Nav bar

Ijumaa, 22 Julai 2022

WAFUGAJI KUELIMISHWA UFUGAJI WA TIJA NA KIBIASHARA, KUONDOKANA NA UMASIKINI

Edward Kondela


Serikali imesema lengo kubwa la Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa wafugaji ni kukuza tija na kuwasaidia kufuga kibiashara ili waweze kunufaika kupitia mifugo yao.

 

Akizungumza (15.07.2022) wakati akimwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa kwenye maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani katika Shamba la mifugo la Mbogo, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema shughuli za ufugaji na uvuvi zimekuwa zikiendeshwa kiasili hivyo kushindwa kukua na kubadili maisha ya wadau wa sekta hizo.

 

Waziri Ndaki amebainisha kuwa imani mbalimbali pia zimekuwa zikitawala kwa wafugaji na wavuvi kwenye shughuli zao na kusababisha kutopokea kwa haraka mabadiliko na kufanya shughuli hizo bila kufuata utaalamu, ujuzi, weledi na kufahamu hitaji la soko ili kufuga kwa tija na kibiashara.

 

“Tumeanza ngazi ya wizara kuzungumza juu ya tija zaidi na biashara zaidi kubadilisha mtazamo wa wafanyabiashara wetu wafahamu kufuga ni kazi ya kitaalamu, hivyo natoa wito tuendelee kuelimisha wafugaji wetu.” Amesema Mhe. Ndaki

 

Naye Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akizungumza katika maonesho hayo ambayo yamehusisha mifugo bora na kisasa wakiwemo ng’ombe, mbuzi na kondoo, amesema fursa ni kubwa sana katika Sekta ya Mifugo na kwamba huo ni mwanzo mzuri wa kupatikana kwa wafugaji waliyo makini katika ufugaji wenye malengo.

 

Ameongeza kuwa uwepo wa mifugo bora na inayotambulika ni rahisi kupatikana kwa bidhaa zitokanazo na mifugo ikiwemo nyama kwa ajili ya soko la ndani na hasa soko la nje ya nchi ili wafanyabiashara na nchi kwa ujumla kuongeza kipato.

 

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Bw. Tixon Nzunda amebainisha kuwa kupitia mifugo ni wakati sasa wa kubadilisha wafugaji kutoka kwenye kufuga kiasili na kufuga kisasa ili waweze kuongeza kipato.

 

Amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi itahakikisha inasimamia malengo yote ya kuwasaidia wafugaji ili Sekta ya Mifugo iwe sehemu salama kwa wafugaji kuwekeza na kunufaika kimaisha kwa kuongeza kipato kupitia ufugaji wa kisasa.

 

Kuhusu ufugaji wa kibiashara, Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji Kibiashara Tanzania (TCCS) Bw. Naweed Mulla ambao wameandaa maonesho hayo ya mifugo na mnada ameelezea uanzishwaji wa chama hicho baada ya kugundua fursa mbalimbali katika Sekta ya Mifugo ambapo wafanyabiashara wa mifugo walikaa pamoja ili kuchangamkia fursa hizo na kutatua changamoto za sekta.

 

Pia, amesema chama hicho kiliamua kuanzisha maonesho hayo ya kila mwaka ili kuhamasisha wananchi hususan vijana kuingia katika ufugaji wa kisasa na kuwatoa katika umasikini.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki na Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Abdallah Ulega wakimsikiliza mmoja wa wataalamu akiwapatia maelezo juu ya ufugaji wa ng’ombe bora wa kisasa wakati wa maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo. (15.07.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa nne kutoka kulia), akipata maelezo juu ya ufugaji wa mbuzi na kondoo bora wa kisasa kutoka kwa mmoja wa wataalamu waliopo kwenye maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo, akiambatana na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (wa tatu kutoka kushoto) na Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji Kibiashara Tanzania (TCCS) Bw. Naweed Mulla (kushoto kwake). (15.07.2022)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw. Tixon Nzunda (katikati) akimsikiliza mmoja wa wataalamu akimwelezea juu ya teknolojia mbalimbali zinazotumika katika Sekta ya Mifugo, wakati katibu mkuu huyo akitembelea mabanda kwenye maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo. (15.07.2022)

Mmoja wa wataalamu kutoka kiwanda cha kuzalisha chanjo cha Hester Biosciences Africa Limited akifafanua juu ya utengenezaji wa chanjo za mifugo kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki na Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Abdallah Ulega kwenye maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo. (15.07.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki na Naibu wa wizara hiyo Mhe. Abdallah Ulega wakiwa kwenye banda la Wizara ya Mifugo na Uvuvi kushuhudia namna shughuli mbalimbali zinazofanywa na wizara pamoja na taasisi zilizo chini ya wizara hiyo, katika kukuza Sekta ya Mifugo wakati wa maonesho ya mifugo na mnada yanayofanyika katika Wilaya Bagamoyo Mkoani Pwani kwenye Shamba la mifugo la Mbogo. (15.07.2022)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni