SERIKALI KUJENGA VIWANDA VIWILI VYA KUZALISHA CHAKULA CHA SAMAKI
Na. Stanley Brayton, WMUV Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeanza Mkakati wa kujenga Viwanda viwili vya chakula cha Samaki ili kuhakikisha chakula hicho kinapatikana kwa wingi na kwa urahisi zaidi, hatua ambayo itatatua changamoto za upatikanaji wa chakula hicho kwa wavuvi. Akizungumza leo Machi 18, 2026 jijini Mwanza katika Kikao cha kujadili Mwongozo wa hiari wa kusimamia wavuvi wadogo, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agness Kisaka Meena amesema kwa sasa Serikali ina Mpango wa kujenga Viwanda viwili vya kuzalisha chakula cha Samaki, Viwanda ambavyo vitajengwa Kilwa na Mwanza. "Viwanda hivi vitajengwa kupitia Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO), na Serikali inategemea viwanda hivi vitakuwa msaada kwa wavuvi na wakuzaji Viumbemaji wote nchini" amesema Bi. Meena Aidha, Bi. Meena amebainisha kuwa kwa kipindi cha nyuma wavuvi walikuwa wanashida sana na vyakula vya Samaki kiasi cha kupelekea vyakula hivyo kuagizwa kutoka nchi za nje na kuwa vya gharama zaidi,...