Nav bar

Jumanne, 28 Oktoba 2025

SERIKALI YAENDELEA KUTOA MAFUNZO YA UPANDIKIZAJI VIFARANGA VYA SAMAKI KWENYE VIZIMBA NA MABWAWA

Na. Stanley Brayton, MWUV

◾ Vifaranga 1,500 vya pandikizwa Viwanja vya Maonesho Nanenane Dodoma.

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea kutoa Mafunzo ya Upandikizaji Vifaranga vya Samaki ili kuwafanya wadau wa Sekta hiyo kuwa na Ujuzi wa kutosha katika kufuga Samaki pamoja na kuwasaidia kuwapa mbinu bora na ya kisasa ya ufugaji Samaki ili kuweza kujipatia kipato na lishe.

Akizungumza katika zoezi hilo la Upandikizaji wa Vifaranga vya Samaki katika Viwanja vya Maonesho ya Nanenane ya Dkt. John Samwel Malecela, leo Oktoba 28, 2025 jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Nazael Madalla amesema lengo kubwa la kupandikiza Samaki katika Vizimba na Mabwawa yaliopo katika Viwanja vya Maonesho ya nanenane ni kuwawezesha wadau wa Sekta kupata Mafunzo ya teknolojia mpya ya ufugaji wa Samaki kwa njia ya Vizimba pamoja na Mabwawa.

"Wizara inaendelea kuhamisha, kuendeleza pamoja na kusimamia shughuli za Ukuzaji Viumbe Maji kwa kutoa Mafunzo mbalimbali ya Ufugaji wa Samaki kwa vitendo kupitia Vizimba na Mabwawa yaliopo Maeneo ya Maonesho ya Nanenane, hivyo ni vyema wadau Kutembelea Maeneo hayo ili kujifunza mbinu bora ya Ufugaji wa Samaki kwa njia hiyo" alisema Dkt. Madalla

Aidha, Dkt. Madalla amesema kuwa hii yote ni kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuwa Huduma za Ugani na kutoa elimu juu ya Ukuzaji Viumbe Maji ziendelee kufanyika ata baada ya kuisha kwa Maonesho ya Nanenane.

Vilevile, Dkt. Madalla ameweka wazi kuwa utekelezaji wa agizo hilo unaendelea kwa ukamilifu na ndio mana siku ya leo wameanza kwa kupandikiza Vifaranga vya Samaki 1,500 katika Mabwawa matatu na kizimba kimoja, na matarijo ya Wizara ni kuwa wadau wengi wa Sekta watapata elimu ya kutosha ya Ukuzaji Viumbe Maji kwa vitendo.

Pia, Dkt. Madalla amewaweka wazi swala la Ufugaji Samaki ni moja ya shughuli muhimu ya Uchumi wa Buluu ambao unaweza wanufaisha wafugaji kwa kuboresha maisha yao na maendeleo ya Taifa kiujumla.

Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji, Dkt. Nazael Madalla (wa pili kulia aliyeshika ndoo), akipandikiza Vifaranga vya Samaki kwenye Bwawa, katika zoezi la Upandikizaji wa Vifaranga hivyo katika Maeneo ya Maonesho ya Nanenane ya Dkt. John Samwel Malecela, Oktoba 28, 2025, Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji, Dkt. Nazael Madalla (wa kwanza kulia), akilisha chakula Samaki wa kwenye Bwawa, katika zoezi la Upandikizaji wa Vifaranga hivyo katika Maeneo ya Maonesho ya Nanenane ya Dkt. John Samwel Malecela, Oktoba 28, 2025, Dodoma.

Maafisa Ukuzaji Viumbe Maji, wakiandaa Vifaranga kwa ajili ya kupandikiza kwenye Vizimba na Mabwawa, katika zoezi la Upandikizaji wa Vifaranga hivyo katika Maeneo ya Maonesho ya Nanenane ya Dkt. John Samwel Malecela, Oktoba 28, 2025, Dodoma.

Picha ni Muonekano wa Vifaranga vya Samaki vikiwa tayari kwa ajili ya kupandikiza kwenye Vizimba na Mabwawa yaliopo Maeneo ya Maonesho ya Nanenane ya Dkt. John Samwel Malecela, wakati wa zoezi la Upandikizaji wa Vifaranga hivyo leo, Oktoba 28, 2025, Dodoma.


Jumatatu, 27 Oktoba 2025

WAVUVI ZIWA NYASA WAKABIDHIWA MTAMBO WA KUKAUSHIA DAGAA NA SOKO LA KUUZIA SAMAKI

Na. Stanley Brayton, MWUV

◾ Wavuvi waahidiwa Vizimba vya kufugia Samaki.

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Taasisi isiyo ya Serikali ya elico Foundation imeikabidhi Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa, Soko la kuuzia Samaki na Mtambo wenye Thamani ya Milioni 129.98 kwa ajili ya kukaushia Dagaa ikiwa na uwezo uliosimikwa wa kukausha mazao hayo kwa wastani wa tani 3 hadi 5 kwa siku, mradi ambao umelenga kuongeza uzalishaji wa mazao hayo yenye kuathiriwa na changamoto ya hali ya tabia ya nchi ambao ulipelekea uchakataji wa zao hilo kuwa duni.

Akizungumza katika Hafla ya Uzinduzi na Kukabidhi Mtambo huo, leo Oktoba 24, 2025, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede amesema Sekta ya Uvuvi imekuwa ikikabiliwa na upotevu mkubwa wa mazao ya uvuvi baada ya kuvunwa, hasa kwa dagaa ambao mara nyingi uharibika kutokana na kukaushia chini, na wakati mwingine mazao hayo hukutana na mchanga, matope, au mvua, na hivyo kupunguza ubora wake, bei yake sokoni na hata kuathiri afya za walaji.

"Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo, imeendelea kuwekeza kwenye miundombinu ya kisasa ikiwemo mitambo ya kukaushia dagaa kwa kutumia nishati ya jua, na leo tunaenda kukabidhi mtambo wenye uwezo wa kukausha dagaa tani 3 hadi 5 kwa siku ambapo dagaa hao wanakuwa na thamani ya Milioni 10.5 hadi Milioni 17.5." alisema Dkt. Mhede

Aidha, Dkt. Mhede amebainisha kuwa Miundombinu hiyo ni uwekezaji katika teknolojia rafiki kwa mazingira endelevu ya mbinu bora za uchakataji wa mazao ya uvuvi, ambazo zitaleta manufaa makubwa kwa wadau wa Sekta hiyo katika kupunguza upotevu wa mazao ya uvuvi baada ya kuvunwa, kuongeza ufanisi na tija katika shughuli za uvuvi, kuboresha ubora na usalama wa samaki na dagaa ili bidhaa ziweze kukidhi viwango vya soko la ndani, Kikanda na kimataifa, na kuongeza kipato cha wavuvi na wachakataji wadogo pamoja na kuongeza thamani katika mnyororo wa uzalishaji.

Vilevile, Dkt. Mhede ameweka wazi kuwa wavuvi wakihakikisha bidhaa za uvuvi zinakuwa safi, bora na salama zinaweza kufungua fursa za masoko mapya, ikiwemo mataifa jirani na hata masoko ya kimataifa, na hii inatokana na Dira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ya kuhakikisha rasilimali za uvuvi zinachangia ipasavyo kwenye uchumi shindani na shirikishi.

Pia, Dkt. Mhede, amewaweka wazi kuwa sasa Serikali imeridhia kwa kuamua siku ya leo Soko la kuuzia Samaki Mbamba Bay lianze kutumika Rasmi na amewaahidi Wavuvi  hao Vizimba vya kufugia Samaki na kuwataka wavuvi, wachakataji na wafanyabiashara wa mazao ya uvuvi kutumia teknolojia hiyo kwa uangalifu na umakini mkubwa, kwani ni jukumu lao kuhakikisha uwekezaji huo wa thamani unaleta manufaa ya kudumu, na Serikali itaendelea kusimamia, kutoa mafunzo, pamoja na kuweka sera na kanuni rafiki ili wavuvi na wadau wengine wa Sekta hii waweze kufaidika na rasilimali hizi.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Nyasa ambaye ni Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, Ndg. Salumu Ismail amesema wao kama Wilaya wamepokea kwa Mikono miwili Mtambo huo na kuahidi kuutunza na kuusimamia katika shughuli zote za uzalishaji.

Ndg. Ismail, amesema teknolojia hiyo ya kisasa ya kukaushia Dagaa kwa kutumia Nishati ya jua na umeme itasaidia sana Wavuvi hasa wakati wa masika, na mazao yatakuwa salama kwani yataweza kukaushwa kwa wingi na kwa haraka zaidi.

Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Elico Foundation, Prof. Evelyne Mbede amesema wao wataendelea kushirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, na wapo tayari kuwasaidia Wavuvi nchini kote katika kuwapatia mitambo mingine ya kukaushia mazao ya Uvuvi.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede (aliyeshika Mkasi), akifurahia baada ya kukata utepe kama ishara ya Uzinduzi na Kukabidhi Mtambo wa kukaushia Dagaa, iliyofanyika katika Mwalo wa Mbamba Bay, Oktoba 24, 2025, Nyasa - Ruvuma.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede, akihutubia wadau wa Sekta ya Uvuvi, katika Hafla ya Uzinduzi na Kukabidhi Mtambo wa kukaushia Dagaa, iliyofanyika katika Mwalo wa Mbamba Bay, Oktoba 24, 2025, Nyasa - Ruvuma.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede (wa pili kushoto), akiweka Jiwe la Msingi, katika Hafla ya Uzinduzi na Kukabidhi Mtambo wa kukaushia Dagaa, iliyofanyika katika Mwalo wa Mbamba Bay, Oktoba 24, 2025, Nyasa - Ruvuma.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede (wa tano kulia), akikagua ubora wa Miundombinu ya Mtambo wa Kukaushia mazao ya Uvuvi, katika Hafla ya Uzinduzi na Kukabidhi Mtambo wa kukaushia Dagaa, iliyofanyika katika Mwalo wa Mbamba Bay, Oktoba 24, 2025, Nyasa - Ruvuma, wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji, Dkt. Nazael Madalla na wa nne kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Uvuvi Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ndg. Christian Nzowa.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede (kushoto aliyesimama), akipeana mkono wa pongezi kwa kazi nzuri ya Ujenzi wa Mtambo wa kukaushia mazao ya Uvuvi na Mwenyekiti wa Bodi ya Elico Foundation, Prof. Evelyne Mbede (wa pili kulia), wakati  wa Hafla ya Uzinduzi na Kukabidhi Mtambo wa kukaushia Dagaa, iliyofanyika katika Mwalo wa Mbamba Bay, Oktoba 24, 2025, Nyasa - Ruvuma.
Picha ni muonekano wa Mtambo wa kukaushia Dagaa, Mwalo wa Mbamba Bay, Oktoba 24, 2025, Nyasa - Ruvuma.




MEENA ATAKA USHIRIKIANO, TAASISI SITA ZA MIFUGO KUWA JENGO MOJA

Na. Edward Kondela

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena amezitaka taasisi sita kutoka sekta ya mifugo zinazojenga ofisi zake katika eneo la Njedengwa, jijini Dodoma, kusimamia ujenzi huo kwa ushirikiano ili ukamilike kwa wakati na viwango vinavyotarajiwa.

Bi. Meena amebainisha hayo leo (21.10.2025) kwenye tukio la utiaji sahihi wa mkataba wa ujenzi wa jengo la ofisi za makao makuu ya taasisi hizo, zilizo chini ya wizara na kukabidhi eneo kwa mkandarasi wa ujenzi wa jengo hilo, ambapo amesema kukamilika kwa ujenzi kutasaidia kuondokana na tatizo la ukosefu wa ofisi bora kwa watumishi.

Akizungumzia juu ya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Bodi ya Maziwa Tanzania (TDB), Bodi ya Nyama Tanzania (TMB), Wakala ya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA), Wakala ya Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA) na Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) ambazo zitakuwa kwenye jengo moja, amesema anatambua TALIRI ndiyo imeingia makubaliano ya kimkataba lakini taasisi zingine tano zisijiweke kando bali zishiriki katika kusimamia ujenzi huo.

Aidha, amemtaka mkandarasi wa ujenzi Kampuni ya CJIETC kutoka China na mkandarasi mshauri wa ujenzi Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), kufanya kazi kwa bidii na umahiri mkubwa ili ujenzi ukamilike kwa wakati na viwango vya juu kama ilivyoonyeshwa kwenye mkataba wa ujenzi wa miezi 24 pamoja na mwaka mmoja wa uangalizi.

Akizungumza kwa niaba ya wakuu wengine wa taasisi zitakazotumia jengo hilo baada ya kukamilika kwake, Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI Prof. Erick Komba, amesema wametumia mfumo ambao ofisi ya Waziri Mkuu ambayo inaratibu ujenzi wa majengo ya serikali jijini Dodoma, imeufurahia kwa taasisi hizo sita kutumia jengo moja katika eneo la ekari 10.

Pia, amesema ofisi ya Waziri Mkuu imesema itashawishi taasisi zingine zilizopo kwenye wizara mbalimbali kutumia mfumo huo wa kuwa na jengo moja, hivyo kurahisisha huduma kwa wananchi.

Naye Mkadiriaji Majenzi kutoka Kampuni ya CJIETC kutoka China Mhandisi Wencleaus Kiziba amesema watahakikisha wanakamilisha ujenzi huo kwa wakati na kulingana na bajeti ya fedha iliyotengwa pamoja na kuzingatia ubora.

Ujenzi wa jengo la ofisi za makao makuu ya TALIRI, TDB, LITA, TVLA, TMB na NARCO unatarajia kutumia takriban shilingi bilioni 54 zote kwa pamoja, ambapo mkandarasi atatekeleza kwa shilingi bilioni 49, TBA ambaye ni mshauri elekezi shilingi bilioni 4.5.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena (katikati), akiwa na viongozi wa taasisi za mifugo zilizo chini ya wizara hiyo wakati akikata utepe wa ujenzi wa jengo la ofisi za makao makuu ya TALIRI, TDB, LITA, TVLA, TMB na NARCO katika eneo la Njedengwa, jijini Dodoma. (21.10.2025)

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena, akiwa kwenye picha ya pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Prof. Erick Komba na mwakilishi wa Kampuni ya CJIETC kutoka China ambayo itajenga jengo la ofisi za makao makuu ya TALIRI, TDB, LITA, TVLA, TMB na NARCO katika eneo la Njedengwa, jijini Dodoma na kushuhudia kazi ya kusafisha eneo hili ikiwa imeshaanza. (21.10.2025)

Muonekano wa picha ya jengo litakalojengwa katika eneo la Njedengwa jijini Dodoma kwa ajili ya ofisi za makao makuu ya taasisi sita zilizo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambazo ni TALIRI, TDB, LITA, TVLA, TMB na NARCO ambapo ujenzi wake utagharimu takriban shilingi bilioni 54 hadi kukamilika kwake. (21.10.2025)

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena (aliyekaa kulia), akishuhudia utiaji sahihi kati ya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) na Kampuni ya CJIETC kutoka China ambayo itajenga jengo la ofisi za makao makuu ya TALIRI, TDB, LITA, TVLA, TMB na NARCO katika eneo la Njedengwa, jijini Dodoma. (21.10.2025)

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena (kulia), Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Prof. Erick Komba (katikati) na mwakilishi wa Kampuni ya CJIETC kutoka China ambayo itajenga jengo la ofisi za makao makuu ya TALIRI, TDB, LITA, TVLA, TMB na NARCO katika eneo la Njedengwa, jijini Dodoma, baada ya kutia sahihi mkataba wa ujenzi wa jengo hilo. (21.10.2025)



SERIKALI KUSHIRIKIANA NA WADAU KUBORESHA LISHE

Na. Martha Mbena, Dodoma. 

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imesema itaendelea kushirikiana na wadau wa kitaifa na kimataifa kutekeleza mikakati inayolenga kuboresha sekta ya lishe kwa kuifanya kuwa na mifumo endelevu nchini.

Hayo yameelezwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi,  Dkt. Edwin Mhede wakati akifungua kikao cha kujadili  mradi wa Initiative on Climate Action and Nutrition (I-CAN) kilichofanyika  leo Oktoba 16, 2025 katika Hoteli ya Rafiki Jijini Dodoma. 

Dkt.  Mhede amesema serikali inafanya kazi na wadau na mashirika mbalimbali kwa kufanya majadiliano ya  jinsi ya kuoanisha masuala ya kisera katika mabadiliko ya tabianchi na lishe bora.

"Yaliyojadiliwa kwenye kikao cha leo yawe chachu ya kuifanya sekta hii ya lishe isogee mbele zaidi lakini mkakati wa mapitio ya sera kuhusu masuala ya lishe ni jambo la muhimu ", amesema Dkt. Mhede.

Amesema wananchi wanategemea kupata afua za serikali zinazohimiza  matumizi ya nishati safi ya  kupikia ambayo ni rafiki kwa mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

Naye, Mkuu wa miradi  kutoka Shirika la Global Alliance for Improved Nutrition (GAIN) Dkt. Winfrida Mayilla amesema kikao hicho kimelenga  kuyatambua masuala ya hali ya hewa na uhusiano wake kwenye lishe na kwa kuzingatia sera za nchi.

"Tuko hapa na wadau mbalimbali kuhakikisha kwamba sera zetu za Nchi hasahasa sera ya chakula na lishe inaingiza mikakati ya kuboresha mabadiliko haya ya tabianchi na tuje na mbinu mbalimbali ili  tukifanya kazi kwa pamoja ilenge kuboresha afya na lishe za watanzania" amesema Dkt. Mayilla.

Kikao cha mradi wa Initiative on Climate Action and Nutrition (I-CAN) kimejadili mabadiliko ya tabianchi, lishe bora pamoja na sera za kitaifa na uhusiano wake katika kuwekeza kwenye kilimo, ufugaji na uvuvi unaostahimili mabadiliko ya hali ya hewa.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede akiongea kwenye kikao cha kujadili mradi wa Initiative on Climate Action Nutrition (I-CAN) ambao umelenga kuboresha utekelezaji wa sera za lishe katika sekta za kilimo, Mifugo na Uvuvi, kikao hicho kimefanyika katika Hoteli ya Rafiki, jijini Dodoma Oktoba 16, 2025.

Mkuu wa Miradi Shirika la GLOBAL ALLIANC FOR IMPROVED NUTRITION, (GAIN) Dkt. Winfrida Mayilla akiwasilisha namna ya  mradi wa (I-CAN) Initiative on Climate Action and Nutrition utakavyotekelezwa na  tathmini ya utekelezaji wa sera Tanzania katika sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa  wadau wa Lishe kwenye kikao  kilichofanyika  hoteli ya Rafiki Jijini Dodoma Oktoba 16,2025.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede (katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa Lishe kutoka Wizarani na taasisi mbalimbali waliohudhuria kikao cha kujadili mradi wa Initiative on Climate Action and Nutrition (I-CAN) mara baada ya kumaliza kikao hicho kilichofanyika katika  hoteli ya Rafiki Jijini Dodoma,Oktoba 16,2025.


SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI ZIMEENDELEA KUBORESHA LISHE NCHINI-MAJALIWA

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa amesema kuwa sekta za Mifugo na Uvuvi zimekuwa vinara kwenye mchango wa protini inayotokana na wanyama na samaki hapa nchini.

Mhe. Majaliwa amesema hayo Oktoba 16,2025 wakati akifunga Maadhimisho ya kitaifa ya Siku ya Chakula Duniani kwenye Viwanja vya  Shule ya Sekondari Usagara mkoani Tanga ambapo amebainisha kuwa hatua hiyo imetokana na maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali kwenye sekta hizo.

“kwa sasa uzalishaji wa nyama umefikia taribani tani laki 6 na mayai takribani milioni 7 huku upande wa Uvuvi uzalishaji wa samaki umefikia hadi zaidi ya tani laki 5 hivyo nitoe rai kwa wananchi kuhakikisha tunaendelea kuhakikisha tunazalisha, tunahifadhi na kutumia vyakula vyenye virutubisho vingi na vyenye ubora wakati wote” Ameongeza Mhe. Majaliwa.

Aidha Mhe. Majaliwa amewataka wananchi hususani wale wanaoishi vijijini kutumia Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani kufanya maamuzi sahihi kuhusu lishe bora inayohitajika kutoka kwenye mazao yatokanayo sekta za na Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

“Hivi sasa kumekuwa na kasumba ya watu wengi kuwa na unene uliopitiliza hivyo ni lazima tuachane na mtindo wa kula kila kitu na badala yake tujielekeze kula chakula bora kama inavyoshauriwa na wataalam wa lishe”Amesema Mhe. Majaliwa.

Katika hatua nyingine Mhe. Majaliwa amewaelekeza wataalam wa sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi kuendelea kutumia mbinu bora za uzalishaji, uhifadhi na matumizi sahihi ya mazao yatokanayo na sekta hizo.

Awali akizungumzia namna maonesho hayo yalivyofanyika, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Dkt. Batilda Buriani amesema kuwa kupitia Maonesho ya mwaka huu wananchi wa mkoa huo wamepata fursa ya kujua teknolojia mbalimbali za Kilimo na Mifugo na Uvuvi na uzalishaji wa mazao yatokanayo na sekta hizo huku pia akibainisha kuwa maonesho hayo yalikuwa chachu ya kuhamasisha unywaji wa maziwa hasa kwa wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari.

Maadhimisho hayo ya 45 tangu kuasisiwa kwake 1981 yalijumuisha taribani waoneshaji 578 na wajasiamali zaidi ya 70 waliofanikiwa kutoa elimu na kufanya biashara ya bidhaa mbalimbali zitokanazo na sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akiangalia moja ya pakiti za dagaa waliokaushwa kwa teknolojia ya Jua muda mfupi baada ya kufika kwenye banda la Wajasiriamali wa zao hilo  wakati wa kilele cha Maadhimisho ya kitaifa ya Siku ya Chakula Duniani yaliyokuwa yakifanyika mkoani Tanga.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akiwaeleza wajasiriamali wa zao la dagaa umuhimu wa kuongeza thamani ya mazao yao muda mfupi baada ya kufika kwenye banda lao Oktoba 16,2025 wakati wa kilele cha Maadhimisho ya kitaifa ya Siku ya Chakula Duniani yaliyokuwa yakifanyika l mkoani Tanga.

Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari nchini (TVLA) mkoa wa Tanga Dkt. Olivia Manangwa (kulia) akimuonesha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa moja ya mashine zinazotumika kupima ubora wa chanjo za Mifugo muda mfupi baada ya Mhe. Majaliwa kufika kwenye banda la Wakala hiyo Oktoba 16,2025.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akikagua moja ya chanjo za Mifugo mara baada ya kufika kwenye banda la Wakala ya Maabara ya Veterinari nchini (TVLA) wakati wa kilele cha Maadhimisho ya kitaifa ya Siku ya Chakula Duniani Oktoba 16,2025 mkoani Tanga. Kulia anayemuelezea ni Meneja wa Wakala hiyo mkoani humo Dkt. Olivia Manangwa.


Alhamisi, 16 Oktoba 2025

WATUMISHI WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI WAPATIWA ELIMU YA MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA

Na. Fausta Njelekela, WMUV, Dodoma 

Watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wamepewa elimu na huduma za upimaji wa Magonjwa yasiyoambukiza mahala pa kazi (NCDs) ikiwa ni sehemu ya kuzuia na kudhibiti magonjwa hayo.

Zoezi hilo limefanyika Oktoba 15, 2025 katika ofisi za Wizara ya Mifugo na Uvuvi zilizopo Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma  ambapo wataalamu kutoka Wizara ya Afya kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Chama cha Kisukari Tanzania (TDB) na Capital City Marathon walitoa huduma hiyo.

Akizungumzia huduma na elimu hiyo Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mkurugenzi Msaidizi Utawala, Bw. Samwel Mwashambwa amesema zoezi hilo litaongeza uelewa na kuwahamasisha watumishi kujua umuhimu wa mtindo bora wa maisha na ufuatiliaji wa afya zao.

Aidha, Bw. Mwashambwa amewashukuru wataalamu kutoka Wizara ya Afya, Chama cha Kisukari Tanzania (TDB) na Capital City Marathon kwa kutoa elimu na upimaji wa magonjwa hayo yasiyoambukiza mahala pa kazi.

Kwa upande wake Afisa Muuguzi Msaidizi kutoka Hospital ya Mkoa wa Dodoma, Bw. Rashid Anzi, amesema zoezi la upimaji wa magonjwa yasiyoambukiza mahala pa kazi limelenga kuongeza ufanisi wa kazi kwa watumishi na litaleta matokeo chanya katika kuongeza nguvu na maendeleo nchini.

"Magonjwa yatakayopimwa leo ni pamoja na kisukari, shinikizo la damu, uzito uliopitiliza na urefu." amesema Bw. Anzi.

Naye, Afisa Uvuvi Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Upendo Hamidu amesema swala la kupima magonjwa yasiyoambukiza mahala pa kazi ni muhimu kwani linamfanya mtumishi kuelewa hali halisi ya Afya yake na kuweza kuongeza ufanisi katika kazi yake.

Afisa Muuguzi Hospitali ya Mkoa wa Dodoma, Bi. Neema Msemo (Kushoto), akitoa Huduma ya vipimo vya Shinikizo la damu (Presha) kwa Afisa Uvuvi Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Upendo Hamidu (kulia), katika zoezi la Utoaji elimu na Upimaji wa Magonjwa yasiyoambukiza Mahali pa kazi, lililofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Oktoba 15, 2025, Dodoma.

Afisa Muuguzi Hospitali ya Mkoa wa Dodoma, Bi. Neema Msemo (Kushoto), akitoa Huduma ya vipimo vya Shinikizo la damu (Presha) baada ya kutoa Kipimo cha Kiwango cha Sukari kwa Dereva Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Renatus Mtumbuka (kulia), katika zoezi la Utoaji elimu na Upimaji wa Magonjwa yasiyoambukiza Mahali pa kazi, lililofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Oktoba 15, 2025, Dodoma.

Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Utawala Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Samwel Mwashambwa (wa tatu kulia), akizungumza na Wauguzi wa Hospital ya Mkoa wa Dodoma kuhusu Huduma za Magonjwa yasiyoambukiza, kabla ya zoezi la Utoaji elimu na Upimaji wa Magonjwa yasiyoambukiza Mahali pa kazi, lililofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Oktoba 15, 2025, Dodoma.

Afisa Tawala Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Jane Kisanga (aliyesimama), akipimwa uzito, katika zoezi la Utoaji elimu na Upimaji wa Magonjwa yasiyoambukiza Mahali pa kazi, lililofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Oktoba 15, 2025, Dodoma.


SERIKALI YAHAMASISHA MATUMIZI YA MAYAI, MAZIWA TANGA

◼️Ni kupitia Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani yanayoendelea mkoani Tanga

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na wadau wake wa Tasnia ya Maziwa na Kuku imeendesha kampeni ya kuhamasisha ulaji wa mayai na unywaji wa maziwa kupitia zoezi la ugawaji wa mazao hayo ya Mifugo kwenye shule za watoto wenye mahitaji maalum lililofanyika Oktoba 13,2025 jijini Tanga.

Akizungumza wakati wa uendeshaji kampeni hiyo, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Bi. Mary Yongolo amebainisha kuwa hatua hiyo inalenga kuinua kiwango cha ulaji wa mazao hayo kwa kujenga utamaduni wa matumizi yake kwa watoto hususan wanafunzi ili kujenga nguvu kazi ya Taifa itakayokuwa imara na yenye afya.

“Kauli mbiu ya Maadhimisho ya mwaka huu inasema Tuungane pamoja kupata lishe bora kwa maisha ya sasa na ya baadaye na maisha ya baadae yanaanza utotoni kwa makundi haya madogo tuliyokuja kuyatembelea hapa” Ameongeza Bi. Yongolo.

Akizungumzia umuhimu wa mayai na maziwa kwa wanafunzi, Afisa Lishe wa mkoa huo Bi. Sakina Mustapha amesema kuwa maziwa yana protini inayosaidia kujenga mwili huku pia akiongezea kuwa zao hilo lina asili ya maji yanayomfanya mnywaji kukidhi kiu yake

“Kwenye maziwa pia kuna madini mbalimbali yanayosaidia kuimarisha mifupa lakini kwa upande wa mayai mbali na kuwa na vitamini na madini mbalimbali kuna mafuta ya asili kupitia kiini chake na vyote hivyo vinasaidia kujenga mwili hususani katika makuzi ya ubongo kwa mtoto” Ameongeza Bi. Mustapha.

Kampeni ya kuhamasisha matumizi ya mazao mbalimbali ya Mifugo na Uvuvi hufanyika kila mwaka wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani kwa lengo la kuinua kiwango cha ulaji wa mazao hayo yanayotajwa kuchangia sehemu kubwa ya protini kwenye mwili wa binadamu.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Mary Yongolo akielezea umuhimu wa ulaji wa mayai na unywaji wa maziwa yaliyosindikwa kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum kutoka Shule ya Msingi Chuda iliyopo mkoani Tanga Oktoba 13,2025.
Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Mary Yongolo (kulia) akiongoza zoezi la ugawaji maziwa na mayai kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum kutoka Shule ya Msingi Chuda iliyopo mkoani Tanga Oktoba 13,2025.
Msimamizi wa Dawati la lishe na Usalama wa Chakula kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Beatrice Mwijage akikabidhi mayai kwa mwakilishi wa wanafunzi wa shule ya Msingi Chuda iliyopo mkoani Tanga kwa lengo la kuhamasisha ulaji wa zao hilo la Mifugo kwa wanafunzi muda mfupi baada ya kufika shuleni hapo Oktoba 13,2025.







Jumatatu, 13 Oktoba 2025

SERIKALI, WADAU KUJA NA MPANGO MKAKATI WA UJUMUISHWAJI BIOANUWAI KATIKA UVUVI

Na Hamisi Hussein - Dar es Salaam.

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetoa rai kwa washirika wa maendeleo ya uvuvi wa kitaifa na kimataifa kuwa mabalozi wa mabadiliko katika jamii wanazotoka  kwa kuendeleza ushirikiano wa kukuza uchumi wa buluu wa Tanzania kupitia ujumuishwaji wa masuala ya bioanuwai katika uvuvi. 

Akifunga warsha ya ujumuishaji Masuala ya Bioanuwai katika Usimamizi wa Uvuvi Oktoba 8, 2025 katika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam, Mwakilishi wa Katibu Mkuu, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Dk. Charles Mhina amesisitiza umuhimu wa kujenga uelewa wa pamoja  wa kuoanisha uhifadhi wa bioanuwai na vipaumbele vya kitaifa, hasa katika nyanja za usalama wa chakula, maendeleo ya kiuchumi, na ustawi wa jamii.

Dkt. Mhina amefafanua kwamba mafanikio ya muda mrefu ya sekta ya uvuvi yanategemea uhifadhi wa mazingira ya majini na hivyo  ni vema masuala yote yaliyomo katika Mfumo wa Kimataifa wa Kunming–Montreal wa Bioanuwai pamoja na Mkakati wa Kitaifa wa Bioanuwai (NBSAP 2025–2030) yakaingizwa katika sera na mifumo ya kitaifa na ya mitaala ya usimamizi wa uvuvi.

“Kila mmoja akienda kuwekeza nguvu katika haya tuliyoyabainisha hapa nina hakika yataenda kuleta mabadiliko katika jamii zetu , kwahiyo washirika wa maendeleo wa kitaifa na kimataifa tukawe mabalozi  katika jamii zetu ili kuongeza uelewa wa uhifadhi wa bioanuwai kwa ajili ya kuwainua wavuvi wadogo” alisema Dkt. Mhina.

Aidha, aliwashukuru wadau wote waliowezesha warsha hiyo wakiwemo FAO kwa msaada wao wa kitaalamu na kifedha, washirika wa maendeleo, taasisi za elimu ya juu, na jamii za wavuvi waliotoa mchango mkubwa katika mjadala wa sera na mbinu za utekelezaji.  

Akiwasilisha  rasimu ya mpango kazi huo Afisa Uvuvi Mkuu ambaye pia ndio mratibu wa SSF Guidelines Dkt.Lilian Ibengwe amefafanua  mapendekezo ya rasimu ya mpango kazi huo kwa kuanisha malengo yaliyopendekezwa na timu ya wataalam, watafiti na wadau wa uvuvi  ambavyo vitazingatiwa wakati wa ujumuishajumasuala ya bioanuwani  katika  uvuvi.

Kwa upande wake mdau wa uvuvi ambaye ni Katibu wa Mtandao wa Wanawake Wavuvi na Wachakataji wa Mazao ya Uvuvi Tanzania (TAWFA) Bi. Hadija Malibiche ameipongeza Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na FAO kwa kuja na majadiliano ya pamoja  yanayolenga kuboresha ustawi wa viumbe maji kwa ajili ya manufaa ya  wavuvi nchini.

Wadau wa maendeleo walioshiriki kufanya mapitio ya rasimu pendekezwa ya mpango kazi huo ni pamoja na  IUCN, GIZ, Benki ya Dunia, Jumuiya ya Ulaya na Tanzania Women Chamber of Commerce (TWCC) ambao kwa pamoja wametoa ushauri na mapendekezo kwa ajili ya utekelezaji wa Mpango huo.
             
       
Mwakilishi wa Katibu Mkuu ambaye ni Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Charles Mhina akifunga Warsha  ya Ujumuishwaji Masuala ya Bioanuwai katika Usimamizi wa Uvuvi iliyofanyika  Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Wadau wa Maendeleo kutoka Benki ya Dunia, IUCN, Umoja wa Ulaya, wakifuatilia uwasilishwaji rasimu ya mpango kazi wa ujumuishwa wa bioanuwai katika uvuvi wakati wa kufunga Warsha  iliyofanyika  Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Usimamizi wa Mazingira na Maendeleo Bi. Editrudi Lukanga akichangia juu ya mpango kazi wa ujumuishwaji wa masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa uvuvi Wakati wa Warsha ya wadau wa bioanuwai iliyofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia oktoba 7 hadi hadi 9, 2025

Afisa Uvuvi Mkuu ambaye ni Mratibu wa SSF Guidelines Kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dk. Lilian Ibengwe akifanya majumuisho ya majadiliano ya wadau katika Warsha iliyofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi  Bi. Hamida Mbwana akiwasilisha mada  wakati wa Warsha ya Ujumuishwaji Masuala ya Bioanuwai katika Usimamizi wa Uvuvi iliyofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam Kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.




Alhamisi, 9 Oktoba 2025

WADAU WAHIMIZWA UMOJA UTUNZAJI RASILIMALI ZA UVUVI

 Ikiwa ni siku ya pili ya warsha ya kujadili ujumuishwaji wa masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa rasilimali za uvuvi wadau wa maendeleo ya sekta ya uvuvi wamehimizwa kuwa na nguvu za pamoja zitakazosaidia kulinda na kutunza rasilimali za bahari na vyanzo vingine vya maji kwa ajili ya shughuli za uvuvi.

Hayo yameelezwa Oktoba 8, 2025 katika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Charles Mhina ambapo amesema serikali na wadau wengine wa maendeleo waweke  jitihada za pamoja katika utunzaji wa  mazingira ya viumbe maji itasaidia kuwa na uvuvi endelevu na kuinua uchumi wa jamii.

Amehimiza washiriki wa warsha hiyo kutumia jukwaa hilo ili kubadilisha mtazamo kuhusu utunzaji wa mazingira ya bahari, vyanzo vya maji na rasilimali za uvuvi ili jamiii iweze kunufaika na sekta ya uvuvi  endelevu na kuondokana na umaskini.

Aidha, Katika siku ya pili ya warsha hiyo majadiliano mbalimbali yamefanyika yakiwa na lengo la kuja na mpango mkakati  utakaosaidia kufanya ujumuishaji wa masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa sekta ya uvuvi.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Charles Mhina akihimiza ushirikiano wa serikali, wadau wa maendeleo na jamii kulinda mazingira ya bahari na rasilimali za uvuvi wakati wa warsha ya ujumuishwaji masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa uvuvi inayoendelea  hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Charles Mhina (Kulia) na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi Nchini ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi wa Uvuvi Bw. Chritian Nzowa wakifuatilia uwasilishwaji wa mada mbalimbali kuhusu ujumuishwaji wa masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa uvuvi wakati wa warsha inayoendelea hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi Nchini ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi wa Uvuvi Bw. Christian Nzowa akizungumza kabla ya kumkaribisha Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Dkt. Charles Mhina kwenye warsha ya ujumuishaji masuala ya bioanuwai katika  usimamizi wa uvuvi, warsha inayofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Afisa Uvuvi Mkuu Bw. Owen Kibona akiwasilisha mapendekezo ya mpango mkakati wa ujumuishwaji masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa sekta ya uvuvi wakati wa warsha inayoendelea katika hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Katibu wa Mtandao wa Wanawake Wavuvi na Wachakataji wa Mazao ya Uvuvi (TAWFA) Bi. Hadija Malibiche akieleza jinsi umoja huo unavyounga jitihada za kulinda bioanuwai katika uvuvi wakati wa warsha hiyo inayifanyika Hoteli ya Giraffe jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Wataalam wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Wadau wa sekta ya uvuvi wakiwa katika majadiliano ya kuandaa mpango kazi wa ujumuishwaji wa masuala ya bioanuwai katika Sekta ya uvuvi wakati wa warsha inayofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia oktoba 7 hadi 9, 2025.


Jumanne, 7 Oktoba 2025

BI. MEENA AFUNGUA WARSHA YA UJUMUISHAJI BIOANUWAI KATIKA USIMAMIZI WA UVUVI

Na Hamisi Hussein - Dar es Salaam

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena amefungua warsha ya ujumuishaji wa masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa uvuvi nchini iliyowakutanisha takribani washiriki 50 katika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam wakiwemo watafiti, wawakilishi wa halmashauri za wilaya, wataalam wa uvuvi wa ndani na wa kimataifa, asasi za kiraia, wawakilishi wa wavuvi wadogo na wadau wa maendeleo.

Akifungua warsha hiyo leo Oktoba 7, 2025, Bi. Meena amewahimiza washiriki hao kuzitambua changamoto zinazoikabili mifumo ya Bioanuwai ili kulinda rasilimali za uvuvi nchini.

"Ndugu washiriki tunapojadili ujumuishaji wa bioanuwai katika usimamizi wa uvuvi, ni muhimu kutambua changamoto zinazoikabili mifumo ya ikolojia nchini ukiwemo uvuvi  haramu ambao umesababisha kupungua kwa samaki  na mabadiliko ya tabianchi ambayo yamekuwa yakibadilisha makazi ya viumbe na kuvuruga mifumo ya uzalishaji wa samaki  mambo haya  yanatishia bioanuwai na ustawi wa jamii." Alisema Bi. Meena.

Alisema ili kukabiliana na changamoto hizo kunahitajika ushirikiano wa pamoja utakaoleta mikakati ya namna bora ya ujumuishaji katika uhifadhi wa bioanuai katika mifumo ya usimamizi ya uvuvi kwa kuzingatia misingi ya uendelevu wa rasilimali ya Uvuvi. 

Kwa upande Wake  Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) nchini Tanzania Dkt. Nyabenyi Tipo amesema Shirika hilo litaendelea kushirikiana na Tanzania katika  kujumuisha Bioanuwai kwenye usimamizi wa sekta ya uvuvi kwa kugusa kundi la vijana na wanawake kunufaika na sekta hiyo kwa kuwa na usalama wa chakula na ajira.

"Ajenda hii inaakisi jukumu kuu la FAO la kuendeleza uvuvi endelevu na mchango wetu wa pamoja katika juhudi za kimataifa za kupunguza umaskini na kujenga mifumo imara ya chakula. Pia inaendana kikamilifu na Mwongozo wa Hiari wa Kuhakikisha Uvuvi Endelevu wa Wavuvi Wadogo, ambao unatoa wito wa usimamizi wa kuwajibika wa rasilimali za uvuvi na kuwawezesha wavuvi wadogo, wanawake na vijana ambao wako katika kiini cha sekta hii" alisema Dkt. Tipo.

Naye Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi nchini ambaye pia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Uvuvi Bw. Christian Nzowa  amesema asilimia 40 ya mazao ya uvuvi hupotea  baada ya kuvunwa kutokana na  miundombinu mibovu, ukosefu wa mafunzo na  matumizi mabaya ya zana za uvuvi lakini serikali imekuja na mikakati ya kupunguza  upotevu wa mazao hayo kwa kujenga miundombinu ya kuanikia samaki na dagaa maeneo ya Tanga, Kilwa, Bagamoyo, Mafia, Ziwa Tanganyika na Kigoma. 

Aliongeza kuwa  uvuvi  wa bahari kuu unachangia asilimia 30 ya mazao ya uvuvi nchini ikilinganishwa na uvuvi wa maji baridi ambao unachangia asilimia 75  ambapo kwa Tanzania Watu milioni 4 wanategemea sekta ya uvuvi huku watu 200, 000 wakinufaika moja kwa moja na sekta hiyo.

Lengo la Warsha hiyo ambayo inafanyika kwa Siku tatu kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025 ni kuleta pamoja wadau wa sekta ya uvuvi na bioanuai ili kujadili, kupanga na kuandaa Mpango wa Utekelezaji wa ujumuishaji wa bioanuai katika usimamizi wa uvuvi kwa kuzingatia Mpango wa Kimataifa wa Bioanuwai (GBF) na Mkakati wa Taifa wa Bioanuwai (NBSAP 2025-2030).

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena akifungua Warsha ya Ujumuishi wa masuala ya Bioanuwai Katika Usimamizi wa Uvuvi nchini, warsha inayofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo (FAO) nchini Tanzania Dkt. Nyabenyi Tipo akiwasilisha taarifa ya utayari wa FAO kwenye ujumuishi wa masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa uvuvi wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo inayofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena (Kushoto) akifanya mazungumzo mafupi na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo (FAO) Nchini Tanzania Dkt. Nyabenyi Tipo kabla ya ufunguzi wa  Warsha ya ujumuishaji wa masuala ya Bioanuwai katika Usimamizi wa uvuvi, Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi Nchini ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi wa Uvuvi Bw. Christian Nzowa akieleza hali ya sekta ya uvuvi nchini Tanzania Wakati wa Warsha ya ujumuishaji wa Masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa uvuvi , inayofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Wadau wa Uvuvi wakifuatilia ufunguzi wa Warsha ya ujumuishaji wa Masuala ya bioanuai katika usimamizi wa uvuvi , warsha inayofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Wataalam mbali mbali kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi pamoja na wadau wa uvuvi wakifuatilia ufunguzi wa Warsha hiyo iliyofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Watafiti kutoka Shirika la Chakula na Kilimo (FAO) wakifuatilia mawasilisho  wakati wa ufunguzi wa Warsha hiyo inayofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuaniza Oktoba 7 hadi 9, 2025.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena (Katikati, waliokaa), Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo (FAO) nchini Tanzania Dkt. Nyabenyi Tipo (Kulia, waliokaa), Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi Nchini Bw. Christian Nzowa (Kushoto) pamoja na washiriki wa warsha ya Ujumuishi wa Masuala ya Bioanuwai katika Usimamizi wa Uvuvi wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ufunguzi wa warsha hiyo inayofanyika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 7 hadi 9, 2025.


Alhamisi, 2 Oktoba 2025

TANZANIA YA TATU AFRIKA MPANGO RASMI WA KUDHIBITI KICHAA CHA MBWA

Na Chiku Makwai: WMU

Serikali kwa kushirikiana na wadau wa afya ya wanyama imeandaa  Mpango  Rasmi wa kutokomeza Ugonjwa wa Kichaa cha Mbwa ikiwa ni moja ya mkakati wa kufikia azma ya Dunia ya kuondokana kabisa na ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi Agnes Meena katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Kichaa cha Mbwa Kitaifa yaliyofanyika leo Septemba 29, 2025 Wilaya ya Kiteto Mkoani Manyara.

Bi. Meena amesema kwamba mpango huo ambao umeshapitiwa na kuridhiwa na Shirika la Afya ya Wanyama duniani (WOAH) utaratibu wa uchanji wa mbwa na paka wote nchini kwa muda wa miaka mitano.

“Kupitia mpango huo, ni imani yetu kwamba hadi kufikia mwaka 2030 Tanzania itakua ni miongoni mwa nchi zitakazokuwa zimeutokomeza ugonjwa huu wa Kichaa cha Mbwa”,amesema Bi Meena.

Aidha, ametoa wito kwa wananchi kutoa taarifa kwa wataalam wa mifugo walio karibu yao au serikali ya mtaa ya eneo husika endapo watakutana na mnyama au mfugo wenye dalili zisizo za kawaida.

Vilevile amesema kuwa mbwa, paka na wanyama wengine  wakitunzwa vizuri wana  umuhimu katika maisha ya kila siku ya binadamu huku akiongeza wasipopewa chanjo ya magonjwa hususani kichaa cha mbwa wanyama hao wanageuka kuwa hatari kwa binadamu.  

“Kwa hiyo lengo la maadhimisho haya ambayo yamesababisha tukusanyike hapa leo ni kukumbushana na kuelimishana zaidi jinsi ya kukabiliana na janga hili la ugonjwa wa kichaa cha mbwa”, amesema Bi Meena.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Huduma za Wanyama wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Benezeth Lutege amebainisha kuwa takwimu zinaonesha mpaka kufikia Septemba 29, 2025 wilayani humo wametoa chanjo kwa Mbwa 3653, Paka 212, Kuhasi Mbwa 96, Paka 5 na Kufunga Vizazi  Mbwa 52, Paka 26. 

Akisoma taarifa ya Wilaya, kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kiteto Bi. Mufandii Msaghaa amesema kwamba wilaya ya Kiteto imejitahidi kuzitekelza sera za serikali kuhusu mifugo hususani kuthibiti magonjwa ya wanyama.

“Serikali imejitahidi kuthibiti magonjwa kwa kutoa kinga ya magonjwa ya wanyama. Kila mwaka wataalam wetu wamekua wakitoa huduma ya chanjo kama sera zinavyotutaka”, amesema Bi. Msaghaa.

Maadhisho ya Ugonjwa wa kichaa mwaka 2025  yamebebwa na kaulimbiu isemayo Kichaa cha Mbwa; “Chukua Hatua Sasa, Mimi, Wewe na Jamii.”


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena akikagua Mabanda ya Madaktari watoa huduma ya chanjo ya kichaa cha Mbwa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Kichaa cha Mbwa Kitaifa yaliyofanyika leo Septemba 29, 2025 wilayani Kiteto mkoa wa Manyara.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena akizungumza na halaiki wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Kichaa cha Mbwa Kitaifa yaliyofanyika leo Septemba 29, 2025 wilayani Kiteto mkoa wa Manyara.

Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt Benezeth Lutege akizungumza jambo wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Kichaa cha Mbwa Kitaifa yaliyofanyika leo Septemba 29, 2025 wilayani Kiteto mkoa wa Manyara.

Katibu Tawala wa Wilaya ya Kiteto Bi. Mufandii Musaghaa akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa wilaya hiyo Mhe. Remidius Mwema (hayupo pichani) wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Kichaa cha Mbwa Kitaifa yaliyofanyika leo Septemba 29, 2025 wilayani Kiteto mkoa wa Manyara.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agnes Meena (katikati) akivalishwa vazi la kimila la kimasai wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Kichaa cha Mbwa Kitaifa yaliyofanyika leo Septemba 29, 2025 wilayani Kiteto mkoa wa Manyara.