TANZANIA KUWA NA MKAKATI MAALUM WA MAWASILIANO WAKATI WA MLIPUKO WA MAGONJWA YA MIFUGO
Na. Chiku Makwai – ARUSHA Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (WOAH), kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, limeanza mchakato wa kuandaa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, hatua inayolenga kuimarisha uwezo wa nchi katika kuzuia, kudhibiti na kukabiliana na milipuko ya magonjwa ya mifugo. Warsha ya kuandaa rasimu hiyo imefunguliwa leo, Juni 1, 2026, katika Ukumbi wa Masailand Hall jijini Arusha na Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo, Dkt. Benezeth Lutege, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Agness K. Meena. Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, Dkt. Lutege amesema mawasiliano yenye ufanisi ni nyenzo muhimu katika kudhibiti na kukabili milipuko ya magonjwa ya mifugo kwa kuwa huwezesha utoaji wa taarifa sahihi kwa wakati kwa wadau wote wanaohusika. Amesema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo ya tahadhari na mwitikio wa haraka ili kuhakikisha magonjwa ya mifugo yanagunduliwa na kudhibitiwa mapem...