Nav bar

Ijumaa, 29 Julai 2022

TAFITI KUBORESHA MAENDELEO YA SEKTA YA UVUVI

Tafiti zinazofanywa kwenye sekta ya uvuvi zinalenga kuhakikisha wadau wa sekta hiyo wanaboresha shughuli zao katika mnyororo wa thamani wa mazao ya uvuvi.

 

Hayo yamesemwa leo (25.07.2022) na mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Kayuni ambaye pia ni Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa sekta hiyo wakati akifungua mafunzo ya kuandaa vijarida sera yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro.

 

Bw. Kayuni amesema kuwa tafiti zinazofanyika ni lazima matokeo yake yawafikie walengwa ambao ni wadau wa sekta ya uvuvi ili kuweza kuwanufaisha na kuboresha shughuli wanazozifanya katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.

 

“Tafiti zinazofanyika ni lazima ziwafikie walengwa, kuzielewa na kuwasaidia kubalidilisha maisha yao katika shughuli wanazozifanyi, hapo tafiti hizo zinakuwa na tija katika kuleta maendeleo ya wadau wa sekta ya uvuvi na taifa kwa ujumla.” alisema Bw. Kayuni

 

Sekta ya Uvuvi imepanga kuzitumia tafiti zinazofanywa kwa lengo la kuboresha sera zinazohusu sekta ya uvuvi ili wadau wa sekta hiyo waweze kunufaika. Bw. Kayuni amesema kuwa tafiti zinazofanywa zikifanyiwa kazi zinawafanya watafiti kuendelea kufanya tafiti zaidi kwa lengo la kuboresha sekta ya uvuvi.

 

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Huduma za Ugani, Prof. Mohammed Sheikh amesema kuwa mafunzo hayo ni kwa ajili ya kusaidia kwenye kutunga sera na kufanya maamuzi ambayo yatasaidia kuipeleka sekta ya uvuvi mbele. Prof. Sheikh amesema Sekta ya Uvuvi imeamua kufanya mafunzo hayo kwa lengo la kuwajengea uwezo wataalam ili kuweza kuzitumia tafiti ambazo zimefanyika ili kuwaletea maendeleo wadau wa sekta hiyo. Pia amesema kuwa matarajio ya mafunzo hayo ni kuhakikisha kuwa tafiti mbalimbali zinazofanyika kuhusu sekta ya uvuvi kutobakia kwenye makaratasi badala yake kwenda kuwafikia wadau na kuleta maendeleo kwenye sekta ya uvuvi.

 

Meneja Seksheni ya Sayansi za Jamii (COSTECH), Bi. Hildegalda Mushi amesema kuwa taasisi yao inafanyakazi ya kuwezesha tafiti mbalimbali ambazo zinalenga kuwezesha maendeleo ya matokeo ya tafiti na kuwezesha maendeleo ya teknolojia. Tafiti hizi zinalengo la kuhakikisha kuwa wadau wa uvuvi wanasonga mbele kimaendeleo na kuhakikisha zinawasaidia watunga sera ili waweze kutunga sera ambazo zinatekelezeka kwa maendeleo ya wadau na taifa kwa ujumla.

 

Mafunzo hayo yamewahusisha wataalam kutoka Sekta ya Uvuvi, Taasisi ya Utafiti ya Uvuvi (TAFIRI), Wakala ya Mafunzo ya Uvuvi (FETA), na COSTECH ambapo washiriki wamepata fursa ya kujadili kwa kina juu ya matokeo ya tafiti zilizofanyika kwa maelengo ya kuipeleka mbele sekta ya uvuvi.


Mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Kayuni akifungua mafunzo ya kuandaa vijarida Sera ambapo amewasihi watafiti kuhakikisha matokeo ya tafiti zao yanakwenda kubadilisha maisha ya wadau waliopo kwenye mnyororo wa thamani wa mazao ya uvuvi. Mafunzo hayo yamefanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. (25.07.2022)

Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Huduma za Ugani, Prof. Mohammed Sheikh akiwasilisha mada ya utangulizi kwenye mafunzo ya kuandaa vijarida Sera yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. Prof. Sheikh amesema kuwa Sekta ya Uvuvi inaendelea kujipanga kuhakikisha matokeo ya tafiti yanakwenda kubadilisha maisha ya wadau wa sekta hiyo. (25.07.2022)


Meneja Seksheni ya Sayansi za Jamii kutoka COSTECH, Bi. Hildegalda Mushi akizungumza na washiriki wa mafunzo ya kuandaa vijarida Sera yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. (25.07.2022)


Baadhi ya Washiriki wa Mafunzo ya kuandaa viharida sera wakifuatilia mada zilizokuwa zinawasilishwa kwenye mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. (25.07.2022) 


Mwakilishi wa Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Kayuni akiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa Mafunzo ya kuandaa vijarida Sera mara baada ya kufungua mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa TAFORI Manispaa ya Morogoro. (25.07.2022)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni