Nav bar

Jumatatu, 9 Oktoba 2023

SERIKALI YADHAMIRIA KUWAINUA VIJANA WA BBT-LIFE KWA KUWATAFUTIA MASOKO YA MIFUGO

SERIKALI kupitia  Wizara ya Mifugo na Uvuvi imesema kuwa inaendelea na majadiliano  na Wadau wa sekta ya Mifugo nchini  ili kuona namna bora ya kushirikiana na vijana waliopo kwenye Programu ya  BBT  -LIFE katika kunenepesha Mifugo na kuisafirisha kwenye masoko ya nje ya nchi.


Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, (Mifugo) Dkt. Daniel Mushi wakati wa  kikao kati ya menejimenti ya sekta mifugo na wadau kuhusu kuwaunga mkono vijana waliopo kwenye programu ya BBT- LIFE , jijini Dodoma, tarehe 06.10.2023.


Dkt.Mushi amebainisha kuwa wamekutana na Kampuni za ELIA FOOD na TANCHOICE  Limited za uchakataji nyama  kwa ajili ya  kutengeneza muunganiko wa BBT -LIFE na Soko kubwa la nje ya nchi la uuzaji wa mazao ya Mifugo ili kukabiliana na changamoto ya masoko ya mifugo kwa vijana wa BBT-LIFE.


"Tumefikiria kuwa tukiwapata  wanunuzi wakubwa wa Mifugo programu yetu ya BBT - LIFE itakuwa imefanikiwa katika kuwawezesha vijana kujiajiri kupitia fursa hii ya wadau “, Amesema Dk. Mushi.


 Pia alisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha Mifugo haisafirishwi nje ya nchi ikiwa hai bali ichakatwe ndani ya nchi ili kuleta ajira kwa vijana hapa nchini na hatimaye kunufaika na rasilimali zilizopo na kuongeza pato la taifa.


Katika hatua nyingine Naibu Katibu Mkuu huyo,amefafanua kuwa,Wizara ya Mifugo na Uvuvi inatarajia kuanzisha Vituo vingine zaidi vya BBT -LIFE  kwa ajili ya Vijana ambao watakuwa wanashirikiana na wadau mbalimbali katika biashara hiyo ya mifugo.


Naye mmoja wa wadau hao Dkt.Sele Luwongo kutoka  kampuni ya TANCHOICE Limited ambayo ni  machinjio na kiwanda cha kuchakata  nyama amesema wao kama sekta binafsi wako tayari kushirikiana na Serikali katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto za masoko kwa mifugo ya vijana waliopo kwenye prigramu ya BBT -LIFE .



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni