Nav bar

Ijumaa, 25 Novemba 2022

SERIKALI YAFANYA MAGEUZI KWENYE SEKTA YA MIFUGO

Na. Martha Mbena.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amesema Serikali kupitia Wizara ya Mifugo imekuja na mageuzi kwa kufuga mifugo bora yenye tija kupitia Ng'ombe aina ya Borani ili kupata kilo nyingi, nyama nyingi na kuzalisha maziwa mengi jambo ambalo litachangia pato la Taifa.


Waziri Ndaki ameyasema hayo (21.11.2022) wakati akikabidhi madume 50 ya Ng'ombe aina ya Borani kwa makundi ya wafugaji wa Wilaya ya Maswa  kwenye hafla fupi iliyofanyika kwenye kata ya Buchambi Mkoani Simiyu.


"Kiasi cha sh 915 milioni kilichotolewa na Serikali kimetumika kununua madume 336 ya Ng'ombe aina ya Borani  ambayo yatakabidhiwa kwenye Wilaya 10 nchi nzima, Kwa hapa Wilaya ya Maswa tumekabidhi haya madume 50, Ombi langu muwatunze kwa kuwaosha mara kwa mara ili wasipate kupe wakapata ugonjwa wa Ndigana," Alisema Waziri Mashimba.


Mhe. Mashimba  aliongeza kuwa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa Ng'ombe hao bure kwa vikundi vyote vya wafugaji na kila kikundi kitapata dume ambalo litapanda majike yasiyopungua 25 kwa mwaka, Lengo ni kuzalisha Ng'ombe wa kisasa na bora zaidi kwa ufugaji.


Alisema kuwa mpango wa Serikali ni kuhamasisha ufugaji wa kisasa wa mifugo michache na kipato kingi na kuongeza kuwa aina hiyo ya Ng'ombe ni tofauti na Ng'ombe wa kawaida na kufafanua kuwa Ng'ombe wa kienyeji wanne ni sawa na Ng'ombe mmoja wa aina ya Borani.


"Niwaambieni tu kuwa kwa madume haya Ng'ombe atakayezaliwa ana uwezo wa kutoa lita 5 mpaka 10 kwa siku lakini wa kienyeji akijitaidi sana anaweza kutoa lita 1 mpaka 5 kwa siku kwa hiyo Ng'ombe wa kienyeji anaingizia serikali pato dogo," Alisema Ndaki.


Naye Mkuu wa Wilaya ya Maswa Aswege Kaminyonge amesema changomoto kubwa ni ukosefu wa pikipiki zitakazotumika katika mizunguko  kwenye vijiji mbalimbali ili kufuatilia mradi huo usije ukakwama.


Vilevile mkuu huyo wa Wilaya aliwataka maafisa watendaji wa kata kufuatilia kwa ukaribu zaidi wafugaji wote waliokabidhiwa madume hayo ili yasidhulike kwa kukosa matunzo.


kwa upande wake Mmiliki wa Shamba la Mifugo Mkoani Kagera, Bw. Josam Ntangeki amesema madume hayo kati ya mwaka mmoja hadi miwili yamepatiwa huduma zote za chanjo na kuwaomba wafugaji kujitaidi kuwapatia Ng'ombe hao huduma zote ikiwapo kuwapatia na chanjo.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) (aliyesimama) akiongea na Wafugaji wa kata ya Buchambi, Wilaya ya Maswa, Mkoa wa Simiyu kwenye hafla ya kukabidhi madume ya Ng'ombe 50 aina ya Borani kwa makundi ya wafugaji wa Wilaya hiyo, 21 Novemba 2022.


Mwakilishi wa kikundi cha Wafugaji kutoka kata ya Buchambi akichagua Dume la Ng'ombe mmoja kwa ajili ya kikundi chake ili waweze kwenda kufuga na kuzalisha zaidi Ng'ombe wa kisasa aina ya Borani, tukio hilo limefanyika 21, Novemba 2022.


Wafugaji wa kata ya Buchambi, Wilaya ya Maswa, Mkoa wa Simiyu wakimsikiliza Mgeni Rasmi, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza na wafugaji hao, wakati wa hafla fupi ya kukabidhi madume ya Ng'ombe 50 aina ya Borani kwenye Wilaya Hiyo, Hafla hiyo imefanyika 21 Novemba 2022.


Mmiliki wa Shamba la Mifugo lililopo kagera, Bw. Josam Ntangeki (katikati) akitoa ushauri kwa wafugaji wa Wilaya ya Maswa waliokabidhiwa madume ya Ng'ombe 50 aina ya Borani jinsi ya kuwatunza kwa kuwaogesha na kuwapatia chanjo ili waepukane na magonjwa, mara baada ya kukabidhiwa na Waziri wa Mifugo (hayupo pichani), makabidhiano hayo yamefanyika katika Wilaya ya Maswa, Mkoa wa Simiyu, 21 Novemba 2022.


Mkuu wa Wilaya ya Maswa Bw. Aswege Kaminyonge akisoma taarifa ya mifugo iliyokiwepo kwenye Wilaya yake na kutoa changamoto mbalimbali ikiwepo ukosefu wa pikipiki zitakazotumika katika mizunguko kwenye vijiji mbalimbali ili kutimiza shughuli za Ufugaji, akitoa taarifa huyo mbele ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi (hayupo pichani) kwenye hafla fupi ya kukabidhi madume ya Ng'ombe kwenye kata ya Buchambi, Wilaya ya Maswa Mkoa wa Simiyu, 21, Novemba 2022

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni