Nav bar

Jumanne, 3 Februari 2026

BBT IWEKEZE KATIKA KUZALISHA MALISHO YA MIFUGO – DKT. BASHIRU

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, amezitaka taasisi zinazotekeleza Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) kutumia maeneo yao kuzalisha malisho ya mifugo ili kuimarisha ufugaji wa kibiashara.

Ametoa kauli hiyo leo Januari 31, 2026 alipokagua Kituo cha BBT cha unenepeshaji wa mbuzi na kondoo Kongwa mkoani Dodoma, akizitaka Kampuni za Ranchi ya Taifa (NARCO), Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) na Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (LITA) kuweka kipaumbele katika uzalishaji wa malisho kibiashara, kutokana na kwamba taasisi hizo zina ardhi, utaalam na uzoefu wa kutosha kufanikisha azma hiyo.

“Vituo vyetu vyote vyenye ardhi kubwa kama hizi TALIRI, NARCO, LITA kwa sababu tunautaalam na uzoefu  mkubwa nguvu zote zipelekwe kwenye uzalishaji wa malisho, mimi ningefurahi kuona  kuwa hii ni BBT ya malisho” alisema Mhe. Balozi Dkt. Bashiru. 

Aidha, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru amehimiza wafugaji kupewa elimu ya uzalishaji wa malisho na kuagiza utekelezaji wa programu hiyo uishirikishe Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana ili kuwafikia vijana wengi zaidi.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa BBT kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mkurugenzi wa Tathmini na Ufuatiliaji Dkt. Daudi Mayeji amesema Wizara hiyo imetengewa dola za Marekani milioni 32.8 sawa na shilingi bilioni 81 kwa ajili ya utekelezaji wa programu hiyo, huku uwekezaji wa awali wa Kituo cha Kongwa ukiwa dola milioni 11.82.

Programu ya BBT ilianza mwaka 2018 kupitia TALIRI kwa kushirikiana na PASS Trust Tanzania, ikilenga kuwawezesha vijana kujiajiri kupitia mnyororo wa thamani wa mifugo na kuchangia uchumi wa taifa.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa  akitoa maelekezo kwa Mhandisi wa Wizara juu ya ulinzi wa miundombinu ya BBT ya Mifugo wakati wa ziara yake kwenye kituo cha  BBT Kongwa  mkoani Dodoma leo Januari 31, 2026.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wapili kulia) akifafanuliwa jambo na Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Prof. Eric Komba (wapili kushoto) wakati wa ziara ya kukagua miundombinu ya Programu ya BBT Mifugo kituo cha Kongwa  mkoani Dodoma leo Januari 31, 2026.

Mabanda ya Mbuzi na Kondoo yanayotakiwa kufanyiwa ukarabati kwa ajili Programu ya BBT ya Mifugo awamu ijayo

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wa pili kulia) akikagua machinjio ya mbuzi na kondoo katika Kituo cha BBT ya Mifugo cha Kongwa Mkoani Dodoma wakati wa ziara yake ya kukagua miundombinu ya pragramu hiyo leo 31, Januari, 2026

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa akitoa maelekezo kwa wataalam kuhusu uzalishaji wa malisho ya mifugo kupitia Programu ya BBT Mifugo machinjio ya mbuzi na kondoo katika Kituo cha BBT ya Mifugo  wakati wa ziara yake ya kukagua miundombinu ya pragramu  hiyo Kituo cha Kongwa mkoani Dodoma leo 31, Januari, 2026

FETA YATAKIWA KUONGEZA UZALISHAJI WA VIFARANGA VYA SAMAKI

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Edwin Mhede ameitaka Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kuongeza uzalishaji wa vifaranga vya samaki ili viweze kukidhi hitajio kubwa lililopo hapa nchini.

Dkt. Mhede ametoa kauli hiyo jana,  29 Januari 2026 alipotembelea FETA Kampasi Kuu ya Mbegani kwa lengo la kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na FETA pamoja na miundombinu ya kujifunzia na kufundishia.

"Niwapongeze kwa utotoleshaji huu wa vifaranga na ufugaji samaki kwa ujumla ila niwasihi muongeze zaidi kasi ya uzalishaji vifaranga ili viende maeneo yenye uhitaji na nyie kujipatia kipato" amesema Dkt. Mhede.

Aidha, ameishauri FETA kuwekeza katika ufugaji samaki (hasa kwenye vizimba) katika maeneo mbalimbali ikiwepo Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika kwa lengo la kutoa mafunzo zaidi kama mashamba darasa na pia uzalishaji wa biashara ili kuongeza mapato.

Awali Mtendaji Mkuu wa FETA, Dkt. Semvua Mzighani amesema kuwa kwasasa FETA inaendelea kutoa mafunzo ya muda mfupi na mrefu katika ufugaji wa samaki ili wananchi na Taifa kwa ujumla lifaidike zaidi na fursa zilizopo katika  Uchumi wa Buluu. Maeneo ya kipaumbele ni pamoja na: ufugaji samaki, ufugaji wa Tango (Jongoo) Bahari, unenepeshaji wa Kaa na kilimo cha Mwani.

Akiwa FETA Dkt. Mhede alipata fursa ya kujionea mazingira mbalimbali ya kufundishia na kujifunzia ikiwemo eneo la utotoleshaji wa vifaranga vya samaki, mabwawa ya kufugia samaki aina ya sato na kambale, eneo la kukaushia samaki na mwani, Zahanati na Idara ya Uvuvi na Ubaharia ambapo alipata fursa kuongea na wanafunzi wa Fani ya Uvuvi na Ubaharia.









Ijumaa, 30 Januari 2026

DKT. BASHIRU AFANYA MAZUNGUMZO NA FAO KUENDELEZA SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amekutana na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Nchini Tanzania Dkt. Nyabenyi Tipo  na kufanya mazungumzo yanayolenga kuendeleza ushirikiano  katika kukuza na kuendeleza sekta za mifugo na uvuvi nchini.

Kikao hicho kimefanyika leo Januari 29, 2026 katika ofisi ndogo za Wizara ya Mifugo na Uvuvi  zilizopo Kambarage Tower Jijini Dodoma ambapo Mwakilishi Mkazi wa FAO nchini Tanzania Dkt. Tipo ametumia nafasi hiyo, pia kujitambulisha na kumpongeza Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kukurwa kwa kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi.

Akizungumza Katika kikao hicho Mhe. Balozi Dkt. Bashiru amesema serikali ya awamu ya sita imetoa kipaumbele kwenye bajeti kwa sekta za uzalishaji ikiwemo kilimo, mifugo na uvuvi, hivyo juhudi zinazofanywa na FAO katika  sekta za  uzalishaji ni  ishara ya kuimarisha uchumi wa wananchi, na kumhakikishia Dkt. Tipo kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi  na FAO zitaendelea kushirikiana  katika kuendeleza sekta hiyo ili kuimarisha uchumi wa wananchi na usalama wa chakula .

Naye, Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO)  Dkt. Nyabenyi Tipo amesema Tanzania imendelea kupiga hatua katika kuchangia  ukuaji wa pato la taifa kupitia sekta za uzalishaji na kamba FAO itaendelea kushirikiana na Tanzania ili kuongeza mchango wa sekta hiyo katika pato la taifa kutoka asilimia 5 ya sasa hadi kufikia asilimia 6.5 katika mwaka unakuja.

FAO imekuwa ikishirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika sekta za mifugo na uvuvi ikiwemo udhibiti wa magonjwa kupitia mpango wa utoaji chanjo, miradi ya ukuzaji viumbe maji pamoja na uwezeshaji wa wafugaji na wavuvi kuongeza uzalishaji na usalama wa chakula.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Kushoto) akisalimiana na  Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Nchini Tanzania, Dkt. Nyabenyi Tipo alipofika kujitambulisha kwa waziri katika Ofisi ndogo za wizara zilizopo Kambarage Tower Jijini Dodoma, Leo Tarehe 29 Januari, 2026.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Kushoto) na  Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Nchini Tanzania, Dkt. Nyabenyi Tipo wakijadiliana jinsi ya kuimarisha ushirikiano baina ya wizara na FAO katika kuendeleza sekta za uzalishaji nchini, Leo Tarehe 29 Januari, 2026 katika Ofisi ndogo za Wizara zilizopo Kambarage Tower Jijini Dodoma.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Katikati) akizungumza na  Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Dkt. Nyabenyi Tipo (wapili kulia) alipofika kujitambulisha kwa waziri katika Ofisi ndogo za wizara zilizopo Kambarage Tower Jijini Dodoma, Leo Tarehe 29 Januari, 2026.


SERIKALI YAELEZA MKAKATI WA WA KUENDELEZA MINADA YA MIFUGO

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, imeeleza mkakati wa Serikali wa kuendeleza Mnada wa Mifugo wa Magena uliopo mpakani, kwa lengo la kukuza biashara ya mifugo na kurahisisha usafirishaji wa mifugo kwenda katika nchi jirani. 

Hayo yamesemwa Leo Januari 29,2026 Bungeni Dodoma na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Kamani, wakati akijibu la swali la mbunge wa Tarime Mjini Mhe. Esther Matiko,aliyetaka kujua  mkakati wa Serikali wa kuendeleza mnada wa Mifugo wa Magema, amesema Mnada wa Magena.

“Katika jitihada za kuendeleza mnada huo, serikali imeendelea kuboresha miundombinu muhimu ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022, kiasi cha shilingi milioni 175.65 kilitengwa na kutumika kujenga mazizi, kipakilio, birika la maji pamoja na vyoo, na miundombinu hiyo imekamilika.”Mhe. Kamani.

Aidha, amesema kuwa pamoja na uwepo wa miundombinu hiyo, Mnada wa Magena bado haufanyi vizuri kutokana na changamoto mbalimbali zikiwemo utoroshaji wa mifugo kwenda nchi jirani unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu, hali inayosababisha idadi ndogo ya mifugo kupelekwa kwenye mnada huo.

Amesema kuwa Ili kukabiliana na changamoto hizo na kuongeza mapato yatokanayo na biashara ya mifugo, Wizara yake  kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa (TAMISEMI) inaendelea kutoa elimu na kuhamasisha wadau kutumia mnada wa Magena kama ilivyokusudiwa wakati wa kuanzishwa kwake, sambamba na kuimarisha udhibiti wa utoroshaji wa mifugo.

Wakati huohuo ameongeza kuwa Serikali inahakikisha kuwa wakulima wazao la mwani wanapata tija kutokana na zao hilo kwa kuwapa elimu na kuwahamasisha kutengeneza vikundi Ili kuweza kupata soko Kwa uharaka.




Jumatano, 28 Januari 2026

KAMANI ATAJA MIKAKATI YA SERIKALI KUONGEZA MAENEO YA MALISHO

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeanza kutekeleza mkakati wa miaka mitano wa kuongeza maeneo kwa ajili ya shughuli za ufugaji kwa kutenga hekta milioni 2.51, ikiwa ni sehemu ya kuongeza maeneo yaliyopimwa na kutengwa kwa shughuli za ufugaji kutoka hekta milioni 3.49 hadi hekta milioni sita kama ilivyoahidiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi  (CCM) ya mwaka 2025- 2030 na hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa kufungua Bunge la 13 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mwezi Novemba 14, 2025.

Kauli hiyo ya serikali imetolewa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani  leo Januari 28, 2026 Bungeni Jijini Dodoma wakati akijibu Swali la Mbunge wa Ngorongoro Mhe. Yannick Ikae Ndoyinyo lililohoji serikali inampango gani wa kuongeza maeneo ya malisho kutoka hekta milioni Tatu hadi hekta milioni sita kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) inavyosema?.

“Mhe. Spika Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na wizara, idara na taasisi  zenye majukumu ya kisheria ya kupanga na kutekeleza mipango ya matumizi bora ya ardhi tumeanza kuandaa mkakati wa miaka mitano wa kutenga hekta milioni 2.51 kwa ajili ya shughuli za ufugaji, wakati wa utekelezaji wa mkakati huu waheshimiwa wabunge wote watashirikishwa” alisema Mhe. Kamani. 

Aidha, Mhe. Kamani amesema wizara itaendelea kutoa taarifa na elimu kwa wafugaji kote nchini kupitia vyombo vya habari kuhusu mabadiliko ya tabianchi ili kuwasaidia wafugaji kuchukua tahadhari ya kuikinga mifugo yao, pia katika kutafuta unafuu wa changamoto ya malisho serikali imeshusha bei ya mbegu za malisho kutoka shilingi 4,000 kwa kilo hadi shilingi 1,000.






DTK. BASHIRU AITAKA TADB KUONGEZA WIGO WA MIKOPO SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa( Mb.) amekutana na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TABD) na kufanya mazungumzo  na yanayolenga kuendeleza ushirikiano kati ya wizara na benki hiyo  na kuitaka kuendeleza miradi ya sekta za mifugo na uvuvi.

Mazungumzo hayo yamefanyika leo 27 Januari 2026 katika ofisi ndogo ya wizara hiyo iliyopo Kambarage Tower Jijini Dodoma, ambapo Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TADB alifika kujitambulisha kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi na kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara hiyo na Benki ya TADB katika kuendeleza sekta za Mifugo na Uvuvi.

Katika Mazungumzo hayo Mhe. Balozi Dkt. Bashiru ameipongeza Benki ya TADB kwa jinsi inavyoshirikiana na wizara na kuiagiza  kupanua wigo wa kuwasaidia wafugaji wadogo kupata mikopo nafuu ili waweze  kuendeleza miradi yao, pamoja na kuongeza ushiriki wa Taasisi za kifedha kupitia TADB katika kutoa mikopo kwenye Sekta ya Mifugo na Uvuvi.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa TADB Bw. Frank Nyabundege  amempongeza Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kwa kuteuliwa kuwa Mbunge na Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi  na kuahidi kuongeza kasi ya utoaji mikopo kwenye Sekta ya Mifugo na Uvuvi hasa kwenye miradi inayowalenga vijana na wanawake.

Aidha,  Bw. Nyabundege aliwasilisha taarifa  fupi kuhusu ushiriki wa TADB katika Maendeleo ya Sekta ya Mifugo na Uvuvi  nchini ambapo kupitia TADB kama  Benki ya  Kisera  inashirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika kutekeleza miradi mbalimbali inayolenga kuleta maendeleo katika Sekta ya Mifugo na Uvuvi ikiwemo  Benki kutoa mikopo ya mradi wa boti, ufugaji samaki kwa njia ya vizimba na  mikopo ya vijana kupitia Programu ya BBT mifugo. 

Kupitia mikopo ya miradi ya boti na vizimba TADB ilipokea kiasi cha Shilingi Bilioni 34.9 kwa ajili ya kutekeleza mradi ambapo hadi sasa kiasi cha Shilingi Bilioni 29.83 kimetolewa kwa wanufaika 5,932 katika mikoa 16 hapa nchini. 

Aidha, TADB kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefanikiwa kutoa jumla ya  boti 219 na vizimba 536 kwa wanufaika wa miradi.  Aidha, kwa kupitia mradi wa vijana wa BBT Mifugo, kiasi cha Shilingi Milioni 847.3 kimetolewa kwa wanufaika 106 kwa miradi ya mikopo isiyo na riba. 

Bw. Nyabundege aliongezea kuwa TADB  imewasilisha ushiriki wake katika kutoa mikopo katika Sekta ndogo ya Maziwa nchini kupitia Mradi wake wa TI3P ambapo kiasi cha Shilingi  bilioni 40 kimetolewa kwa wafugaji na  wasindikaji wa maziwa nchini. Aidha, kupitia mradi wa TI3P TADB imefanikiwa kurekebisha na kujenga vituo 23 vya kukusanya maziwa vyenye thamani ya Shilingi bilioni 1.1 kwa kushirikiana wafugaji,Wizara, Halmashauri na wasindikaji wa maziwa.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wa kwanza, kushoto) akitoa maelekezo  kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) Bw. Frank Nyabundege (wa pili, kulia) alipofika kujitambulisha kwa waziri leo Januari 27, 2026 Ofisi ndogo ya Wizara iliyopo Kambarage Tower, Jijini Dodoma.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa  akitoa maelekezo wakati akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) leo Januari 27, 2026 Ofisi ndogo ya Wizara iliyopo Kambarage Tower, Jijini Dodoma.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) Bw. Frank Nyabundege akitoa taarifa kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kuhusu utekelezaji wa miradi ya sekta za mifugo na uvuvi alipofika kujitambulisha kwa waziri leo Januari 27, 2026 Ofisi ndogo ya Wizara iliyopo Kambarage Tower, Jijini Dodoma.


Jumanne, 27 Januari 2026

VCT YASAJILI WATAALAM WA MIFUGO 293 WENYE SIFA STAHIKI

Na. Stanley Brayton, WMUV

Vituo 130 vya Huduma za Afya ya Wanyama vysajiliwa.

Baraza la Veterinari Tanzania (VCT) limekamilisha mapitio na kusajili Wataalam wa Wanyama wenye sifa stahiki, pamoja na kusajili Vituo mbalimbali vya kutoa Huduma za Afya ya Wanyama, ikiwa ni moja ya utekelezaji wa Sheria ya Veterinari SURA 319.

Akizungumza katika Kikao cha 62 cha Baraza cha kujadili utekelezaji wa shughuli za Baraza hilo kwa Robo ya pili ya mwaka wa 2025/2026, leo Januari 27, 2026 Dodoma, Mwenyekiti wa Baraza la Veterinari Tanzania (VCT), Prof. Lughano Kusiluka amesema Baraza limepitia na kuridhia kuwapa usajili watoa Huduma za Afya ya Wanyama 293 na Vituo 130 vya utoaji Huduma za Afya ya Wanyama.

“usajili huu umefanyika kwa kuzingatia Sheria ya Veterinari SURA 319, kwa kuangalia vigezo mbalimbali stahiki.” amesema Prof. Kusiluka

Aidha, Prof. Kusiluka amewataka Wataalam hao na Vituo hivyo kutoa Huduma hizo kwa uweledi na utaalam kwa wafugaji na kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu za nchi katika kutoa Huduma hizo ambazo zimewekwa katika Sheria ya Veterinari.

Vilevile, Prof. Kusiluka amewataka wafugaji kuwatumia Wataalam hao ambao wamesajiliwa  na Baraza kwa kufuata Sheria ili kuepukana na athari ambazo zinaweza kuleta madhara katika Mifugo yao, yatokanayo na Wataalam wasiosajiliwa.

Kwa Upande wake, Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania (VCT) ambaye pia ni Katibu wa Baraza hilo, Dkt.  Amani Kilemile amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Waziri wake mwenye dhamana, Mhe. Bashiru Ally Kakurwa inaendelea kuhakikisha kuwa wafugaji na Mifugo wanapata Huduma Bora ambayo inatolewa na Wataalam ambao wamethibitishwa na kupewa Usajili pamoja na leseni kutoka Mamlaka husika.


Mwenyekiti wa Baraza la Veterinari Tanzania (VCT), Prof. Lughano Kusiluka, akielekeza jambo kwa Wajumbe wa Baraza hilo kuhusu Usajili wa Wataalam wa Huduma za Afya ya Wanyama, katika Kikao cha 62 cha Baraza cha kujadili utekelezaji wa shughuli za Baraza hilo kwa Robo ya pili ya mwaka wa 2025/2026, kilichofanyika katika Ukumbi wa Royal Village, Januari 27, 2026 Dodoma.

Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania (VCT) ambaye pia ni Katibu wa Baraza hilo, Dkt. Amani Kilemile, akielezea hali ya maombi ya Vituo vya kutolea Huduma za Afya ya Wanyama, katika Kikao cha 62 cha Baraza cha kujadili utekelezaji wa shughuli za Baraza hilo kwa Robo ya pili ya mwaka wa 2025/2026, kilichofanyika katika Ukumbi wa Royal Village, Januari 27, 2026 Dodoma.

Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo Nchini, Dkt. Benezeth Lutege, akichangia hoja, katika Kikao cha 62 cha Baraza cha kujadili utekelezaji wa shughuli za Baraza hilo kwa Robo ya pili ya mwaka wa 2025/2026, kilichofanyika katika Ukumbi wa Royal Village, Januari 27, 2026 Dodoma.

Wakili Mwandamizi Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bi. Mariam Haji, akitoa ushauri wa kisheria katika kupitisha maombi ya Wataalam na Vituo vya Huduma za Afya ya Wanyama, katika Kikao cha 62 cha Baraza cha kujadili utekelezaji wa shughuli za Baraza hilo kwa Robo ya pili ya mwaka wa 2025/2026, kilichofanyika katika Ukumbi wa Royal Village, Januari 27, 2026 Dodoma.

Baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Veterinari Tanzania (VCT) wakipitia Orodha na maombi ya Vituo mbalimbali vya kutolea Huduma za Afya ya Wanyama, wakiwa katika Kikao cha 62 cha Baraza cha kujadili utekelezaji wa shughuli za Baraza hilo kwa Robo ya pili ya mwaka wa 2025/2026, kilichofanyika katika Ukumbi wa Royal Village, Januari 27, 2026 Dodoma.

Picha ni baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Veterinari Tanzania (VCT) wakiwa katika Kikao cha 62 cha Baraza cha kujadili utekelezaji wa shughuli za Baraza hilo kwa Robo ya pili ya mwaka wa 2025/2026, kilichofanyika katika Ukumbi wa Royal Village, Januari 27, 2026 Dodoma.





MHE. KAMANI AINADI MAMLAKA YA UVUVI BUNGENI

◼️Agusia pia uwekezaji kwenye Viwanda vya nyama

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani amelieleza Bunge kuwa katika kukabiliana na changamoto ya Uvuvi usiofuata sheria Serikali kupitia Wizara yake ipo kwenye hatua za mwisho za kuanzisha mamlaka ya Uvuvi itakayofanikisha kudhibiti changamoto hiyo kwenye maeneo yote ya Uvuvi nchini.

Mhe. Kamani amesema Januari 27,2026 Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu maswali ya wabunge mbalimbali waliotaka kufahamu hatua ambazo Serikali imechukua katika kudhibiti vitendo vya Uvuvi usiofuta Sheria ambapo amesema kuwa hatua hiyo itarahisisha utekelezaji wa Mpango kabambe wa sekta ya Uvuvi wa mwaka 2021-2037 wenye kipumbele cha kuanzisha, kufufua, kuendeleza na kuimarisha viwanda vya kuchakata mazao ya Uvuvi nchini.

“Mhe. Spika ili kuhakikisha viwanda vyetu vinafanya kazi kulingana na matarajio ya Serikali, Wizara ipo katika hatua za maamuzi kulingana na taratibu za Serikali  kuanzisha mamlaka ya Uvuvi kwa lengo la Usimamizi wa rasilimali za Uvuvi na kupambana na Uvuvi usiozingatia sheria” Amesema Mhe. Kamani.

Aidha Mhe. Kamani amebainisha hatua za awali ambazo Wizara yake imezitekeleza ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa malighafi ya samaki ikiwa ni pamoja na kuweka maboya 32 yenye thamani ya shilingi milioni 224 katika eneo la Uchelele mkoani Mwanza.

Mhe. Kamani ameongeza kuwa Wizara yake imeendelea kuhamasisha ufugaji samaki kwa njia ya Vizimba ili kuongeza kiwango cha upatikanaji wa samaki na kuchochea uwekezaji wa sekta binafsi kwenye viwanda.

Akijibu swali linalohusiana na mikakati ya Serikali kwenye ujenzi wa Viwanda vya nyama, Mhe. Kamani amesema kuwa Wizara yake inaendelea kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ili wawekeze kwenye eneo hilo huku pia akisisitiza kuendelea kuhamasisha wafugaji wote nchini kufuga kisasa ili viwanda hivyo viweze kupata mazao yenye ubora.



Jumatatu, 26 Januari 2026

DKT. BASHIRU AZIAGIZA LITA, TARILI KUFANYA MAGEUZI SEKTA YA MIFUGO

 Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa ameitaka Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (LITA) na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) kutumia mafunzo na tafiti za mifugo za kisasa  kuwanufaisha wafugaji nchini.

Mhe. Balozi Dkt. Bashiru ametoa agizo hilo leo Januari 24, 2026 wakati wa ziara yake kwenye taasisi hizo zilizopo Mabuki mkoani Mwanza, ambapo amesema tafiti na mafunzo  ya mifugo yanayoendana na wakati yatumike kuwabadilisha wafugaji kufuga kisasa.

“Utafiti wetu mzuri, mafunzo yetu mazuri vitumike kwenda kubadilisha wafugaji, sisi tuwachague wale ambao wameshabadilika na wamewekeza , tuwape utaalam zaidi ili watumike kama wasambazaji wa teknolojia” alisema Mhe. Balozi Dkt. Bashiru.

Aidha, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru aliitaka LITA kufanya ufuatiliaji wa utaalam unaotolewa kwa wafugaji kutokana na mafunzo yanayotolewa na Wakala huo huku TALIRI ikiagizwa kufuatilia matumizi ya tafiti kutoka kwa wadau wa sekta ya mifugo.

Katika hatua nyingine alihimiza wataalam kuzingatia maadili ya taaluma katika kuwahudumia wafugaji ili kuimarisha ushirikiano utakaokuza sekta ya mifugo nchini.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa  akitoa maelekezo  kwa Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (LITA) na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) kuhusu mageuzi ya sekta ya mifugo nchini wakati wa ziara yake  kwenye  taasisi hizo leo Januari 24, 2026 Mabuki, Mkoani Mwanza.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wapili, kulia) akizungumza na baadhi ya wanafunzi wanasoma  katika Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (LITA)  wakati alipotembelea  kukagua shughuli zinazofanywa na wakala hao leo Januari 24, 2026 Mabuki, Mkoani Mwanza.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kulia) akikagua Mitamba inayopatikana katika shamba la kuzalishia mifugo la Mabuki wakati wa Ziara yake  leo Januari 24, 2026 Mabuki, Mkoani Mwanza.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kulia) akikagua Mitamba inayozalishwa katika shamba la kuzalishia mifugo la Mabuki wakati wa Ziara yake  leo Januari 24, 2026 Mabuki, Mkoani Mwanza.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Wa nne, Kushoto) akikagua Mbegu ya Mbuzi  wanaozalishwa na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) wakati alipotembelea taasisi hiyo leo Januari 24, 2026 Mabuki, Mkoani Mwanza.


TAWFA YAJIVUNIA MAFANIKIO WALIYOYAFIKIA, WAISHUKURU SERIKALI

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake wanaojishughulisha na Uvuvi Tanzania (TAWFA), Bi. Beatrice Mmbaga amekutana na Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agness Meena, Jijini Dodoma Januari 22, 2026 kwa lengo la kuishukuru serikali na kueleza mafanikio waliyoyapata  tangu kuanzishwa kwake mwaka 2019. 

Mwenyekiti huyo  wa TAWFA, Bi. Mmbaga akiwasilisha taarifa yake ya mafanikio alisema  kuwa TAWFA imefanikiwa kuanzisha kanda mbalimbali ikiwemo  Kanda ya Maji ya Bahari na Pwani, Kanda ya Ziwa Tanganyika, Kanda ya Ziwa Victoria pamoja , Kanda ya Ziwa Nyasa na Maji Madogo huku akifafanua kuwa hatua hiyo imeongeza ushiriki wa wanawake, upatikanaji wa mitaji elimu na vitendea kazi. 

“Zaidi ya wanawake 2000 wa TAWFA wamefaidika na VICOBA kwa kupata mikopo yenye riba nafuu yenye thamani ya Tshs. zaidi ya 160,000,000, huku TAWFA ikiendelea  kuimarika kwa kitambulika kikanda na Kimataifa ambapo sasa ni mwanachama wa World FisherFolks na African Women FishWorkers Association (AWFISHNET)”, alibainisha Bi. Mmbaga

Akiwasilisha taarifa yake hiyo, Bi. Mmbaga alisema vipaumbele vyao mbalimbali ikiwemo kupata ithibati ya ubora ya TBS ili waweze kusafirisha bidhaa zao nje ya nchi, upatikanaji  wa vitambulisho, kuwaunganisha  wanachama wao na taasisi za kifedha pamoja na Masoko ya Nje na kuwawezesha Wanachama mafunzo ya uongozi na elimu ya namna ya kuendesha vikundi vyao huku wakiiomba wizara kuwasaidia vitendea kazi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agness Meena baada ya kusilikiliza taarifa yao hiyo aliwaeleza kuwa Wizara kama mlezi wao itaendelea kushirikiana na TAWFA kwa kuwaunganisha na taasisi mbalimbali za kifedha  pamoja na benki, hatua itakayowasaidia wanachama wa chama hicho kupata mikopo na mitaji kwa ajili ya kuendeleza shughuli za uvuvi.

Aidha, Bi. Meena aliwahimiza  viongozi hao wa TAWFA kuendelea kujiimarisha zaidi kwa lengo la kuweka misingi mizuri ya kujitegemea zaidi kiuchumi na kukuza shughuli zao ili kuimarisha mchango wa wanawake katika sekta ya uvuvi nchini huku akiwahimiza  kuanzisha vyama vya ushirika vya  kifedha (SACCOS) ili kuwawezesha wanachama kupata mitaji.  

Awali,  Mwakilishi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Bi. Prisca  Issangya alieleza kuwa  lengo la FAO ni kuinua wanawake kiuchumi kwa kuwawezesha kupata elimu na uwezo huku akiendelea kubainisha kuwa FAO iko tayari kushirikiana na TAWFA katika kuwaunganisha wanawake na mashirika ya fedha ili kuwasaidia kupata rasilimali zitakazowawezesha kukuza shughuli zao.

Picha ya pamoja ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, watendaji wa Wizara na viongozi wa TAWFA baada ya kikao cha kujadili maendeleo ya wanawake katika sekta ya mifugo na uvuvi  Januari 22, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agness Meena, akizungumza na viongozi wa TAWFA kuhusu umuhimu wakujiimsrisha zaidi Ili kuweza kujijengea uwezo wa kujitegemea kiuchumi, upatikanaji wa mitaji na kukuza ushiriki wa wanawake katika sekta ya mifugo na uvuvi Januari 22, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Mwenyekiti wa TAWFA Bi. Beatrice Mmbaga akiwasilisha taarifa ya mafanikio, changamoto na vipaumbele vya chama wakati wa kikao na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Januari 22, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Mwakilishi wa FAO, Bi. Prisca John, akitoa maelezo kuhusu mchango wa FAO katika kuinua wanawake katika sekta ya  uvuvi wakati wa kikao cha TAWFA kilichofanyika Januari 22, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Mkurugenzi Msaidizi wa Uvuvi Dkt. Baraka Sekadende akizungumza wakati wa kikao kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na viongozi wa TAWFA kilichofanyika Januari 22, 2026 Makao Makuu ya Wizara, Mtumba Jijini Dodoma


SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI KUONGOZWA KISAYANSI

Na. Edward Kondela

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amesema serikali itazingatia masuala ya kitaalamu, ushauri wa kisayansi na tafiti katika kuendeleza sekta za mifugo na uvuvi.

Mhe. Balozi Dkt. Bashiru amebainisha hayo leo (22.01.2026), alipofanya ziara ya kikazi katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kilichopo Mkoani Morogoro, ili kuweka pamoja makubaliano ya kushirikiana kati ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi na SUA.

Akizungumza na baadhi ya wanachuo, wakati akijionea shughuli mbalimbali zinazofanywa chuoni hapo, amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amemuelekeza kuzingatia masuala ya kitaalamu, ushauri wa kisayansi na tafiti katika kuendeleza sekta za mifugo na uvuvi.

“Wizara imepewa maelekezo ya Mhe. Rais pamoja na Dira ya Maendeleo ya miaka 25 inatuelekeza kutoka kufuga kienyeji na kufuga kisasa pamoja na kufuga kwa tija na ufanisi.” Amefafanua Mhe. Balozi Dkt. Bashiru

Aidha, ameongeza kuwa SUA ni moja ya vyuo vyenye heshima nchini katika masuala ya mafunzo, ushauri wa kitaalamu na masuala ya utafiti kwenye kilimo, mifugo, uvuvi na misitu.

Amewataka wanachuo hao kusoma na baadae kufanya tafiti, kwa kuwa eneo la malisho ya mifugo lina biashara kubwa zikiwemo mbegu zake na kwamba wizara na SUA zimeunda kamati katika maeneo ya utafiti, mafunzo na ushauri wa kitaalamu, hususan katika ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba na mabwawa, malisho ya mifugo, maabara pamoja na kuongeza nguvu katika ufugaji wa kuku.

Awali, akizungumza wakati wa kikao kilichoshirikisha uongozi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na SUA, Makamu Mkuu wa chuo hicho Prof. Raphael Chibunda amesema kutokana na tasnia ya maziwa kuendelea kuku hapa nchini, chuo hicho kimeamua kuanzisha kozi kwa ajili ya kutoa wataalamu wa tasnia hiyo.

Amefafanua kuwa lengo la chuo ni kuboresha ili kila mhitimu anayetoka chuoni hapo awe na utaalamu wa kujitosheleza katika nyanja mbalimbali na kuweza kufanya kazi kwa ufasaha katika sekta binafsi na umma.

Pia, amesema kwa upande wa madaktari wa mifugo SUA imeendelea kuboresha vifaa vya kufundishia ili kuhakikisha wanatoka madktari wenye uwezo zaidi kadri muda unavyozidi kwenda.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Edwin Mhede akizungumzia uzalishaji wa vifaranga vya samaki, amesema ni wakati wa kuzingatia mbari za aina ya vifaranga ili kupata vinavyoweza kuzalishwa kwa muda mfupi.

Amesema ni muhimu kupatikana kwa vifaranga vya namna hiyo kulingana na uhitaji wa soko kwa kuwa watu wengi wamekuwa wakijikita katika ufugaji wa samaki.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kushoto), akiwa na Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dkt. Edwin Mhede wakati alipofanya ziara ya kikazi katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), kilichopo Mkoani Morogoro, ambapo alipata fursa ya kushuhudia hatua za uzalishaji wa vifaranga vya samaki. (22.01.2026)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa akipanda mbegu za malisho wakati alipofanya ziara ya kikazi Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), kilichopo Mkoani Morogoro. (22.01.2026)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kushoto), akishuhudia namna wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), kilichopo Mkoani Morogoro, wakimfanyia upasuaji paka katika hospitali ya rufaa ya wanyama iliyopo chuoni hapo. (22.01.2026)

Baadhi ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), kilichopo Mkoani Morogoro, wakifurahia jambo na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kulia), alipofanya ziara ya kikazi chuoni hapo na kutembelea hospitali ya rufaa ya wanyama. (22.01.2026)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, akipatiwa maelezo juu ya uzalishaji wa vifaranga vya samaki aina ya kambale, baada ya kufanya ziara ya kikazi katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), kilichopo Mkoani Morogoro. (22.01.2026)

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), kilichopo Mkoani Morogoro, Prof. Raphael Chibunda (kulia), akizungumza na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kushoto) na Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dkt. Edwin Mhede wakati Mhe. Balozi Bashiru alipofanya ziara ya kikazi katika chuo hicho ili kuimarisha ushirikiano na makubaliano kati ya wizara na SUA kwenye masuala ya kitaalamu, ushauri wa kisayansi na tafiti. (22.01.2026)