Nav bar

Ijumaa, 29 Julai 2022

SERIKALI YATAMBUA MCHANGO WA WANAWAKE SEKTA YA UVUVI

Serikali imesema wanawake wamekuwa na mchango mkubwa katika kusimamia rasilimali za uvuvi na wamekuwa wadau wakubwa katika kuhakikisha kuwa, biashara ya mazao ya uvuvi inaimarika ndani na nje ya nchi.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Msaidizi anayesimamia suala la udhibiti ubora wa Mazao ya uvuvi na masoko, Bw. Steven Lukanga kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah wakati akizindua mtandao wa wanawake, wanaojihusisha na Shughuli za Uvuvi Tanzania (TAWFA) Kanda ya Ziwa Tanganyika ambapo amewataka wanawake kufanya kazi kwa kushirikiana ili kuwa na sauti moja itakayowasaidia katika kutatua changato mbalimbali, Julai 27,2022 Mkoani Kigoma.
Alisema mchango huo wa wanawake unastahili kupewa thamani kubwa hasa katika kuweka mikakati ya kusimamia changamoto zao ikiwemo kuanzisha Dawati la Jinsia la Uvuvi Wizarani ili shughuli za masuala ya wanawake ziweze kuratibiwa.
“ninatambua kuwa wanawake wamejiunga katika vikundi mbalimbali ambavyo vinarahisisha utendaji wa shughuli zao za uvuvi na shughuli nyingine katika mnyororo wa thamani, pamoja na hayo vikundi hivi vinakabiliwa na changamoto kama upatikanaji wa masoko, taarifa mbalimbali za bei ambapo shughuli zao zina kuwa ngumu ” alisema Bw. Lukanga
Aidha alisema Wizara imeweka juhudi katika kutatua changamoto mbalimbali za wadau wa Sekta ya Uvuvi ili kuongeza mchango wa Sekta kwenye uchumi wa nchi ili kuboresha mazingira ya kufanya biashara za mazao ya uvuvi, kuzuia uvuvi haramu, kuzuia utoroshwaji holela wa rasilimali za uvuvi, na kuwezesha uvuvi endelevu.
Aliongeza kuwa Juhudi hizi zinalenga kuwezesha wafanyabiashara wa mazao ya uvuvi ambao 50% ni wanawake ili waweze kuhimili ushindani wa kibiashara ndani na nje ya nchi na kuwashukuru shirika la FAO kupitia Mradi wa Fish4ACP unaotekeleza mradi na kuimarisha Mnyororo wa thamani katika Ziwa Tanganyika.
“Juhudi hizo zote, zinalenga kuwaunganisha wanawake wa Tanzania nzima, kupitia vikundi vyao Ili kuwa na sauti ya pamoja, kubadilishana mawazo na uzoefu katika kupata uhakika wa masoko kupitia mtandao huu pamoja na mambo mengine.”
Naye Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia uendelezaji wa rasilimali za uvuvi Bi. Merisia Palazo alisema wanawake wote wanaojishughulisha katika mnyororo wa Uvuvi wanatambulika na ndio maana kukawa na jukwaa linalowawezesha kuelezea mambo yao mbalibali yanayowakabili.
Aidha Mratibu wa Sekta ya Uvuvi Kitaifa kutoka Shirika la chakula na kilimo la umoja wa Mataifa (FAO), Bi. Oliva Mkumbo alisema lengo la kuanzishwa kwa jukwaa hilo ni kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia uvuvi ili kuinua kipato cha familia na kuondokana na umasikini.
Aliongeza kuwa kutokana na mchango mkubwa wa kina mama katika shughuli za kiuchumi mradi huo unalenga kumgusa kila mwanamke huku akisema kama shirika litaendelea kufungua matawi katika maeneo mbalimbali na hatimaye sekta ya uvuvi kuwa yenye tija.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanawake Wanaojihusisha na Shughuli za Uvuvi Tanzania (TAWFA), Kitaifa Beatrice Mmbaga alieleza kuwa kuzinduliwa kwa jukwaa hilo ni sehemu ya kutatua changamoto zinazowakabili kina mama katika nyanja ya uvuvi.


Mwenyekiti wa Kikosi Kazi cha Kitaifa kinachoratibu Muongozo wa Kuendeleza Uvuvi Mdogo nchini, Bw. Yahaya Mgawe ( wa pili kulia) akieleza jambo alipotembelea na kuona kazi zinazofanyika katika Mwalo wa Kibirizi mkoani Kigoma, Julai 28, 2022


Baadhi ya wanachama wa Mtandao wa Wanawake wanaojihusisha na Shughuli za Uvuvi Tanzania (TAWFA) wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wao mara baada ya kutembelea Mwalo wa Kibirizi mkoani Kigoma kujionea shughuli zinazofanyika katika Mwalo huo, Julai 28, 2022.

​SERIKALI YATAMBUA MCHANGO WA WANAWAKE SEKTA YA UVUVI

 Serikali imesema wanawake wamekuwa na mchango mkubwa katika kusimamia rasilimali za uvuvi na wamekuwa wadau wakubwa katika kuhakikisha kuwa, biashara ya mazao ya uvuvi inaimarika ndani na nje ya nchi.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Msaidizi anayesimamia suala la udhibiti ubora wa Mazao ya uvuvi na masoko, Bw. Steven Lukanga kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah wakati akizindua mtandao wa wanawake, wanaojihusisha na Shughuli za Uvuvi Tanzania (TAWFA) Kanda ya Ziwa Tanganyika ambapo amewataka wanawake kufanya kazi kwa kushirikiana ili kuwa na sauti moja itakayowasaidia katika kutatua changato mbalimbali, Julai 27,2022 Mkoani Kigoma.

Alisema mchango huo wa wanawake unastahili kupewa thamani kubwa hasa katika kuweka mikakati ya kusimamia changamoto zao ikiwemo kuanzisha Dawati la Jinsia la Uvuvi Wizarani ili shughuli za masuala ya wanawake ziweze kuratibiwa.

“ninatambua kuwa wanawake wamejiunga katika vikundi mbalimbali ambavyo vinarahisisha utendaji wa shughuli zao za uvuvi na shughuli nyingine katika mnyororo wa thamani, pamoja na hayo vikundi hivi vinakabiliwa na changamoto kama upatikanaji wa masoko, taarifa mbalimbali za bei ambapo shughuli zao zina kuwa ngumu ” alisema Bw. Lukanga

Aidha alisema Wizara imeweka juhudi katika kutatua changamoto mbalimbali za wadau wa Sekta ya Uvuvi ili kuongeza mchango wa Sekta kwenye uchumi wa nchi ili kuboresha mazingira ya kufanya biashara za mazao ya uvuvi, kuzuia uvuvi haramu, kuzuia utoroshwaji holela wa rasilimali za uvuvi, na kuwezesha uvuvi endelevu.

Aliongeza kuwa Juhudi hizi zinalenga kuwezesha wafanyabiashara wa mazao ya uvuvi ambao 50% ni wanawake ili waweze kuhimili ushindani wa kibiashara ndani na nje ya nchi na kuwashukuru shirika la FAO kupitia Mradi wa Fish4ACP unaotekeleza mradi na kuimarisha Mnyororo wa thamani katika Ziwa Tanganyika.

“Juhudi hizo zote, zinalenga kuwaunganisha wanawake wa Tanzania nzima, kupitia vikundi vyao Ili kuwa na sauti ya pamoja, kubadilishana mawazo na uzoefu katika kupata uhakika wa masoko kupitia mtandao huu pamoja na mambo mengine.”

Naye Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia uendelezaji wa rasilimali za uvuvi Bi. Merisia Palazo alisema wanawake wote wanaojishughulisha katika mnyororo wa Uvuvi wanatambulika na ndio maana kukawa na jukwaa linalowawezesha kuelezea mambo yao mbalibali yanayowakabili.

Aidha Mratibu wa Sekta ya Uvuvi Kitaifa kutoka Shirika la chakula na kilimo la umoja wa Mataifa (FAO), Bi. Oliva Mkumbo alisema lengo la kuanzishwa kwa jukwaa hilo ni kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia uvuvi ili kuinua kipato cha familia na kuondokana na umasikini.

Aliongeza kuwa kutokana na mchango mkubwa wa kina mama katika shughuli za kiuchumi mradi huo unalenga kumgusa kila mwanamke huku akisema kama shirika litaendelea kufungua matawi katika maeneo mbalimbali na hatimaye sekta ya uvuvi kuwa yenye tija.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanawake Wanaojihusisha na Shughuli za Uvuvi Tanzania (TAWFA), Kitaifa Beatrice Mmbaga alieleza kuwa kuzinduliwa kwa jukwaa hilo ni sehemu ya kutatua changamoto zinazowakabili kina mama katika nyanja ya uvuvi.



​HOMA YA MGUNDA ISIWE KIKWAZO CHA KUTOKULA NYAMA

Na. Edward Kondela


Serikali imesema ugonjwa wa Homa ya Mgunda usiwe kikwazo cha watanzania kutokula nyama na kwamba asilimia tisini ya nyama inayopitia kwenye machinjio rasmi iko salama.


Akizungumza jijini Dodoma (27.07.2022) kupitia vyombo mbalimbali vya habari, Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Hezron Nonga amesema, nyama ya mnyama anayechinjwa kwenye machinjio rasmi huwa inakaguliwa na mtaalamu wa mifugo wa serikali kabla ya kwenda sokoni ili kuepusha madhara yoyote kwa binadamu.


Prof. Nonga amebainisha kuwa kutokana na utafiti uliofanywa umebaini kuwa mnyama ambaye ameathirika na vimelea vya ugonjwa wa Homa ya Mgunda akitolea mfano wa ng’ombe, nyama yake inakuwa na rangi ya njano hivyo ni rahisi kwa mtaalam wa mifugo kubaini nyama hiyo machinjioni na kutoruhusu kupelekwa sokoni.


“Kuchinja mifugo kwenye machinjio na nyama ikaguliwe na daktari au mtaalamu wa mifugo wa serikali kwa kuwa tushaona ng’ombe akipata shida ya Homa ya Mgunda, nyama yake inakuwa na rangi ya njano hivyo mtaalam atagundua kuwa haifai kwa matumizi ya binadamu, hivyo watanzania watakuwa salama.” Amesema Prof. Nonga


Ameongeza kuwa njia nyingine ya watanzania kujikinga na ugonjwa wa Homa ya Mgunda ni kuhakikisha nyama inapikwa vyema na kuiva ili kuua vimelea vya ugonjwa huo ambavyo vinaishi kwenye majimaji ya mnyama ambaye ameathirika, ukiwemo mkojo na kinyesi chake.


Aidha, Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Hezron Nonga amewataka watanzania kutokula nyama ya wanyama wasiyo rasmi kwenye chakula akiwemo panya kwa kuwa amebainika kuwa ni moja ya wanyama ambao wanahusishwa kwa kiasi kikubwa kubeba vimelea vya ugonjwa wa Homa ya Mgunda na magonjwa mengine.


Amefafanua kuwa ulaji wa nyama ni muhimu katika mwili wa binadamu kwa kuwa ni chanzo cha Protein katika daraja la kwanza ikiwa ni pamoja na kinga mwilini, hivyo watanzania wanatakiwa kula nyama iliyo rasmi katika kundi la chakula, kununua nyama iliyokaguliwa na mtaalamu wa mifugo wa serikali kwenye machinjio rasmi pamoja na kuipika nyama hiyo vyema na kuiva ili kuua vimelea vya ugonjwa wa Homa ya Mgunda pamoja na magonjwa mengine.


Pia, amewaasa wafugaji kuhakikisha wanachanja mifugo yao dhidi ya magonjwa mbalimbali ukiwemo ugonjwa wa Homa ya Mgunda ambao umekuwepo kwa siku nyingi lakini umeanza kuonesha athari kwa binadamu.


Kwa upande wake Msajili wa Bodi ya Nyama Tanzania Dkt. Daniel Mushi amewatahadharisha watanzania wanaokula nyama kwenye maeneo mbalimbali yakiwemo ya starehe kuhakikisha nyama imechomwa na kukauka vizuri na kutokuwa na damu kwa kuwa ikipikwa vizuri hakuna sababu ya kuogopa ugonjwa wa Homa ya Mgunda kwa sababu vimelea vyake vinakufa kwenye mapishi yanayofikia nyuzi joto sabini (70).


Dkt. Mushi amewaasa pia watanzania kununua nyama kwenye maduka yaliyosajiliwa na kukaguliwa ambapo nyama iliyokaguliwa inakuwa na mhuri kwenye mguu wa nyuma wa mnyama na kuwataka kuacha kula nyama kutoka kwenye machinjio yasiyo rasmi yasiyoeleweka au nyama inayopatikana mitaani kwa bei nafuu kwa kuwa ni hatari kwa afya ya binadamu.


Ameongeza kuwa ni wajibu kwa watoa huduma kwenye maduka ya nyama kutakiwa kupimwa afya zao kila baada ya miezi sita ili wasiwe chanzo cha maradhi mengine kwa walaji wa nyama wanazouza.


Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Bodi ya Nyama Tanzania zimelazimika kutoa taarifa juu ya ugonjwa wa Homa ya Mgunda kwa nyama inayopatikana kutoka kwenye mifugo hapa nchini, kutokana na uwepo wa baadhi ya taarifa zisizo sahihi juu ya uwepo wa ugonjwa huo na ulaji wa nyama.

Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Hezron Nonga akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) jijini Dodoma na kuwaasa watanzania kuwa ugonjwa wa Homa ya Mgunda usiwe kikwazo kwao kula nyama bali wapate nyama kwenye machinjio rasmi ambapo nyama hizo zinakaguliwa na mtaalamu wa mifugo kutoka serikalini. (27.07.2022)


Msajili wa Bodi ya Nyama Tanzania Dkt. Daniel Mushi akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) jijini Dodoma na kuwashauri watanzania wapate nyama kwenye machinjio rasmi na ipikwe iive vyema kufikia nyuzi joto sabini (70) kabla ya kula ili kuua vimelea vya ugonjwa wa Homa ya Mgunda pamoja na kuhakikisha nyama wanayokula kwenye maeneo ya starehe inachomwa vizuri na kukaushwa damu yake. (27.07.2022)

SAUDI ARABIA YAKUSUDIA KUWEKEZA KWENYE RANCHI YA RUVU

Nchi ya Saudi Arabia kupitia  kampuni binafsi ya Kilimo ya “Crown” iliyopo nchini humo inakusudia kuwekeza kwenye ranchi ya Ruvu iliyopo mkoani Pwani ikiwa ni hatua ya awali kabla ya kujenga miundombinu ya kusindika mazao ya mifugo nchini.


Hayo yamebainishwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki muda mfupi baada ya kumalizika kwa kikao baina yake na Mkurugenzi Mtedaji  wa Kampuni hiyo Bw. Mohammad Iftikhar kilichofanyika leo (27.07.2022) kwenye Ofisi za Wizara hiyo zilizopo jijini Dar-es-salaam.


Mhe. Ndaki amebainisha kuwa ujio wa wawekezaji hao unatokana na uboreshwaji wa shughuli za ufugaji unaoendelea nchini ambao kwa kiasi kikubwa umechochea ongezeko la uzalishaji wa mazao ya nyama, maziwa na ngozi.


“Nimewaeleza wakutane na kampuni yetu ya ranchi za Taifa (NARCO) na leo mchana watakutana Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo na Mwenyekiti wa Bodi wa kampuni hiyo ili waweze kuzungumza kwa undani kwa sababu fursa za uwekezaji kwenye ranchi zetu za taifa ni nyingi na hata sasa tunafikiria tupate mwekezaji mwingine kwenye ranchi yetu ya Mzeri ambayo tumepanga iwe maalum kwa uwekezaji wa ng’ombe wa maziwa pekee” Amesema Mhe. Ndaki.


Mbali na ranchi za Ruvu na Mzeri, Mhe. Ndaki ameongeza kuwa Wizara yake  ipo mbioni kutafuta mwekezaji kwenye ranchi ya “Mwisa II” iliyopo Wilaya ya Muleba mkoani Kagera ambaye atawekeza kwa upande wa viwanda vya nyama, maziwa, chakula cha mifugo na uzalishaji wa malisho ya mifugo.


“Uwekezaji huo unaweza kuwa wa namna mbalimbali kwa sababu sisi tunayo ardhi tunaweza kuwapa kwa makubaliano maalum kisha wao wanaweza kujenga viwanda vya kuchakata nyama, kuzalisha vyakula vya mifugo, walime malisho na ikiwezekana wanaweza kunenepesha mifugo kwenye ranchi zote hizi ili hatimaye wauze wanyama hai au mazao yake” Amebainisha Mhe. Ndaki.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya kilimo ya “Crown” kutoka nchini Saudi Arabia Bw. Mohammad Iftikhar amesema kuwa uamuzi wao wa kuwekeza kwenye sekta ya Mifugo nchini unatokana na ongezeko la mahitaji ya nyama nchini Saudi Arabia na mazingira wezeshi ya uwekezaji yaliyopo nchini.


“Kwanza tumevutiwa na suala la NARCO kumilikiwa na serikali kwa asilimia 100 jambo ambalo linatoa fursa ya kupata wawekezaji stahiki wakati wote na tumepitia andiko linalohusu ranchi zote zilizopo hapa Tanzania na kuona tuanze na Ruvu kisha maeneo mengine yatafuata” Amesema Bw. Iftikhar.


Ujio wa wawekezaji hao ni muendelezo wa matunda yanayotokana na ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan aliyoifanya nchini humo wiki kadhaa zilizopita ambapo aliwaalika wafanyabiashara  mbalimbali kufika nchini na kuwekeza kwenye sekta mbalimbali za uzalishaji ili kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (kushoto) akimueleza Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya kilimo ya "Crown" kutoka nchini Saudi Arabia Bw. Mohammad Iftikhar yaliyomo kwenye andiko la Ranchi za Taifa (aliloshika Bw. Iftikhar) wakati wa kikao baina yao kilichofanyika leo (27.07.2022) kwenye Ofisi za Wizara hiyo zilizopo jijini Dar-es-salaam.


TAFITI KUBORESHA MAENDELEO YA SEKTA YA UVUVI

Tafiti zinazofanywa kwenye sekta ya uvuvi zinalenga kuhakikisha wadau wa sekta hiyo wanaboresha shughuli zao katika mnyororo wa thamani wa mazao ya uvuvi.

 

Hayo yamesemwa leo (25.07.2022) na mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Kayuni ambaye pia ni Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa sekta hiyo wakati akifungua mafunzo ya kuandaa vijarida sera yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro.

 

Bw. Kayuni amesema kuwa tafiti zinazofanyika ni lazima matokeo yake yawafikie walengwa ambao ni wadau wa sekta ya uvuvi ili kuweza kuwanufaisha na kuboresha shughuli wanazozifanya katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.

 

“Tafiti zinazofanyika ni lazima ziwafikie walengwa, kuzielewa na kuwasaidia kubalidilisha maisha yao katika shughuli wanazozifanyi, hapo tafiti hizo zinakuwa na tija katika kuleta maendeleo ya wadau wa sekta ya uvuvi na taifa kwa ujumla.” alisema Bw. Kayuni

 

Sekta ya Uvuvi imepanga kuzitumia tafiti zinazofanywa kwa lengo la kuboresha sera zinazohusu sekta ya uvuvi ili wadau wa sekta hiyo waweze kunufaika. Bw. Kayuni amesema kuwa tafiti zinazofanywa zikifanyiwa kazi zinawafanya watafiti kuendelea kufanya tafiti zaidi kwa lengo la kuboresha sekta ya uvuvi.

 

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Huduma za Ugani, Prof. Mohammed Sheikh amesema kuwa mafunzo hayo ni kwa ajili ya kusaidia kwenye kutunga sera na kufanya maamuzi ambayo yatasaidia kuipeleka sekta ya uvuvi mbele. Prof. Sheikh amesema Sekta ya Uvuvi imeamua kufanya mafunzo hayo kwa lengo la kuwajengea uwezo wataalam ili kuweza kuzitumia tafiti ambazo zimefanyika ili kuwaletea maendeleo wadau wa sekta hiyo. Pia amesema kuwa matarajio ya mafunzo hayo ni kuhakikisha kuwa tafiti mbalimbali zinazofanyika kuhusu sekta ya uvuvi kutobakia kwenye makaratasi badala yake kwenda kuwafikia wadau na kuleta maendeleo kwenye sekta ya uvuvi.

 

Meneja Seksheni ya Sayansi za Jamii (COSTECH), Bi. Hildegalda Mushi amesema kuwa taasisi yao inafanyakazi ya kuwezesha tafiti mbalimbali ambazo zinalenga kuwezesha maendeleo ya matokeo ya tafiti na kuwezesha maendeleo ya teknolojia. Tafiti hizi zinalengo la kuhakikisha kuwa wadau wa uvuvi wanasonga mbele kimaendeleo na kuhakikisha zinawasaidia watunga sera ili waweze kutunga sera ambazo zinatekelezeka kwa maendeleo ya wadau na taifa kwa ujumla.

 

Mafunzo hayo yamewahusisha wataalam kutoka Sekta ya Uvuvi, Taasisi ya Utafiti ya Uvuvi (TAFIRI), Wakala ya Mafunzo ya Uvuvi (FETA), na COSTECH ambapo washiriki wamepata fursa ya kujadili kwa kina juu ya matokeo ya tafiti zilizofanyika kwa maelengo ya kuipeleka mbele sekta ya uvuvi.


Mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Kayuni akifungua mafunzo ya kuandaa vijarida Sera ambapo amewasihi watafiti kuhakikisha matokeo ya tafiti zao yanakwenda kubadilisha maisha ya wadau waliopo kwenye mnyororo wa thamani wa mazao ya uvuvi. Mafunzo hayo yamefanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. (25.07.2022)

Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Huduma za Ugani, Prof. Mohammed Sheikh akiwasilisha mada ya utangulizi kwenye mafunzo ya kuandaa vijarida Sera yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. Prof. Sheikh amesema kuwa Sekta ya Uvuvi inaendelea kujipanga kuhakikisha matokeo ya tafiti yanakwenda kubadilisha maisha ya wadau wa sekta hiyo. (25.07.2022)


Meneja Seksheni ya Sayansi za Jamii kutoka COSTECH, Bi. Hildegalda Mushi akizungumza na washiriki wa mafunzo ya kuandaa vijarida Sera yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. (25.07.2022)


Baadhi ya Washiriki wa Mafunzo ya kuandaa viharida sera wakifuatilia mada zilizokuwa zinawasilishwa kwenye mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. (25.07.2022) 


Mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Kayuni akiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa Mafunzo ya kuandaa vijarida Sera mara baada ya kufungua mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. (25.07.2022)

Jumapili, 24 Julai 2022

VIFARANGA VYA KUKU KUTOKA NJE YA NCHI MWISHO JULAI 30

Na. Edward Kondela

 Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amesema baada ya tarehe 30 mwezi huu, hakuna vifaranga vya kuku vitakavyoingizwa hapa nchini na kwamba serikali haitoi tena vibali vya kuingiza vifaranga hivyo.

 Naibu Waziri Ulega amebainisha hayo (22.07.2022) jijini Dodoma wakati wa kikao cha wizara na wadau wa tasnia ya kuku, kujadili namna ya kukuza tasnia hiyo ambapo lengo la hatua hiyo ni utekelezaji wa sheria ya mwaka 2006 ambapo serikali imekuwa ikizuia uingizaji wa vifaranga nchini kutoka nje ya nchi ili kudhibiti ugonjwa wa mafua ya ndege kwa mifugo jamii ya ndege na kulinda wazalishaji wa kuku ndani ya nchi.

Akizungumza wakati akifunga kikao hicho kilichojadili ajenda mbalimbali zikiwemo za upatikanaji wa vifaranga vya kuku, chakula cha kuku na bei ya kuku sokoni, Mhe. Ulega amesema ni mategemeo kuwa serikali haitaona vifaranga vinaingizwa nchini kutoka nje ya nchi na kutaka kuwepo kwa mfumo wa taarifa zinazohusu wazalishaji wa vifaranga vya kuku kuanzia wazalishaji wakubwa hadi wadogo ambao wamesajiliwa na kutoa taarifa serikalini ili kuiwezesha kujua kiwango cha uzalishaji na kuwa na takwimu sahihi juu ya mahitaji ya vifaranga nchini.

“Ni mategemeo yetu ni kutokuona baada ya tarehe 30 mtu anaingiza vifaranga hapa nchini kutoka mahali popote pale, jambo la pili kuwepo na mfumo ambao utasaidia serikali kujua ni kiasi gani cha uzalishaji vifaranga ndani ya nchi yetu ili kujipima uwezo wetu na mahitaji yetu ndani ya nchi.” Amesema Mhe. Ulega

Awali Naibu Waziri Ulega akizungumza wakati akifungua kikao hicho cha wizara na wadau wa tasnia ya kuku amesema tasnia hiyo imekua kwa kasi miaka ya hivi karibuni kutokana na kuwepo kwa soko linalotokana na ongezeko la watu na kipato, ongezeko la uwekezaji na uwepo wa mazingira bora ya uwekezaji katika tasnia ya kuku, urahisi wa kufuga kuku na uwezekano mkubwa wa kuwamiliki kuliko wanyama wakubwa. 

Kwa upande wake Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Bw. Stephen Michael akizungumza kwenye kikao hicho amesema kutokana na umuhimu wa tasnia ya kuku katika Mpango Kabambe wa Sekta ya Mifugo wa Mwaka 2016 umefanya tathmini na kubainisha kuwa hadi kufikia Mwaka 2031 kutakuwa na upungufu wa nyama kwa tani milioni 1.8 hivyo tasnia ya kuku ni rahisi ikitiliwa mkazo itasaidia katika kuongeza uzalishaji wa nyama nchini.

Bw. Michael ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Masoko katika Wizara ya Mifugo na Uvuvi, amesema ufugaji wa kuku ni njia rahisi na ambayo haihitaji maeneo makubwa na miundombinu mingi tofauti na mifugo mingine hivyo kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kimeunganisha wadau wa tasnia hiyo pamoja na kutatua changamoto zilizopo kwa kuzingatia uwepo wa taasisi mbalimbali zinazotoa mikopo kwa vijana na akina mama na vikundi mbalimbali ambao wengi wamejizatiti katika biashara ya kuku.

Naye Katibu wa Chama cha Wadau wa Kuku Tanzania (PAT) Bw. Manase Mrindwa amebainisha changamoto za chakula cha kuku kuwa kimefikia hadi Shilingi Elfu 80 kwa mfuko mmoja kwa mwezi wa Julai ambapo kunatokana hasa na ongezeko la bei ya mahindi na mashudu ya soya kwenye soko la Tanzania.

Bw. Mrindwa amebainisha pia changamoto ya kutokea kwa uhaba wa vifaranga kwa wakati fulani wa mwaka, huku mitaani bado viko vifaranga visivyo bora ambavyo vinawafikia wafugaji hususan wafugaji wadogo.

Kikao cha wadau wa tasnia ya kuku kilichoandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kimejumuisha menejimenti ya wizara Sekta ya Mifugo, wazalishaji wa vifaranga vya kuku, chakula cha kuku na wafugaji wa kuku ambapo wametoa maoni mbalimbali ya namna ya kuboresha tasnia hiyo na kuomba kuwepo kwa vikao vya namna hiyo mara kwa mara lengo likiwa ni kukuza tasnia hiyo kwa kuirasimisha na kuwepo kwa machinjio maalum kwa ajili ya kuku na bei elekezi ya kuku sokoni.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb), akizungumza kwenye kikao cha wadau wa tasnia ya kuku kilichofanyika jijini Dodoma na kuweka wazi kuwa baada ya tarehe 30 mwezi huu, hakuna vifaranga vya kuku vitakavyoingizwa hapa nchini kutoka nje ya nchi na kwamba serikali haitoi tena vibali vya kuingiza vifaranga hivyo ili kuzuia ugonjwa mafua ya ndege na kulinda wazalishaji wa vifaranga wa ndani ya nchi. (22.07.2022)


Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Bw. Stephen Michael ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Masoko akizungumza kwenye kikao cha wadau wa tasnia ya kuku kilichofanyika jijini Dodoma ambapo amesema katika Mpango Kabambe wa Sekta ya Mifugo wa Mwaka 2016 umefanya tathmini na kuainisha kuwa hadi kufikia Mwaka 2031 kutakuwa na upungufu wa nyama kwa tani milioni 1.8 hivyo tasnia ya kuku ni rahisi ikitiliwa mkazo itasaidia katika kuongeza uzalishaji wa nyama nchini. (22.07.2022)


Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Sekta ya Mifugo Bw. Evance Ntiyalundura akiwa kwenye kikao cha wadau wa tasnia ya kuku jijini Dodoma ambapo amefafanua hatua mbalimbali katika kukuza tasnia hiyo ikiwemo ya kuimarisha ushirikiano baina ya serikali na wadau wa tasnia. (22.07.2022)


Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Hezron Nonga, akiwa mmoja wa washiriki katika kikao cha wadau wa tasnia ya kuku kilichofanyika jijini Dodoma na kuelezea umuhimu wa wadau kujisajili kwenye mfumo ili kutambulika kisheria na namna serikali inavyotoa vibali mbalimbali vya kusafirisha mifugo kikiwemo cha kuku. (22.07.2022)


Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji wa Nyanda za Malisho na Rasilimali za Vyakula vya Mifugo Dkt. Asimwe Rweguza akifafanua umuhimu wa matumizi ya vyakula bora vya mifugo hususan vya kuku na kuwakumbusha wazalishaji wa vyakula hivyo kutumia maabara ya Wakala ya Veterinari Tanzania (TVLA) kuhakiki ubora wa vyakula wakati aliposhiriki kikao cha wadau wa tasnia ya kuku kilichofanyika jijini Dodoma. (22.07.2022)


Msajili wa Bodi ya Nyama nchini Dkt. Daniel Mushi akitolea ufafanuzi ombi la wafugaji wa kuku kuwepo kwa machinjio ya kuku kila wilaya ili kuzuia uuzwaji holela wa kuku na kuwepo kwa bei elekezi ya kuku sokoni, wakati aliposhiriki kikao cha wadau wa tasnia ya kuku kilichofanyika jijini Dodoma. (22.07.2022)


Katibu wa Chama cha Wadau wa Kuku Tanzania (PAT) Bw. Manase Mrindwa akielezea changamoto za chakula cha kuku kuwa kumetokea ongezeko la bei ya chakula cha kuku hadi kufikia Shilingi Elfu 80 kwa mfuko mmoja kwa mwezi wa Julai kutokana na ongezeko la bei ya mahindi na mashudu ya soya kwenye soko la Tanzania pamoja na kuelezea uwepo wa uhaba wa vifaranga, wakati akisoma taarifa ya chama hicho kwenye kikao cha wadau wa tasnia ya kuku kilichofanyika jijini Dodoma. (22.07.2022).


Muonekano wa washiriki katika kikao cha wadau wa tasnia ya kuku kilichoandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambapo kimejumuisha menejimenti ya wizara Sekta ya Mifugo, wazalishaji wa vifaranga vya kuku, chakula cha kuku na wafugaji wa kuku ambapo wametoa maoni mbalimbali ya namna ya kuboresha tasnia hiyo na kuomba kuwepo kwa vikao vya namna hiyo mara kwa mara lengo likiwa ni kukuza tasnia. (22.07.2022).


Picha ya pamoja ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) akiwa na menejimenti ya wizara Sekta ya Mifugo na baadhi ya wadau wa tasnia ya kuku walioshiriki kikao kilichofanyika jijini Dodoma kilichowahusisha wazalishaji wa vifaranga vya kuku, chakula cha kuku na wafugaji wa kuku, lengo likiwa ni kujadili changamoto mbalimbali za tasnia ya kuku nchini. (22.07.2022)

Ijumaa, 22 Julai 2022

WATAFITI WATAKIWA KUSAIDIA SEKTA YA MIFUGO

Na Mbaraka Kambona, 


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amewataka Watafiti wa Mifugo nchini kuhakikisha wanafanya tafiti zitakazosaidia Sekta ya Mifugo kuzalisha kwa tija na kuwa na mchango mkubwa katika pato la taifa.


Waziri Ndaki alitoa wito huo wakati akifungua Mkutano wa Wadau wa Sekta ya Mifugo uliofanyika jijini Dodoma Julai 21, 2022.


Akiongea na wadau hao, Waziri Ndaki alisema wafugaji wengi nchini bado wanafuga kienyeji  na kupelekea sekta ya mifugo kutokuwa na tija kubwa, hivyo ni wakati sasa watafiti wasaidie kutatua changamoto hiyo. 


"Kama tutaendelea kufuga kama tunavyofuga leo kwa kuswaga Ng'ombe, baada ya miaka kumi ijayo tutaleta shida kwenye nchi hii, kwa sababu maeneo ya malisho yamepungua, hivyo watafiti watusaidie kuja na majibu yanayolenga kutatua changamoto hii, tuone namna gani tutakabiliana na jambo hili", alisema


Aliongeza kwa kusema kuwa kwa upande wa Wizara kuanzia mwaka huu wa fedha  wamejipanga kufanya kampeni kubwa ya kuwaelimisha wafugaji nchi nzima kuhusu ufugaji bora na wenye tija.  


"Tutaanza kutoa elimu  mwaka huu kuwaelimisha wafugaji kuhusu ufugaji bora na tutaendelea mpaka ujumbe huu wa kufuga kwa tija uwe umefika kwa wafugaji wote nchini", alifafanua


Aliendelea kusema kuwa Wizara imetenga bajeti kwa ajili ya kuelimisha wafugaji kuhusu malisho ya mifugo na mabadiliko ya tabia nchi ili wabadilike kutoka kufuga kiasili na kufanya ufugaji wa kibiashara.


Kuhusu uhaba wa Wataalamu wa Ugani, Waziri Ndaki alisema mwaka huu serikali itaajiri Maafisa Ugani zaidi ya 300 ili kupunguza changamoto hiyo huku akiongeza kuwa watanunua  pikipiki zaidi ya 1000 kwa ajili ya kuwawezesha maafisa hao kuwahudumia wafugaji kwa urahisi.


Naye, Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi(Mifugo), Dkt. Charles Mhina alisema kuwa maendeleo ya sekta ya mifugo kwa kiasi kikubwa yanachangiwa na sekta binafsi hivyo Serikali itaendelea kuweke Mazingira mazuri kwa wadau hao ili sekta hiyo iweze kuwa na mchango mkubwa katika pato la taifa.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wadau wa Sekta binafsi waliohudhuria Mkutano wa Wadau wa Mifugo uliofanyika jijini Dodoma Julai 21, 2022. Kulia kwake ni Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Charles Mhina.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akiongea wakati akifungua Mkutano wa  Wadau wa Sekta ya Mifugo uliofanyika jijini Dodoma Julai 21, 2022.


Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Charles Mhina akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki kufungua Mkutano wa Wadau wa Sekta ya Mifugo uliofanyika jijini Dodoma Julai 21, 2022.


Mkurugenzi, Idara ya Uzalishaji na Maendeleo ya Masoko(Mifugo), Bw. Steven Michael akiwasilisha mada kuhusu Mafanikio ya Sekta ya Mifugo wakati wa utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Mifugo(TLMP) katika Mkutano wa Wadau wa Sekta ya Mifugo uliofanyika jijini Dodoma Julai 21, 2022.


Mkurugenzi wa Uendelezaji wa Maeneo ya Malisho na Rasilimali za Vyakula, Dkt. Asimwe Rwiguza (kushoto) akiteta jambo na Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango(Mifugo), Bw. Mbaraka Stambuli katika Mkutano wa Wadau wa Sekta ya Mifugo uliofanyika jijini Dodoma Julai 21, 2022.

WAFUGAJI KUELIMISHWA UFUGAJI WA TIJA NA KIBIASHARA, KUONDOKANA NA UMASIKINI

Edward Kondela


Serikali imesema lengo kubwa la Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa wafugaji ni kukuza tija na kuwasaidia kufuga kibiashara ili waweze kunufaika kupitia mifugo yao.

 

Akizungumza (15.07.2022) wakati akimwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa kwenye maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani katika Shamba la mifugo la Mbogo, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema shughuli za ufugaji na uvuvi zimekuwa zikiendeshwa kiasili hivyo kushindwa kukua na kubadili maisha ya wadau wa sekta hizo.

 

Waziri Ndaki amebainisha kuwa imani mbalimbali pia zimekuwa zikitawala kwa wafugaji na wavuvi kwenye shughuli zao na kusababisha kutopokea kwa haraka mabadiliko na kufanya shughuli hizo bila kufuata utaalamu, ujuzi, weledi na kufahamu hitaji la soko ili kufuga kwa tija na kibiashara.

 

“Tumeanza ngazi ya wizara kuzungumza juu ya tija zaidi na biashara zaidi kubadilisha mtazamo wa wafanyabiashara wetu wafahamu kufuga ni kazi ya kitaalamu, hivyo natoa wito tuendelee kuelimisha wafugaji wetu.” Amesema Mhe. Ndaki

 

Naye Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akizungumza katika maonesho hayo ambayo yamehusisha mifugo bora na kisasa wakiwemo ng’ombe, mbuzi na kondoo, amesema fursa ni kubwa sana katika Sekta ya Mifugo na kwamba huo ni mwanzo mzuri wa kupatikana kwa wafugaji waliyo makini katika ufugaji wenye malengo.

 

Ameongeza kuwa uwepo wa mifugo bora na inayotambulika ni rahisi kupatikana kwa bidhaa zitokanazo na mifugo ikiwemo nyama kwa ajili ya soko la ndani na hasa soko la nje ya nchi ili wafanyabiashara na nchi kwa ujumla kuongeza kipato.

 

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Bw. Tixon Nzunda amebainisha kuwa kupitia mifugo ni wakati sasa wa kubadilisha wafugaji kutoka kwenye kufuga kiasili na kufuga kisasa ili waweze kuongeza kipato.

 

Amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi itahakikisha inasimamia malengo yote ya kuwasaidia wafugaji ili Sekta ya Mifugo iwe sehemu salama kwa wafugaji kuwekeza na kunufaika kimaisha kwa kuongeza kipato kupitia ufugaji wa kisasa.

 

Kuhusu ufugaji wa kibiashara, Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji Kibiashara Tanzania (TCCS) Bw. Naweed Mulla ambao wameandaa maonesho hayo ya mifugo na mnada ameelezea uanzishwaji wa chama hicho baada ya kugundua fursa mbalimbali katika Sekta ya Mifugo ambapo wafanyabiashara wa mifugo walikaa pamoja ili kuchangamkia fursa hizo na kutatua changamoto za sekta.

 

Pia, amesema chama hicho kiliamua kuanzisha maonesho hayo ya kila mwaka ili kuhamasisha wananchi hususan vijana kuingia katika ufugaji wa kisasa na kuwatoa katika umasikini.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki na Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Abdallah Ulega wakimsikiliza mmoja wa wataalamu akiwapatia maelezo juu ya ufugaji wa ng’ombe bora wa kisasa wakati wa maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo. (15.07.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa nne kutoka kulia), akipata maelezo juu ya ufugaji wa mbuzi na kondoo bora wa kisasa kutoka kwa mmoja wa wataalamu waliopo kwenye maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo, akiambatana na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (wa tatu kutoka kushoto) na Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji Kibiashara Tanzania (TCCS) Bw. Naweed Mulla (kushoto kwake). (15.07.2022)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw. Tixon Nzunda (katikati) akimsikiliza mmoja wa wataalamu akimwelezea juu ya teknolojia mbalimbali zinazotumika katika Sekta ya Mifugo, wakati katibu mkuu huyo akitembelea mabanda kwenye maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo. (15.07.2022)

Mmoja wa wataalamu kutoka kiwanda cha kuzalisha chanjo cha Hester Biosciences Africa Limited akifafanua juu ya utengenezaji wa chanjo za mifugo kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki na Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Abdallah Ulega kwenye maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo. (15.07.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki na Naibu wa wizara hiyo Mhe. Abdallah Ulega wakiwa kwenye banda la Wizara ya Mifugo na Uvuvi kushuhudia namna shughuli mbalimbali zinazofanywa na wizara pamoja na taasisi zilizo chini ya wizara hiyo, katika kukuza Sekta ya Mifugo wakati wa maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo. (15.07.2022)

WAZIRI NDAKI AAGIZA BODI YA USHAURI KUJIKITA KWENYE URASIMISHAJI SEKTA YA MAZIWA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amewataka wajumbe wa bodi ya ushauri ya Bodi ya Maziwa Tanzania kutatua changamoto zilizopo katika sekta ya maziwa nchini ikiwemo kurasimisha sekta hiyo kwa kasi na kuweka vituo ambavyo vitakusanya maziwa Kwa pamoja ili kuondokana na masoko yasiyo rasmi na kusaidia  kuongeza uzalishaji wa maziwa nchini.

 

Mheshimiwa Ndaki amezungumza hayo jijini Dodoma leo Julai 14, 2022 wakati akifanya uzinduzi wa Bodi ya Ushauri ya Bodi ya Maziwa Tanzania ambapo amesema kuwa uzalishaji wa maziwa nchini upo chini ambapo kwa sasa wastani wa lita bilioni 3.4 ndizo zinazozalishwa huku kiwango cha unywaji wa maziwa kikiwa ni lita 62 tu kwa mwaka kwa Mtanzania mmoja.

 

Kwa upande wake Msajili wa Bodi ya Maziwa nchini Dkt . George Msalya amebainisha mafanikio ya Bodi hiyo mpaka hivi sasa ikiwa ni pamoja na kukua kwa sekta ya maziwa nchini mpaka kufikia asilimia 2.3, kuratibu vituo 238 vya kukusanyia maziwa.

 

"Sekta yetu inakua kwa asilimia 2.3 ikichangia asilimia mbili ya pato la Taifa, uzalishaji wa Maziwa umefikia lita Bilioni 3.4 kutoka lita Bilioni 1.38 kwa mwaka 2005 wakati ambapo Bodi ilianza kufanya kazi zake rasmi." amesema Msajili Dkt. Msalya

 

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri kutoka Bodi ya Maziwa  Prof. Zacharia Samweli Masanyiwa mbali na kumshukuru Mhe. Ndaki kutokana na imani yake kwake na kuamua kumteua kushika nafasi hiyo, ameahidi kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Mhe. Ndaki kwa kuhakikisha yeye pamoja na wajumbe wengine wa Bodi kwa wanatumia taaluma zao ili kubadili changamoto zinazoikabili sekta ya maziwa nchini kuwa fursa.

 

Kwa upande wake  mwakilishi wa Chama cha Wasindikaji Maziwa Tanzania (TAMPA) Bw. Abdallah Nyalandu amesema anaamini Bodi hiyo itatatua changamoto walizonazo ikiwemo vifaa vya kusafirishia maziwa.

 

Kuundwa Kwa Bodi ya Ushauri ya Bodi ya Maziwa Tanzania kunatokana na kutokuwepo Kwa bodi kwa muda wa Miaka minne tangu Bodi hiyo kumaliza muda wake 2019.