Nav bar

Jumatatu, 19 Januari 2026

BUNGE LAPIGWA MSASA KUHUSU SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI

Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo wamepewa semina  kuhusu Majukumu mbali mbali yanayofanywa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi pamoja na Taasisi zake.

Semina hiyo ya siku 2 imeanza leo Januari 19, 2026 Bungeni Jijini Dodoma ambapo mara baada ya kupewa semina hiyo wabunge hao kupitia kwa Mwenyekiti  wa Kamati hiyo Mhe. Deudatus Mwanyika walitoa maelekezo mbalimbali ikiwemo kuharakisha mchakato wa kuunda Mamlaka ya uvuvi nchini ili kusaidia usimamizi wa rasilimali za uvuvi na kuongeza tija ya kiuchumi na usalama wa chakula kupitia uzalishaji wa malisho ya mifugo.

“Pamoja na Jitihada hizo, lakini tunaomba huu mchakato wa kuunda mamlaka ya uvuvi uharakishwe kwa sababu usimamizi wa uvuvi bado unachangamoto, vilevile suala la malisho liangalieni “ alisema Mhe. Mwanyika.

Akitolea ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizoibuliwa na wajumbe wa kamati hiyo, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amesema Wizara yake inaendelea kuimarisha sekta ya uvuvi kwa kujenga Bandari ya Uvuvi ambayo  ujenzi wake umefikia asimia 90 na mkandarasi anatarajiwa kukabidhi bandari hiyo ifikapo Machi 31 Mwaka huu. 

Balozi Dkt. Bashiru amesema baada ya kukamilika kwa bandari hiyo, serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itanunua meli mbili kwa ajili ya shughuli za uvuvi wa bahari kuu ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa lengo la serikali la kuwa na meli tano za uvuvi.

Semina hiyo iliyolenga kuliongezea Bunge uelewa kuhusu sekta ya Mifugo na Uvuvi na mabadiliko yanayotarajiwa katika sekta hiyo itaendelea Januari 20,2026 katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo Mhe. Deodatus Mwanyika akitoa maelekezo kwa Viongozi na watendaji wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi mara baada ya kamati yake kupitishwa kwenye majukumu na maendeleo ya Sekta ya Mifugo na Uvuvi Januari 19,2026 Bungeni jijini Dodoma.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa akizungumza wakati wa semina ya kuipitisha  Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo kwenye majukumu na Maendeleo ya Sekta ya Mifugo na Uvuvi iliyofanyika Januari 19,2026 Bungeni jijini Dodoma.

Sehemu ya Watendaji Wakuu wa Taasisi na Wakurugenzi wa Idara mbalimbali kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi wakiwa kwenye semina elekezi ya kuipitisha kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo kwenye majukumu na Maendeleo ya Sekta ya Mifugo na Uvuvi iliyofanyika Januari 19,2026 Bungeni jijini Dodoma.

SERIKALI, IFAD KUENDELEZA MIRADI YA SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Mb.), amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) ambapo wamejadili kuhusu miradi inayotekelezwa kuendeleza sekta ya mifugo na uvuvi.

Akizungumza katika Kikao hicho kilichofanyika leo Januari 16, 2026, Ofisini kwake Mtumba, jijini Dodoma, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru ameonesha kufurahishwa na ujio wa ujumbe huo ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wa IFAD nchini.

Amesema serikali ya awamu ya sita imeendelea kuimarisha mazingira kuwa rafiki ili kuruhusu wawekezaji na sekta binafsi kushiriki katika kusukuma maendeleo ya wananchi.

Ujumbe huo wa IFAD  umeongozwa na Mkurugenzi wa Nchi na Mwakilishi wake nchini Tanzania Bw. Seth Meng pamoja na Mratibu wa Mpango wa Nchi wa IFAD Bi. Jacqueline Machangu.

Majadiliano hayo yalijikita kujadili mradi wa Mageuzi ya Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi (C-SDTP) na Mradi wa Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayotekelezwa kati ya sekta ya mifugo na uvuvi.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Wa kwanza, kushoto) akizungumza Ujumbe wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) nchini Tanzania kujadili miradi inayotekelezwa katika sekta ya mifugo na uvuvi, wakati wa Kikao kilichofanyika ofisini kwake leo Januari 16, 2026 Mtumba, Jijini Dodoma.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Kushoto) akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkurugenzi  wa Nchi na Mwakilishi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Seth Meng (Katikati) akielezea mpango wa utekelezaji wa miradi ya sekta ya mifugo na uvuvi  Januari 16, 2026 Mtumba, Jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Nchi na Mwakilishi wa IFAD Bw. Seth Meng (Kulia) akimpa maelezo Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kuhusu utekelezaji wa miradi ya sekta za mifugo na uvuvi wakati wa majadiliano yaliyofanyika Ofisi ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi Januari 16, 2026 Mtumba, Jijini Dodoma.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Katikati), Mkurugenzi wa Nchi na Mwakilishi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo, IFAD Bw. Seth Meng (Kushoto) na Mratibu wa Mpango wa Nchi wa IFAD Bi. Jaqueline Machangu (Kulia) wakiwa katika picha ya pamoja baada ya majadiliano yaliyofanyika Ofisi ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi  Januari 16, 2026 Mtumba, Jijini Dodoma.

WAKUZAJI VIUMBEMAJI 2000 KUJENGEWA UWEZO WA MBINU BORA ZA UFUGAJI SAMAKI

Na. Stanley Brayton, WMUV

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea kutekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP), ikiwa na lengo la kuwajengea uwezo wakuzaji viumbemaji katika uzalishaji wa samaki, kutengeneza chakula cha samaki, usimamizi wa mabwawa na masuala ya jinsia na lishe ili kuimarisha mifumo jumuishi ya usalama wa chakula.

Akizungumza katika kikao kazi cha kutekeleza programu hiyo, leo Januari 15, 2026 wilayani Songea mkoani Ruvuma, Katibu Tawala Msaidizi wa Uchumi na Uzalishaji Mali Mkoa wa Ruvuma, Bw. Deogratius Sibula amesema  programu ya (AFDP), inayotekelezwa kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ni nyenzo muhimu ya Serikali katika kuimarisha Sekta ya Ukuzaji viumbemaji nchini.

“Programu hii itafanyika katika halmashauri tano za Mkoa wa Ruvuma ambazo ni Halmashauri ya Manispaa ya Songea, Halmashauri za Wilaya ya Mbiga, Namtumbo, Nyasa na Tunduru.” amesema Bw. Sibula

Aidha, Bw. Sibula amesema kuwa Utekelezaji wa Majukumu ya Programu hiyo inalenga kutoa mafunzo kwa wakuzaji viumbemaji 2,000 katika Mkoa wa Ruvuma, ambapo, katika awamu hii utafanyika katika kata 25 ndani ya Halmashauri hizo 5 za Mkoa wa Ruvuma, kuanzia tarehe 15 Januari 2026 hadi tarehe 22 Januari 2026.

Vilevile, Bw. Sibula amebainisha kuwa mafunzo haya ni fursa kwa wakuzaji viumbemaji na yatakuwa na tija kubwa kwa wafugaji wa samaki wa Mkoani Ruvuma na kuhamsha hali ya ufugaji kutoka ule wa kujikimu na kuwa na ufugaji wa kibiashara unaozingatia mbinu bora za ufugaji.

Kwa Upande wake, Afisa Uvuvi Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambaye ni Afisa Kiungo wa Programu ya AFDP, Bi. Mkomanile Mahundi amesema zoezi hilo litajumuisha wataalamu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu (PMO) pamoja na wataalam kutoka Halmashauri nane za mkoa wa Ruvuma. 

Bi. Mahundi amebainisha kuwa mafunzo hayo ni endelevu na yataendelea kutolewa katika mikoa mbalimbali nchini ikiwemo Mkoa wa Morogoro, Tanga, Geita pamoja na Mkoa wa Tabora.

Katibu Tawala Msaidizi wa Uchumi na Uzalishaji Mali Mkoa wa Ruvuma, Bw. Deogratius Sibula (mstari wa mbele katikati), akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa Sekta ya Uvuvi, baada ya Kikao kazi cha kutekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kinacholenga kuwajengea uwezo wakuzaji Viumbemaji nchini, kilichofanyika katika Ukumbi wa Songea Club, Januari 15, 2026 Ruvuma.

Afisa Uvuvi Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambaye ni Afisa Kiungo wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP), Bi. Mkomanile Mahundi, akizungumza na wadau wa Sekta ya Uvuvi, katika Kikao kazi cha kutekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kinacholenga kuwajengea Uwezo wakuzaji Viumbemaji nchini, kilichofanyika katika Ukumbi wa Songea Club, Januari 15, 2026 Ruvuma.

Mtaalamu wa Jinsia na Lishe Ofisi ya Waziri Mkuu, Bi. Irene Mmbando, akiwasilisha Mada kuhusu utambuzi wa walengwa wanaojihusisha na masuala ya Ukuzaji Viumbe Maji (Samaki) kwenye Mabwawa, watika wa Kikao kazi cha kutekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kinacholenga kuwajengea Uwezo wakuzaji Viumbemaji nchini, kilichofanyika katika Ukumbi wa Songea Club, Januari 15, 2026 Ruvuma.

Picha ni baadhi ya wadau wa Sekta ya Uvuvi, wakimsikiliza Katibu Tawala Msaidizi wa Uchumi na Uzalishaji Mali, Bw. Deogratius Sibula (hayupo pichani), katika Kikao kazi cha kutekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kinacholenga kuwajengea Uwezo wakuzaji Viumbemaji nchini, kilichofanyika katika Ukumbi wa Songea Club, Januari 15, 2026 Ruvuma.





Mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma ambaye ni Katibu Tawala Msaidizi wa Uchumi na Uzalishaji Mali, Bw. Deogratius Sibula, akihutubia wadau wa Sekta ya Uvuvi, katika Kikao kazi cha kutekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kinacholenga kuwajengea Uwezo wakuzaji Viumbemaji nchini, kilichofanyika katika Ukumbi wa Songea Club, Januari 15, 2026 Ruvuma.




DKT. BASHIRU APIGA MARUFUKU MAAMUZI YANAYOATHIRI BIASHARA ZA WAFUGAJI, WAVUVI

◼️Ni kufuatia mzozo uliotokea mkoani Tanga

◼️Asisitiza mazungumzo yachukue nafasi kubwa zaidi

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amepiga marufuku kwa wasimamizi wa sheria katika ngazi zote kwa upande wa sekta za Mifugo na Uvuvi kufanya maamuzi yatakayoathiri mwenendo wa biashara kwa wadau wa sekta hizo.

Balozi Dkt. Bashiru amesema hayo Januari 15, 2025 mkoani Dodoma wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa machinjio ya nyama ya Serikali iliyopo maeneo ya Kizota ambapo amewataka wasimamizi hao kuhakikisha wanaafikiana na wawekezaji na wafanyabiashara hao kwa njia ya mazungumzo.

“Haya niliyoyaona Tanga hata kama ni Halmashauri bado ni Serikali na bahati nzuri Halmashauri zote zipo chini ya Mhe. Waziri Mkuu kwa hiyo Halmashauri zote na Wizara tujizuie kufanya kazi za udhibiti kwa namna ambayo itatikisa na kuathiri shughuli za kiuchumi kwenye sekta hizi” Ameongeza Balozi Dkt. Bashiru.

Aidha Balozi Dkt. Bashiru amewataka wataalam hao kutoa muda nyongeza kwa wafanyabishara hao na notisi ili kuwapa fursa ya kutekeleza matakwa ya sheria kabla ya kufunga bishara zao.

“Ukifunga shughuli yake kwa siku moja, watoto wake hawawezi kula na hiyo pesa hupati” Amehitimisha Balozi Dkt. Bashiru.

Kuhusiana na Machinjio ya Serikali aliyoikagua, Balozi Dkt. Bashiru amemtaka Mkurugenzi wa Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) ambaye Machinjio hiyo ipo chini yake Bw. Mohamedi Mbwana kushughulikia dosari zote alizoziona na kuhakikisha inakuwa kwenye mazingira mazuri wakati wote.






Jumanne, 13 Januari 2026

BADILISHENI HATIMILIKI YA KIWANJA CHA UJENZI WA TAASISI - DKT. BASHIRU

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, ameagiza kubadilishwa kwa hati miliki ya kiwanja kinachotumika kwenye mradi wa ujenzi wa jengo la ofisi za makao makuu ya Taasisi sita zilizo chini ya Wizara yake kutoka Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) kwenda kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Balozi Dkt. Bashiru ametoa agizo hilo Januari 13, 2026 wakati wa ziara yake ya kukagua maendeleo ya mradi huo unaotekelezwa eneo la Njedengwa jijini Dodoma ambapo amesisitiza kuwa hatua hiyo ni muhimu kiutawala na kisheria na itahakikisha umiliki halali wa mali ya Serikali na kuwezesha matumizi endelevu ya jengo hilo mara baada ya kukamilika.

Balozi Dkt. Kakurwa amesema kuwa jengo hilo linajengwa kwa lengo la kuzikutanisha taasisi hizo ili kuboresha uratibu wa shughuli za kiutendaji, kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi pamoja na kupunguza gharama za uendeshaji wa ofisi zilizokuwa zikitumika maeneo tofauti.

“Ni lazima taratibu zote za umiliki wa ardhi zikamilishwe kwa wakati ili kuepusha changamoto za kisheria na kiutendaji hapo baadaye na hati ya kiwanja hiki inapaswa kuwa chini ya Katibu Mkuu wa Wizara ili kuwezesha usimamizi mzuri wa mradi na jengo lenyewe,” amesema Balozi Dkt. Bashiru

Aidha, Balozi Dkt. Bashiru amewataka wasimamizi wa mradi na wakandarasi kuhakikisha wanazingatia viwango vya ubora, thamani ya fedha na ratiba ya utekelezaji kama ilivyoainishwa kwenye mkataba huku akisisitiza kuwa Serikali haina nia ya kuona miradi ya maendeleo ikikwama kutokana na uzembe au kutokamilisha taratibu muhimu ambapo amemtaka Mshauri Mwelekezi wa mradi huo ambaye ni Wakala wa Majengo nchini (TBA) kuhakikisha anapitisha vibali vyote muhimu kwa haraka ili kuepuka kuchelewesha kukamilika kwa mradi huo.

Kwa upande wao, viongozi na wataalamu wa Wizara hiyo wamekiri kupokea maelekezo hayo ambapo wameahidi  kuyafanyia kazi haraka iwezekanavyo kwa kufuata  taratibu zote za kisheria, sambamba na kuendelea kusimamia utekelezaji wa ujenzi huo ili kukamilika kwa wakati uliopangwa.

Mradi wa ujenzi wa jengo la ofisi za makao makuu ya taasisi sita zilizo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi unaotarajiwa kutumia zaidi ya Tshs. Bilioni 49 ni miongoni mwa miradi ya kimkakati inayolenga kuimarisha utendaji wa Wizara, kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wa umma na kuchochea maendeleo ya sekta ya mifugo na uvuvi nchini.




Jumatatu, 12 Januari 2026

DKT. BASHIRU ACHARUKA WAFUGAJI KUJERUHI WAKULIMA IRAMBA

◼️Serikali kugharamia matibabu yao 

◼️Aagiza wahusika wakamatwe mara moja

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amekasirishwa na kitendo cha wafugaji Wilaya ya Iramba mkoani Singida kuijeruhi vibaya kwa panga familia ya watu wawili wanaofanya shughuli za kilimo Wilayani humo.

Hayo yamefahamika alipofika Wilayani hapo Januari 10,2026 ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa ziara zake za kusikiliza na kutatua changamoto za wafugaji na wavuvi nchini ambapo mmoja wa wakulima wa Wilaya hiyo Bw. Mkoma Mustapha alielezea namna wafugaji walivyomshambulia yeye na mtoto wa kaka yake.

“Kwenye tukio hilo mimi nilipigwa mkononi na kuvunjika vidole vitatu na mguuni nilipigwa nikapasuka na mgongoni nikivua shati utanionea huruma na nilipotoka hospitali nikaenda polisi ili kujua hatma ya walionijeruhi nikajibiwa kwamba walionifanyia hivi imeshindikana kuwakamata” Ameeleza Bw. Mustapha.

Akizungumza mara baada ya kumsikiliza mkulima huyo, Balozi Dkt. Bashiru alielekeza Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Iramba igharamie matibabu yote ya Mkulima hiyo ikiwa ni pamoja na kurejesha gharama alizotumia mpaka sasa.

“La pili wote waliohusika kwenye tukio hilo watafutwe wakamatwe na wafikishwe mbele ya vyombo vya sheria lakini tusichochee chuki kutokana na tukio hili” Amesema Balozi Dkt. Bashiru.

Aidha Balozi Dkt. Bashiru ameuelekeza uongozi wa kijiji, Mtendaji wa kata na polisi jamii wa eneo husika chini ya usimamizi wa Kamanda wa Polisi wa Wilaya hiyo kwenda kutoa elimu kwa wakulima na wafugaji kuhusu umuhimu wa kufanya shughuli zao kwa mujibu wa sheria na kujizuia kuchukua sheria mkononi.

Akiwa Wilayani Mkalama kwenye kijiji cha Nyahaa eneo la Bukundi Balozi Dkt. Bashiru alipokea malalamiko ya baadhi ya wafugaji wa eneo hilo kuvamiwa na kupigwa na wafugaji wa Wilaya ya Meatu ambapo aliwaeleza wafugaji hao kuwa atafanya jitihada za kwenda kuzungumza na kuwasikiliza wafugaji wa upande wa Simiyu kabla ya kufanya uamuzi wa jambo hilo.

Balozi Dkt. Bashiru na Naibu wake Mhe. Ng’wasi Kamani wamehitimisha rasmi ziara yao ya takribani mikoa 13 waliyoianza Desemba 10,2025 ambayo ililenga kujitambulisha,kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wafugaji na wavuvi nchini.

Jumamosi, 10 Januari 2026

DKT. BASHIRU AWAPIGIA CHAPUO WAFUGAJI KUPATA MIKOPO

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amesema kuwa Serikali inakusudia kuweka utaratibu utakawawezesha wafugaji kupata mikopo kupitia Taasisi za fedha nchini kama ilivyo upande wa Wakulima.

Balozi Dkt. Bashiru amebainisha hayo Januari 09,2026 wakati akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Ushetu mkoani Shinyanga ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wafugaji na wavuvi nchini.

“Wakulima wanakopeshwa lakini mara chache sana wafugaji kukopeshwa na kama huwezi kukopesheka ni vigumu sana kupiga hatua kubwa lakini tatizo tulilonalo mabenki yetu gharama za mikopo zipo juu watu wanaogopa kufilisiwa” Ameongeza Balozi Dkt. Bashiru.

Aidha Balozi Dkt. Bashiru amesisitiza kuwa Serikali itahakikisha mikopo itakayotolewa kwa wafugaji inakuwa ya gharama nafuu kwa upande wa riba huku pia ikiwa na uwezo wa kulipwa hatua ambayo ameeleza kuwa itawasaidia wafugaji hao kufuga kisasa.

Mbali na kuzungumza na wafugaji na wavuvi wa Wilaya ya Ushetu, Balozi Dkt. Bashiru pia alitembelea na kukagua kiwanda kinachotarajiwa kusindika maziwa cha Jambo ,Machinjio ya Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga na Eneo la kupumzishia Mifugo la Chibe.



MHE. KAMANI AHITIMISHA MAFUNZO KWA WAJASIRIAMALI 350 WA SEKTA YA UVUVI

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng'wasi Kamani amewataka wajasiriamali 350 wa sekta ya uvuvi waliopata mafunzo ya kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi kutumia ujuzi walioupata kwa ajili ya kuongeza ajira, Kipato na kuchagia Maendeleo ya Taifa.

Akizungumza wakati wa kufunga Mafunzo hayo Leo Januari 9, 2026 katika Ukumbi wa Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Kampasi ya Nyegezi Mhe. Kamani amesema serikali inaendelea kuunga Mkono wajasiriamali wanaojihusisha na uongezaji wa thamani ya mazao ya uvuvi ili kupanua biashara zao.

"Mafunzo hayo yanaakisi dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwawezesha wananchi kiuchumi, hususan wanawake na vijana, kupitia fursa za Uchumi wa Buluu, leo mnapopewa vyeti mnakabidhiwa dhima ya kwenda kutumia ujuzi wenu kuongeza ajira, kipato na maendeleo ya Taifa” alisema Mhe. Kamani.

Aidha, aliongeza kuwa serikali imetenga kiasi cha shilingi Bilioni moja kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi ili kuongeza ufanisi unaolenga kutoa mafunzo bora ya kukuza sekta ya uvuvi na uchumi wa buluu

Kwa Upande wake, Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Dkt. Semvua Mzighani amesema mafunzo hayo yaliyofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Ubelgiji la ENABEL kupitia mradi wa Green and Smart Cities (IncluCities) yamelenga kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi, ushindani wa bidhaa sokoni na kuongeza kipato cha kaya.

 Awali wawakilishi wa Kundi la Vijana na Kina Mama Wajasiriliamali wakiwasilisha risala yao kwa mgeni rasmi walieleza kuwa mafunzo hayo yataenda kubadilisha mfumo mzima wa uchakataji na uongezaji wa thamani wa mazao ya Uvuvi tofauti na hapo awali walipokuwa wakitumia njia za jadi.

Jumla ya kina mama wajasiriamali 200 wamehitimu mafunzo ya usindikaji wa mazao ya samaki, huku vijana 150 wakipata mafunzo ya utayari kazini katika ukuzaji viumbe maji.

Naibu waziri wa Mifugo Na Uvuvi Mhe. Ng'wasi Kamani( Wa pili, kulia) akitunuku cheti kwa Bi. Joyce Christopher akiwa ni mmoja kati ya washiriki 350 waliohitimu mafunzo ya muda mfupi juu ya ufugaji samaki na ukuzaji viumbe maji FETA Nyegezi wakati wa kuhitimisha mafunzo hayo leo Januari 9, 2026.

Naibu waziri wa Mifugo Na Uvuvi Mhe. Ng'wasi Kamani( Wa kwanza, kulia) akikagua mazao ya uvuvi yalioongezewa thamani na Kina Mama wajasiriamali waliopata mafunzo ya muda mfupi juu ya ufugaji samaki na ukuzaji viumbe maji FETA Nyegezi leo Januari 9, 2026.

Mtendaji Mkuu wa  Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Dkt. Semvua Mzighani akizungumza wakati wa hafla ya kutunuku vyeti vijana na  kina Mama Wajasiriamali  350 walioshiriki mafunzo ya muda mfupi ya ufugaji samaki na ukuzaji viumbe maji FETA Nyegezi Leo Januari 9, 2026.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu, ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji Dkt. Nazael Madalla akielezea hali ya sekta ya Uvuvi nchini wakati wa kufunga mafunzo ya muda mfupi juu ya ufugaji samaki na ukuzaji viumbe maji FETA Nyegezi leo Januari 9, 2026.

Naibu waziri wa Mifugo Na Uvuvi Mhe. Ng'wasi Kamani (kati kati, waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja  na washiriki 350 waliohitimu mafunzo ya muda mfupi juu ya ufugaji samaki na ukuzaji viumbe maji FETA Nyegezi wakati wa hafla ya kuhitimisha mafunzo hayo leo Januari 9, 2026.

Naibu waziri wa Mifugo Na Uvuvi Mhe. Ng'wasi Kamani akizungumza na washiriki 350 waliohitimu mafunzo ya muda mfupi juu ya ufugaji samaki na ukuzaji viumbe maji FETA Nyegezi wakati wa hafla ya kuhitimisha mafunzo hayo leo Januari 9, 2026.

DKT. BASHIRU AAGIZA KUUNDWA KWA CHOMBO CHA KUUNGANISHA WASAFIRISHAJI WA NYAMA NJE YA NCHI

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally amemwagiza Msajili wa Bodi ya Nyama Tanzania kukutana na wawekezaji wanaosafirisha nyama nje ya nchi ili kuunda chombo kitakachowaunganisha  kwa ajili ya uendeshaji wa biashara ya nyama kimataifa na kutatua changamoto zinazowakabili wawekezaji hao.

Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally ametoa agizo hilo leo  Januari 8, 2026 baada ya kutembelea Kiwanda cha Nyama cha Chobo Investment Company kilichopo Usagara mkoani Mwanza, ambapo amesema ili changamoto za wawekezaji ziweze kutatuliwa  ni muhimu kuwa na umoja kwa wawekezaji hao.

"Serikali haiwezi kutatua changamoto za mwekezaji mmoja mmoja, sasa Msajili wa Bodi ya Nyama, kwahiyo maelekezo yangu pamoja na chombo hicho, nitayarishie kikao na wauzaji wa nyama nje ya nchi kati kati ya mwezi wa pili, kile kikao ndio kitazaa umoja wa chombo imara " alisema Mhe. Balozi Dkt. Bashiru.

Aidha,  Mhe. Balozi Dkt. Bashiru amemwangiza Msajili wa Bodi ya Nyama Tanzania kwa kushirikia na Idara ya Uzalishaji na Masoko (DPMD) kuunda timu ya wataalam itakayofanya mapitio ya mradi na shughuli zinazotelezwa na Kiwanda cha Chobo Investment Company ili  kutathmini sababu zilizomsababishia  mwekezaji kuchelewe kuanza uzalishaji.

Kwa Upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho  Bw. John Chobo amesema wawekezaji wanakumbana na changamoto mbalimbali wanaposafirisha nyama nje ya nchi hivyo amependekeza usafirishaji wa nyama uwe unafanyika ukiwa kwenye taswira ya nchi.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wa pili, kulia) akipokea maelezo kutoka Mkurugenzi wa Kiwanda cha Nyama cha Chobo Investiment Company  kuhusu shughuli zinazofanywa na  Kiwanda hicho mara baada ya kukitembelea kiwanda hicho eneo la  Usagara, Mwanza Januari 8, 2026 .





WIZARA ZA KISEKTA KUSHIRIKIANA KUHUDUMIA WAFUGAJI

Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeanza kufanya mazungumzo ya awali na Wizara za Kilimo na Maji ili kushirikiana kwenye maeneo ambayo Wizara hizo zinaingiliana kisekta.

Hayo yamebainishwa Januari 08,2026 na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani wakati akizungumza na wafugaji kwenye mnada wa Mifugo wa Ndala uliopo Nzega mkoani Tabora.

“Sisi kama Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumeona tukianza kufanya kazi peke yetu hatuwezi kukimbia kwa mwendo mrefu na maelekezo ya Mhe. Rais ni kwamba kwa miaka hii mitano tukimbie kwa mwendo mrefu zaidi hivyo Mhe. Waziri ameshaanza mikakati ya kufanya vikao na Mawaziri wa Kilimo, na Maji” Ameongeza Mhe. Kamani.

Mhe. Kamani ameeleza kuwa kupitia mashirikiano hayo wafugaji wanatarajiwa kupata sehemu za kunyweshea mifugo yao kupitia skimu za umwagiliaji zinazoendeshwa na Wizara ya Kilimo na miradi mikubwa inayotekelezwa na Wizara ya Maji.

Aidha Mhe. Kamani amesisitiza kuwa wakati mabwawa hayo yakiendelea kujengwa kupitia mpango wa muda mrefu,Wizara yake imeshaanza kuandaa utaratibu wa kutekeleza mpango wa muda mfupi wa kuchimba visima virefu vitakavyowasaidia wafugaji wengi kunyweshea mifugo yao.

Akigusia upande wa malisho ya Mifugo, Mhe. Kamani amewataka wafugaji hao kufika kwenye mashamba ya Serikali kununua mbegu zinazopatikana kwa bei ya rukuzu ambapo amewahakikishia ubora na wingi wa malisho yatokanayo na mbegu hizo ukilinganisha na ukubwa wa maeneo watakayoenda kupanda.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani akizungumza na wafugaji aliowakuta kwenye mnada wa Ndala uliopo Nzega mkoani Tabora Januari 08,2026.

Mkurugenzi wa Uendelezaji nyanda za malisho na Rasilimali za Vyakula vya wanyama Dkt. Asimwe Rwiguza (kulia) akimdokeza jambo Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani muda mfupi baada ya kufika kwenye mnada wa Ndala uliopo Nzega mkoani Tabora Januari 08,2026.

MAAFISA MIFUGO NA UVUVI WAFUATENI WAFUGAJI, WAVUVI WALIPO - KAMANI

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani amewataka Maafisa Mifugo na Uvuvi kote nchini kuwafuata wafugaji na wavuvi kwenye maeneo yao kwa ajili ya kuwahudumia badala ya kuwasubiri ofisini.

Mhe. Kamani amesema hayo kwenye mkutano wa wafugaji, wavuvi na wadau wa sekta hizo kwa ujumla uliofanyika Januari 07,2026 Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu ambapo amesisitiza kuwa huo ndo mwelekeo wa Viongozi wakuu wa Wizara hiyo na Serikali kwa ujumla hivi sasa.

“Kama Mhe. Waziri anazunguka mkoa kwa mkoa kwenda kuonana na wadau wake ni kwa vipi wewe unapata nguvu ya kukaa ofisini na kutokwenda kuwatembelea?” Amehoji Mhe. Kamani.

Aidha Mhe. Kamani amewasisitiza Maafisa hao kuhakikisha wanatatua changamoto watakazozikuta kwa wadau wao badala ya kuwalazimu wafugaji hao na wavuvi kuwafuata ofisini kama ilivyozoeleka hapo awali.

“Huu ndo utamaduni ambao Balozi Daktari Bashiru Ally Kakurwa ameagiza uanze kuanzia sasa na kwa wale ambao wataonekana ni wavivu waanze kukaa mkao wa kujirekebisha kwa sababu watashindwa kuendana na kasi ya Mhe. Waziri, Wizara na Mhe. Rais hivyo tutalazimika kuwaweka pembeni” Amehitimisha Mhe. Kamani.

Awali kabla ya kushiriki mkutano huo, Mhe. Kamani alimtembelea mmoja wa wafugaji na wakulima wa malisho ya mifugo mkoani humo Dkt. Mathias Abuya ambapo alitoa rai kwa wafugaji wengine kutumia shamba lake kama shamba darasa.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani (kushoto) na mfugaji wa mfano kutoka mkoani Simiyu Dkt. Mathias Abuya wakiweka nyasi kwenye mashine maalum kwa ajili ya kuchakata muda mfupi baada ya Mhe. Kamani kumtembelea mfugaji huyo Januari 07,2026, Bariadi mkoani Simiyu.

Mfugaji wa mfano kutoka mkoani Simiyu Dkt. Mathias Abuya (katikati) akimueleza Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani namna anavyoendesha mradi wake wa kufuga kuku muda mfupi baada ya Mhe. Kamani kumtembelea Januari 07,2026, Bariadi mkoani Simiyu.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani akivalishwa vazi maalum la wafugaji wakati wa Mkutano wa Wafugaji, Wavuvi na wadau wengine wa sekta hizo uliofanyika Januari 07,2026 Bariadi mkoani Simiyu.

MAENDELEO YA SEKTA BINAFSI NI JUKUMU LETU - KAMANI

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi kamani amesema kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha sekta binafsi inapiga hatua katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kiuchumi na maendeleo kwa ujumla.

Mhe. kamani amesema hayo wakati wa ziara yake ya kuitembelea kampuni inayojihusisha na uzalishaji wa kuku wa mayai na nyama ya Lake Zone Farm iliyopo Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza Januari 06,2026 ambapo amesisitiza Serikali itaendelea kusukuma juhudi za sekta binafsi katika ili kufikia malengo waliyojiwekea.

“Tunajua tunapofanya hivyo tunasaidia kuwanyanyua na wengine ambao kupitia nyinyi watajifunza hiki mnachofanya hivyo naamini tukiendelea na ubunifu huu na sisi kama Wizara tukasaidia kushusha gharama za chakula cha tutarahisisha zaidi mazingira ya wafugaji wetu wa kuku kupata chakula cha kutosha kwa gharama nafuu na kwa misingi hiyo hata bidhaa mtakazopeleka kwenye jamii zitapatikana kwa gharama nafuu pia” Ameongeza Mhe. Kamani.

Aidha Mhe. Kamani ametoa rai kwa wafugaji wakubwa kutengeneza mfumo wa kuwashirikisha na kuwanyanyua wafugaji wengine jambo ambalo anaamini litaongeza tija kwenye ufugaji na kunyanyua jamii zinazowazunguka wafugaji hao.

“Bado tunahitaji wazalishaji wengi zaidi kwa sababu mahitaji ya protini kwenye Mifugo ni makubwa na ndio maana hapa unaona pamoja na kuwa na kuku wengi bado ikifika muda wa kuwauza wale waliohitimisha muda wa kuzalisha mayai bado hupati shida ya soko” Ameongeza Mhe. Kamani.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa kampuni hiyo Bi. Joyce kabago ameishukuru Serikali kwa kuwawezesha kuagiza vifaa vya kufugia kuku bila tozo na kuwawezesha wataalam ambao huwatembelea na kuwapatia huduma stahiki.





Jumatatu, 5 Januari 2026

RUBAMBAGWE IKAMILIKE MACHI 30-DKT. BASHIRU

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa ameeelekeza mradi wa kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji cha Rubambagwe kilichopo Chato mkoani Geita kikamilike ifikapo Machi 30,2026.

Balozi Dkt. Bashiru amesema hayo mara baada ya kufika na kukagua kituo hicho Januari 05,2026 ambapo ameonesha kushangazwa na hali ya kutoendelea kwa shughuli za ujenzi kituoni hapo pamoja na kutengwa kwa fedha zilizopangwa kutekeleza shughuli hiyo.

“Kwa mkandarasi ambaye ana “tight schedule” ya kazi nyingi kama ninavyoziona hapa kungekuwa na shughuli zinazoendelea lakini sioni Cement, kokoto wala shughuli yoyote” Amesema Balozi Dkt. Bashiru.

Kufuatia hali hiyo Balozi Dkt. Bashiru amemwelekeza Mhandisi wa Wizara hiyo Bw. George Kwandu kuwasilisha nakala za mpango wa utekelezaji wa awamu ya pili ya ujenzi huo ofisini kwake, Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya, Mbunge, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato, Chama cha Mapinduzi, Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo na Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ili wafuatilie kwa kila wiki hatua kwa hatua ujenzi wa Taasisi hiyo na kuhakikisha unakamilika katika tarehe tajwa.

Aidha Balozi Dkt. Bashiru amemwelekeza Mkuu wa mkoa huo Mhe. Martin Shigela na kamati ya Usalama ya Mkoa huo kufuatilia utekelezaji wa mpango kazi huo kulingana na fedha zinazotolewa na Serikali kwenye mradi huo.