Nav bar

Alhamisi, 30 Juni 2022

NZUNDA WATAKA VIJANA KUCHANGAMKIA FURSA ZINAZOTOLEWA NA SERIKALI NA ASASI BINAFSI

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw. Tixon Nzunda amewataka vijana kuchangamkia fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali pamoja na Asasi binafsi ili kuweza kupambana na tatizo la ukosefu wa Ajira nchini


Nzunda ameyasema hayo jana tarehe 29Juni 2022 Mjini Morogoro wakati wa hafla ya tathimini na ufungaji wa mradi wa uchumi kwa Vijana uliokuwa unafadhiliwa na shirika la Care International Tanzania.


"Kupitia maradi huu wa Uchumi kwa Vijana, baadhi ya vijana waliobahatika kuingia katika Mradi huu wameweza kunufaika na Mafunzo ya ufugaji  na kujitegemea, sasa ni wajibu wao kuhakikisha elimu hii inawafikia vijana  wengine pamoja na makundi mengine". Alisema Nzunda.

 

Aidha, Nzunda aliongeza kwa kusema, “Ripoti ya mradi huu imeonyesha kwamba mpaka kufikia Mei 2022, vikundi 1040 viliundwa vikiwa na idadi kubwa ya Vijana wa Kike na wanawake kwa asilimia 64. Natoa pongezi za dhati kwa Halmashauri zote katika Mikoa ya Morogoro, Njombe na Mbeya kwani ndio waliosimamia kazi ya uundaji wa vikundi hivi.”


Nzunda alisema kuwa kwa mfumo huo ni dhahiri kwamba, hata shirika la Care International Tanzania au wadau wengine wasipo kuwepo, vijana wataendelea na wanaweza kuendelea  kuhamasishana kaunda Vikundi mbalimbali vya Ufugaji  kwa lengo la kujikwamua kiuchumi.


Vilevile, Katibu Mkuu Mifugo Bw. Nzunda ametoa maelekezo kwa  Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Mikoa na Halmashauri  kuhakikisha vikundi vyote 1040 vilivyoundwa na kuwezeshwa na Care International Tanzania vinafuatiliwa na kusaidiwa kwa kutoa ushauri wa kitaalam ikiwa  ni pamoja na kusaidiwa kupata mikopo ya asilimia 15 kwa ajili wa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.


Nzunda amewataka Maafisa Biashara wa Halmashauri  kushirikiana na maafisa maendeleo ya Jamii, ili vikundi ambavyo vimeanza uzalisha katika maeneo mbalimbali katika Mikoa ambayo mradi huo wa Uchumi kwa Vijana ulikuwa unatekelezwa, kuhakikisha vikundi hivyo vinapata uhakika wa soko la bidhaa hizo zinazozalishwa.


"Tumefahamishwa kuwa katika mradi huu wa uchumi, vijana wengi wamejikita katika ufugaji wa Kuku, Ng’ombe na Nguruwe, hivyo naelekeza kurugenzi ya Utafiti, Mafunzo na Ugani kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) pamoja na LITA kuhakikisha mnafuatilia vikundi hivi vilivyoanza uzalishaji, na kushirikiana nao katika kutafuta masoko ya uhakika ya bidhaa hizo za Mifugo wanazozalisha".Alisema Nzunda.


Pia, ninaelekeza Kurugenzi za Mafunzo, utafiti na Ugani katika Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) na Wizara ya Kilimo kuona namna bora zitakavyotumia miongozo na mikakati mbalimbali iliyotumika kutekeleza mradi  huu wa Uchumi kwa Vijana na kuchukua  baadhi ya mbinu bora na kuzijumuisha katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kurugenzi zao katika Wizara zote mbili ili kuleta ufanisi mkubwa.


Katibu Mkuu  Mifugo Bw. Tixon Nzunda amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mama Samia Suluhu Hassan itaendelea kuweka mazingira rafiki kwa kuhakisha vijana wanaweza kujiajili kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo nchini.


Awali Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw.Tixon Nzunda alibainisha Misingi ya Mafanikio kwa Vijana kuwa ni pamoja na  kuwa na Moyo wa kupenda kazi na kujituma, Uadilifu na uaminifu ili vijana waendelee kuaminika, Ubunifu na uthubutu.


Msingi mwingine wa Mafanikio kwa Vijana Nzunda alitaja kuwa ni Matumizi sahihi ya rasirimali, Kuwa na Maono na malengo ya kuona mbali, utunzaji na matumizi sahihi ya taarifa na uzalendo na utu mwema.


Katika Hatua nyingine, Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro Bi. Mariamu Mtunguja aliwaomba wasimamizi wa mradi huo kutoka Care International Tanzania kuhakikisha wanawafikia vijana wengi katika maeneo ambayo mradi huo haujafika ili kuweza kuwanusuru vijana ambao hawana ajira.


Naye mkurugenzi Mkazi wa Care International Tanzania  Bi. Prudence Masako amesema kuwa Care International imekuwa na miradi kadhaa wa kadhaa ikiwemo ya kuimarisha afya ya mama na mtoto, Usawa wa Kijinsia na kwa sasa wamejikita katika kuimarisha uchumi wa vijana.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Miradi kutoka Care International Tanzania, Haika Mtui amesema kuwa waliamua kuja na mradi wa Uchumi kwa Vijana mara baada ya kugundua kuwa kundi kubwa la Vijana halina ajira hivyo kuja na mbinu ya kuwajengea uwezo katika Ufugaji, Kilimo na ufundi ili waweze kujiajiri.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw.Tixon Nzunda (wa tatu kutoka kushoto)akikagua moja ya kazi za ufundi za vijana walionufaika na Mradi wa "Uchumi kwa Vijana" mjini morogoro jana 29 juni 2022.Wengine katika Picha ni wageni waalikwa pamoja na Vijana wanufaika wa mradi huo.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) kulia, akisikiliza moja ya wasilisho la Tathimini ya mradi wa Uchumi kwa Vijana (anayewasilisha hayupo Pichani).Wengine ni Mariam Mtunguja, Katibu Tawala mkoa wa Morogoro na Haika Mtui, Mkurugenzi wa Miradi Care International Tanzania.



Baadhi ya Washiriki wa Hafla ya tathimini ya Mradi wa Uchumi kwa Vijana pamoja na Wageni waalikwa  iliyofanyika jana tarehe 29/06/2022  Mjini Morogoro.


MAENEO YALIYOTENGWA KWA AJILI YA MALISHO YA MIFUGO YATAKIWA KUSAJILIWA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amesema kuwa maeneo yote ya malisho yaliyotengwa kwenye halmashauri yanatakiwa kusajiliwa na kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali.

 

Waziri Ndaki ameyasema hayo leo (26.06.2022) kwenye mkutano wa hadhara na wafugaji uliofanyika kwenye Kijiji cha Kongwa wilayani Morogoro ambapo aliwaeleza wafugaji hao kuwa halmashauri zikishatenga maeneo kwa ajili ya malisho zinatakiwa kuyawasilisha kwenye Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili yasajiliwe na kutangazwa kwenye gazeti la serikali.

 

"Halmashauri zinatakiwa mara baada ya kutenga maeneo ya malisho katika vijiji, zinatakiwa kuyawasilisha maeneo hayo Wizarani ili yasajiliwe na kutangazwa kwenye gazeti la serikali, kwa kufanya hivyo itakuwa ni vigumu mtu kubadilisha matumizi ya maeneo hayo kwa kuwa yatakuwa yanalindwa kisheria," alisema

 

Waziri Ndaki amewataka wafugaji hao kupanda malisho kwenye maeneo ambayo tayari yameshatengwa kwa ajili ya malisho badala ya kutegemea malisho ya asili peke yake. Wizara inaendelea kutoa elimu na kuhamasisha wafugaji kupanda malisho ili kuweza kukabiliana na tatizo la upungufu wa malisho hasa kipindi cha kiangazi.

 

Wafugaji wametakiwa kuacha tabia ya kuwakaribisha wafugaji kutoka maeneo mengine kuja kulisha mifugo kwenye maeneo yao kutokana na uchache wa malisho katika maeneo waliyopo. Hivyo pindi wanapowakaribisha wafugaji kutoka nje malisho katika maeneo hayo humalizika kwa haraka na kusababisha mifugo kuanza kufa kwa kukosa malisho.

 

Vilevile wafugaji hao wametakiwa kuanza kufanya tathmini ya kiasi cha mifugo waliyonayo na kiasi cha malisho kilichopo mpaka kuelekea msimu wa mvua kuanza. Wafugaji wametakiwa endapo wataona mifugo ni mingi kuliko malisho yaliyopo, kuanza kuvuna mifugo hiyo na kubakiza kiasi cha mifugo kitakachoendana na malicho yaliyopo badala ya kusubiri mifugo ikabiliane na kiangazi kikali ianze kufa ndipo waiuze kwa bei ya hasara kwa kuwa mifugo afya yake haitakuwa nzuri.

 

Waziri Ndaki pia amewaahidi wafugaji kwenye Jimbo la Morogoro Kusini kuwa Wizara itawajengea Malambo matatu na Majosho tatu, hii ni baada ya kusikiliza changamoto zinazowakabili wafugaji zilizowasilishwa na Katibu wa Chama cha Wafugaji wakati anawasilisha taarifa yake.

 

Naye Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini, Mhe. Innocent Kalogeris amesema kuwa kwa sasa upo umuhimu wa kuupitia upya mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye vijiji kwa kuwa lipo ongezeko kubwa la wafugaji na wakulima ili mpango huo uweze kwenda sawa na hali halisi ya sasa.

 

Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msonda naye amesema kuwa serikali imeshafanya mambo mengi katika kutengeneza mazingira mazuri ya kuwawezesha wafugaji, kinachotakiwa sasa ni kila mmoja kuhakikisha anatimiza wajibu wake na wafugaji kufuata maelekezo / ushauri wanaopewa na wataalam.

 

Aidha, amesema kuwa zipo changamoto ambazo zinatakiwa kutatuliwa kwenye ngazi ya Kijiji, Kata na Wilaya ambazo hazihitaji ngazi ya Wizara, hivyo atawasimamia wahusika ili kuhakikisha changamoto hizo zinatatuliwa kwenye ngazi hizo.

 

Katika ziara yake Wilayani Morogoro, Waziri Ndaki pia alifanya mkutano wa hadhara na wafugaji katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki ambapo aliwasihi wafugaji hao kushiriki kwenye zoezi la Sensa ya Watu na Makazi kwa kuwa ni muhimu kwa mipango ya maendeleo ya nchi.

 

Pia aliendelea kuwahamasisha wafugaji kuhakikisha wanavalisha mifugo yao hereni za utambuzi zoezi ambalo linaendelea ambalo nalo lina faida kubwa katika kukuza Sekta ya Mifugo. Waziri Ndaki pia amewaahidi wafugaji wa Jimbo hilo kuwa Wizara itawajengea Majosho matatu.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na wafugaji wa Kata ya Mvua kwenye Kijiji cha Kongwa wilayani Morogoro ambapo amewataka wafugaji hao kuanza kulima malisho katika maeneo yao na kutunza nyanda za malisho zilizopo, vilevile kutojihusisha na migogoro ya aina yoyote katika jamii wanazoishi. (26.06.2022)


Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando akitolea ufafanuzi baadhi ya hoja zilizotolewa na wafugaji kupitia uongozi wao ambapo amesema zipo changamoto ambazo zinaweza kutatuliwa kwenye ngazi ya Kijiji, Kata hadi Wilaya, hivyo changamoto za aina hiyo hazihitaji kuisubiri Wizara watazishughulikia wenyewe ndani ya Wilaya. (26.06.2022)


Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini, Mhe. Innocent Kalogeris akizungumzia changamoto zilizopo kwenye jimbo lake kwa upande wa wafugaji wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Kijiji cha Kongwa wilayani Morogoro, ambapo ameshauri mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye vijiji uboreshwe ili uendane na hali ya sasa kwa kuwa wafugaji na wakulima wameongezeka. (26.06.2022)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (kulia) akimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando (kushoto) kadi ya uanachama wa Chama cha Wafugaji wakati wa mkutano wa hadhara na wafugaji uliofanyika kwenye Kijiji cha Kongwa wilayani Morogoro. (26.06.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (kulia) akimkabidhi Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini, Mhe. Innocent Kalogeris (kushoto) kadi ya uanachama wa Chama cha Wafugaji wakati wa mkutano wa hadhara na wafugaji uliofanyika kwenye Kijiji cha Kongwa wilayani Morogoro. (26.06.2022)


Baadhi ya wafugaji wa Kata ya Mvua wakimsikiliza Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (hayupo pichani) wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Kijiji cha Kongwa wilayani Morogoro. (26.06.2022)

NZUNDA AZINDUA MRADI WA UNENEPESHAJI, UZALISHAJI CHAKULA CHA MIFUGO

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Tixon Nzunda amezidua Mradi wa uandaaji wa lishe bora ya gharama nafuu kwa unenepeshaji wa Ng’ombe nchini uliofanyika kwenye ofisi za taasisi ya Utafiti wa Mifugo(TALIRI) kanda ya Mashariki jijini tanga Juni 23, 2022.


Katika uzinduzi huo, Nzunda alisema kwamba mradi huo ni ushirikiano kati ya Wizara na COSTECH kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa nyama bora ambazo zinakwenda kuwa malighafi kwenye viwanda, lishe bora kwa wananchi, kupunguza pengo la vyakula vya mifugo kwa kutengeneza mashamba makubwa ya utafiti na mashamba darasa ya malisho ili wafugaji waweze kujifunza na kupata maeneo ya kufuga pamoja na  kutoa elimu kwa wafugaji, wasindikaji na wafanyabiashara wa mazao ya Mifugo.


“Nimeona kazi nzuri mnazozifanya hasa kwenye kituo cha unenepeshaji wa Mifugo ya Nyama, ule ni mfano mzuri wa kuigwa, tunataka vituo hivyo viwe vingi zaidi, tuwawezeshe vijana wanaotoka vyuoni  mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri, tutakuwa tumewatengenezea ajira za kudumu, tutakuwa na uhakika  wa kurudisha fedha na watatoa darasa kwa wengine kupitia elimu ya unenepeshaji,”alisema


“Tumeandaa mpango mkubwa wa mabadiliko ya Sekta ya Mifugo, ili tuweze kujenga tija, tuweze kuimarisha huduma za afya ya Mifugo, tuweze kupata masoko ya uhakika ya Mifugo na bidhaa za Mifugo, na kuwa na mfumo imara wa upatikanaji wa masoko na mfumo imara wa upatikanaji wa malisho kwa kuwaruhusu sekta binafsi kushiriki,” aliongeza


Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti ya Mifugo (TALIRI), Prof. Erick Komba alisema kuwa taasisi hiyo ilianzishwa kwa lengo la kusimamia na kufanya tafiti za Mifugo Tanzania Bara, kuibua, kutathimini na kusambaza teknolojia bora za Mifugo. 


“Tafiti tunazozifanya ni pamoja na tafiti za malisho, tafiti za vyakula za Mifugo, uzazi wa Mifugo, uzalishaji wa Mifugo na tafiti za mbali (mbegu) za Mifugo ambapo tafiti hizo zinawezeshwa na Serikali Kuu, wadau wa maendeleo kutoka ndani na nje ya nchi,”alisema


Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo (TALIRI), Kanda ya Mashariki, Tanga, Dkt. Zabron Nziku aliongeza kuwa, mradi huo una thamani ya shilingi milioni 120 na msingi wa mradi huu ni kutengeneza lishe bora ambayo itaweza kusaidia upatikanaji wa nyama bora na yenye bei nafuu kwa walaji.


Uzinduzi wa mradi wa uandaaji wa lishe bora ya gharama nafuu kwa unenepeshaji wa Ng’ombe Tanzania ulishirikisha wadau mbalimbali ambao ni viongozi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), viongozi Kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga, maafisa mifugo kutoka Halmashauri za Mkoa wa Tanga, watengenezaji wa vyakula vya Mifugo, Wanenepeshaji, wafugaji pamoja na wafadhili wa Mradi (COSTECH).


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw. Tixon Nzunda akipata maelezo kuhusu namna vijana walivyowezeshwa kutengeneza mradi wa Majani vlVunde (Saileji) yatakayotomika kunenepesha Mifugo kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Mifugo (TALIRI) Kanda ya Mashariki Tanga Dkt. Zabron Nziku alipotembelea Taasisi hiyo kwa ajili ya uzinduzi wa Mradi wa uandaaji wa lishe bora ya gharama nafuu kwa unenepeshaji wa Ng’ombe nchini uliofanyika kwenye ofisi za TALIRI Tanga Juni 23, 2022.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw. Tixon Nzunda akipata maelezo ya namna ya uoteshaji wa malisho ya Mifugo kutoka kwa Mtafiti Mwandamizi wa Taasisi ya Mifugo (TALIRI) Kanda ya Mashariki Tanga Bw. Walter Mangesho alipotembelea Taasisi hiyo kwa ajili ya uzinduzi wa Mradi wa uandaaji wa lishe bora ya gharama nafuu kwa unenepeshaji wa Ng’ombe nchini uliofanyika kwenye ofisi za TALIRI Tanga Juni 23, 2022.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Tixon Nzunda akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika kwenye Taasisi ya Mifugo (TALIRI) Kanda ya Mashariki Tanga kwa ajili ya uzinduzi wa  Mradi wa uandaaji wa lishe bora ya gharama nafuu kwa unenepeshaji wa Ng’ombe nchini uliofanyika kwenye ofisi za TALIRI kanda ya Mashariki Jijini Tanga Juni 23, 2022.



Jumamosi, 25 Juni 2022

WAZIRI NDAKI AKABIDHI INJINI ZA BOTI KWA AJILI YA WAVUVI

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amekabidhi injini za boti kwa ajili ya wavuvi katika Halmashauri za Wilaya za Pangani, Mtwara Mjini na Iringa.

 

Akizungumza kabla ya kukabidhi injini hizo leo (24.06.2022) Waziri Ndaki alisema kuwa Wizara imeendelea na utaratibu wake wa kuwawezesha wavuvi kwa kuwapatia vifaa vinakavyowasaidia kuongeza uwezo wa kuvua mazao ya uvuvi kwa wingi ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya uvuvi hapa nchini.

 

“Injini za Boti tunazozikabidhi leo zina uwezo wa nguvu ya farasi 15 na tunazitoa kwenye Halmashauri za Wilaya za Pangani, Mtwara Mjini na Iringa ambapo kila Halmashauri itapata injini moja kwa ajili ya kuwawezesha wavuvi kuongeza uwezo wao wa kuvua lakini pia kulinda rasilimali za uvuvi,” alisema

 

Waziri Ndaki amewasihi wavuvi kuhakikisha wanavitunza vifaa wanavyopatiwa na Wizara pamoja na Wadau wengine wa uvuvi na kuhakikisha wanavitumia kwa matumizi yaliyokusudiwa ikiwa ni pamoja na ulinzi wa rasilimali za uvuvi.

 

Aidha, Waziri Ndaki amesema kuwa Serikali kupitia Wizara imejipanga kununua injini nyingine 250 za boti katika mwaka wa fedha wa 2022/2023 na kama kutakuwa na uwezakano zinaweza kuongezeka injini 70 zaidi ambapo kutakuwa na jumla ya injini 320.

 

Lengo ni kuhakikisha uzalishaji wa mazao ya uvuvi unaongezeka na mchango wake katika kukuza kipato cha mvuvi na taifa kwa ujumla kinaongezeka. Kwa kufanya hivyo lengo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan litakuwa limetimia kwa kuhakikisha kipato cha wavuvi kinaongezeka na mchango wa uvuvi kwenye pato la taifa unaongezeka.

 

Vilevile Waziri Ndaki amesema kuwa injini hizo zitakazo nunuliwa zitatolewa kwenye vyama vya ushiriki vya wavuvi na hata kwa mvuvi mmoja mmoja mwenye uwezo kwa kuwa zitakuwa zikikopeshwa kwa riba ndogo sana ambayo haitawaumiza wavuvi.

 

Naye Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso akizungumza baada ya kupokea injini moja ya boti kwa niaba ya wananchi wa Pangani ameishukuru Wizara kwa kuwapatia injini hiyo na kwamba itakwenda kuwa msaada mkubwa kwa wavuvi katika shughuli zao za uvuvi ikiwa ni pamoja na ulinzi wa rasilimaliza uvuvi. Lakini pia ameishukuru wizara kwa kuamua kujenga soko la samaki Pangani na kwamba wanapangani wataendelea kutoa ushirikiano kwa Wizara.

 

Mbunge wa Mtwara Mjini, Mhe. Hassan Mtenga licha ya kuishukuru Wizara kwa kuwakabidhi injini ya boti, ameiomba Wizara kuendelea kuwawezesha wavuvi kwenye vifaa vingine vya uvuvi ikiwemo majokofu ya kuhifadhia mazao ya uvuvi.

 

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Uvuvi, Dkt. Nazael Madala amesema kuwa Wizara imekuwa na utaratibu wa kuwawezesha wavuvi kwa kuwapatia vifaa mbalimbali vinavyowasaidia kuweza kuongeza uwezo wao wa kuvua mazao hayo kwa wingi zaidi. 


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) akizungumza kabla ya kukabidhi Injini tatu za Boti zenye uwezo wa nguvu ya farasi 15 kwa wabunge wa majimbo ya Pangani, Mtwara Mjini na Iringa Vijijini ili ziweze kwenda kuwasaidia wavuvi katika shughuli zao za uvuvi ikiwa ni pamoja na ulinzi wa rasilimali za uvuvi, ambapo pia alisisitiza watumiaji wa injini hizo wazitumie kwa matumizi yaliyokusudiwa na si vinginevyo. Hafla hii imefanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022) 

Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso (Mb) akiipongeza Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi) kwa kuipatia Jimbo lake la Pangani Injini moja ya Boti yenye uwezo wa nguvu ya farasi 15 kwa kuwa itakwenda kuwasaidia wavuvi katika shughuli zao za uvuvi lakini pia katika kulinda rasilimali za uvuvi. Hafla hii imefanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022) 



Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi), Dkt. Nazael Madala akitoa maelezo kuhusu malengo ya sekta katika kuwawezesha wavuvi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Mifugo na Uvuvi kuzungumza na kukabidhi injini tatu za boti zenye uwezo wa nguvu ya farasi 15. Hafla hii imefanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022)


Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani kutoka Sekta ya Uvuvi, Prof. Mohammed Sheikh akielezea uwezo wa Injini tatu za Boti ambazo zina uwezo wa nguvu ya farasi 15 wakati wa hafla ya kukabidhi injini hizo. Lakini pia alisema kuwa mpaka sasa Wizara imeshanunua jumla ya injini za boti 26. Hafla hii imefanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022)


Mbunge wa Mtwara Mjini, Mhe. Hassan Mtenga (Mb) akiishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi) kwa kulipatia Jimbo lake la Mtwara Mjini Injini moja ya Boti yenye uwezo wa nguvu ya farasi 15 wakati wa hafla ya kukabidhi injini hizo, ambapo amesema hayo yote yamewezekana kutokana na kuwepo kwa uongozi sikivu na wenye mshikamano. Hafla hii imefanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022)


Mbunge wa Kalenga, Mhe. Jackson Kiswaga (Mb) akiipongeza Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi) kwa kuipatia Jimbo lake la Pangani Injini moja ya Boti yenye uwezo wa nguvu ya farasi 15 wakati wa hafla ya kukabidhi kwa kuwa itakwenda kuwasaidia wavuvi katika shughuli zao za uvuvi lakini pia katika kulinda rasilimali za uvuvi. Hafla hii imefanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022)



Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (kulia) akimkabidhi injini ya boti Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso (kushoto) aliyeipokea kwa niaba ya wananchi wa Pangani wakati wa hafla ya kukabidhi injini hizo iliyofanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (kulia) akimkabidhi injini ya boti Mbunge wa Kalenga, Mhe. Jackson Kiswaga (kushoto) aliyeipokea kwa niaba ya wananchi wa Pangani wakati wa hafla ya kukabidhi injini hizo iliyofanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022)



Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (kulia) akimkabidhi injini ya boti Mbunge wa Mtwara Mjini, Mhe. Hassan Mtenga (kushoto) aliyeipokea kwa niaba ya wananchi wa Pangani wakati wa hafla ya kukabidhi injini hizo iliyofanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022)




Picha ya pamoja ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (wa nne kutoka kushoto), Waziri wa Maji, Jumaa Aweso (wa tatu kutoka kulia) Waheshimiwa Wabunge wa Majimbo ya Mtwara Mjini na Kalenga na Watendaji wa Sekta ya Uvuvi mara baada ya kukabishi injini tatu za boti zenye uwezo wa nguvu ya farasi 15. Hafla hii imefanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo kwenye jengo la Benki ya NBC Jijini Dodoma. (24.06.2022)


Ijumaa, 24 Juni 2022

VIJANA KUWEZESHWA UFUGAJI KIBIASHARA

Na Mbaraka Kambona,


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega ameitaka taasisi ya Utafiti wa Mifugo(TALIRI) na taasisi inayoshughulika na kilimo biashara(PASS) kupitia mradi wanaoutekeleza wa  kunenepesha mbuzi kuhakikisha vijana wengi wanapata ujuzi huo ili waweze kuwa na fursa pana ya ajira na kukuza uchumi wao .


Ulega alitoa maelekezo hayo katika kikao kazi cha kupata taarifa ya utekelezaji wa mradi wa kunenepesha mbuzi unaotekelezwa kwa ushirikiano na taasisi hizo mbili kilichofanyika jijini Dodoma Juni 22, 2022.


Alisema mradi huo ni lazima ujikite katika kuwasaidia vijana wengi kupata ujuzi wa kufuga kibiashara na kuwawekea mfumo mzuri utakaowasaidia kuwezeshwa kifedha ili wawe na mitaji ya kutosha kuendesha biashara ya mifugo.


“Tunataka tutoe ajira kwa vijana, hivyo ni lazima kuwatengeneza vijana wengi watakaokuwa na ujuzi wa kunenepesha mifugo, sasa hivi wanaofanya unenepeshaji wapo na wanawezeshwa na benki zetu, lakini tunataka tupate vijana wengi zaidi watakaotengenezwa kupitia mradi huu, tukiweka nguvu yetu hapo vizuri naamini tutawezesha vijana wengi kujiajiri,”alisema


Aidha, aliongeza kwa kusema kuwa sasa sekta ya mifugo inakabiliwa na changamoto kubwa ya malisho  hivyo ni muhimu wakajikita katika kuzalisha malisho ili mifugo iwe na malisho ya kutosha wakati wote jambo litakalopelekea mifugo hiyo kuwa na uzito wenye thamani sokoni.


"Katika taarifa zenu nimewasikia hapa mmeeleza mambo mengi mnayotarajia kufanya kupitia mradi mnaotekeleza, ushauri wangu ni muhimu mkachagua mambo machache mtakayoweza kutekeleza vizuri awamu kwa awamu kuliko kubeba mambo mengi na mwisho wa siku msiweze kufikia malengo," alisema Ulega


Kufuatia changamoto ya kufa kwa mifugo iliyoikumba nchi hivi karibuni aliwataka wao kama Wataalamu kuhakikisha wanatumia taaluma zao kikamilifu ili kupunguza vifo vya mifugo nchini.


Halikadhalika aliitaka Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) kusaidia wadau hao wa sekta ya mifugo kwa kuandaa mipango mizuri ya biashara na kutoa mikopo nafuu kwa wafugaji ili waweze kufanya ufugaji wenye tija. 


Naye, Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani, Dkt. Angelo Mwilawa alisema kuwa kwa muda sasa viwanda vingi vya kuchakata nyama hapa nchini vimekuwa vikifanya kazi chini ya uwezo wake hivyo kupitia mradi huo unaotekelezwa na TALIRI kwa kushirikiana na PASS ukisimamiwa vizuri utakwenda kuwa sehemu ya utatuzi wa changamoto hiyo.


Aliongeza kwa kusema kuwa mradi huo pia utashirikisha Halmashauri nchini ili vijana waliopo katika maeneo hayoo waweze kushirikishwa vizuri katika kujifunza unenepeshaji wa mifugo na kuboresha maisha yao.


Mradi  huo wa kunenepesha mbuzi umeanzishwa mahsusi kwa lengo la kuwaanda na kuwawezesha vijana kushiriki mafunzo ya ujasiriamali kwa vitendo ili hatimaye kuwekeza kwenye ufugaji kibiashara na kuongeza fursa za ajira kupitia sekta ya mifugo nchini.



TARILI, PASS WATAKIWA KUWA NA VIPAUMBELE VICHACHE

Na Mbaraka Kambona,


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega ameitaka taasisi ya Utafiti wa Mifugo(TALIRI) na taasisi inayoshughulika na kilimo biashara(PASS) kuhakikisha wanakuwa na  vipaumbele vichache watakavyoweza kutekeleza vyema ili mradi wa kunenepesha mbuzi wanaoutekeleza uweze kufikia malengo waliyokusudia.


Ulega alitoa maelekezo hayo katika kikao kazi cha kupata taarifa ya utekelezaji wa mradi wa kunenepesha mbuzi unaotekelezwa kwa ushirikiano na taasisi hizo mbili kilichofanyika jijini Dodoma Juni 22, 2022.


Alisema kwa sasa sekta ya mifugo inakabiliwa na changamoto kubwa ya malisho na uhaba wa malighafi zinazotokana na mifugo hivyo ni muhimu wakajikita katika kuzalisha malisho ili mifugo iwe na malisho ya kutosha wakati wote jambo litakalopelekea mifugo hiyo kuwa na uzito na kuwa na thamani sokoni.


"Katika taarifa zenu nimewasikia hapa mmeeleza mambo mengi mnayotarajia kufanya kupitia mradi mnaotekeleza, ushauri wangu ni muhimu mkachagua mambo machache mtakayoweza kutekeleza vizuri awamu kwa awamu kuliko kubeba mambo mengi na mwisho wa siku msiweze kufikia malengo," alisema Ulega


Aliongeza kwa kuwahimiza kujikita hasa katika unenepeshaji wa mbuzi na uzalishaji wa malisho huku akiwataka kutumia utaalamu wao kufundisha vijana ufugaji wa biashara ili waweze kujiajiri na kujiongezea kipato.


Aidha, kufuatia changamoto ya kufa kwa mifugo iliyoikumba nchi hivi karibuni aliwataka wao kama Wataalamu kuhakikisha wanatumia taaluma zao kikamilifu ili kupunguza vifo vya mifugo nchini.


Halikadhalika aliitaka Benki ya Maendeleo ya Kilimo(TADB) kusaidia wadau hao wa sekta ya mifugo kwa kuandaa mipango mizuri ya biashara na kutoa mikopo nafuu kwa wafugaji ili waweze kufanya ufugaji wenye tija. 


Naye, Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani, Dkt. Angelo Mwilawa alisema kuwa kwa muda sasa viwanda vingi vya kuchakata nyama hapa nchini vimekuwa vikifanya kazi chini ya uwezo wake hivyo kupitia mradi huo unaotekelezwa na TALIRI kwa kushirikiana na PASS ukisimamiwa vizuri utakwenda kuwa sehemu ya utatuzi wa changamoto hiyo.


Aliongeza kwa kusema kuwa mradi huo pia utashirikisha Halmashauri nchini ili vijana waliopo katika maeneo hayoo waweze kushirikishwa vizuri katika kujifunza unenepeshaji wa mifugo na kuboresha maisha yao.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (kulia) akiongea katika kikao kazi cha kupata taarifa ya utekelezaji wa mradi wa kunenepesha mbuzi unaotekelezwa na taasisi ya Utafiti wa Mifugo(TALIRI) na taasisi inayojishughulisha na masuala ya kilimo biashara(PASS) katika kituo cha Kongwa kilichofanyika jijini Dodoma Juni 22, 2022. Katika kikao hicho Mhe. Ulega alizitaka taasisi hizo kuhakikisha zinajikita katika vipaumbele vichache vinavyoweza kupimika na kuleta tija inayotarajiwa.

Mkurugenzi, Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani (sekta ya Mifugo), Dkt. Angelo Mwilawa (kushoto) akieleza kwa ufupi lengo la kikao  kazi cha kupata taarifa ya utekelezaji wa mradi wa kunenepesha mbuzi unaotekelezwa na taasisi ya Utafiti wa Mifugo(TALIRI) na taasisi inayojishughulisha na masuala ya kilimo biashara(PASS) katika kituo cha Kongwa kilichofanyika jijini Dodoma Juni 22, 2022.

Kaimu Mkurugenzi, Idara ya Sera na Mipango (sekta ya mifugo), Bw. Mbaraka Stambuli akifafanua jambo katika kikao kazi cha kupata taarifa ya utekelezaji wa mradi wa kunenepesha mbuzi unaotekelezwa na taasisi ya Utafiti wa Mifugo(TALIRI) na taasisi inayojishughulisha na masuala ya kilimo biashara(PASS) katika kituo cha Kongwa kilichofanyika jijini Dodoma Juni 22, 2022.

Pichani ni Sehemu ya washiriki wa kikao kazi cha kupata taarifa ya utekelezaji wa mradi wa kunenepesha mbuzi unaotekelezwa na taasisi ya Utafiti wa Mifugo(TALIRI) na taasisi inayojishughulisha na masuala ya kilimo biashara(PASS) katika kituo cha Kongwa kilichofanyika jijini Dodoma Juni 22, 2022.


MIFUGO NA UVUVI YATUNUKIWA TUZO YA UTAWALA BORA

Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Mifugo) imeshika nafasi ya pili kwenye tuzo za Utawala Bora zinazotolewa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kufanya vizuri kwenye upande wa utendaji bora katika utoaji wa huduma kwa watumishi na wananchi kwa mwaka wa fedha 2021/2022.


Akipokea tuzo hiyo kwenye ofisi za Wizara zilizopo Mtumba Jijini Dodoma Juni 21, 2022 Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Mifugo, Bwana Tixon Nzunda alisema kuwa tuzo hiyo imepatikana kutokana na ushirikiano mkubwa ulipo katika kufanya kazi kama timu, kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji kwa umma.


“Nitumie fursa hii kuwashukuru watumishi wote wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuwezesha tuzo hii kupatikana, tumefanyiwa tathimini kwenye eneo la utawala bora ambapo tumeshika nafasi ya pili, tuchukue hii kama changamoto kwa kufanya vizuri zaidi kwenye tuzo zingine,” 


“Nishani hii ni kama chachu ya kufanya mabadiliko makubwa ili mwaka ujao tusiongoze tu kwenye masuala ya utawala bora, masuala ya ushughulikiaji wa malalamiko, taarifa za watumishi, lakini pia tuwe vinara katika kusimamia miradi ya maendeleo katika sekta zetu, kuanzia minada, mabwawa, visima, majosho, ufuatiliaji wa miradi na kuhakikisha kwamba thamani ya fedha ya miradi yetu inapatikana.” Alisema Bwana Nzunda


Akiongea kwenye makabidhiano ya Tuzo hiyo, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Sekta ya Mifugo, Dtk. Charles Mhina alisema tuzo hiyo ya Utendaji Bora imetolewa Mei 27, 2022 kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Mifugo) kwa kufanya vizuri kwenye uingizwaji wa taarifa sahihi katika mfumo wa taarifa za utumishi na mishahara. 


Vigezo vingine ni pamoja na uhuishaji wa taarifa kwenye mfumo kwa wakati, ushughulikiaji wa malalamiko ya watumishi na wananchi kwa wakati, kuzingatia na kutekeleza sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma na sheria mbalimbali za nchi katika kazi zote za kila siku.


Tuzo hizi za Utawala Bora zinazotolewa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kila mwaka na zinajumuisha wizara zote zilizopo Tanzania bara ambapo nafasi ya kwanza imechukuliwa na Ofisi ya Rais Ikulu, nafasi ya pili imechukuliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi na nafasi ya tatu imechukuliwa na  Wizara ya Fedha na Mipango.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughurikia Sekta ya Mifugo, Bwana Tixon Nzunda (aliyeshika Tuzo) akiongea na baadhi ya watumishi kwenye ofisi za Wizara zilizopo Mtumba Jijini Dodoma mara baada ya kukabidhiwa Tuzo ya mshindi wa pili ya Utawala Bora iliyotolewa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kufanya vizuri kwenye upande wa utendaji bora katika utoaji wa huduma kwa watumishi na wananchi kwa mwaka wa fedha 2021/2022,  Juni 21, 2022.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dtk. Charles Mhina (kushoto) akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Mifugo Bwana Tixon Nzunda kuhusu vigezo vilivyotumiwa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwenye utoaji wa Tuzo za Utawala bora na kupelekea Wizara ya Mifugo na Uvuvi kushika nafasi ya pili kwa mwaka wa fedha 2021/2022, kwenye ofisi za Wizara zilizopo Mtumba Jijini Dodoma Juni 21, 2022.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Mifugo Bwana Tixon Nzunda akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watumishi kwenye ofisi za Wizara zilizopo Mtumba Jijini Dodoma mara baada ya kukabidhiwa Tuzo ya mshindi wa pili ya Utawala Bora iliyotolewa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kufanya vizuri kwenye upande wa utendaji bora katika utoaji wa huduma kwa watumishi na wananchi kwa mwaka wa fedha 2021/2022, Juni 21, 2022.


KAMATI YA BUNGE YA KILIMO MIFUGO NA MAJI YAITAKA NAIC KUTOA ELIMU NA UHAMASISHAJI WA UHIMILISHAJI MBEGU BORA ZA MIFUGO

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, Dkt. Christine Ishengoma amekitaka Kituo cha Taifa cha Uhimilishaji (NAIC) kutoa elimu na uhamasishaji juu ya umuhimu na faida za kufanya uhimilishaji ili kuweza kupata mifugo na mazao bora ya mifugo.

Maelekezo hayo yametolewa leo Juni 18, 2022 wakati wa ziara ya kamati hiyo iliyotembelea kituo hicho pamoja na Chuo cha Mafunzo ya Mifugo Kampasi ya Tengeru mkoani Arusha ambapo walisema kuwa pamoja na kituo hicho kuwa cha muda mrefu na kuwa na matawi katika Kanda mbalimbali bado mwamko wa wafugaji katika kufanya uhimilishaji ni mdogo kutoka na wafugaji kukosa elimu sahihi juu ya suala hilo.

Dkt. Ishengoma alisema kuwa kamati wametembelea na wameona teknolojia ya hali ya juu na yenye manufaa kwa wafugaji iliyopo katika kituo hicho lakini changamoto iliyopo ni mwitikio mdogo wa wafugaji katika kutumia teknolojia hiyo.

“Tumeona kuanzia ukusanyaji wa mbegu na jinsi zinavyofanyiwa vipimo lakini pia tumeelezwa kila dume na aina ya mbegu yake ambapo sasa kinachotakiwa ni elimu na uhamasishaji kwa wafugaji ilib waweze kuitikia jambo hili la uhimilishaji na kuweze kubadilisha na kuboresha mifugo yao na kuboresha mazao yao,” alisema Dkt. Ishengoma.

Mbunge wa Moshi Vijiji, Profesa Patrick Ndakidemi alisema kuwa hali ni mbaya kwa wafugaji katika majimbo yao hivyo kwa mbegu walizoziona katika kituo hicho ni vema wagani wakawafikia wafugaji na kuwapa elimu juu ya teknolojia hiyo  ili waweze kuboresha mifugo yao.

“Kusema ukweli hali ni mbaya huko kuna maeneo mengine ambayo hawataamini kuwa tuna kitu kikubwa hivi ambacho kinaweza kutoa huduma nchi nzima kwahiyo langu kubwa na muomba Mhe. Waziri na timu yake ya wataalamu kuboresha shughuli za ugani juu ya uhimishaji ili iweze kuwafikia wafugaji huko waliko, tuweze kuboresha wale Ng'ombe wa kienyeji kwani bila ugani mambo hayataenda vizuri,” alisema Profesa Ndakidemi.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega alisema kuwa pamoja na kuwa na mifugo wengi nchini lakini kuna wakati viwanda vinakosa usambazaji hivyo wizara kwa sasa ina mpango wa kwenda kuzungumza na wafugaji ili waipokee teknolojia hiyo ya uhimilishaji lakini pia kutoa mafunzo wa wataalam wa mifugo ili waweze kazi ya uhimilishaji iweze kufanyika kwa kuzingatia utaalam.

“Lakini pia tutaviongezea vituo hivi nguvu ili kuweza kuboresha zaidi kwasababu vimechoka lakini pia kuendelea kufanya tafiti za kina ili kuweza kupata matokeo mazuri zaidi kulingana na aina ya Ng'ombe lengo likiwa ni kuboresha mifugo yetu hapa nchini lakini pia na vipato vya wafugaji,” Alisema Ulega.

Vilevile Wizara kupitia kupitia Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo hapa nchini imepanga kutoa mafunzo ili wahitimu katika vyuo hivyo waweze kujiajiri kwenye ufugaji na sio kutegemea kuajiriwa. wajasiriamali wa mifugo na uvuvi lakini pia

Awali akisoma taarifa Kaimu Mkurugenzi wa Kituo cha Taifa cha Uhimilishaji (NAIC), Dkt. Dafay Bura alisema kuwa lengo la kuanzishwa kwa huduma ya uhimishaji ni kusambaza mbegu bora zitakazoweza kuongeza uzalishaji wa nyama na maziwa ili kuinua pato la mfugaji na taifa kwa ujumla pamoja na kuimarisha lishe.

Dkt Bura alisema uhimilishaji huo unasaidia kuongeza uzalishaji wa Ng'ombe wa kisasa, kuinua kiwango cha Ng'ombe wa asili pamoja na kuokoa fedha za kigeni ambazo zingetumika kuagiza nje ya nchi mazao yatokanayo na mifugo kama vile nyama na maziwa.

“Uhimilishaji huu una faida nyingi mojawapo ni kuzuia kuenea kwa magonjwa ya vizazi, kupunguza gharama za kutunza madume, kuepukana na hatari za madume kujeruhiwa, kupata ndama wengi kutoka kwa dume bora, kutumia mbegu za dume bora kwa muda mrefu hata kama amevunjika au amekwisha kufa pamoja na kuwa na wigo mpana wa aina ya mbegu unayohitaji,” Alisema Dkt Bura.

“Tuna jumla ya madume ya Ng'ombe 33 ambapo kutokana na takwimu za Ng'ombe nchini kuwa kubwa wizara kwa kushirikiana na kituo hiki tuanendelea na uhamasishaji wa shughuli za uhimilishaji  kupitia programu maalum ya jambo ya uhimilishaji katika halmashauri mbalimbali na kwa mwaka wa fedha 2021/2022 zaidi ya Ng'ombe 3000 walihimishwa bure ikiwemo wilaya ya Ngorongoro, Pangani, Muweza, Lushoto na Mkinga lakini pia bado tunakabiliwa na changamoto ya mwitikio mdogo wa wafugaji hivyo tunahitaji kufanya kazi zaidi ili kukuza uelewa kuhusu manufaa ya uhimishaji,” Alisema.

Naye mtendaji mkuu wa wakala wa mafunzo ya mifugo (LITA), Dkt. Pius Mwambele akisoma taarifa ya chuo hicho alisema kuwa chuo kina wajibu wa kuchangia upatikanaji wa wataalamu wa mifugo nchini kwani waliopo ni 3800 huku mahitaji yakiwa ni 17,400 lakini pia kuwezesha umahiri wa ujasiriamali kwa vijana ili waweze kujiajiri pamoja na kuongeza upatikanaji wa mbegu na bidhaa bora za mifugo kwa ajili ya kuwahudumia jamii ya watanzania.


“Mafanikio tuliyonayo ni pamoja na kuongezeka kwa udahili kutoka 798 mwaka 2012/2013 hadi kufikia 3,972 ya mwaka 2021/2022 pamoja na kuongezeka kwa mapato ya ndani kutoka bilioni 3 hadi bilioni 4.7 lakini pia tunakabiliwa na changamoto miundombinu mibovu ya madarasa na mabweni kutokana na uchakavu,” alisema Dkt Mwambele.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, Mhe. Dkt. Christine Ishengoma (Mb) akiwasalimu Viongozi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi pamoja na Mkoa wa Arusha mara baada ya kufika kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwa ajili ya kusaini kitabu cha wageni. Kulia kwake ni Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega na kushoto kwake ni Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Mhe. Mhandisi Richard Ruyango. Kushoto ni Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Charles Mhina. (18.06.2022)

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (Mb) akizungumza kwenye kikao kifupi na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji wakati kamati hiyo ilipotembelea Chuo cha Mafunzo ya Mifugo Kampasi ya Tengeru ambapo amewaeleza wajumbe hao kuwa Serikali imepanga kutoa mafunzo yatakayowasaidia wahitimu kwenda kujiajiri na sio kutegemea kuajiriwa. Kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Christine Ishengoma (Mb) na kulia ni Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Charles Mhina. (18.06.2022)


Wataalam kutoka Kituo cha Taifa cha Uhimilishaji (NAIC) wakitoa maelezo juu ya namna kituo hicho kinavyofanya kazi kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji wakati kamati hiyo ilipotembelea kituoni hapo kwa lengo la kuona namna kinavyofanya kazi. (18.06.2022)


Viongozi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji wakifuatilia maelekezo yaliyokuwa yanatolewa na wataalam wa Kituo cha Taifa cha Uhimilishaji (hawapo pichani) wakati kamati hiyo ilipoingia kwenye maabara ya iliyopo hapo kituoni kwa lengo la kuona jinsi maabara hiyo inavyofanya kazi. (18.06.2022)


Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo (LITA), Dkt. Pius Mwambene (kushoto) akitoa maelezo kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji wakati kamati hiyo ilipotembelea Kumbi za Mihadhara zilizojengwa kwenye Chuo cha Mafunzo ya Mifugo Kampasi ya Tengeru. (18.06.2022)

Viongozi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo (LITA), Dkt. Pius Mwambene (kushoto) wakati kamati hiyo ilipotembelea maabara zilizopo kwenye Chuo cha Mafunzo ya Mifugo Kampasi ya Tengeru. (18.06.2022)