Nav bar

Alhamisi, 25 Februari 2021

GEKUL AMSIMAMISHA KAZI MKUU WA KITUO CHA UKAGUZI WA MIFUGO RUVU DARAJANI

Na Mbaraka Kambona, Pwani

 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul amemsimamisha kazi Mkuu wa Kituo cha Ukaguzi wa Mifugo cha Ruvu Darajani, Gabriel Lyakurwa kwa tuhuma za kutorosha mifugo na kusababisha upotevu wa mapato ya Serikali, huku akimuagiza Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi, Evarist Ndikilo kuwachukulia hatua Watumishi waliochini ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo ambao walikuwa wanashirikiana na Mkuu huyo wa kituo. 

 

Gekul alitoa maamuzi hayo baada ya Mkuu huyo wa Mkoa wa Pwani kuibua tuhuma hizo katika ziara yake aliyoifanya kwenye kituo hicho kilichopo Ruvu Darajani, Wilayani Bagamoyo Februari 24, 2021.

 

Mhandisi Ndikilo alisema uchunguzi alioufanya umebaini kuwa Mkuu wa kituo hicho amekuwa akishirikiana na wenzake wasiowaaminifu kutorosha mifugo inayopelekwa katika kituo hicho kwa ajili ya kukaguliwa kabla ya kuruhusiwa kupelekwa katika maeneo mengine ya minada.

 

“Mhe. Naibu Waziri nimefanya uchunguzi wa kina na kugundua kuwa utoroshaji huu unahusisha mtandao wa watu wengi wakiwemo baadhi ya Wananchi, Wafanyabiashara na Watumishi wa Serikali…, kwa mfano tarehe 17 mwezi huu wa pili kuna Magari matano yalileta ng’ombe katika kituo hiki kwa ajili ya kukaguliwa lakini ni gari moja tu lililokwenda Dar es Salaam kama kawaida ilivyo, huku mengine yaliyobaki yakichepushwa na mifugo ilipelekwa Kisarawe, Kibaha na Kijiji cha Kidogozero kinyemela,” alisema Mhandisi Ndikilo

 

Kufuatia tuhuma hizo, Naibu Waziri Gekul alitoa maagizo hayo ya kusimamishwa kazi mkuu huyo wa kituo huku akisema kuwa Wizara itaunda tume maalum kwa ajili ya kwenda kuchunguza tuhuma hizo ikiwemo kupitia mahesabu yote ili kubaini ni kwa kiasi gani mapato ya Serikali yamepotea na wale wote watakaoonekana kuhusika katika upotevu huo watachukuliwa hatua kali.

 

"Hatuwezi kucheza na maduhuli ya Serikali, haiwezekani tuwe na ng’ombe zaidi ya milioni 33 lakini mchango wa sekta ya mifugo katika pato la taifa hauzidi asilimia 7, ni kwa sababu ya michezo kama hii, hatutakubali, na tutakwenda kukagua katika maeneo yote ya minada," alisema Gekul

 

Naye, Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete alisema kuwa katika jambo ambalo wamekuwa wakilisemea sana ni kituo hicho kukithiri kwa vitendo vya ubadhilifu ambavyo vimekuwa vikichangia Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo kupoteza mapato.

 

Ridhiwani alimuomba Naibu Waziri huyo kuhakikisha anachukua hatua madhubuti za kudhibiti vitendo hivyo vya ubadhirifu ikiwemo kuondoa mtandao wote wa waharifu ili halmashauri iweze kupata mapato yanayostahili.


Msimamizi  wa Ujenzi wa Bwawa la Kunyweshea Mifugo la Chamakweza, Robert Baltazar akimuonesha michoro ya bwawa hilo, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (wa kwanza kulia) alipotembelea kukagua maendeleo ya ujenzi wa bwawa hilo lililopo Chalinze, Wilayani Bagamoyo, Mkoani Pwani Februari 24, 2021. Wa pili kutoka kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi, Evarist Ndikilo.

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Malisho na Rasilimali za Vyakula vya Mifugo, Rogers Shengoto akijibu moja ya hoja ziliyoibuliwa katika ziara ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul aliyoifanya Mkoani Pwani Februari 24, 2021.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul akijadiliana jambo na Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi Evarist Ndikilo (kushoto) na Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete (kulia) alipofanya ziara kukagua Kituo cha Ukaguzi wa Mifugo cha Ruvu Darajani kilichopo Wilayani Bagamoyo, Mkoani Pwani Februari 24, 2021.




WAZIRI NDAKI ATAKA KUAINISHWA MIPAKA YA HIFADHI YA BAHARI KUONDOA MIGOGORO NA WAVUVI

Na. Edward Kondela

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amekitaka Kitengo cha Hifadhi ya Bahari na Maeneo Tengefu (MPRU) kuhakikisha hadi kufikia Mwezi Agosti Mwaka 2021 kinaweka alama za mipaka katika maeneo yote ya hifadhi za bahari ili kuondoa migogoro kati yao na wavuvi.

 

Akizungumza jana (23.02.2021) na wananchi katika Kata ya Jibondo iliyopo Wilaya ya Mafia Mkoani Pwani, Waziri Ndaki ametaka kuwekwa kwa alama za mipaka hiyo baada ya baadhi ya wananchi kulalamikia kutozwa faini mara kwa mara kwa tuhuma za kufanya shughuli za uvuvi kwenye maeneo hayo ambayo hayaruhusiwi kisheria kwa shughuli hizo.

 

Aidha, Waziri Ndaki akiwa ameambatana na naibu waziri wa wizara hiyo Mhe. Pauline Gekul, amewataka wavuvi kuhakikisha pindi wanapokamatwa kwa makosa mbalimbali ambayo ni kinyume na sheria ya uvuvi kuhakikisha wanapatiwa risiti inayotambulika na serikali ya kieletroniki (EFD) na kuonya watumishi wa serikali wanaopokea fedha za faini bila kutoa risiti hizo.

 

“Tuweke mipaka ya hifadhi ieleweke hapa ndiyo mwanzo na hapa ndiyo mwisho, hadi mwezi wa nane maeneo tengefu yawe na mipaka yake ya hifadhi ya bahari, pia tushirikishe wananchi na viongozi wao siyo kuweka tu mipaka, pia kwa mtu anayekutwa na kosa la kwenda kinyume na sheria ya uvuvi akilipa faini apewe risiti ya serikali ya kieletroniki (EFD).” Amesema Waziri Ndaki

 

Pia, waziri huyo ametaka kufanyika kwa utafiti zaidi ndani ya mwezi mmoja juu ya matumizi ya aina mbalimbali za nyavu za uvuvi baada ya kupata malalamiko ya mara kwa mara kutoka kwa wavuvi ambao wamekuwa wakilalamikia baadhi ya nyavu ambazo wanatakiwa kuzitumia kisheria kwa ajili ya uvuvi kutokuwa na sifa ya kukamata mazao ya samaki katika maeneo yao.

 

Amemuelekeza Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah kuhakikisha kufikia Tarehe 23 mwezi Machi Mwaka 2021, awe amempatia taarifa hiyo ili iweze kutoa mwongozo wa maamuzi ya nyavu ambazo zina tija kwa shughuli za uvuvi.

 

Katika mkutano huo wa hadhara na wananchi wa Kata ya Jibondo Wilaya ya Mafia Mkoani Pwani, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amepiga marufuku kitendo cha baadhi ya maafisa uvuvi kuwakamata wafanyabiashara wa samaki waliyopo mitaani yakiwemo maeneo ya kuuzia vyakula kwa madai samaki wanaouzwa katika eneo hilo hawana sifa kisheria badala yake watafute vyanzo vya maeneo ambayo watu wanavua samaki hao.

 

“Kuna mambo ambayo sipendi sitaki kabisa kusikia afisa uvuvi anaenda sokoni kutafuta samaki ambao wapo kinyume cha sheria na kuwanyanyasa akinamama wanaokaanga samaki, wakiona samaki wa namna hiyo wanapaswa kuwauliza aliyewauzia ili wapate chanzo halisi cha samaki walipovuliwa badala ya kumnyanyasa mfanyabiashara ambaye anauza chakula au kununua samaki anapeleka nyumbani kwa ajili ya mboga.” Amefafanua Waziri Ndaki

 

Kuhusu kilimo cha zao la mwani Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah amesema zao hilo limekuwa likilalamikiwa kwa kuuzwa kwa bei ndogo hali ambayo imekuwa ikiwafanya wakulima hao wasipate mafanikio na kuwataka wakulima wasiingie mikataba ya kuuza zao la mwani badala yake wauze kwa wafanyabiashara ambao wanakuwa na bei nzuri yenye tija kwao.  

 

Dkt. Tamatamah amesema wizara itahakikisha inasimamia zao hilo kwa kuwa limekuwa mkombozi mkubwa kwa akinamama wengi katika Ukanda wa Pwani pamoja na kuwataka waliongezee thamani kwa kutengeneza bidhaa mbalimbali zikiwemo sabuni.

 

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mafia Mhe. Juma Salum Ali amepongeza namna Wizara ya Mifugo na Uvuvi inavyohakikisha inasimamia maeneo ya hifadhi ya bahari kupitia Kitengo cha Hifadhi ya Bahari na Maeneo Tengefu (MPRU) huku akitaka kutatuliwa kwa baadhi ya changamoto ambazo zinaleta hali ya kitengo hicho kushindwa kushirikiana na wananchi.

 

Mhe. Ali amefafanua kuwa baadhi ya watumishi wa kitengo hicho wamekuwa wakishindwa kufanya kazi kwa kufuata ueledi wa kazi yao na kuweka maslahi binafsi hali ambayo imekuwa ikizorotesha hali ya uhifadhi ukizingatia Wilaya ya Mafia bado ina maeneo mengi ambayo yana wingi wa samaki kwa ajili ya shughuli za uvuvi.

 

Kwa upande wao baadhi ya wananchi waliofika katika mkutano huo wamemuelezea Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo na kuelezea namna walivyo na imani kubwa na waziri huyo katika kutatua changamoto zao ili waweze kufanya shughuli za uvuvi bila bughudha na waweze kufuata sheria za nchi.

 

Aidha, Waziri Ndaki akiwa katika Kata ya Kilindoni Wilayani Mafia, amezungumza na baadhi ya wavuvi na kuwataka wafanye shughuli za uvuvi kwa kutumia taa nyakati za usiku wakati Wizara ya Mifugo na Uvuvi ikiendelea kufanya tafiti ya taa bora zaidi ambazo hazina madhara wakati wa kuvua samaki.

 

Mhe. Ndaki amelazimika kutoa ufafanuzi huo baada ya kulalamikiwa na baadhi ya wavuvi kushindwa kufanya shughuli zao nyakati za usiku kwa kuzuiwa kutumia taa kama chambo kwa ajili ya kukamatia samaki.

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amefanya ziara ya kikazi ya siku mbili katika Wilaya ya Mafia Mkoani Pwani akiambatana na Naibu Waziri Mhe. Pauline Gekul ambapo Waziri Ndaki amepata fursa ya kuzungumza na baadhi ya wavuvi na kujionea hifadhi ya bahari na maeneo tengefu.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na baadhi ya wakazi wa Kata ya Kilindoni iliyopo Wilaya ya Mafia Mkoani Pwani alipofanya ziara ya kikazi ya siku mbili wilayani humo na kutaka wavuvi waendelee na shughuli zao kwa kutumia taa kuvua samaki nyakati za usiku wakati wizara hiyo ikifanya tafiti zaidi za taa bora ambazo hazina madhara katika shughuli za uvuvi. (23.02.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (katikati) akijadiliana jambo na Naibu Waziri Mhe. Pauline Gekul na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah wakati alipofanya ziara ya kikazi ya siku mbili wilayani humo. (23.02.2021) Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (katikati) akijadiliana jambo na Naibu Waziri Mhe. Pauline Gekul na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah wakati alipofanya ziara ya kikazi ya siku mbili wilayani humo. (23.02.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza kulia) akipata maelezo kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah wakati wakiwa kwenye boti maalum yenye kioo chini ambayo imewawezesha kujionea maeneo ya mazalia ya samaki yaliyopo kwenye Bahari ya Hindi, wakati Waziri Ndaki alipofanya ziara ya kikazi ya siku mbili Wilayani Mafia. Pembeni ya Dkt. Tamatamah ni Naibu Waziri Mhe. Pauline Gekul. (23.02.2021)




Ijumaa, 19 Februari 2021

TALIRI YAJIKITA KUTATUA CHANGAMOTO ZA WAFUGAJI

 Na Mbaraka Kambona, Mpwapwa

 

Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Dkt. Jonas Kizima amesema utafiti wanaoufanya umejikita katika kutatua changamoto za mbegu bora za mifugo na mbegu bora za malisho kwa wafugaji ili sekta ya mifugo iweze kuchangia vyema katika pato la Taifa.

 

Dkt.  Kizima aliyasema hayo alipotembelea kukagua shughuli zinazofanywa na Kituo cha TALIRI Mpwapwa kilichopo Wilayani Mpwapwa, Mkoani Dodoma Februari 18, 2021.

 

Alisema kuwa lengo la utafiti wanaoufanya ni kuhakikisha wanapata mbegu bora za mifugo na kuzalisha mbego bora za malisho ya mifugo ambazo zitakazosaidia kutatua changamoto za upatikanaji wa mbegu bora za mifugo zinazohimili mazingira yaliyopo na malisho inayoikabili nchi kwa sasa.

 

Aliongeza kuwa kwa sasa taasisi hiyo inaendelea na kufanya Tathmini ya ubora, ustahimilivu na makuzi ya malisho ya mifugo yatakayofaa kwa chakula cha kutosha kwa ajili ya mifugo.

 

Kwa mujibu wa Dkt. Kizima, matokeo yoyote ya utafiti lazima yabadilishwe kuwa biashara kwa sababu wafugaji wakifanya ufugaji unaoendana na mazingira yao itawasaidia kutengeneza uchumi na kuwaongezea tija katika ufugaji wao.

 

“Tafiti tunazozifanya zinalenga kuimarisha mnyororo wa thamani wa mifugo ili mchango wa sekta ya mifugo uweze kuonekana katika uchumi wa kati,” alisema Dkt. Kizima

 

Dkt. Kizima alisema kuwa TALIRI imesambaza vituo vyake katika Kanda Saba nchini ili kuwa karibu na wafugaji kuwasaidia kutatua changamoto zao ili waweze kufanya ufugaji wenye tija.

 

Alisema vituo hivyo vipo katika Kanda ya Mashariki, Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Kati, Kanda ya Kusini, Kanda ya Magharibi, Kanda ya Ziwa na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

 

Naye, Mkurugenzi, Idara ya Utafiti, Mafunzo na Huduma za Ugani, Dkt. Angello Mwilawa alisema kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi imezihamasisha Halmashauri zote nchini kuanzisha mashamba darasa ya malisho ili wafugaji waweze kujifunza na kupata mbegu bora za malisho kwa ajili ya mifugo.

 

“Tunawahimiza wafugaji kuona umuhimu wa kulima malisho ili yaweze kuwasaidia kupata lishe ya uhakika kwa mifugo yao na pia kwa kulima malisho kutawapunguzia migogoro ya mara kwa mara kati yao na wakulima,” alisema Dkt. Mwilawa

 

Aliongeza kuwa wanawahamasisha wafugaji hususan walio katika nyanda kame wastawishe malisho ya mifugo wakati wa masika na kuyatunza ili yaweze kuwasaidia kulisha mifugo yao wakati wa kiangazi.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Dkt. Jonas Kizima akiongea na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) alipotembelea Kituo cha taasisi hiyo cha TALIRI Mpwapwa kilichopo Wilayani Mpwawa kukagua shughuli zinazofanywa na kituo hicho Februari 18, 2021.

Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Huduma za Ugani, Dkt. Angello Mwilawa akiongea na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) wakati alipokuwa anaeleza kuhusu utafiti wa malisho unaofanywa na Kituo cha Utafiti wa Mifugo (TALIRI) Mpwapwa kilichopo Wilayani Mpwapwa alipotembelea   moja ya Shamba la Malisho ya mifugo la kituo hicho Februari 18, 2021. Kulia kwake ni Kaimu Mkurugenzi Msaidizi, Utafiti na Mafunzo, Dkt. Hassan Mruttu.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Dkt. Jonas Kizima (katikati- aliyevaa suti nyeusi) akijadiliana jambo na baadhi ya Viongozi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Maafisa wengine wa kituo cha TALIRI Mpwapwa alipotembelea kituo hicho Februari 18, 2021.

Pichani ni Josho la Nunge. Josho hilo la kihistoria lilijengwa Wilayani Mpwapwa na    Wajerumani mwaka 1905 likiwa ni josho la kwanza kujengwa Afrika Mashariki. Tangu Josho hilo lijengwe mpaka sasa lina umri wa miaka 116 na bado linatumika likiwa katika hali nzuri kama linavyoonekana pichani. (18.02.2020)

Baadhi ya Ng'ombe wanaofugwa katika kituo cha TALIRI Mpwapwa kilichopo Wilayani Mpwapwa wakinywa maji katika kisima kilichotengwa kando ya Josho la Nunge kwa ajili ya kunyweshea mifugo. 

Alhamisi, 18 Februari 2021

MAWAKALA WA KUKU WASIOTAMBULIKA KUKAMATWA

Na. Edward Kondela

 

Chama cha Wafugaji wa Kuku wa Nyama  nchini (TABROFA) kimetakiwa kuwa na ushirikiano ili kutokomeza changamoto wanazozipata wafanyabiashara wa kuku hasa mawakala wasiotambulika wanaouza vifaranga vya kuku wa nyama pamoja na vyakula vya kuku kwa bei ya juu katika maeneo mbalimbali nchini.

 

Akizungumza katika mkutano wa wafanyabiashara na wazalishaji wa vifaranga vya kuku wa nyama jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amesema mawakala wanaotumiwa na wenye viwanda vya kutotolesha vifaranga kama hawajasajiliwa wakamatwe.

 

“Kuanzia sasa mawakala wa wauzaji wa vifaranga vya kuku pamoja na chakula cha kuku nataka wafuatiliwe na waeleze wapi walisajiliwa”. Amesema Mhe.Ndaki.

 

Aidha, Mhe. Ndaki amewataka wafugaji wote wanaouza kuku wa nyama  kujisajili  Bodi ya Nyama nchini (TMB) kwa ajili ya biashara kwani hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa atakayekaidi.

 

Pia, waziri huyo amewataka wafugaji wa kuku wa nyama kuanza kuuza kuku kwa uzito badala ya kukadiria ili waweze kuendana na gharama halisi za ufugaji na kupata faida ili ufugaji uwe na tija kwao na kutaka TABROFA kusimamia hilo na kuwachukulia hatua wafugaji watakaoenda kinyume na hilo.

 

Ameongeza kuwa sekta ya ufugaji ni muhimu kwa pato la nchi na kuwataka wataalamu wa mifugo kufanya tafiti za mifugo kwa kuwalenga wafugaji wenyewe kwa kubaini changamoto zao sio kuwatumia wasomi.

 

“Tuache kufanya tafiti kwa kuwatumia bwana shamba na bibi shamba ambao hawafikishi ujumbe kwa wafugaji  kuhusu elimu dhidi ya tafiti zilizofanyika,” ameeleza.

 

Naye Kaimu Msajili wa Bodi ya Nyama Bw. Imani Sichwale amewataka wafugaji hao kuacha kufuga kuku kwa mazoea bali wafuge kitaalamu kwa kuweka bajeti ya ufugaji kwa lengo la kukuza tasnia yao.

 

Hata hivyo Bw. Sichwale amesema kuwa nyama inasoko nje ya nchi kuliko kuku kwa sababu haijapata vigezo vya uuzaji nje ya nchi.

 

Amesema asilimia 80 ya wafugaji wa kuku wa nyama ni wanawake hivyo amewataka kushikilia tasnia hiyo kwa lengo la kuondoa umaskini kuanzia ngazi ya familia hadi taifa kwa ujumla.

 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji wa Kuku wa Nyama nchini (TABROFA) Bw. Costa Mrema amesema katika tafiti walizozifanya zimebaini kuwa ulaji wa kuku wa nyama Tanzania ni kati ya kuku laki 9 hadi milioni 1.2 kwa wiki.

 

“Idadi hiyo 70% ya walaji wa kuku wa nyama ni katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani ikifuatiwa na mikoa ya Arusha, Mwanza, Kilimanjaro na Dodoma”. Amesema Bw. Mrema.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza katika mkutano wa wafanyabiashara na wazalishaji wa vifaranga vya kuku wa nyama jijini Dar es Salaam, ambapo ameagiza kuchukuliwa hatua kwa mawakala wa kuku wasiotambulika pamoja na kuagiza Chama cha Wafugaji wa Kuku wa Nyama nchini (TABROFA) kuwataka wanachama wake kuuza kuku kwa uzito badala ya kukadiria. (17.02.2021)

Kaimu Msajili wa Bodi ya Nyama nchini (TMB) Bw. Imani Sichalwe akiwataka wafugaji wa kuku kujisajili katika bodi hiyo ili kufanya shughuli ya ufugaji kuwa rasmi kwao na kuweza kupata fursa mbalimbali zinazojitokeza pamoja na kusaidiwa kutatua changamoto zinazowakabili. (17.02.2021)


Mkurugenzi Msaidizi Ukaguzi wa Nyama na Mazao Yake kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Gibonce Kayuni, akiwataka wafugaji wa kuku wa nyama (hawapo pichani) kuweka kumbukumbu sahihi za ufugaji, kushirikisha wataalamu na kuishirikisha wizara katika msaada wa kisheria mara wanapopata hasara kutokana na kuuziwa vifaranga visivyo na sifa.  Dkt. Kayuni amebainisha hayo katika mkutano wa wafanyabiashara na wazalishaji wa vifaranga vya kuku wa nyama jijini Dar es Salaam. (17.02.2021)

Mtendaji Mkuu Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo nchini (LITA) Dkt. Pius Mwambene akizungumza katika mkutano wa wafanyabiashara na wazalishaji wa vifaranga vya kuku wa nyama jijini Dar es Salaam na kuwataka wafugaji kujiunga LITA ili wapatiwe elimu bora ya ufugaji. (17.02.2021)

Baadhi ya wafugaji wa kuku wa nyama jijini Dar es Salaam, wakionesha mzani unaoweza kupima kuku kwa mara moja kuanzia Kilogramu mbili hadi 300 na kuiomba serikali kusimamia azma yao ya kuuza kuku kwa uzito badala ya bei ya kukadiria ambayo imekuwa ikiwapa hasara kubwa na kushindwa kuendelea na ufugaji. (17.02.2021)

Baadhi ya washiriki wa mkutano wa wafanyabiashara na wazalishaji wa vifaranga vya kuku wa nyama jijini Dar es Salaam, wakisikiliza hoja mbalimbali ambazo zilikuwa zikiwasilishwa ambapo mgeni rasmi katika mkutano huo alikuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki. (17.02.2021)





WAZIRI NDAKI AKUTANA NA MWAKILISHI WA UMOJA WA MATAIFA KWENYE PROGRAMU YA CHAKULA DUNIANI UN WFP

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (kushoto) akijadili jambo na mwakilishi wa Umoja wa Mataifa kwenye programu ya Chakula Duniani UN WFP, Bi. Sarah Gordon - Gibson mara baada ya kuwasili na kujitambulisha na kuangalia maeneo ya mashirikiano ofisini kwake mtumba jijini Dodoma. (16.02.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (wa nne kutoka kulia) akiongea na mwakilishi wa Umoja wa Mataifa kwenye Programu ya Chakula Duniani UN WFP, Bi. Sarah Gordon - Gibson (wa tatu kutoka kulia) pamoja na maafisa wengine alioambatana nao wakati walipomtembelea ofisini kwake Mtumba jijini Dodoma lengo likiwa ni kujitambulisha na kuangalia maeneo ya mashirikiano. (16.02.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (wa pili kutoka kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na mwakilishi wa Umoja wa Mataifa kwenye programu ya Chakula Duniani UN WFP Bi. Sarah Gordon - Gibson (wa pili kutoka kulia) na Maafisa wengine walioambatana nae mara baada ya kujitambulisha na kuangalia maeneo ya mashirikiano leo kwenye Ofisi za Wizara hiyo, mtumba jijini Dodoma. (16.02.2021)



 

UHABA WA WATAALAM WENYE UJUZI KILIO KWA WAWEKEZAJI

Na Mbaraka Kambona, Pwani

 

Mratibu na Mkurugenzi wa Operesheni, Kiwanda cha Kutengeneza Chanjo cha Hester, Tina Towo Sokoine amesema kuwa lengo la kiwanda hicho ni kutumia Wataalam wa ndani lakini uhaba wa Wataalam wa masuala ya sayansi wenye ujuzi hasa wa vitendo unaelekea   kukwamisha dhamira yao hiyo.

 

Towo aliyasema hayo alipokuwa akitoa taarifa ya utekelezaji wa kiwanda hicho kwa Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel alipotembelea kiwanda hicho kilichopo Wilayani Kibaha, Mkoani Pwani Februari 13, 2021.

 

Alisema kuwa kwa sasa wana wataalamu watatu tu kutoka nje ya nchi ambao wamewaajiri katika Kiwanda hicho lakini   kwa hali ilivyo wanaona watashindwa na labda wanaweza kuomba vibali vingine vya kuajiri wataalamu kutoka nje.

 

“Nia yetu ni kufanyakazi na Watanzania tu lakini bado vijana wengi tunaowafanyia usahili wanakosa ujuzi hasa wa vitendo, tunaiomba Serikali na Vyuo vinavyoandaa hawa Wataalam kuhakikisha wanajikita katika elimu ya vitendo na sio nadharia peke yake ili kukidhi mahitaji ya sasa na kulinda ajira za Watanzania,” alisema Towo

 

Kuhusu uzalishaji, Towo alisema kuwa wanatarajia kuzalisha chanjo ya kwanza mwezi wa nne mwaka huu, huku akiiomba Serikali kuona uwezekano wa taasisi zinazohusika na kusimamia uwekezaji kuunganishwa ziwe na lugha ya pamoja ili kumfanya muwekezaji aweze kupata huduma zote sehemu moja bila kuhangaika kama ilivyosasa.

 

Naye Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel aliutaka Uongozi wa Kiwanda hicho kuhakikisha wanazalisha chanjo zenye ubora ili nchi iweze kuondokana na utegemezi wa chanjo na bidhaa nyingine za mifugo kutoka nchi za nje.

 

 

“Lengo la Wizara ni kuhakikisha kuwa nchi inaondokana na uagizaji wa chanjo kutoka nje, tunatamani kuwa na chanjo tunazoweza kudhibiti ubora wake na tuwe na uhakika nayo, hivyo uwepo wa kiwanda hiki kutatusaidia kuzalisha chanjo hapa hapa nchini ili kukidhi mahitaji ya Wafugaji wetu na Watanzania kwa ujumla,” alisema Prof. Ole Gabriel

 

Aliongeza kwa kusema kuwa Serikali inaweka mazingira mazuri ya uwekezaji ili mahitaji ya wafugaji na wananchi yawe yanashughulikiwa ndani ya nchi.

 

Aidha, Prof. Ole Gabriel aliwaomba Wafugaji na Watanzania kuanza kujenga utamaduni wa kuthamini bidhaa za ndani na waondokane na ile dhana ya kwamba bidhaa bora ni ile inayotoka nje, wakithamini vya ndani wataongeza pato la Taifa na kukuza uchumi wa nchi.

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akibadilishana mawazo na Mkuu wa Kiwanda cha Kutengeneza Chanjo cha Hester,  Dkt. Umapati Dasgupta (kushoto) muda mfupi baada ya kumaliza kutembelea kiwanda hicho kilichopo Wilayani Kibaha, Mkoani Pwani Februari 13, 2021.

Mkuu wa Kiwanda cha Kutengeneza Chanjo cha Hester, Dkt. Umapati Dasgupta (kulia) akimueleza jambo Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) alipotembelea kukagua kiwanda hicho kilichopo Wilayani Kibaha, Mkoani Pwani Februari 13, 2021.

Mtaalam wa Kuendesha Mitambo katika Kiwanda cha Kutengeneza Chanjo cha Hester, Geofrey Mahende (kulia) akitoa maelezo ya namna anavyofanyakazi yake kwa Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) alipotembelea kukagua kiwanda hicho kilichopo Wilayani Kibaha, Mkoani Pwani Februari 13, 2021.

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wataalam wa Kitanzania wanaofanyakazi katika Kiwanda cha kutengeneza Chanjo cha Hester alipotembelea kiwanda hicho kilichopo Mkoani Pwani Februari 13, 2021. Wa kwanza kushoto ni Mratibu na Mkurugenzi wa Operesheni, Tina Towo Sokoine.





PROF. GABRIEL AELEZA KWA UFUPI UMUHIMU WA KIWANDA CHA ACE LEATHER TANZANIA Ltd.

 

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akieleza kwa ufupi umuhimu wa Kiwanda cha Ace Leather Tanzania Ltd katika kuleta maendeleo ya Sekta ya Mifugo hususan katika tasnia ya ngozi mapema leo wakati wa uzinduzi wa Kiwanda hicho uliofanyika Mkoani Morogoro Februari 12, 2021.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Kiwanda cha kuchakata Ngozi cha Ace Leather Tanzania Ltd kilichopo Kihonda, Mkoani Morogoro Februari 12, 2021. Kulia kwake ni Mmiliki wa Kiwanda hicho, Rostam Aziz. Wa kwanza kulia, mstari wa nyuma ni Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel. Wengine ni Viongozi Wakuu wa Serikali na baadhi ya wamiliki wa kiwanda hicho.


Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akimueleza jambo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Selemani Jafo (katikati) walipokutana katika uzinduzi wa Kiwanda cha kuchakata Ngozi cha Ace Leather Tanzania Ltd uliofanyika Mkoani Morogoro leo Februari 12, 2021. Wa kwanza kushoto ni Mkuu wa Kituo cha Polisi Wilaya ya Morogoro Mjini, Georgina Matagi.


NARCO YAAGIZWA KUWANYANG'ANYA VITALU WALIOKIUKA MKATABA

Na Mbaraka Kambona,

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki ameiagiza Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) kuwanyang'anya wale wote walioshindwa kuendeleza vitalu walivyokodishwa  katika ranchi za kampuni hiyo kwa sababu wamekiuka masharti ya mkataba.

 

Ndaki alitoa agizo hilo alipokutana na Viongozi wa Chama cha Wafugaji katika kikao cha kujadili Maendeleo ya Sekta ya Mifugo kilichofanyika jijiji Dodoma Februari 10, 2021.

 

Alisema kuwa kuna watu wengi wamekodishwa maeneo katika ranchi za taifa lakini wamezitelekeza na wengine wamekodisha watu wengine ambao wanatumia maeneo hayo kinyume na makubaliano ya mkataba.

 

"Ikifika tarehe 15 mwezi huu, wale wote waliochukua vitalu na wamekodisha watu wengine wanyang'anywe maeneo hayo na hatutajali mikataba yao kwani wameshakiuka masharti," alisema Ndaki

 

Aliongeza kwa kusema kuwa baada ya tarehe 15 kupita wataanza kuwasaka wote waliochukua maeneo hayo na kuwanyang'anya ili wapewe wafugaji makini waweze kutumia maeneo hayo kuweka mifugo yao.

 

Kuhusu baadhi ya Wananchi wanaoishi karibu na ranchi kuvamia maeneo hayo, Ndaki alitumia nafasi hiyo pia kuwataka waondoke katika maeneo hayo na wasipofanya hivyo wataondolewa.

 

Aliendelea kusema kuwa wameanza mikakati ya kuiweka vizuri NARCO ili maeneo makubwa iliyonayo ambayo mengine hawayatumii vizuri yagawiwe kwa wafugaji watakaoweza kuyatumia kufanya ufugaji wa kisasa nah atua waliyoanza nayo ni kupunguza bei ya kukodisha vitalu.

 

"Tumekubaliana kuwa bei ya kukodisha kitalu iwe ni shilingi elfu tatu mia tano (3500) kwa Ekari moja na sio zaidi ya hapo," alisema Ndaki

 

Waziri Ndaki alisema kuwa wameielekeza NARCO kuwa katika yale maeneo waliyoyatenga kwa ajili ya ukodishaji watenge asilimia thelathini (30) kwa ajili ya kuwakodisha wafugaji wanaoishi karibu na maeneo ya ranchi hizo ili kupunguza migogoro na uvamizi wa maeneo hayo.

 

"Hata maeneo yetu yaliyotengwa kwa ajili ya kupumzishia mifugo (holding grounds) tutayapunguza ili nayo tuwape NARCO ili wayakodishe kwa wafugaji wetu, tunaamua kufanya haya ili kutibu tatizo la malisho na wafugaji waondokane na kutangatanga," alifafanua Ndaki

 

Mapema wiki hii Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NARCO, Paul Kimiti alitangaza kuwa ekari moja ya kitalu katika ranchi hizo itakodishwa kwa shilingi elfu tatu mia tano (3500).

Katibu Tawala, Mkoa wa Kagera, Prof. Faustin Kamuzora (wa kwanza kulia) akimueleza jambo Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (wakwanza kushoto) walipokutana katika kikao cha kujadili Maendeleo ya Sekta ya Mifugo kilichofanyika jijini Dodoma Februari 10, 2021. Wa pili kushoto ni Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel na wa pili kutoka kulia ni Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji Tanzania, Jeremiah Wambura.


Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akifafanua jambo kwa baadhi ya wafugaji waliohudhuria kikao cha kujadili Maendeleo ya Sekta ya Mifugo kilichofanyika jijiji Dodoma Februari 10, 2021.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (kulia) akiteta jambo na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro walipokutana katika kikao cha kujadili Maendeleo ya Sekta ya Mifugo kilichofanyika jijini Dodoma Februari 10, 2021.

WATUMISHI WA UMMA WANAOINGIZA KWA MAKUSUDI MIFUGO KWENYE HIFADHI NA KUNYANYASA WAFUGAJI WAONYWA

Na. Edward Kondela

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema atazungumza na Waziri wa Maliasili na Utalii kuhusu kitendo cha baadhi ya watumishi wa umma walio chini ya wizara hiyo, ambao wamekuwa wakiielekeza mifugo kwa makusudi kuingia kwenye hifadhi za taifa ili waikamate na kuwaonea wafugaji kwa kuwalipisha tozo pamoja na kutaifisha mifugo hiyo.

 

Waziri Ndaki amezungumza hayo jana (09.02.2021) wakati akihitimisha ziara yake ya siku mbili Mkoani Kilimanjaro, kwa kuzungumza na baadhi ya wafugaji katika Wilaya ya Siha mkoani humo mara baada ya kutembelea Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) na Ranchi ya West Kilimanjaro  zilizopo katika wilaya hiyo ili kujionea namna wanavyotekeleza majukumu yao.

 

Amesema kitendo hicho cha kifisadi hakiwezi kuvumilika na kwamba watuhumiwa wote watatafutwa na kukamatwa ili hatua kali za kisheria ziweze kuchukuliwa ikiwemo kufukuzwa kazi.

 

“Ninajua kuna wakati tunaonewa unakuta ng’ombe wako pembeni ya hifadhi wanapelekwa kwa lazima ndani ya hifadhi, nimesema nazungumza na mwenzangu wa maliasili na utalii na kumwambia huo mtindo hapana, tuwasake watu wako kwa sababu wenye tabia hiyo siyo wafugaji ni watu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, hao tunaanza kuwasaka mmoja mmoja maeneo yote wanayokaa karibu na wafugaji tutawabaini na wanachokifanya ni kitendo cha kiharamu na ufisadi kwa sababu una bunduki unamtisha mfugaji halafu unawapeleka kwa lazima ng’ombe kwenye hifadhi hiyo na kusema umewakamata ng’ombe kwenye hifadhi hatutaelewana.” Amesema Mhe. Ndaki 

 

Ameongeza kuwa kitendo hicho lazima kikemewe kwa kuwa kinarudisha nyuma uwekezaji katika Sekta ya Mifugo na kutaka watumishi wa umma pamoja na wafugaji kufuata sheria, taratibu na kanuni za nchi na kwamba lazima kukomesha hatua hiyo kwa sababu inasababisha migogoro kati ya wafugaji na hifadhi za taifa na kwamba kuna wakati wafugaji wanaelewa maeneo ya hifadhi, lakini wakipeleka mifugo karibu na maeneo hayo wananyanyaswa na mifugo yao kulazimishwa kuingia ndani ya hifadhi ili ionekane wameingiza mifugo ndani ya hifadhi.

 

Katika hatua nyingine, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki ameitaka Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) kufikia Jumatano ijayo, iwe imeandaa taarifa ya mifugo iliyopo kwenye ranchi zote hapa nchini, zikiwemo za kiwango cha mifugo inayozaliwa, kufa na aina ya mifugo iliyopo ili kuona kinachoendelea katika ranchi hizo.

 

Amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel, kuhakikisha anasimamia zoezi hilo ili taarifa hizo aweze kuzipata siku hiyo ya Jumatano, ikiwa ni lengo la kuhakikisha mifugo ya serikali inakuwa na tija kwa taifa.

 

“Tunataka rasilimali ya mifugo inufaishe taifa na wananchi hawa hatuwezi kuwa na rasilimali ambayo hatujui iko kiasi gani.” Amefafanua Mhe, Ndaki.  

 

Pia ameitaka NARCO kuhakikisha inatumia teknolojia ya kisasa ya kuwawekea mifugo iliyopo kwenye ranchi zake ili kudhibiti vitendo vya wizi wa mifugo ambavyo vimekuwa vikijitokeza katika ranchi zake na kuisababishia hasara za mara kwa mara.

 

Kuhusu uwekezaji wa NARCO katika duka la kuuzia nyama lililopo Kata ya Sanya Juu Wilaya ya Siha Mkoani Kilimanjaro, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki ameitaka kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo kufanya uchunguzi juu ya utendaji wa duka hilo baada ya kutoridhishwa na taarifa zilizorekodiwa tangu kuanza kwake kazi ya uuzaji nyama.

 

Waziri Ndaki ameongeza kuwa kumekuwa na taarifa za mauzo kidogo ya nyama ambayo hayalingani na uhitaji wa nyama eneo husika, huku akitaka mmoja wa mawakala ambaye aliwahi kuwa na utaratibu wa kununua nyama katika Ranchi ya West Kilimanjaro kwa bei ya jumla na kwenda kuuza kwenye duka lake kuchunguzwa na kuitaka kamati hiyo kuwachukulia hatua za kisheria wale wote watakaobainika kuhujumu utendaji kazi wa duka.

 

Kwa upande wao baadhi ya wafugaji waliohudhuria mkutano huo wamelalamikia uvamizi wa wanyamapori ambao wamekuwa wakiingia katika maeneo yao na kuharibu mazao na malisho ya mifugo hali ambayo imekuwa ikiwarudisha nyuma katika utendaji wao wa kazi.

 

Wameongeza kuwa kitendo hicho kimeathiri kwa kiasi kikubwa malisho ya mifugo na kuiomba serikali kuangalia hatua ambazo inaweza kuchukua ili kudhibiti kitendo hicho ambacho kimekuwa kikiwarudisha nyuma mara kwa mara pamoja na kufanya mikakati mbalimbali ya kuhakikisha dawa na chanjo za mifugo zinawafikia ili kudhibiti magonjwa ya mifugo ambayo yamekuwa yakiathiri kwa kiasi kikubwa mifugo yao.

 

Awali kabla ya kikao hicho na baadhi ya Wafugaji wa Wilaya ya Siha, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiwa katika Ranchi ya West Kilimanjaro inayosimamiwa na Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) kujionea utendaji kazi wa ranchi hiyo pamoja na kupokea taarifa ya namna ranchi hiyo inafanya kazi kutoka kwa meneja wa ranchi hiyo Bw. Raymond Lutege ambaye amemuambia Waziri Ndaki kuwa ranchi hiyo iko katika hatua mbalimbali za kuhakikisha mbegu bora za mifugo wakiwemo ng’ombe na kondoo zinapatikana ili wafugaji waweze kufuga kisasa kwa kuwa na mifugo bora.

 

Waziri Ndaki akiwa katika Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) Kituo cha Wilaya ya Siha, mara baada ya kusomewa taarifa ya kituo na Kaimu Mkurugenzi wa Kanda ya Kaskazini Dkt. Athuman Nguluma, waziri huyo ameitaka TALIRI kuhakikisha tafiti inazofanya ziwe na tija kwa wafugaji na taifa kwa ujumla ili tasnia ya ufugaji iweze kubadilika na kuwa ya kisasa zaidi.

 

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Siha Mhe. Onesmo Buswelu amesema anaimani kubwa na utendaji kazi wa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki kwa namna alivyoanza kusimamia sekta za mifugo na uvuvi na kuonesha nia thabiti ya kutatua changamoto zilizopo katika sekta hizo.

 

Ameongeza kuwa serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa ikifanya jitihada kuhakikisha wafugaji wananufaika kwa kiasi kikubwa pamoja na kuondoa migogoro kati ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na baadhi ya wafugaji katika Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kituo cha Wilaya ya Siha, wakati akihitimisha ziara yake ya kikazi ya siku mbili Mkoani Kilimanjaro na kuwataka wafugaji wafuge kisasa na kuwahakikishia kuwa wizara itaendelea kusimamia maslahi ya wafugaji nchini. (09.02.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akisalimiana na baadhi ya wafugaji wa jamii ya kimaasai mara baada ya kuzungumza nao alipotembelea Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kituo cha Wilaya ya Siha, wakati akihitimisha ziara yake ya kikazi ya siku mbili Mkoani Kilimanjarao.  (09.02.2021)

Picha ya pamoja ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiwa na uongozi wa Wilaya ya Siha, na baadhi ya kinamama wa jamii ya kimaasai mara baada ya kuzungumza na baadhi ya wafugaji wa jamii hiyo, alipotembelea Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kituo cha Wilaya ya Siha, wakati akihitimisha ziara yake ya kikazi ya siku mbili Mkoani Kilimanjaro. (09.02.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akifafanua jambo kwa Meneja wa Ranchi ya West Kilimanjaro Bw. Raymond Lutege (wa kwanza kulia) mara baada ya Waziri Ndaki kufika katika ranchi hiyo siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi ya siku mbili Mkoani Kilimanjaro na kutaka ranchi zote za taifa kutumia teknolojia ya kisasa katika kudhibiti wizi wa mifugo katika ranchi hizo. (09.02.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (katikati) akipatiwa maelezo ya mbegu bora za mbuzi na Kaimu Mkurugenzi wa Kanda ya Kaskazini wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) Dkt. Athuman Nguluma, mara baada ya Waziri Ndaki kutembelea kituo cha taasisi hiyo kilichopo Wilaya ya Siha Mkoani Kilimanjaro wakati akihitimisha ziara yake ya kikazi ya siku mbili mkoani humo na kuitaka TALIRI ihakikishe matokeo ya tafiti zake yanakuwa na tija kwa wafugaji. (09.02.2021)

Muonekano wa duka la kuuzia nyama linalomilikiwa na Ranchi ya West Kilimanjaro iliyo chini ya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO), ambalo Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki ameitaka kamati ya ulinzi na usalama ya Wilaya ya Siha kufanya uchunguzi wa utendaji kazi wa duka hilo baada ya kutoridhishwa na namna linavyoendeshwa tangu kuanzishwa kwake. (09.02.2021)