WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI MBIONI KUANZISHA KITUO CHA HUDUMA KWA WATEJA
Wizara ya Mifugo na Uvuvi ipo katika hatua za mwisho za kuanzisha Kituo cha Huduma kwa Wateja kitakacholenga kupokea, kusikiliza na kushughulikia changamoto za wadau wa sekta ya mifugo na uvuvi, sambamba na kutoa taarifa na ufafanuzi kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na Wizara. Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi kuhusu utoaji wa huduma bora kwa wateja yaliyofanyika leo, Julai 8, 2026, jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Charles Mhina, amesema hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za wizara kuboresha utoaji wa huduma kwa wafugaji, wavuvi na wadau wengine wa sekta hizo. Dkt. Mhina amesema mafunzo hayo yanawahusisha wataalamu walioteuliwa kutoka idara na vitengo mbalimbali vya wizara, kwa lengo la kuwajengea uwezo na ujuzi katika utoaji wa huduma bora kwa wateja, ambao utakuwa msingi wa ufanisi wa Kituo cha Huduma kwa Wateja...