Nav bar

Jumatatu, 21 Februari 2022

RUANGWA WAKABIDHIWA VIFARANGA VYA KUKU ZAIDI YA 3000


Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetoa vifaranga vya kuku 3060 kwa vikundi  vya  wanawake Wilayani Ruangwa Mkoani Lindi ikiwa ni katika utekelezaji wa sera ya kuwakwamua wananchi kiuchumi.

Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaranga hivyo Februari 9, 2022 kwa vikundi vya kina mama,  Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti na Mafunzo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi,  Dkt Hassan Mruttu alisema mradi huo wa ufugaji kuku utakuwa wa shamba darasa.

Alisema Wizara iliona ni vyema kuanza kutoa kuku kwa vikundi viwili (2) cha Alonga na Kichawana kama shamba darasa ambapo baada ya wiki 4 watatakiwa kusambaza katika vikundi vingine ili navyo viweze kufuga.

"Sisi kama Wizara tunatekeleza ilani ya CCM tukiwa chini ya Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye ni mbunge wa hapa kwa hiyo katika kubuni namna ya kumkwamua mwanachi tukasema hatuwezi kumfikia mtu mmoja bali kwa kuanzisha mashamba darasa ambapo  vikundi vinakuwa vikijifunza na baada ya wiki nne vinapatiwa kuku kama mtaji wao" alisema

Akitoa shukrani kwa niaba ya ofisi ya Mbunge wa jimbo la Ruangwa, Msaidizi wa Waziri jimboni, Bw. Ramadhani Matola alisema wanaishukuru Wizara kwa kuendelea kutekeleza vyema ilani ya CCM ambayo kwa asilimia kubwa inalenga kumkwamua mwananchi wa chini.

Alisema kwa kupatiwa kuku hao kutawasaidia wananchi wa jimbo hilo kuondokana na umasikini kwa kufuga kisasa na kibiashara ambapo wataweza kuinua kipato chao na taifa kwa ujumla.

Kampuni ya AKM GLITTER ndio iliyopewa dhamana na Serikali ya kuzalisha na kusambaza kuku hao katika wilaya ya Ruangwa ambapo wameahidi kutekeleza zoezi hilo kwa ufanisi na kuhakikisha kila kikundi tarajiwa kinanufaika na mradi huo.

Kupitia Afisa Mifugo wa kampuni hiyo  Bw.Hamim Dauri alisema kampuni inaamini kupitia vikundi vya kina mama na vijana wakiwezeshwa kufuga mifugo midogo kama kuku wanaweza kuinua maisha yao kwasababu hawatumii gharama kubwa katika ukuzaji

"Tunashukuru Serikali kutuamini na tunaahidi kufanya kazi kwa umakini kuhakikisha malengo ya Serikali yanafikiwa kwa sababu tunaamini katika ufugaji wa kibiashara na pia tunaamini tukimuwezesha kijana au mama kufuga mifugo midogo itamuondolea umasikini" alisema

Kwa upande wa baadhi ya wanakikundi ambao ndio wanufaika walisema wanatambua kuwa dhamana waliyopewa ni kubwa kwa kuanza na shamba darasa hilo kwani vikundi vingine vinategemea kupata kuku kutoka kwao.


Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti na Mafunzo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Hassan Mruttu akiongea na akina mama wa kikundi cha Kichawana mara baada ya kukabidhiwa vifaranga vya kuku na kuwasihi kuvitunza vifaranga hivyo kwani ni mtaji utakao wasaidia kujikwamua kiuchumi Februari 09, 2022 Ruangwa Mkoani Lindi. 

 

Msaidizi wa Mhe. Waziri Mkuu jimboni Bw. Ramadhani Matola akikabidhi vifaranga vya kuku kwenye shamba darasa litakalo simamiwa na kikundi cha  akina mama cha Alonga Ruangwa Mkoani Lindi, Februari 09,2022. 

 

Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti na Mafunzo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Hassan Mruttu (wa tano kutoka kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na akina mama wa kikundi cha Alonga, maafisa Mifugo na Msaidizi wa Waziri wa Ruangwa mara baada ya kukabidhi vifaranga vya kuku kwa wanakikundi hao. Februari 09, 2022. 


Jumatatu, 7 Februari 2022

WAFANYABIASHARA WA NJE WANAONUNUA MAZAO YA UVUVI KATIKA MIALO KUCHUKULIWA HATUA

Na Mbaraka Kambona, Mwanza

Waziri wa Mifugo na uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amewaagiza Watendaji wa wizara hiyo kwa kushirikiana na Watendaji wa Halmashauri kote nchini kuhakikisha wafanyabiashara wanaotoka nje ya nchi wananunua mazao ya uvuvi katika masoko yaliyopangwa na serikali na sio kwenye mialo kama baadhi yao wanavyofanya sasa ili kuepuka kupoteza mapato ya serikali yatokanayo na mazao hayo. 

Waziri Ndaki alitoa agizo hilo wakati alipofanya kikao kilichohusisha watendaji wa wizara ya mifugo na uvuvi (sekta ya uvuvi), wafanyabiashara na wadau wa sekta hiyo kutoka halmashauri ya jiji la Mwanza Februari 2, 2022.

Alitoa agizo hilo baada ya wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao katika soko la Kimataifa la Kirumba kumweleza kuwa wapo baadhi ya wafanyabiashara kutoka mataifa ya jirani ambao wananunua mazao ya uvuvi katika mialo badala ya kwenda sokoni na kusababisha serikali kukosa mapato.

“Kama kuna wafanyabiashara kutoka nje ya nchi wanakwenda kununua mazao ya uvuvi huko visiwani, hao wanatenda makosa, wanapaswa wakamatwe na wafunguliwe mashitaka, naomba mamlaka husika kuanza kufuatilia malalamiko hayo ili kukomesha upotevu wa mapato,” alisema Mhe. Ndaki

Aidha, alitumia nafasi hiyo pia kusema kuwa kama kuna baadhi ya viongozi na watendaji wa serikali wanashirikiana na wafanyabiashara hao nao watafuatiliwa na kupelekwa kwa mamlaka zao husika ili wachukuliwe hatua.

Awali, akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Soko la Kimataifa la Kirumba lililopo jijini Mwanza, Fikiri Magafu alimweleza Waziri Ndaki kuwa kuna wafanyabiashara wengi kutoka nchi jirani wanaokwenda katika visiwa vilivyopo ndani ya Ziwa Viktoria na kununua mazao hayo bila kufuata utaratibu jambo ambalo linafanya wao kuwa na wakati mgumu wa kibiashara.

Katika hatua nyingine,  wafanyabiashara hao waliiomba serikali kurekebisha baadhi ya tozo na kuangalia upya utoaji wa leseni za biashara kwa wafanyabiashara wa ndani na wa nje ili kuwajengea mazingira mazuri ya kulipa kodi kwa serikali jambo ambalo Waziri Ndaki alisema wamepokea maombi hayo huku akiahidi kuwa wao kama wizara kwa kushirikiana  na watendaji wa halmashauri watapitia upya kodi na tozo zilizopo  kwa mujibu wa sheria na kuzirekebisha ili kuwawezesha wafanyabiashara kufanya shughuli zao kwa tija.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akiongea na Wafanyabiashara wa mazao ya uvuvi wanaofanya shughuli zao Mkoani Mwanza katika Mkutano wa kusikiliza kero za Wafanyabiashara hao kilichofanyika mkoani mwanza Februari 2, 2022. Baada ya kusikiliza kero zao alizitolea maelekezo huku akiahidi kuwa watapitia upya kodi na tozo na kurekebisha zile zinazoonekana kuwa kikwazo ili kuwawezesha wafanyabiashara kufanya shughuli zao kwa tija. 

 

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah (kulia) akitoa neno la utangulizi wakati akiongea na Wafanyabiashara wa Mazao ya Uvuvi wanaofanya shughuli zao Mkoani Mwanza katika Mkutano wa kusikiliza kero za Wafanyabiashara hao kilichofanyika mkoani mwanza  Februari 2, 2022. 


 

ULEGA ALIHAKIKISHIA BUNGE MAFANIKIO YA WAVUVI KWENYE UCHUMI WA BULUU*


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amelihakikishia bunge kuwa uchumi wa buluu kwa upande wa Tanzania bara utatekelezwa katika eneo kubwa zaidi kutokana na kuamua kuutekeleza katika vyanzo vyote vya maji vilivyopo nchini.

Mhe. Ulega ameyasema hayo wakati akijibu swali la mmoja  wa wajumbe wa kamati ya kudumu ya bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji ambaye alitaka kufahamu namna uchumi wa buluu unavyotekelezwa kwa upande wa Tanzania bara wakati wa kikao cha kamati hiyo kilichofanyika  (03.02.2022) kwenye moja ya kumbi za Bunge jijini Dodoma

Mhe. Ulega amesema kuwa upande wa Tanzania bara una vyanzo vingi zaidi vya maji ikilinganishwa na Zanzibar  na tayari Wizara yake imeanza hatua ya awali ya utekelezaji wa dhana hiyo kwa vitendo kwa   kuwaelimisha wavuvi juu ya fursa mbalimbali zilizopo kwenye mazao mbalimbali ya Uvuvi.

“Mhe. Mwenyekiti hivi karibuni nilikuwa mkoani Tanga nikiwaelimisha wananchi juu ya fursa mbalimbali zilizopo kwenye uchumi wa buluu kwa sababu uchumi huu hauishii tu kuvua kwenye vyanzo vya asilli bali zipo fursa pana zaidi ikiwemo ufugaji wa viumbe maji kwa upande wa baharini au maji ya ndani kama vile Ziwa Nyasa na vyanzo vingine” Amesema Mhe. Ulega

Mhe. Ulega amebainisha kuwa Uchumi wa buluu utawafanya wavuvi waliopo hapa nchini kujipatia kipato kikubwa zaidi ukilinganisha na kile wanachokipata kwa hivi sasa kwa sababu watapata fursa ya kujipatia fedha za kigeni kupitia mazao mbalimbali ya Uvuvi kama vile kaa, majongoo bahari, lulu na mwani.

“Leo ukimwambia mvuvi kuwa kuna fedha nyingi sana inapatikana kwenye samaki aina ya kaa anaweza  asikuelewe lakini kwa hivi sasa kilo moja ya kaa inauzwa shilingi 25, 000 na kilo moja hiyo ni wastani wa kaa wawili tu tena ambao hawana gharama kwenye utunzaji wao kwa sababu unawaweka tu kwenye maji ya baharini na kila kitu wanakipata humu, kama utawawekea chakula basi ni kidogo sana” Amesisitiza Mhe. Ulega.

Mhe. Ulega amebainisha kuwa hatua inayofuata baada ya kuwaelimisha wananchi juu ya fursa zilizopo kwenye uchumi wa buluu ni kuandaa mikutano na warsha mbalimbali zitakazojumuisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ili kuufungua uchumi huo kwa wadau hao wa sekta binafsi ambao aliwataja kama walengwa wakuu katika utekelezaji wa uchumi huo.

Kwa upande wake mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Simanjiro, Mhe. Christopher Ole Sendeka amesema kuwa sekta ya Uvuvi pamoja na kazi kubwa wanayofanya bado kiasi cha bajeti kilichotengwa na kinachopelekwa kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali ni kidogo na hivyo aliwaomba wajumbe wa kamati hiyo kuungana kwa pamoja na kuwasilisha chagamoto hiyo kwa wahusika.

Kabla ya kuhitimisha kikao hicho, Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Christine Ishengoma amewataka wataalam wa sekta hiyo kuendelea kuwa karibu na wadau wake hasa wale waliojiingiza kwenye shughuli za ukuzaji viumbe maji ambapo alisema kuwa suala hilo ndo litapunguza upungufu wa samaki uliopo  hapa nchini kwa hivi sasa.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (kulia) akiwaeleza wajumbe wa kamati ya kudumu ya bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji namna uchumi wa buluu ulivyoanza kutekelezwa kwa upande wa Tanzania bara wakati wa kikao cha kamati hiyo kilichofanyika  (03.02.2022) kwenye moja ya kumbi za bunge jijini Dodoma.

 


 

SERIKALI YAELEZA MIKAKATI YA KUKABILIANA NA ATHARI ZA UKAME KWENYE MIFUGO

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, upande wa sekta ya Mifugo imebainisha mikakati iliyoiweka ili kukabiliana na athari za ukame ulioiathiri mifugo katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango kwa upande wa sekta hiyo, Mbaraka Stambuli wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji ya robo mwaka mbele ya kamati ya kudumu ya Kilimo, Mifugo na Maji kwenye kikao kilichofanyika  (02.02.2022) kwenye moja ya Kumbi za Bunge jijini Dodoma.

“Mhe. Mwenyekiti moja ya mikakati tuliyoiweka kama Wizara ni kupeleka lita 2906 za dawa ili kuua kupe na mbung’o katika Halmashauri zilizoathirika zaidi lakini pia Wizara inajenga majosho 32 yenye thamani ya shilingi milioni 500 ili kuchochea uogeshaji kwa lengo la kudhibiti magonjwa kwenye maeneo yaliyoathirika zaidi” Amesema Stambuli.

Stambuli amebainisha mkakati mwingine kuwa ni pamoja na Wizara yake  kushirikiana na Wizara ya Maji kuchimba visima virefu 6 katika Wilaya za Simanjiro, Same, Kibaha, Chalinze na Morogoro pamoja na miundombinu yake ambavyo vyote kwa pamoja vina thamani ya shilingi bilioni 1 jambo ambalo litapunguza hali ya ukame kwa kiasi kikubwa.

“Lakini pia mkakati wa muda wa kati utakaoanza mwaka ujao wa fedha, Wizara itatenga fedha kwa ajili ya uanzishaji wa miundombinu ya maji, majosho na malisho ya mifugo katika maeneo yaliyoathiriwa zaidi na ukame wa mwaka huu” Amesema Stambuli.

Akichangia suala hilo, Mbunge wa Viti maalum kutoka mkoa wa Manyara Mhe. Yustina Rahhi amewashauri wafugaji kote nchini kuanza kufuga kisasa kwa kuzingatia maeneo na malisho yaliyopo badala ya kufuga mifugo mingi bila kuzingatia hali ya upatikanaji wa maji na malisho.

“Mhe. Mwenyekiti ni wakati sasa kwa wafugaji kuachana na ufugaji usio na tija kwa sababu unakuwa na ng’ombe 1000 au 2000 afu mwisho wa siku idadi kubwa wanakufa kwa kukosa malisho na maji na unakuta hata hao wanaobaki ukienda kupima uzito wao wanaishia kwenye kilo 100” Amesema Mhe. Rahhi.

Akizungumzia yale ambayo kamati imeyaona kupitia taarifa waliyowasilishiwa kwa upande wa Sekta ya Mifugo, Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Christine Ishengoma amesema kuwa kamati yake inatambua namna changamoto ya ufinyu wa bajeti inavyokwamisha utekelezaji wa shughuli mbalimbali za sekta hiyo ambapo ameahidi kuifanyia kazi changamoto hiyo.

“Lakini pia nitoe rai kwa Wataalam wote wa Sekta ya Mifugo kuendelea kutumia kiasi cha fedha mnacholetewa kutekeleza zaidi maeneo ya vipaumbele ili kupunguza changamoto za wafugaji zilizopo hivi sasa” Amesema Mhe. Ishengoma.

Akitoa neno la shukrani kwa wajumbe wa kamati hiyo, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega ameahidi kufanyia kazi maoni na ushauri uliotolewa na wajumbe wa kamati hiyo ambapo ameihakikishia kamati hiyo kushirikiana na wataalam wake katika kuhakikisha wanaendelea kushughulikia changamoto zinazowakabili wafugaji nchini.

Kikao cha kamati hiyo kitaendelea tena kesho (03.02.2021) ambapo sekta ya Uvuvi itawasilisha taarifa yake ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali zinazohusu sekta hiyo.  


Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango (Mifugo) Bw. Mbaraka Stambuli (kulia) akiwasilisha taarifa ya utekelezaji ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) kwa wajumbe wa Kamati ya kudumu ya Kilimo, Mifugo na Maji wakati wa kikao cha kamati hiyo kilichofanyika   (02.02.2022) kwenye moja ya kumbi za Bunge jijini Dodoma.

 

Baadhi ya wajumbe wa kamati ya kudumu  ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji wakifuatilia uwasilishaji wa taarifa ya utekelezaji ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) iliyowasilishwa na Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango (Mifugo) Bw.Mbaraka Stambuli (hayupo pichani) wakati wa kikao cha kamati hiyo kilichofanyika   (02.02.2022) kwenye moja ya kumbi za Bunge jijini Dodoma. 

 

 

 

 

 

UZALISHAJI VIFARANGA VYA SAMAKI WAWEKEWA MKAKATI ENDELEVU

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeweka mikakati endelevu ya kuhakikisha inazalisha kwa wingi vifaranga vya samaki na kutoa elimu juu ya ufugaji wa samaki kwa wananchi ili kuongeza tija na kipato kwa Wafugaji na Taifa kwa ujumla.

Mkurugenzi wa Ukuzaji Viumbe  Maji wa  Wizara hiyo , Dkt. Nazael  Madalla  alisema hayo Februari 1,2022  katika mafunzo rejea kwa maofisa ugani wa halmashauri za  mikoa ya Dar es Salaam, Tanga , Arusha , Pwani na Kilimanjaro yanayofanyika Mkoani Morogoro.

Dkt. Madalla alisema mafunzo hayo yamelenga   kuhamasisha,  kuendeleza , kusimamia tasnia ya ukuzaji viumbe maji nchini na kuzalisha kwa tija .

Aliendelea kusema kuwa vituo vinavyozalisha vifaranga wa samaki kwa Sasa ni vitatu ambavyo ni  Ruhila kilichopo  mkoa wa Ruvuma,  Mwamapuli  mkoani Tabora, na Kingolwira Morogoro.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo,  mwaka 2020/2021 vituo hivyo  vitatu viliwezakuzalisha jumla  ya vifaranga vya samaki 1,901,717.

“Uzalishaji wa vifaranga vya Samaki katika vituo hivyo ni kama ifuatavyo, Kituo cha Ruhila kilizalisha vifaranga 972,305, Mwamapuli vifaranga 457,812 na cha hapa Kingolwira vifaranga 471,600 ", alisema Dk Madalla.

Aliongeza kwa kusema kuwa wizara imejipanga kuhakikisha ufugaji wa samaki unakuwa endelevu na wenye tija kwa wafugaji.

“kuanzishwa kwa vituo hivyo vya ukuzaji viumbe maji unakwenda sambamba na utoaji elimu sahihi ya ufugaji wa samaki pamoja na uzalishaji vifaranga vya Samaki", alifafanua

Aidha, aliwahimiza Watanzania kujitokeza kufuga samaki na viumbe maji wengine ili kujiongezea kipato chao na Taifa kwa ujumla.

Pamoja na hayo alitumia fursa hiyo kuwahimiza wananchi kupenda kula samaki na dagaa kwa wingi akisema kuwa madini mengi yanayopatikana ndani yake yanasaidia katika kupambana na magonjwa kwenye mwili wa binadamu.

Naye  Katibu Tawala Msaidizi, Uchumi na Uzalishaji Mali Mkoa wa Morogoro, Dkt. Rozalia Rwegasira  akisoma hotuba ya  Katibu Tawala wa Mkoa  huo, Mariam Mtunguja alisema kuwa wizara inatarajia kufikia lengo la mpango wa tatu wa maendeleo wa Taifa wa miaka mitano  kwa kuzalisha tani 50,000 za mazao ya ukuzaji wa viumbe maji kwa mwaka ifikapo mwaka 2025/2026.

Hivyo aliwataka Watanzania kuchangamkia fursa zilizopo katika uchumi wa bluu kutokana na kuwepo rasilimali maji ikiwemo bahari, maziwa, mito na maeneo oevu ambayo yanatoa wigo mpana wa kufanya shughuli za ufugaji wa samaki na viumbe wengine wa majini.

Dkt. Rwegasira aliongeza kuwa pamoja na Serikali kuwekeza nguvu kubwa katika sekta ya mifugo na uvuvi, bado kuna uzalishaji mdogo  wa mazao ya viumbe maji ukilinganisha na fursa zilizopo nchini.

“Tasnia ya ukuzaji viumbe maji inakabiliwa na upungufu wa maofisa ugani 15,323 ambapo kwa sasa kuna maofisa ugani 677 ikilinganishwa na mahitaji ya maofisa ugani 16, 000” alisema Dk Rwegasira.

Dk Rwegasira aliwataka maofisa ugani waliopo kupeleka teknolojia walioipata kwa watanzania ili waweze kufuga samaki na viumbe maji wengine kwa njia ya kisasa zaidi ili kukidhi mahitaji ya  soko la kimataifa  kwani kwa sasa kuna uhitaji mkubwa wa kitoweo cha samaki.

Kwa upande wao  washiriki wa mafuzo hayo Lucia Balilemwa pamoja na Emmanuel Ntobi  kwa nyakati tofauti waliishukuru serikali kwa kuwapatia mafunzo rejea hayo  na kwamba watayatumia kubadirisha maisha ya wananchi katika maeneo  walikotoka  juu ya  ufugaji bora wa samaki  na hivyo itapunguza changamoto ya uvuvi haramu.


Picha ya Pamoja ya Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Uchumi na Uzalishaji (Morogoro), Dkt. Rozalia Rwegasila (katikati waliokaa) Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji, Dkt. Nazael Madalla (kushoto), Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji Baridi, Dkt. Imani Kapinga (kulia) na Washiriki wa Mafunzo Rejea ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Kilimanjaro na Pwani mara baada ya kufunguliwa kwa mafunzo hayo,yanayoendelea katika kituo cha Kingolwira Mkoani Morogoro. (01.02.2022).* 






 

Ijumaa, 4 Februari 2022

SERIKALI YAENDELEA KUWAJALI WAVUVI WADOGO

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi Sekta ya Uvuvi imeendelea kuwajali wavuvi wadogo kwa kuanzisha mradi wa kupunguza umasikini na kuongeza usalama wa chakula na lishe unaozingatia usawa wa kijinsia. 

Hayo yamesemwa leo (03.02.2022) na Mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu, Bw. Amos Machilika wakati akifungua Warsha ambayo imewashirikisha wadau mbalimbali kutoka katika taasisi za serikali, mashirika binafsi, Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) na baadhi ya Halmashauri zenye shughuli za uvuvi. Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Hotel ya Edema Manispaa ya Morogoro.

 

Bw. Machilika amesema kuwa katika kutekeleza Mwongozo wa Hiari wa kuendeleza uvuvi mdogo, Wizara imeandaa Mpango Kazi wa Kitaifa wa kutekeleza mwongozo huo ambao ulipitishwa na wadau wote na sasa unakwenda kutekelezwa.

 

Lengo la kuwa na warsha hiyo ya wadau ni kuwakutanisha wadau na kuwafahamisha kuhusu utekelezaji wa mpango wa huo wa kitaifa, pia kutambulisha mradi utakaotekeleza mpango kazi wa kitaifa. Kupitia mradi huo serikali inatarajia jamii hasa za wavuvi kupunguza umaskini, kuboresha lishe na kuongeza kipato kupitia shughuli zinazofanyika kutokana na mnyororo wa thamani wa mazao yatokanayo na uvuvi mdogo. Vilevile katika Warsha hiyo washiriki watafahamishwa kuhusu maadhimisho ya mwaka ya kitaifa ya uvuvi mdogo na ukuzaji viumbe maji wa mwaka huu 2022. Mradi huo utatekelezwa kwa muda wa miaka miwili.

 

Naye mwakilishi wa FAO kwa upande wa sekta ya uvuvi, Dkt. Oliva Mkumbo amesema kuwa Tanzania ndio nchi ya kwanza kuandaa Mpango kazi wa kitaifa wa kutekeleza mwongozo wa hiari. Pia ameipongeza serikali kwa kuendelea kuwajali akina mama wanaojishughulisha na uvuvi mdogo ikiwa ni pamoja na Jukwaa la Wanawake (TAWFA)

 

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi, Didas Mtambalike amesema kuwa mradi huu utaanza kutekelezwa katika Halmashauri tano za Kilwa, Pangani, Mwanga, Kigoma na Ilemela. Vilevile amesema kuwa Wizara imefanikiwa kuanzisha jukwaa la wanawake wanaojishughulisha na uvuvi, kuandaa mpango kazi wa utekelezaji mwongozo wa hiari, kuandaa mradi huo kwa kushirikiana na FAO na kuanzisha dawati la jinsia wizarani linalosimamiwa na mvuvi.

 

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Usimamizi wa Mradi, Bi. Fatma Sobo ameishukuru serikali kwa kuendelea kuwajali wavuvi wadogo hasa kwa kuzingatia jinsia. Pia amepongeza uanzishwaji wa mradi huo kwa kuwa utasaidia sana katika kupunguza umasikini, kuwa na uhakika wa chakula na lishe bora, pamoja na kuwaongezea kipato wavuvi wadogo.


Mwakilishi wa Katibu Mkuu anayesimamia Sekta ya Uvuvi, Bw. Amos Machilika (aliyesimama) akifungua Warsha ya kutambulisha Mradi wa Kupunguza Umasikini na Kuongeza Usalama wa Chakula na Lishe kwa wavuvi wadogo unaozingatia usawa wa kijinsia ambapo amesema kuwa Wizara imeandaa Mpango Kazi wa Kitaifa wa kutekeleza Mwongozo wa Hiari. Kutoka kushoto ni Mwakilishi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Dkt. Oliva Mkumbo, Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi, Bw. Didas Mtambalike, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Usimamizi wa Mradi, Bi. Fatma Sobo na Mwakilishi wa Jukwaa la Wanawake (TAWFA). Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Edema Hotel Manispaa ya Morogoro. (03.02.2022)


Mwakilishi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Dkt. Oliva Mkumbo (kushoto) akizungumza na washiriki (hawapo pichani) wa Warsha ya kutambulisha Mradi wa Kupunguza Umasikini na Kuongeza Usalama wa Chakula na Lishe kwa wavuvi wadogo unaozingatia usawa wa kijinsia. Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Edema Hotel Manispaa ya Morogoro. (03.02.2022)


Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi, Bw. Didas Mtambalike (aliyesimama) akizungumza kabla ya kufunguliwa kwa Warsha ya kutambulisha Mradi wa Kupunguza Umasikini na Kuongeza Usalama wa Chakula na Lishe kwa wavuvi wadogo unaozingatia usawa wa kijinsia. Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Edema Hotel Manispaa ya Morogoro. (03.02.2022)


Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Usimamizi wa Mradi, Bi. Fatma Sobo (aliyesimama) akitoa maelezo mafupi kuhusu mradi wakati wa Warsha ya kutambulisha Mradi wa Kupunguza Umasikini na Kuongeza Usalama wa Chakula na Lishe kwa wavuvi wadogo unaozingatia usawa wa kijinsia. Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Edema Hotel Manispaa ya Morogoro. (03.02.2022)

Mwakilishi wa Jukwaa la Wanawake (TAWFA), Beatrice Mbaga (kulia) akitoa salam wakati wa Warsha ya kutambulisha Mradi wa Kupunguza Umasikini na Kuongeza Usalama wa Chakula na Lishe kwa wavuvi wadogo unaozingatia usawa wa kijinsia. Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Edema Hotel Manispaa ya Morogoro. (03.02.2022)


Afisa Uvuvi Mwandamizi, Bi. Upendo Hamidu akiwasilisha mada kwenye Warsha ya kutambulisha Mradi wa Kupunguza Umasikini na Kuongeza Usalama wa Chakula na Lishe kwa wavuvi wadogo unaozingatia usawa wa kijinsia. Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Edema Hotel Manispaa ya Morogoro. (03.02.2022)


Picha ya pamoja ya Mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi, Bw. Amos Machilika (katikati waliokaa) na Washiriki wa warsha ya kutambulisha Mradi wa Kupunguza Umasikini na Kuongeza Usalama wa Chakula na Lishe kwa wavuvi wadogo unaozingatia usawa wa kijinsia. Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Edema Hotel Manispaa ya Morogoro. (03.02.2022)


Mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi, Bw. Amos Machilika (kushoto) akikabidhi vitabu vya Mwongozo wa Hiari wa Kuhakikisha Uvuvi Mdogo Unakuwa Endelevu kwa baadhi ya washiriki wa Washiriki wa warsha ya kutambulisha Mradi wa Kupunguza Umasikini na Kuongeza Usalama wa Chakula na Lishe kwa wavuvi wadogo unaozingatia usawa wa kijinsia. Warsha hiyo imefanyika katika ukumbi wa Edema Hotel Manispaa ya Morogoro. (03.02.2022)


Jumanne, 1 Februari 2022

WAFUGAJI KIBAHA WAKABIDHIWA DUME LA KISASA

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe.  Abdallah Ulega amekabidhi Ng'ombe dume wa kisasa kwa wafugaji wa kijiji cha Miziguni kata ya Magindu, halmashauri ya Kibaha Vijijini, Mkoani Pwani kwa ajili ya kuboresha koosafu za mifugo yao.

Akizungumza wakati wa kukabidhi dume hilo Januari 30, 2022 Naibu Waziri Ulega alisema kuwa Ng'ombe huyo ametolewa na mdau wa mifugo kutoka shamba la Canbe ikiwa ni katika jitihada za kuunga mkono Serikali ya awamu ya sita katika ufugaji wa kisasa na kuboresha Mifugo.

Aliwataka wafugaji hao kuweka utaratibu mzuri kwa watu wote ambao wanahitaji mbegu ya dume hilo pamoja na kulitunza vizuri ili liweze kuhudumia majike mengi na kwa muda mrefu zaidi.

"Nawaombeni sana dume hili litumike kwa ajili ya kuboreshea mifugo yetu, wekeni utaratibu mzuri wafugaji wote wanaotaka kupandisha majike yao wasikose fursa hiyo hapa, pia mlifanyie uchunguzi wa mara kwa mara lisije likapata ugonjwa wa kutupa mimba kwasababu atakuwa anahudumia mitamba mingi kwa hiyo ni rahisi sana kuhamisha ugonjwa" alisema Ulega

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ulega amewataka wanawake jamii ya wafugaji wanaojishughulisha na uuzaji wa maziwa kuanzisha chama vya ushirika kitakacho wasaidia kuuza maziwa  bila changamoto yeyote.

Alisema pamoja na mambo mengine ushirika huo pia utawasaidia akina mama kupata mikopo kutoka katika benki ya kilimo (TADB).

Aliongeza kuwa mpango wa Serikali ni pamoja na kuleta miradi ya maji maeneo ya ukame Ili kuondokana na adha iliyotokea hapo nyuma ya kupoteza Mifugo mingi, na hivyo kuchimba mabwawa na malambo yatakayoenda kuwasaidia wafugaji.

"Tayari wadau wetu kutoka Heifer international wameahidi kutoa mabirika 10 ya kuwekea   maziwa na jokofu moja kwa ajili ya kusaidia akina mama wa Magindu wanaouza maziwa kuweza kuboresha bidhaa zao na kuuza kwa bei nzuri"

Kwa upande wake Mbunge wa Kibaha vijijini Mhe. Michael Mwakamo amemshukuru Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwa hatua nzuri wanazozichukua katika kukabiliana na changamoto ya malisho.

Alisema wamepokea maelekezo ya Wizara pamoja na elimu waliyoipata ikiwemo ya kilimo cha Malisho na uanzishwaji wa chama cha ushirika cha akina mama wauza maziwa ambapo wataanza kufanyia kazi mara moja ili kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akabidhi ng'ombe dume aina ya borani kwa wafugaji wa kijiji cha Miziguni kata ya Magindu na kuwataka wafugaji hao walitunze dume hilo na kuhakikisha halipati ugomjwa wa kutupa mimba ili liweze kuwasaidia zaidi katika kuboresha Mifugo yao na kupata mbegu Bora zaidi. Januari 30, 2022 Mkoani Pwani.