Nav bar

Ijumaa, 22 Julai 2022

WAZIRI NDAKI AAGIZA BODI YA USHAURI KUJIKITA KWENYE URASIMISHAJI SEKTA YA MAZIWA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amewataka wajumbe wa bodi ya ushauri ya Bodi ya Maziwa Tanzania kutatua changamoto zilizopo katika sekta ya maziwa nchini ikiwemo kurasimisha sekta hiyo kwa kasi na kuweka vituo ambavyo vitakusanya maziwa Kwa pamoja ili kuondokana na masoko yasiyo rasmi na kusaidia  kuongeza uzalishaji wa maziwa nchini.

 

Mheshimiwa Ndaki amezungumza hayo jijini Dodoma leo Julai 14, 2022 wakati akifanya uzinduzi wa Bodi ya Ushauri ya Bodi ya Maziwa Tanzania ambapo amesema kuwa uzalishaji wa maziwa nchini upo chini ambapo kwa sasa wastani wa lita bilioni 3.4 ndizo zinazozalishwa huku kiwango cha unywaji wa maziwa kikiwa ni lita 62 tu kwa mwaka kwa Mtanzania mmoja.

 

Kwa upande wake Msajili wa Bodi ya Maziwa nchini Dkt . George Msalya amebainisha mafanikio ya Bodi hiyo mpaka hivi sasa ikiwa ni pamoja na kukua kwa sekta ya maziwa nchini mpaka kufikia asilimia 2.3, kuratibu vituo 238 vya kukusanyia maziwa.

 

"Sekta yetu inakua kwa asilimia 2.3 ikichangia asilimia mbili ya pato la Taifa, uzalishaji wa Maziwa umefikia lita Bilioni 3.4 kutoka lita Bilioni 1.38 kwa mwaka 2005 wakati ambapo Bodi ilianza kufanya kazi zake rasmi." amesema Msajili Dkt. Msalya

 

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri kutoka Bodi ya Maziwa  Prof. Zacharia Samweli Masanyiwa mbali na kumshukuru Mhe. Ndaki kutokana na imani yake kwake na kuamua kumteua kushika nafasi hiyo, ameahidi kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Mhe. Ndaki kwa kuhakikisha yeye pamoja na wajumbe wengine wa Bodi kwa wanatumia taaluma zao ili kubadili changamoto zinazoikabili sekta ya maziwa nchini kuwa fursa.

 

Kwa upande wake  mwakilishi wa Chama cha Wasindikaji Maziwa Tanzania (TAMPA) Bw. Abdallah Nyalandu amesema anaamini Bodi hiyo itatatua changamoto walizonazo ikiwemo vifaa vya kusafirishia maziwa.

 

Kuundwa Kwa Bodi ya Ushauri ya Bodi ya Maziwa Tanzania kunatokana na kutokuwepo Kwa bodi kwa muda wa Miaka minne tangu Bodi hiyo kumaliza muda wake 2019.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni