Nav bar

Ijumaa, 25 Novemba 2022

UGAWAJI WA MADUME BORA YA NG’OMBE NI UTEKELEZAJI WA MPANGO WA MABADILIKO WA SEKTA YA MIFUGO - NDAKI

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amesema ugawaji wa madume ya bora ya ng’ombe ni utekelezaji wa mpango wa mabadiliko wa Sekta ya Mifugo.

 

Waziri Ndaki ameyasema hayo leo (24.11.2022) wilayani Chamwino Mkoani Dodoma wakati alipokuwa anagawa madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran ambapo kila mmoja ana uwezo wa kupanda majike 25 kwa mwaka, kwa vikundi vya wafugaji kwa lengo la kwenda kuboresha mifugo yao ambayo mingi ni ya asili.

 

“Mifugo mingi iliyopo hapa nchini ni ya asili na uzalishaji wake wa nyama na maziwa kwa mfugo ni ndogo, hivyo kwa kuanza kuboresha mifugo kwa kutumia madume haya pamoja na njia ya uhimilishaji kutasaidia wafugaji kuwa na mifugo michache ambayo itakuwa na uzalishaji mkubwa wa nyama na maziwa,” Alisema

 

Ng’ombe wa asili huzalisha nyama kilo 80 -120 kwa ng’ombe wakati baada ya kuboreshwa kwa kosaafu mfugaji anaweza kupata kilo 150 – 200 kwa ng’ombe. Lakini pia kwenye upande wa maziwa ng’ombe hawa walioboreshwa kosaafu huwa na uwezo wa kutoa kati ya lita 5 – 10 za maziwa na hivyo kumfanya mfugaji apate tija zaidi tofauti na mfugaji wa ng’ombe wa asili.

 

Wafugaji wametakiwa kuyatunza madume hayo kwa kufuata taratibu zote wanazoelekezwa na wataalam wa mifugo.  Lakini pia Waziri Ndaki amevitaka vikundi ambavyo vimepatiwa madume hayo kuyatumia kwa kushirikiana na wafugaji wengine ili kuhakikisha tija inapatikana kwa wafugaji ndani ya Wilaya ya Chamwino.

 

Kaimu Katibu Mkuu Sekta ya Mifugo, Dkt. Asimwe Rwiguza amesema Wizara inaendelea kutekeleza mpango wa mabadiliko wa sekta hiyo ambapo licha ya kazi ya uboreshaji wa kosaafu inayoendelea, wafugaji wanaendelea kupatiwa elimu kuhusu malisho ya mifugo.

 

Wizara inaendelea kuanzisha mashamba darasa ya malisho ya mifugo kwa lengo la kutoa elimu ya kilimo cha malisho na namna ya kuyatunza malisho hayo pamoja na nyanda za malisho ili malisho hayo yaweze kuwasaidia wakati wa kiangazi kikali.

 

Naye Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Gift Msuya amesema kuwa uongozi wa Wilaya utakwenda kusimamia utekelezaji wa mpango wa mabadiliko wa sekta ya mifugo kwa kuhakikisha madume hayo yaliyogawiwa kwenye vikundi yanatunzwa na kutumika ili kuboresha kosaafu.

 

Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Maendeleo ya Masoko kutoka Sekta ya Mifugo, Bw. Stephen Michael amesema kuwa takribani asilimia 97 ya ng’ombe waliopo nchini ni wa asili hivyo katika kutekeleza mpango wa mabadiliko wa sekta, Wizara imepanga kununua mitamba 1,160,000 ambayo itapelekwa kwenye mashamba ya serikali. Hivyo kutokana na uzalishaji wake wafugaji wataweza kupata ng’ombe bora hapa nchini badala ya kutegemea kuagiza kutoka nje.

 

Aidha, Wizara inaendelea na zoezi la uhimilishaji mifugo ambapo tayari imeshapanga kuhimilisha takribani ng’ombe 373,000 katika mwaka wa fedha 2022/2023 kwenye maeneo ambayo hawatapata madume hayo.

 

Mwakilishi wa taasisi ya PASS Trust, Langelika Kalebi amesema kuwa taasisi hiyo ni mwezeshaji ikichochea maendeleo kwenye kilimo (mifugo, uvuvi, mazao, na mazao ya porini). Taasisi hiyo ipo nchi nzima ikichochea maendeleo kwenye upatikanaji wa mitaji na elimu, hivyo wanaongezea dhamana katika kurahisisha upatikanaji wa mitaji kwa mtu mmoja, vikundi, vyama vya ushirika.

 

Naye mwenyekiti wa wafugaji Wilaya ya Chamwino, Bw. John Kochocho ameishukuru serikali kupitia Sekta ya Mifugo kwa kuwapelekea wafugaji madume hayo ya ng’ombe yatakayokwenda kuboresha kosaafu na hivyo kuwafanya wazalishe kwa tija na kibiashara.

 

Serikali ya awamu ya sita ya Mhe Rais Samia Suluhu Hassan kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefanikiwa kununua jumla ya madume bora ya ng’ombe wa nyama 366 aina ya Boran kama sehemu ya jitihada za kuendelea kuboresha tija ya ng’ombe tulionao nchini.


Baadhi ya Wafugaji na Viongozi wakisikiliza hotuba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki wakati wa hafla ya kugawa Madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran kwa Vikundi vya wafugaji katika wilayani Chamwino Mkoani Dodoma. (24.11.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na wafugaji pamoja na viongozi wakati wa hafla ya kugawa madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran kwa Vikundi vya wafugaji katika wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma ambapo aliwataka wafugaji hao kuhakikisha wanayatunza madume hayo ili lengo la serikali la kuboresha kosaafu liweze kutimia na wafugaji waweze kuwa na mifugo michache yenye tija. (24.11.2022)


Kaimu Katibu Mkuu Sekta ya Mifugo, Dkt. Asimwe Rwiguza akiuelezea mpango wa mabadiliko wa Sekta ya Mifugo wakati wa hafla ya kugawa Madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran kwa Vikundi vya wafugaji katika wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma, ambapo amesema Wizara imepanga kuanzisha mashamba darasa ya kilimo cha malisho kwa lengo la kuwaelimisha wafugaji juu ya kilimo hicho, utunzaji wa malisho na nyanda za malisho ili waweze kukabiliana na tatizo la malisho wakati wa kiangazi kikali. (24.11.2022)


Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Maendeleo ya Masoko (WMUV), Bw. Stephen Michael akiwaeleza wafugaji kuhusu mpango wa Wizara wa kuhimilisha ng’ombe 373,000 katika mwaka wa fedha 2022/2023, hivyo kwa wafugaji ambao hawatafikiwa na madume bora watapatiwa huduma ya uhimilishaji. Amewaeleza hayo wakati wa hafla ya kugawa Madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran kwa Vikundi vya wafugaji katika wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma. (24.11.2022)


Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Gift Msuya akitoa salam za wilaya ameishukuru Wizara kwa kuamua kupeleka madume bora 50 ya ng’ombe katika wilaya hiyo na kwamba uongozi wa wilaya utakuwa ukifanya ufuatiliaji wa karibu ili kuhakikisha tija ya uwepo wa madume hayo inaonekana kama ilivyokusudiwa na serikali. Mhe. Msuya ameyasema hayo wakati wa hafla ya kugawa Madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran kwa Vikundi vya wafugaji katika wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma. (24.11.2022)


Meneja wa Taasisi ya PASS Trust kutoka Mwanza, Bi. Langelika Kalebi akizungumza na wafugaji wakati wa hafla ya kugawa Madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran kwa Vikundi vya wafugaji katika wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma. (24.11.2022)


Mwenyekiti wa Wafugaji Wilaya ya Chamwino, Bw. John Kochocho akitoa neno la shukrani kwa Sekta ya Mifugo mara baada ya kukabidhi Madume ya Ng’ombe wakati wa hafla ya kugawa Madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran kwa Vikundi vya wafugaji katika wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma. (24.11.2022)


Baadhi ya Wafugaji na Viongozi wakisikiliza hotuba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki wakati wa hafla ya kugawa Madume bora 50 ya ng’ombe aina ya boran kwa Vikundi vya wafugaji katika wilayani Chamwino Mkoani Dodoma. (24.11.2022)

 


Mtaalam Mwandamizi wa Uvuvi na Ukuzaji Viumbe Maji kutoka Mfuko wa kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) Bw. Richard Abila (kulia) akimpa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (katikati) tathmini fupi ya yale waliyoyaona kwenye utekelezaji wa awali wa Mradi wa Maendeleo ya Kilimo na Uvuvi (AFDP) hapa nchini tukio lililofanyika mapema leo (24.11.2022) kwenye Ofisi za Wizara hiyo zilizopo eneo la Mtumba jijini Dodoma. Kushoto ni Mwakilishi wa Katibu Mkuu anayeshughulikia Sekta ya Uvuvi Bw.Stephen Lukanga.

TVLA YATOA CHANJO KWA BAADHI YA WAFUGAJI WA KUKU WILAYANI BAHI

 


Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Kanda ya Kati Dkt. Japhet Nkagaga wa (kwanza kulia) mwenye boksi la plastiki la kuhifadhia chanjo  za mifugo, akitoa chanjo kwa ajili ya kuchanja Mifugo na pia ametoa elimu kwa moja ya Kikundi  cha wafugaji wa kuku katika Kijiji cha Ilindi Wilayani Bahia,ambapo amewataka wafugaji hao kuona   umuhimu wa kuchanja kuku kutumia chanjo ya I-2 dhidi ya ugonjwa Kideri ili kuwanusuru na vifo vya kuku wao  katika Kikundi chao,ambapo ugonjwa huo ukiingia katika kaya ya mmoja wenu unauawa kuku takriban wote katika kaya.Lengo la kutoa elimu hii ni utaratibu wa Wakala ya  Maabara ya veterinari kanda ya Kati waliojiwekea wa kutoa huduma ya afya ya Mifugo kwa wafugaji  kanda hiyo katika kuadhimisha Wiki ya Wakala ya Maabara ya Veterinari kanda ya Kati  Dodoma.(23.11.2022).


Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Kanda ya Kati Dodoma Dkt.Japhet Nkagaga akichanja Ng'ombe katika Kijiji cha Ilindi Kata ya Ilindi Wilayani Bahi Mkoa wa Dodoma zaidi ya ng'ombe 350 wamechanjwa katika zoezi hilo katika Kata ya Ilindi dhidi ya ugonjwa wa Homa ya Mapafu ya Ng'ombe (CBPP) ambao unaua Mifugo  katika wilaya ya Bahi na hata Dodoma kwa ujumla wake.  (23.11.2022)


Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Kanda ya Kati Dodoma Dkt.Jophet Nkagaga  mwenye Overoll la blue ( kushoto ) akitoa elimu katika Kijiji cha Ilindi Wilayani Bahi Mkoani Dodoma kuhusu umuhimu wa kudhibiti magonjwa Mifugo kwa kuchanja dhidi ya magonjwa hatari kwa kuuwa Mifugo hususan Ng'ombe,Mbuzi ,Mbwa na paka alitaja baadhi ya magonjwa hayo kuwa ni Homa ya mapafu ya ng'ombe (CBPP), Homa ya Mapafu Mbuzi ( CCPP), Miguu na Midomo,(FMD),Kutupa Mimba,Kichaa cha Mbwa ni lazima kuchanja dhidi ya magonjwa haya ili kuepuka hasara atayopata mfugaji endapo ng'ombe ataugua na kufa. Lengo la elimu hii ni utaratibu wa kanda  kuhakikisha wafugaji wanapata huduma mbalimbali za za afya ya mifugo katika kipindi cha maadhimisho ya Wiki ya wakala ya Maabara ya Veterinari Kanda ya Kati Dodoma  kuanzia tarehe 21 hadi 25.11.2022 huduma hizo ni Kuchanja,Kutibu, kuogesha,kuandaa vyakula vya Mifugo.(23.11.2022)


Mfugaji wa Kuku wa kienye katika Kijiji cha Ilindi, mwenye flana  ya njano ambaye pia ni mwna kikundi cha umoja cha wafugaji wa kuku hao bw.John Lusinde anachanja kuku baada ya kupata elimu ya kuchanja kuku dhidi ya ugonjwa wa Kideri, hivyo atakuwa mwalimu wa wafugaji wengine kijijini na atakuwa akiwachanjia kuku katika kikudi hicho ambapo. Matumizi ya Chanjo ya I - 2 ni kuweka matone 2 ya chanjo ya l - 2 katika jicho la kuku chanjo hiyo itarudiwa baada ya miezi mitatu.(23.11.2022)

UZINDUZI WA MRADI WA "MAZIWA FAIDA TANZANIA"

 


MBEGU ZA MALISHO ZIPATIKANE KWENYE MADUKA YA PEMBEJEO-ULEGA.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega ameitaka Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kuhakikisha mbegu za malisho bora ya Mifugo zinapatikana kwenye maduka ya pembejeo za Kilimo na Mifugo ili kuwawezesha wafugaji kuzalisha malisho kwa urahisi zaidi.


Mhe. Ulega ameyasema hayo kwenye hafla ya uzinduzi wa Mradi wa Faida Maziwa Tanzania uliofanyika jana (22.11.2022) kwenye Viwanja vya Ofisi za Taasisi hiyo kanda ya Mashariki zilizopo jijini Tanga.


"Moja ya jambo ambalo litatupa heshima kubwa sana ni kuhakikisha mbegu za malisho zinauzwa kama zilivyo mbegu za mazao mengine kama mahindi, mpunga na mengineyo kwa sababh tunatumia nguvu kubwa sana kuwahamisha wafugaji kuzalisha malisho bora kwa ajili ya Mifugo yao lakini mbegu za malisho hayo hazipatikani kwa urahisi hivyo ni muhimu sasa zikaanza kupatikana kwenye maduka yote ya pembejeo na hilo ninaagiza lifanyike haraka sana" Amesisitiza Mhe. Ulega.


Mhe. Ulega amebainisha kuwa hatua hiyo ikifikiwa, Nchi itakuwa imepiga hatua kwa vitendo kuelekea kwenye ufugaji wa kisasa na kutoa fursa kwa wazalishaji wa malisho hayo kujikita kikamilifu kwenye biashara ya malisho ambayo imeendelea kukua kwa kasi hivi karibuni.


" Kila mfugaji mwenye nia ya dhati ya kufanya shughuli hiyo ameshakubali kubadilika ili apate tija kwenye ufugaji wake na mojawapo ya mambo anayopaswa kufanya ni kuzalisha malisho yanayokidhi mifugo yake na kinyume na hapo ni aidha atapata hasara kwenye ufugaji wake au ataharibu mazingira" Amesisitiza Mhe.Ulega.


Akizungumzia kuhusiana na Mradi wa Faida Maziwa Tanzania Mhe. Ulega amebainisha kuwa mradi huo kwa kuanzia utalenga zaidi kujenga uwezo kwa wafugaji wa ng'ombe wa maziwa wanawake na vijana wasiopungua elfu 3 kwa kanda ya Mashariki na kufanya tafiti zenye matokeo chanja kwenye vikwazo vilivyopo katika mnyororo wa biashara ya maziwa kuanzia shambani, kiwandani hadi kufika kwa mlaji.


"Lakini pia mradi huu utatafiti juu ya malisho bora yanayoweza kuongeza uzalishaji wa maziwa ndani ya kaya, ng'ombe bora wa maziwa anayefaa kwa kanda ya mashariki kwa kuzingatia hali ya hewa na mabadiliko ya tabia nchi, kuimarisha huduma za ugani na ushirika kwenye Mkoa wa Tanga na kuimarisha miundombinu ya utafiti hasa maabara na mashamba darasa ya ufugaji ng'ombe bora wa maziwa na uzalishaji malisho ya Mifugo" Ameongeza Mhe. Ulega.


Kwa upande wake Balozi wa Ireland nchini Tanzania Bi. Mary O' Neill amesema kuwa mradi huo ni muendelezo wa mahusiano mazuri kati ya nchi yake na Tanzania ambapo amebainisha kuwa wanataka kuhakikisha mradi huo unatengeneza dira na somo endelevu kwa wafugaji wa ng'ombe wa maziwa ili iwasaidie hata mara baada ya mradi huo kukamilika.


"Uzinduzi wa mradi huu ni ishara ya mabadiliko kwenye sekta ya Ufugaji wa ng'ombe wa Maziwa nchini Tanzania na ni matumaini yetu kwa kutekeleza mkakati wa mabadiliko wa sekta ya Mifugo, Wizara itaendelea kuhamasisha ushiriki wa kila mdau aliyepp kwenye mnyororo wa thamani wa ufugaji wa ng'ombe wa maziwa bila kusahau makundi maalum hasa wanawake" Amesema Bi. O'Neill.


Bi. Oneil alitumia sehemu ya uzinduzi wa mradi huo kumkabidhi Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega jumla ya pikipiki 8 zitakazotumiwa na Maafisa ugani wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza kutekeleza shuguli zao na gari moja litakalotumiwa na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kwenye utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kitafiti.


Akizungumzia kusudio la kutekeleza mradi huo katika maeneo mengie nchini, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) Prof. Erick Komba amesema kuwa mbali na kufanya utafiti huo katika kanda ya Mashariki, matokeo yake yatasambazwa nchi nzima ili kuongeza tija kwenye kila hatua iliyopo kwenye mnyororo wa thamani wa maziwa nchini.


“Tunatekeleza mradi huu na nchi ya Ireland kwa sababu wao wanafanya vizuri sana kwenye upande wa uzalishaji na biashara ya Maziwa kwa ujumla hivyo naamini tutapeana uzoefu wa kutosha wa kitafiti kuhusu malisho ya mifugo, mbari na namna bora ya kutunza ng’ombe wa maziwa ili wazalishe maziwa kwa wingi” Amemalizia Prof. Komba


Mradi wa Maziwa Faida Tanzania unalenga kuongeza kiwango cha maziwa kwa kuboresha malisho ya ng'ombe wa maziwa na unatekelezwa kwa kipindi cha Miaka 5 ambapo kila mwaka unatarajia kutumia zaidi ya shilingi bilioni 6.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega na Balozi wa Ireland nchini Tanzania Bi. Mary O’Neill (katikati) wakikata utepe kuashiria uzinduzi wa pikipiki 8 na gari moja vyote vikikabidhiwa na Bi. O’Neill kwa niaba ya Serikali ya Ireland jana (22.11.2022) ili vitumike  wakati wa utekelezaji wa mradi wa Faida Maziwa Tanzania unaotarajiwa kutekelezwa kwa miaka 5 hapa nchini. Kushoto ni Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Dkt. Charles Mhina na kulia ni Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga Bw. Albogasti Kimasa.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (kulia) akimfafanulia Balozi wa Ireland nchini Tanzania Bi. Mary O’Neill (kushoto) namna mbegu za malisho ya mifugo zinavyopandwa katika mashamba mbalimbali hapa nchini muda mfupi kabla ya uzinduzi wa mradi wa Faida Maziwa Tanzania uliofanyika jana (22.11.2022) kwenye Viwanja vya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kanda ya Mashariki jijini Tanga.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (kulia) akitoa maelekezo kwa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kuhakikisha mbegu za malisho zinapatikana  kwenye maduka yote ya  pembejeo nchini muda mfupi baada ya kufika kwenye Viwanja vya Taasisi hiyo kanda ya Mashariki jijini Tanga jana (22.11.2023)  ambapo pia alizindua mradi wa Faida Maziwa Tanzania. Kushoto ni Balozi wa Ireland nchini Tanzania Bi. Mary O’Neill na katikati ni Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI Pro. Erick Komba.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Kulia)  na Balozi wa Ireland nchini Tanzania Bi. Mary O’Neill (kushoto) wakiwasha pikipiki muda mfupi baada ya pande hizo kukabidhiana vitendea kazi hivyo vitakavyotumiwa na Maafisa Ugani wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza kwenye utekelezaji wa mradi wa Faida Maziwa Tanzania uliozinduliwa rasmi jana (22.11.2022) kwenye hafla iliyofanyika viwanja vya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) Kanda ya Mashariki jijini Tanga.

Balozi wa Ireland nchini Tanzania Bi. Mary O’Neill (kushoto) akisalimia na Msajili wa Bodi ya Maziwa nchini (TDB) Dkt. George Msalya muda mfupi jana (22.11.2022) baada ya kuwasili kwenye viwanja vya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) Kanda ya Mashariki jijini Tanga ambako alishiriki uzinduzi wa mradi wa Faida Maziwa Tanzania unaotekelezwa baina ya nchi ya Ireland na Tanzania. Katikati ni Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Dkt. Charles Mhina.

Balozi wa Ireland nchini Tanzania Bi. Mary O’Neill (kushoto) akisalimia na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) Prof. Erick Komba muda mfupi jana (22.11.2022) baada ya kuwasili kwenye viwanja vya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) Kanda ya Mashariki jijini Tanga ambako alishiriki uzinduzi wa mradi wa Faida Maziwa Tanzania unaotekelezwa baina ya nchi ya Ireland na Tanzania. Katikati anayeshuhudia ni Mratibu wa Mradi huo kutoka TALIRI  Dkt. Zabron Nziku.

MAADHIMISHO YA WIKI YA TVLA

 


 


Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah (wa pili kutoka kulia, mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe kutoka Wizara mbalimbali za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kwenye mkutano wa siku mbili wa Makatibu Wakuu (Committee of Senior Officials) wa Jumuiya ya IORA  unaofanyika Jijini Dhaka, Bangladesh kuanzia Novemba 22-23, 2022. Dkt. Tamatamah ameongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo ambao unatarajiwa  kuhitimishwa na kikao cha Baraza la Mawaziri kitakachofanyika Novemba 24, 2022. Ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Baraza la Mawaziri utaongozwa na Mhe. Suleiman Masoud Makame, Waziri wa Uchumi wa Buluu na  Uvuvi wa SMZ.


Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah akitoa ufafanuzi kuhusu baadhi ya hoja zilizojitokeza kuhusu Tanzania kwenye mkutano wa siku mbili wa Makatibu Wakuu (Committee of Senior Officials) wa Jumuiya ya IORA  unaofanyika Jijini Dhaka, Bangladesh kuanzia Novemba 22-23, 2022. Dkt. Tamatamah anaongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo ambao unatarajiwa  kuhitimishwa na kikao cha Baraza la Mawaziri kitakachofanyika Novemba 24, 2022. Ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Baraza la Mawaziri utaongozwa na Mhe. Suleiman Masoud Makame, Waziri wa Uchumi wa Buluu na  Uvuvi wa SMZ.

KONGAMANO LA PILI LA KITAIFA LA WADAU LA KUJADILI NAMNA YA PAMOJA YA KUZUIA USUGU WA VIMELEA VYA MAGONJWA DHIDI YA DAWA

 


Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo, Prof. Hezron Nonga akitoa neno la utangulizi wakati wa Kongamano la pili la Kitaifa la wadau la  kujadili  namna ya pamoja ya kuzuia usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa linalofanyika kwa siku mbili jijini Dar es Salaam kuanzia Novemba 22-23, 2022. Kongamano hilo ni miongoni mwa matukio ya Wiki ya kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu usugu wa vimelea dhidi ya dawa  iliyoanza Novemba 18-23, 2022. Kongamano hilo limeandaliwa na Wizara ya Afya, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Vyuo Vikuu, Taasisi za Utafiti na Wadau wa Maendeleo.


Sehemu ya Wadau wa  Kongamano la Kitaifa la  kujadili namna ya pamoja ya kuzuia usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa wakifuatilia matukio mbalimbali yanayoendelea  katika kongamano hilo linalofanyika kwa siku mbili jijini Dar es Salaam kuanzia Novemba 22-23, 2022.


Pichani ni muonekano wa sehemu ya ukumbi wa mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania ambapo Kongamano la pili la Kitaifa la wadau la kujadili  namna ya pamoja ya kuzuia usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa linapofanyika kwa siku mbili jijini Dar es Salaam kuanzia Novemba 22-23, 2022.

SERIKALI YAPONGEZA SEKTA BINAFSI KWA KUKUZA SEKTA YA UVUVI

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imelipongeza Shirika la Kimataifa la Uhifadhi wa Mazingira na Wanyamapori (WWF) kwa kuviwezesha vikundi saba vya ujasiriamali vya uvuvi kwa jumla ya Shilingi Milioni Thelathini na Tano, pikipiki nne, boti tatu na injini zake, pamoja na makoti 30 ya kujiokoa (life jackets) kwa halmashauri mbili za Wilaya za Kilwa Mkoani Lindi na Kibiti Mkoani Pwani.


Shukrani hizo zimetolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah katika hotuba yake iliyosomwa na Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Uvuvi na Ukuzaji Viumbe Maji, Bw. Anthony Dadu wakati wa maadhimisho ya siku ya mvuvi duniani yanayokwenda sambamba na Mwaka wa Kimataifa wa Wavuvi Wadogo na Wakuzaji Viumbe Maji 2022 (International Year of Artisanal Fisheries and Aquaculture (IYAFA) yaliyofanyika katika kijiji cha Somanga Wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi.


Amesema hatua hiyo itaongeza chachu ya usimamizi bora wa rasilimali za uvuvi utakaopelekea upatikanaji kwa wingi wa mazao ya uvuvi yenye ubora na hivyo kuwezesha jamii kupata lishe bora na kuongeza kipato ikizingatiwa mafanikio katika usimamizi wa rasilimali za uvuvi yanategemea sana vitendea kazi imara.


"Nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mkurugenzi Mkazi wa WWF Dkt. Amani Ngusaru kwa kuendelea kuwajali na kuwawezesha wananchi wetu katika kuimarisha shughuli zao za kiuchumi na hivyo kuleta tija katika maisha yao" alisema Bw. Dadu katika taarifa hiyo.


Aidha amewataka viongozi wa vijiji ambao watanufaika na zana hizo ikiwemo Nyamatungutungu, Marendego, Njia nne, Somanga Kusini, Somanga Kaskazini, Songosongo, Pombwe, Jaja, Kiomboni, Msala, Dongo, Kilindoni, Chunguruma, na Ndagoni kutimiza wajibu wao mkubwa wa kushirikiana kuvitunza vitendea kazi hivyo ili vinufaishe taifa na familia zao.


Hali kadhalika aliwataka wakurugenzi wa halmashauri zote kuhakikisha wanapata taarifa za mara kwa mara juu ya matumizi sahihi na yaliyokusudiwa kupitia vifaa hivvyo. 


"Nitoe wito kwa halmashauri husika kuona umuhimu wa kuweka utaratibu mzuri utakaowezesha Vikundi vya Kusimamia Rasilimali ya Uvuvi Mwaloni (BMU) katika halmashauri zenu zinanufaika na vifaa hivi pale wanapohitaji kuvitumia katika maeneo yao." Alisema Bw. Dadu


Aidha amewakumbusha kuwa kila mmoja ana wajibu wa kuhakikisha Sheria ya Uvuvi na Kanuni zake zinazingatiwa hali itakayosababisha waendelee kunufaika na fursa nyingi zilizopo katika sekta ya uvuvi. 


Akiwasilisha mada kuhusu dhima ya siku ya mvuvi duniani Mratibu wa Programu ya Bahari na Pwani WWF Dkt. Modesta Medard amesema kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Shirika la Kilimo na Chakula Duniani la Umoja wa Mataifa (FAO) inaonesha zaidi ya theluthi mbili ya samaki wote duniani wamevuliwa kupita kiasi au wamevuliwa wote na zaidi ya theluthi moja wako katika hali ya kupungua.


Amesema sababu ya kupungua huko ni kutokana na kutoweka kwa makazi ya samaki, uchafuzi wa mazingira na ongezeko la joto duniani ambapo siku ya mvuvi duniani inasaidia kutambulisha umuhimu wa sekta ya uvuvi kwa maisha ya binadamu, viumbe maji kwenye mito, maziwa na bahari.


"Samaki wanamchango mkubwa katika uhakika wa chakula duniani ni muhimu kwa lishe bora ya watu wote ulimwenguni hususan kwa jamii zilizopo karibu na mito maziwa na bahari" alisema.

Mkurugenzi Msaidizi Huduma za ugani wa uvuvi na ukuzaji viumbe maji kutoka waizara ya mifugo na uvuvi, Bw. Anthony Dadu akiongea na Wavuvi wa Kijiji cha somanga wilaya ya kilwa wakati wa maadhimisho ya siku ya mvuvi duniani yaliyofanyika kijijini hapo mkoani Lindi, Novemba 21, 2022

Mkurugenzi Mkaazi wa Shirika la Kimataifa la Uhifadhi wa Mazingira na wanyama pori (WWF), Dkt. Amani Ngusaro akieleza vitu walivyoleta kwa ajili ya wavuvi ikiwa ni pamoja na pikipiki nne, boti aina ya faiba tatu na mikopo wakati wa maadhimisho ya siku ya mvuvi duniani yaliyofanyika kwenye kijiji cha somanga mkoani Lindi, Novemba 21, 2022.

Mkurugenzi Msaidizi Huduma za ugani wa Uvuvi na Ukuzaji viumbe maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Anthony Dadu akikata utepe ishara ya kukabidhi pikipiki kwa wavuvi zilizotolewa na Shirika la kimataifa la uhifadhi wa mazingira na  wanyamapori (WWF)Mkoani Lindi, Novemba 21, 2022.

Moja ya boti zilizotolewa na Shirika la kimataifa la uhifadhi wa mazingira na wanyamapori (WWF) Ili kuwasaidia wavuvi kufanya uvuvi endelevu na wenye tija kwenye kijiji cha Somanga, Wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi, Novemba 21,2022.

Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Ugani wa uvuvi na Ukuzaji viumbe maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Anthony Dadu (kushoto) akifanya usafi kwenye fukwe za bahari na baadhi ya wavuvi ikiwa ni siku ya maadhimisho ya mvuvi duniani yaliyofanyika kwenye kijiji cha Somanga, kilwa Mkoani Lindi, Novemba 21,2022.

Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Ugani wa uvuvi na Ukuzaji viumbe maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Anthony Dadu (wa tano kutoka kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na vikundi vya vijana wanaojishughulisha na Uvuvi mara baada ya kufanya usafi kwenye fukwe ya bahari kwenye kijiji cha Somanga Wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi, wa tatu  kulia ni Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara hiyo Bi. Upendo Hamidu. Novemba 21,2022

SERIKALI YAFANYA MAGEUZI KWENYE SEKTA YA MIFUGO

Na. Martha Mbena.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amesema Serikali kupitia Wizara ya Mifugo imekuja na mageuzi kwa kufuga mifugo bora yenye tija kupitia Ng'ombe aina ya Borani ili kupata kilo nyingi, nyama nyingi na kuzalisha maziwa mengi jambo ambalo litachangia pato la Taifa.


Waziri Ndaki ameyasema hayo (21.11.2022) wakati akikabidhi madume 50 ya Ng'ombe aina ya Borani kwa makundi ya wafugaji wa Wilaya ya Maswa  kwenye hafla fupi iliyofanyika kwenye kata ya Buchambi Mkoani Simiyu.


"Kiasi cha sh 915 milioni kilichotolewa na Serikali kimetumika kununua madume 336 ya Ng'ombe aina ya Borani  ambayo yatakabidhiwa kwenye Wilaya 10 nchi nzima, Kwa hapa Wilaya ya Maswa tumekabidhi haya madume 50, Ombi langu muwatunze kwa kuwaosha mara kwa mara ili wasipate kupe wakapata ugonjwa wa Ndigana," Alisema Waziri Mashimba.


Mhe. Mashimba  aliongeza kuwa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa Ng'ombe hao bure kwa vikundi vyote vya wafugaji na kila kikundi kitapata dume ambalo litapanda majike yasiyopungua 25 kwa mwaka, Lengo ni kuzalisha Ng'ombe wa kisasa na bora zaidi kwa ufugaji.


Alisema kuwa mpango wa Serikali ni kuhamasisha ufugaji wa kisasa wa mifugo michache na kipato kingi na kuongeza kuwa aina hiyo ya Ng'ombe ni tofauti na Ng'ombe wa kawaida na kufafanua kuwa Ng'ombe wa kienyeji wanne ni sawa na Ng'ombe mmoja wa aina ya Borani.


"Niwaambieni tu kuwa kwa madume haya Ng'ombe atakayezaliwa ana uwezo wa kutoa lita 5 mpaka 10 kwa siku lakini wa kienyeji akijitaidi sana anaweza kutoa lita 1 mpaka 5 kwa siku kwa hiyo Ng'ombe wa kienyeji anaingizia serikali pato dogo," Alisema Ndaki.


Naye Mkuu wa Wilaya ya Maswa Aswege Kaminyonge amesema changomoto kubwa ni ukosefu wa pikipiki zitakazotumika katika mizunguko  kwenye vijiji mbalimbali ili kufuatilia mradi huo usije ukakwama.


Vilevile mkuu huyo wa Wilaya aliwataka maafisa watendaji wa kata kufuatilia kwa ukaribu zaidi wafugaji wote waliokabidhiwa madume hayo ili yasidhulike kwa kukosa matunzo.


kwa upande wake Mmiliki wa Shamba la Mifugo Mkoani Kagera, Bw. Josam Ntangeki amesema madume hayo kati ya mwaka mmoja hadi miwili yamepatiwa huduma zote za chanjo na kuwaomba wafugaji kujitaidi kuwapatia Ng'ombe hao huduma zote ikiwapo kuwapatia na chanjo.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) (aliyesimama) akiongea na Wafugaji wa kata ya Buchambi, Wilaya ya Maswa, Mkoa wa Simiyu kwenye hafla ya kukabidhi madume ya Ng'ombe 50 aina ya Borani kwa makundi ya wafugaji wa Wilaya hiyo, 21 Novemba 2022.


Mwakilishi wa kikundi cha Wafugaji kutoka kata ya Buchambi akichagua Dume la Ng'ombe mmoja kwa ajili ya kikundi chake ili waweze kwenda kufuga na kuzalisha zaidi Ng'ombe wa kisasa aina ya Borani, tukio hilo limefanyika 21, Novemba 2022.


Wafugaji wa kata ya Buchambi, Wilaya ya Maswa, Mkoa wa Simiyu wakimsikiliza Mgeni Rasmi, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza na wafugaji hao, wakati wa hafla fupi ya kukabidhi madume ya Ng'ombe 50 aina ya Borani kwenye Wilaya Hiyo, Hafla hiyo imefanyika 21 Novemba 2022.


Mmiliki wa Shamba la Mifugo lililopo kagera, Bw. Josam Ntangeki (katikati) akitoa ushauri kwa wafugaji wa Wilaya ya Maswa waliokabidhiwa madume ya Ng'ombe 50 aina ya Borani jinsi ya kuwatunza kwa kuwaogesha na kuwapatia chanjo ili waepukane na magonjwa, mara baada ya kukabidhiwa na Waziri wa Mifugo (hayupo pichani), makabidhiano hayo yamefanyika katika Wilaya ya Maswa, Mkoa wa Simiyu, 21 Novemba 2022.


Mkuu wa Wilaya ya Maswa Bw. Aswege Kaminyonge akisoma taarifa ya mifugo iliyokiwepo kwenye Wilaya yake na kutoa changamoto mbalimbali ikiwepo ukosefu wa pikipiki zitakazotumika katika mizunguko kwenye vijiji mbalimbali ili kutimiza shughuli za Ufugaji, akitoa taarifa huyo mbele ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi (hayupo pichani) kwenye hafla fupi ya kukabidhi madume ya Ng'ombe kwenye kata ya Buchambi, Wilaya ya Maswa Mkoa wa Simiyu, 21, Novemba 2022

TVLA KANDA YA KATI YATOA ELIMU YA KWA WAFUGAJI

 


Meneja Wakala ya Maabara ya Mifugo Tanzania ( TVLA ) kanda ya kati Dodoma Dkt.Japhet Joas Nkangaga akiwa ofisini kwake Dodoma ameleza ratiba watakavyo tekeleza utoaji elimu kwa wafugaji katika maadhimisho ya wiki TVLA ni pamoja na kesho tarehe 22.11.2022 wataenda kutoa elimu  Halmashauri ya Dodoma vijijini,shule ya Amani,Mlezi na Kilimani.Tarehe 23.11.2022 timu ya wataalam itakuwa Hamashauri ya Bahi kuchanja Mifugo ya wafugaji na 24.11.2022 timu hiyo ya wataalam itakuwa Dodoma Jiji kuchukua sampuli ili kuchunguza magonjwa mbalimbali CBPP na kuchanja kuku dhidi ya ugonjwa wa Kideri. (21.11.2022)


Baadhi ya Wataalam wa TVLA Kanda ya kati wakiongozwa na Dkt.Harrison Gabriel  kushoto wakiwa na mteja wao ambaye amekuja kupa huduma ya elimu ya uchanjaji kuku dhidi ya kideri cha kuku leo katika ofisi za TVLA Kanda ya kati.Kauli Mbiu ya Maadhimisho hayo ni,"Tambua,Tibu na Udhibiti wa magonjwa ya Mifugo".( 21.11.2022 )


Maadhimisho ya wiki ya TVLA Kanda ya kati yameanza leo.ambapo maadhimisho hayo yanafanyika kwa kutoa huduma mbalimbali  kwa kufanfanya shughuli mbalimbLi za za kutoa huduma za afya ya  Mifugo ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wafugaji wanaozunguka Mkoa huo.baadhi shughuli zinazofanyika ni pamoja na kutoa elimu ya udhibiti wa magonjwa,kutibu magonjwa na kutafiti vyakula vya Mifugo.kwa wafugaji wa mkoa wa Dodoma na vitongoji vyake.(21.11.2022).

MAABARA ZA TVLA SASA ZAFANYA KAZI KIDIGITALI

Na Mbaraka Kambona,


Wakala ya Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA) imewezeshwa vifaa vya kisasa katika maabara zake ambapo sasa wamekuwa na  uwezo wa kutambua kwa haraka vimelea vya magonjwa ya mifugo ndani ya dakika 15 tofauti na hapo awali ambapo ilikuwa inawachukua kati ya masaa 24 hadi 36.


Hayo yamefahamika  leo Novemba 21, 2022, jijini Dar es Salaam wakati  Mwakilishi kutoka Taasisi ya American Society for Microbiology, Dkt. Wes Kim akimkabidhi  Mwakilishi wa Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi(Mifugo), Prof. Hezron Nonga nyaraka za vifaa vya maabara ambavyo vimegharimu zaidi ya Shilingi za Kitanzania Milioni 600.


Akizungumza baada ya makabidhiano hayo, Prof. Nonga alisema kuwa lengo la kuboresha maabara hizo ni kuzijengea uwezo hasa kwenye kubaini uwepo wa vimelea ambavyo vimepelekea matumizi makubwa ya dawa za antibayotiki kwenye mifugo hasa kuku.


“Kutokana na mazingira tuliyonayo Tanzania, uwepo wa vimelea haukwepeki kutokana na joto, mvua na hali ya unyevunyevu, na vimekuwa kikwazo kwenye uzalishaji na uzalianaji wa mifugo yetu, hivyo basi tunapokuwa na maabara zilizoboreshwa zaidi inakuwa ni rahisi kubaini aina ya kimelea na kuweza kujua aina ya dawa ambayo inaweza kutumika kutibu na kumsaidia mfugaji kufuga kwa tija na kuepukana na maradhi,”alisema Prof. Nonga


Aliongeza kwa kusema kuwa ili kuweza kupambana vyema na vimelea hivyo ni muhimu wadau wa mifugo wa ndani na nje ya nchi kuwekeza kwenye sekta ya mifugo ili iweze kuwa na tija zaidi kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.


Naye, Mtendaji Mkuu, Wakala ya Maabara ya Mifugo (TVLA), Dkt. Stella Bitanyi alisema msaada huo walioupata kutoka kwa taasisi ya Fleming Fund kupitia taasisi ya American Society for Microbiology umesaidia kuwawezesha kufanya kazi zao kwa haraka zaidi.


“Kabla ya kupata vifaa hivi ilikuwa inatuchukua masaa zaidi ya 24 kutambua vimelea vya magonjwa ya mifugo lakini baada ya kupata msaada huu sasa tunaweza kutambua vimelea ndani ya dakika 15 tu,”alifafanua Dkt. Bitanyi


Aliongeza kuwa teknolojia hiyo ya kisasa waliyoipata inafanya maabara zao ziendane na teknolojia iliyopo duniani ambayo inawawezesha pia kutambua aina ya kimelea na ukoo wake.


Kwa upande wa Mwakilishi kutoka Taasisi ya American Society for Microbiology, Dkt. Wes Kim alisema kuwa wataendelea kutoa ushirikiano kwa serikali katika kupambana na vimelea vya magonjwa ya  mifugo ili kuweka msingi mzuri wa afya ya mifugo na usalama wa chakula kwa jamii.  


Aidha, taasisi hiyo pia iko mbioni kuzisaidia maabara nyingine zilizo chini ya TVLA ikiwemo ya Iringa ambayo hivi karibuni nayo itakabidhiwa vifaa kwa lengo hilo hilo la  kuboresha utendaji wa maabara nchini.


Wakala ya Maabara ya Mifugo(TVLA) ni Wakala ya Serikali iliyo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi yenye vituo 11 vilivyopo katika mikoa ya Dodoma, Iringa, Mwanza, Arusha, Tabora, Mtwara, Sumbawanga, Simiyu, Kigoma na Tanga.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Hezron Nonga(Kushoto) akipeana mkono na Mwakilishi wa Taasisi ya American Society for Microbiology, Dkt. Wes Kim muda mfupi baada ya kusaini nyaraka za makabidhiano ya vifaa vya maabara vilivyokabidhiwa kwa Wakala ya Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA) katika hafla fupi ya makabidhiano iliyofanyika jijini Dar es Salaam Novemba 21, 2022.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Hezron Nonga(Kushoto) na Mwakilishi wa Taasisi ya American Society for Microbiology, Dkt. Wes Kim(kulia) wakisaini nyaraka za makabidhiano ya vifaa vya maabara vilivyokabidhiwa kwa Wakala ya Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA) katika hafla fupi ya makabidhiano iliyofanyika jijini Dar es Salaam  Novemba 21, 2022. Wa kwanza kushoto aliyesimama ni Mkurugenzi Mtendaji wa TVLA, Dkt. Stella Bitanyi. Kulia ni Afisa kutoka taasisi ya American Society for Microbiology, Ade Olarewaju.

Mkuu wa Maabara ya Bakteliorojia kutoka Wakala ya Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA), Godwin Minga (kushoto) akitoa maelezo kwa Mwakilishi wa  Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Hezron Nonga(Kulia) na mgeni wake, Mwakilishi wa Taasisi ya American Society for Microbiology, Dkt. Wes Kim kuhusu mashine inayotumika kutambua vimelea vya magonjwa ya mifugo inavyofanya kazi walipotembelea maabara hiyo iliyopo  jijini Dar es Salaam Novemba 21, 2022.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Hezron Nonga(wa Sita kutoka Kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na  Mwakilishi wa Taasisi ya American Society for Microbiology, Dkt. Wes Kim (wa tano kutoka kushoto) walipotembelea moja ya maabara za  Wakala ya Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA) iliyopo jijini Dar es Salaam Novemba 21, 2022. Wengine katika picha ni Viongozi mbalimbali kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wakala ya Maabara ya Mifugo, na Maafisa kutoka taasisi ya American Society for Microbiology.

ULEGA: TUMIENI TEHAMA KUWAFIKIA WAFUGAJI

Na. Edward Kondela


Wataalamu wa mifugo nchini wametakiwa kuhakikisha wanatumia vyema Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuwafikia wafugaji wengi na kutatua changamoto zao.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amebainisha hayo (18.11.2022) katika Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza, wakati akifunga mafunzo rejea ya baadhi ya wataalamu wa mifugo kuanzia ngazi ya kijiji hadi mkoa kutoka Kanda ya Ziwa Magharibi inayohusisha mikoa ya Mwanza, Kagera na Geita yaliyoandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, akisema kuwa idadi ya wataalamu wa mifugo waliopo nchini kwa sasa haitoshelezi kila mfugaji kufikiwa na mtaalamu kwa wakati.


Naibu Waziri Ulega ameongeza kuwa kutokana na ukuaji wa tekonolojia wafugaji wengi wanatumia simu za mkononi hivyo zikitumika vyema kwa kushirikiana na wataalamu wa mifugo kupitia mfumo wa M-Kilimo kwa ajili ya huduma za ugani itakuwa ni njia rahisi kwa wafugaji kutatuliwa changamoto zao kwa haraka zaidi na kupata ushauri wa ufugaji bora na kisasa.


“Lazima wataalamu wetu muwe watumiaji wazuri wa hii mitandao ya kitaaluma ili kupeleka teknolojia kwa wafugaji wetu kwa kuwa hatuna uwezo wa kutosheleza wataalamu kila kijiji upungufu ni mkubwa.” Amesema Mhe. Ulega


Aidha, amewataka wataalamu hao kuhakikisha wanajiwekea malengo kwa kuwa na wafugaji wachache kila baada ya muda ambao wanawafuatilia kwa karibu kuhakikisha wafugaji hao wanakuwa na maeneo yao wenyewe wanayoyamiliki na kuwapatia elimu na huduma bora za mifugo.


Amesema kwa kufanya hivyo wataalamu wa mifugo wataweza pia kuwafikia wafugaji ambao nao watatoa elimu kwa wenzao juu ya huduma bora za mifugo na kuwahamasisha kumiliki maeneo na kuwa na hatimiliki.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Angelo Mwilawa amesema jukumu la wizara ni kusambaza tekonolojia sahihi na zenye ubora ili kuleta mabadiliko chanya kwa wadau mbalimbali wa mifugo na kuwafikia wafugaji kwenye maeneo yao ya kazi kuanzia ngazi ya kijiji hadi mkoa.


Ameongeza kuwa katika mafunzo hayo mada mbalimbali zimewasilishwa ikianza na mabadiliko makubwa ambayo sekta ya mifugo inatekeleza pamoja na maboresho makubwa yaliyofanyika kwenye Sera ya Mifugo ya Mwaka 2006 kuhakikisha wataalamu wa mifugo wanajengewa uwezo na kuainisha maeneo muhimu ya mpango mkubwa wa mabadiliko.


Pia, amesema mafunzo hayo yamegusia juu ya uendelezaji wa malisho ya mifugo na maji ambapo wafugaji wamekuwa wakipata changamoto hususan nyakati za kiangazi na kuwafanya kuhamahama kutafuta malisho na maji pamoja na namna wafugaji wanavyoweza kudhibiti magonjwa ya mifugo.


Nao baadhi ya washiriki wa mafunzo rejea, wamesema mafunzo hayo yamewakumbusha mambo muhimu ya kufanya kwa wafugaji ili waweze kufuga kisasa na kudhibiti magonjwa ya mifugo.


Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa ikiendeleza mafunzo rejea kwa wataalamu wa mifugo kutoka maeneo mbalimbali nchini ili kuhakikisha inawakumbusha mambo muhimu ya kuzingatia katika taaluma ya mifugo ili wafugaji waweze kufuga kisasa na kudhibiti magonjwa ya mifugo.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akizungumza wakati wa kufunga mafunzo rejea kwa baadhi ya wataalamu wa mifugo (hawapo pichani) kutoka Kanda ya Ziwa Magharibi inayojumuisha mikoa ya Mwanza, Kagera na Geita yaliyofanyika katika Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza ambapo amewataka kuhakikisha wanatumia vyema Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuwafikia wafugaji wengi na kutatua changamoto zao. (18.11.2022)

Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza Mhe. Veronika Kessy akizungumzia hali ya sekta ya mifugo katika wilaya hiyo na kuishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa namna inavyohakikisha inatoa mafunzo rejea kwa wataalamu wa mifugo. Mhe. Kessy amezungumza hayo wakati wa kufungwa kwa mafunzo rejea kwa baadhi ya wataalamu wa mifugo (hawapo pichani) kutoka Kanda ya Ziwa Magharibi inayojumuisha mikoa ya Mwanza, Kagera na Geita yaliyofanyika katika Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza. (18.11.2022)

Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Angelo Mwilawa akizungumza wakati wa kufunga mafunzo rejea kwa baadhi ya wataalamu wa mifugo (hawapo pichani) kutoka Kanda ya Ziwa Magharibi inayojumuisha mikoa ya Mwanza, Kagera na Geita yaliyofanyika katika Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza ambapo amesema jukumu la wizara ni kusambaza tekonolojia sahihi na zenye ubora ili kuleta mabadiliko chanya kwa wadau mbalimbali wa mifugo na kuwafikia wafugaji kwenye maeneo yao ya kazi kuanzia ngazi ya kijiji hadi mkoa. (18.11.2022)

Baadhi ya wataalamu wa mifugo kutoka Kanda ya Ziwa Magharibi inayojumuisha mikoa ya Mwanza, Kagera na Geita waliohudhuria mafunzo rejea ya siku mbili yaliyofanyika katika Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza ili kuwakumbusha juu ya taaluma ya mifugo na kubadilishana ujuzi wa namna bora ya kuwahudumia wafugaji. (18.11.2022)

 


TVLA KUTOA HUDUMA YA CHANJO, KUPIMA MIFUGO BURE

Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania imepanga kutoa huduma ya Chanjo pamoja na upimaji wa magonjwa ya mifugo bure kwa maeneo yatakayobainishwa kwenye vituo vya 11 vilivyopo Tanzania nzima kuanzia tarehe 21/11/2022 hadi tarehe 25/11/2022 ikiwa ni maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwake.


Akizungumza na vyombo vya habari Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania-TVLA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Dkt.Qwari Bura kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa TVLA Dkt. Stella Bitanyi siku ya tarehe 20/11/2022 mtaa wa Bomani Mkoani Iringa kwa ajili ya kuutambulisha Umma alisema kwamba wakala imepanga kuwafikia wafugaji na kurudisha kile ilichokipata kwa jamii ikiwa ni Maadhimisho ya Miaka 10 tangu kuanzishwa kwake mwaka 2012.


Dkt. Bura alisema kwamba wakala ilizinduliwa rasmi tarehe 11 Julai, 2012 na Katibu Mkuu Kiongozi na hadi kufikia mwaka huu 2022 Wakala imetimiza miaka 10 tangu kuanzishwa kwake kutokana na kuunganishwa kwa iliyokuwa Maabara Kuu ya Mifugo (CVL), Vituo vya Kanda vya Uchunguzi na Utambuzi wa Magonjwa ya Mifugo (VICs), Taasisi ya Utafiti wa Ndorobo (TTRI) Tanga na Kituo cha Utafiti wa Ndorobo (TTRC) Kigoma.


“Shughuri zitakazofanywa kwenye maadhimisho hayo ni pamoja na Uchanjaji wa Mifugo Bure kwa maeneo yatakayobainishwa, Kufanya upimaji wa magonjwa ya Mifugo Bure kwa maeneo yatakayobainishwa, Kutoa Elimu kuhusiana na huduma zinazotolewa na TVLA, Utoaji wa Elimu ya Mifugo, Kutembelea vituo vya watoto yatima na kutoa misaada pamoja na Kufanya Ufunguzi wa Jengo Jipya la Maabara na Ofisi Kituo cha Iringa.” Alisema Dkt. Bura


Dkt. Bura aliongeza kuwa kwa upande wa Kituo cha Iringa kinachohudumia mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya na Ruvuma, wamepanga Kutembelea wafugaji wa kuku wa asili na kufanya mikutano na wafugaji kwa lengo la kutoa Elimu hususan huduma za upimaji wa mgaonjwa na chanjo. Kufanya upimaji wa magonjwa ya Mifugo Bure kwenye kituo chetu cha zamani kilichopo mtaa wa Boma Manispaa ya Iringa.


Zingine ni uchanjaji wa kuku Bure kwenye kata zitakazotembelewa, Kutoa chanjo ya Ugonjwa wa MDONDO wa kuku kwa wafugaji, kufanya Ufunguzi wa Jengo Jipya la Maabara na Ofisi Kituo cha Iringa pamoja na kuzindua tovuti mpya ya TVLA, Mfumo wa Usajili na Utoaji wa Vibali wa Viuatilifu vya Wanyama pamoja na uzinduzi wa namba ya mawasiliano ya Huduma kwa Mteja. 


 “Wakala inajivunia mafanikio makubwa iliyoyapata toka kuanzishwa kwake kwani imeongeza mapato yake ya ndani kutoka Shilingi Milioni 220 mwaka 2013/2014 hadi kufikia Shilingi bilioni 3.1 mwaka 2021/2022 sawa na ongezeko la asilimia 1,409, Uzalishaji na usambazaji wa chanjo kutoka chanjo moja (1) ya Mdondo Mwaka 2013/2014 na hadi chanjo 7 mwaka 2022, Kusogeza huduma za uchunguzi na utambuzi wa magonjwa karibu na wananchi.”


“Mafanikio mengine ni Uboreshaji wa maabara ya kupima ubora wa vyakula vya mifugo, Kushiriki katika utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja, kupata ithibati ya kimataifa (accreditation) katika vipimo 10 vya kimaabara na Kujenga uwezo katika kusajili na kutoa vibali vya viuatilifu vya wanyama.” Alisema Dkt. Bura


Aina 7 za chanjo zinazozalishwa na TVLA ni pamoja na Chanjo stahimilivu joto ya kukinga kuku dhidi ya ugonjwa wa Mdondo, Chanjo ya ugonjwa wa Kimeta, Chanjo ya ugonjwa wa Chambavu, Chanjo ya Homa ya Mapafu ya Ng’ombe, Chanjo ya ugonjwa wa Kutupa Mimba, Chanjo mchanganyiko wa Kimeta na Chambavu pamoja na Chanjo ya Homa ya Mapafu ya Mbuzi. 

Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania-TVLA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Dkt.Qwari Bura akitoa taarifa kwa vyombo vya habari (havipo pichani) siku ya tarehe 20/11/2022 kuhusiana maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwa Wakala na shuguli zitakazofanyika kuanzia tarehe 21/11/2022 hadi tarehe 25/11/2022 kwa lengo kuwafikia wafugaji na kurudisha kile ilichokipata kwa jamii kwenye vituo vyake vyote  11 vilivyopo Tanzania nzima.