema wilaya imejipanga kupokea wawekezaji na kwamba suala la umeme upo katika vijiji vyote, mradi wa maji unaendelea kukamilishwa kwenye maeneo ambayo yanachangamoto na kwa upande wa barabara mkandarasi anaendelea na kazi. Hivyo wawekezaji walio na nia wamekaribishwa kuwekeza wilayani Pangani. Lakini pia ameiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuangalia uwezekano wa kujenga bandari ya mifugo wilayani humo ili mifugo na mazao yake yawe yanasafirishwa kupitia bandari hiyo.

 

Kongamano hilo ambalo lilikuwa na lengo la kutangaza fursa mbalimbali zilizopo wilayani pangani liliwashirikisha wadau kutoka sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja na wizara za kisekta na taasisi ambapo wawakilishi walipata fursa ya kuelezea nini taasisi zao zinafanya ili kuweka mazingira sahihi ya biashara na uwekezaji.

 

 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti akizungumza na wadau walioshiriki kwenye uzinduzi wa Kampeni ya Upandaji wa Malisho, Uchimbaji wa Visima na Malambo katika Mashamba Binafsi ya Wafugaji, Hamasa ya Kilimo Biashara na Rafiki kwa Mazingira




RAIS SAMIA AMEDHAMIRIA KUWAINUA WAVUVI TANZANIA - ULEGA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuwainua wavuvi kwa kuwawezesha vifaa vya kisasa vya uvuvi ikiwemo maboti na vizimba ili waweze kuboresha maisha yao.


Waziri Ulega ameyasema hayo wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa vizimba na boti leo Oktoba 3, 2023 jijini Mwanza.

"Mradi huu wa ugawaji wa maboti na vizimba kwa wavuvi bila riba ni wa kwanza, haujawahi kufanywa na yeyote, Rais Dkt. Samia ndio wa kwanza kuutekeleza, ametoa jumla ya shilingi bilioni 25 kwa ajili ya kuwezesha wavuvi kupata vifaa vya kisasa ili kuboresha maisha yao", amesema Ulega

Ameongeza kwa kusema kuwa Rais Dkt. Samia anafanya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi kwa vitendo na hivi karibuni atagawa kwa wavuvi wa Kanda ya ziwa boti takriban 55 na vizimba 615.





PETE MIFUGO NA UVUVI YAIADHIBU RAS SINGIDA

Timu ya Mpira wa pete kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendeleza wimbi lake la ushindi kwenye michuano ya SHIMIWI baada ya kufanikiwa kuifunga timu ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida kwa jumla ya magoli 25-11 mchezo uliochezwa leo Oktoba 03, 2023 kwenye uwanja wa RUCU B mkoani Iringa.


Kwa ushindi huo timu hiyo imezidi kujiweka kwenye mazingira mazuri ya kutinga hatua ya 16 bora ambapo sasa italazimika kusubiri kukamilika kwa michezo mingine hatua ya makundi ili kubaini timu zilizofuzu hatua hiyo.



MPIRA WA MIGUU WATINGA 16 BORA SHIMIWI 2023

◾ Ni baada ya kutoa suluhu dhidi ya MSD 


Timu ya soka kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefanikiwa kufuzu hatua ya 16 bora ya Michuano ya SHIMIWI inayoendelea mkoani Iringa baada ya kutoka suluhu na timu ya MSD kwenye mchezo uliopigwa Uwanja wa mkwawa 2 leo Oktoba 03, 2023.


Mchezo huo uliokuwa na upinzani mkali kutokana na kila timu kuhitaji pointi 3 muhimu ili iweze kufuzu hatua hiyo ulishuhudia timu zote zikitengeneza nafasi na kushindwa kuzitumia jambo lililoufanya kuwa mgumu zaidi hasa kwa upande wa MSD ambao kwa namna yoyote walihitaji kushinda mchezo wa leo.


Upinzani mkali uliokuwepo baina ya timu hizo mbili ulishuhudia mlinzi wa kati Abdallah Bajwala kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na kiungo Omary Kibaranga kutoka MSD wakitolewa nje kwa kadi nyekundu ambapo Bajwala alioneshwa kadi hiyo baada ya kuunawa mpira huku akiwa mchezaji wa mwisho kwenye lango lao na Kibaranga aliadhibiwa mara baada ya kumsukuma mwamuzi baada ya kutoridhika uamuzi wake.


Kwa matokeo hayo Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetangulia kwenye hatua ya 16 bora ikiwa  imefikisha pointi 6 huku ikisubiri timu ya pili kati ya Mawasiliano na TAKUKURU ambao wanakutana leo na kila mmoja akiwa na pointi 4. 


Kama yoyote kati ya timu hizo itaibuka na ushindi itafikisha pointi 7 na kuongoza kundi huku Wizara ya Mifugo na Uvuvi wakishika nafasi ya pili na kama watatoa sare ya aina yoyote timu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi itasalia kinara wa kundi hilo.



KAMBA WANAWAKE WAFUZU 16 BORA

Ni baada ya kuwagaragaza RAS Kilimanjaro 


Timu ya kamba upande wa wanawake kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefanikiwa kutinga hatua ya 16 bora ya michuano ya SHIMIWI inayoendelea mkoani Iringa baada ya kushinda mvuto 1-0 dhidi ya timu ya Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro leo Oktoba 03, 2023 mchezo uliofanyika kwenye uwanja wa Mkwawa.


Timu hiyo iliibuka na ushindi huo kwenye raundi ya pili ya mchezo huo ambapo raundi ya kwanza iliisha kwa timu hizo kutoshana nguvu.


Timu hiyo inakuwa ya pili kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi kufuzu hatua hiyo ikitanguliwa na ile ya Kamba wanaume ambayo ilifuzu mara baada ya mechi zake tatu za awali.



Ijumaa, 6 Oktoba 2023

WAZIRI ULEGA ATAJA FAIDA LUKUKI ZILIZOPATIKANA KUTOKANA NA MKUTANO WA AGRF 2023

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amesema kufuatia Jukwaa la Mkutano wa Mifumo ya Chakula Barani Afrika (AGRF), Sekta ya Mifugo na Uvuvi hapa nchini zimenufaika kwa kupata fursa mbalimbali za kibiashara, uwekezaji, mitaji na masoko.


Waziri Ulega alibainisha hayo leo Oktoba 2, 2023 wakati wa mkutano na Waandishi wa Habari kuwaelezea  mafanikio yaliyopatikana kutokana uwepo wa Mkutano wa Mifumo ya Chakula Barani Afrika (AGRF) uliofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Septemba 5 hadi 8, 2023.


Alisema kupitia mkutano huo  Tanzania  ilipata fursa ya kuonesha programu bunifu ya BBT ambayo ni programu ya kielelezo ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan na kupelekea kupata ahadi ya kuungwa mkono kwa Kiasi cha Dola za Marekani milioni 500 zilitolewa na wahisani kwa ajili ya kufadhili programu hiyo.


Vilevile, alisema, Benki ya CRDB imetoa ahadi ya kiasi cha Dola Milioni 50 kama mikopo yenye masharti nafuu kwa ajili ya kusaidia Vijana waliopo katika sekta za Mifugo na Uvuvi kupata mitaji.


Halikadhalika, aliendelea kufafanua kuwa, uwepo wa mkutano huo, ulivutia wadau takriban 5,400 kutoka nchi 90, ambao walipata fursa mbalimbali za kujadili mageuzi ambayo yataunda mustakabali wa bara la Afrika.


Awali, Waziri Ulega alitumia fursa hiyo kutoa shukrani  za dhati kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake wenye mtazamo wa mbali wenye dhamira ya kuinua sekta za uzalishaji zikiwemo sekta za mifugo na uvuvi.



Jumatano, 4 Oktoba 2023

KAMPENI YA TUTUNZANE MVOMERO DAWA YA MIGOGORO YA ARDHI


 

 


Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (LITA) Dkt. Pius Mwambene (katikati) akiongea na wafugaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya ufugaji bora wa ng'ombe wa maziwa, chini ya mradi wa maziwa faida, yaliofanyika LITA kampasi ya Buhuri Mkoani Tanga, Septemba 29,2023

WADAU WAKUTANA KUTATHIMINI MRADI WA USIMAMIZI WA RASILIMALI ZA BAHARI

Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Kamati tendaji ya mradi wa ushirikiano kati ya Nairobi Convention na Southwest Indian Ocean Commission imekutana jijini Tanga kwa ajili ya kufanya tathmini ya mradi huo unaolenga usimamizi wa mazingira ya bahari na nchi kavu pamoja na usimamizi wa rasilimali za uvuvi

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI ), Dkt. Ismael Kimirei Oktoba 04,2023 ambapo amesema kuwa mradi huo unaotekelezwa katika Wilaya ya Mkinga na Pemba unalenga kutoa majibu ya mahitaji katika uchumi wa buluu

Tumeanzia eneo la Mkinga kwa sababu huu ni mradi wa ushirikiano kati ya Tanzania, Msumbiji na Madagascar na tunategemea kwamba utapanuka kwenda nchi nyingine na ukiangalia upande wa kaskazini mwa bahari ya Hindi kuna nchi ya Kenya ambayo tunatarajia iwe mdau katika mradi huu" amesema Bi. Oliver

Naye Mratibu wa Mradi unaoshughulikia maendeleo ya usimamizi wa rasilimali za bahari kutoka Shirika la Chakula na kilimo (FAO) Bi. Oliver Mkumbo amesema kuwa mradi huo unathamani ya dola za marekani milioni 8 ambazo zimegawanywa katika nchi tatu

"Kubwa ni kuangalia namna gani tuboreshe mazingira lakini wakati huo huo kuangalia rasilimali zilizopo ukanda wa Pwani zimekuwa endelevu na maisha ya watu yameboreshwa kwa shughuli zinazofanyika

Kwa upande wake Afisa uvuvi wa  Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga Bw. Ezra Katete amesema kuwa mradi huo umesaidia kwa kiasi kikubwa kutoa elimu kwa wananchi juu ya  kushirikishwa kulinda maeneo yao hususani katika utunzaji wa mazingira na kufanya uvuvi endelevu.


Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania Dkt. Ismael Kimirei akiongea na wajumbe  wakati wa kufungua kikao cha kamati tendaji cha mradi wa ushirikiano wa SWIOFIC Nairobi Convention  kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha VETA Mkoani Tanga, Oktoba 04,2023.

Mratibu wa Mradi unaoshughulikia maendeleo ya usimamizi wa rasilimali za bahari, Bi. Oliva Mkumbo akichangia hoja wakati wa kikao cha kamati tendaji cha mradi wa ushirikiano wa SWIOFIC Nairobi Convention  kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha VETA Mkoani Tanga, Oktoba 04,2023.

Mkurugenzi Msaidizi wa Uendelezaji wa Rasilimali za uvuvi, Idara ya Uvuvi Bi. Merisia Mparazo akiwasilisha mada kwa wadau wa uvuvi (hawapo pichani) wakati wa kikao cha kamati tendaji cha mradi wa ushirikiano wa SWIOFIC Nairobi Convention  kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha VETA Mkoani Tanga, Oktoba 04,2023.

Afisa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Idara ya Mazingira Bi. Magdalena Ngotolainyo akiwasilisha mada kwa wadau wa uvuvi (hawapo pichani) wakati wa kikao cha kamati tendaji cha mradi wa ushirikiano wa SWIOFIC Nairobi Convention  kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha VETA Mkoani Tanga, Oktoba 04,2023.

Meneja wa Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu nchini Dkt. Immaculate Sware Semesi akichangia hoja wakati wa kikao cha kamati tendaji cha mradi wa ushirikiano wa SWIOFIC Nairobi Convention kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha VETA Mkoani Tanga, Oktoba 04,2023.

Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Tumaini Chambua  akiwasilisha mada wakati wa kikao cha kamati tendaji cha mradi wa ushirikiano wa SWIOFIC Nairobi Convention  kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha VETA Mkoani Tanga, Oktoba 04,2023.

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) Dkt. Ismael Kimirei (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wawakilishi kutoka Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) , wawakilishi kutoka Nairobi Convention Secretariate na watendaji kutoka Wizara ya mifugo na Uvuvi mara baada ya kikao cha kamati tendaji cha mradi wa ushirikiano wa SWIOFIC Nairobi Convention  kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha VETA Mkoani Tanga, Oktoba 04,2023.

Mratibu wa Mradi Kikanda Bi. Ulrika Gunnartz akiwasilisha mada wakati wa kikao cha kamati tendaji cha mradi wa ushirikiano wa SWIOFIC Nairobi Convention kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha VETA Mkoani Tanga, Oktoba 04,2023.