Nav bar

Jumatatu, 7 Februari 2022

UZALISHAJI VIFARANGA VYA SAMAKI WAWEKEWA MKAKATI ENDELEVU

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeweka mikakati endelevu ya kuhakikisha inazalisha kwa wingi vifaranga vya samaki na kutoa elimu juu ya ufugaji wa samaki kwa wananchi ili kuongeza tija na kipato kwa Wafugaji na Taifa kwa ujumla.

Mkurugenzi wa Ukuzaji Viumbe  Maji wa  Wizara hiyo , Dkt. Nazael  Madalla  alisema hayo Februari 1,2022  katika mafunzo rejea kwa maofisa ugani wa halmashauri za  mikoa ya Dar es Salaam, Tanga , Arusha , Pwani na Kilimanjaro yanayofanyika Mkoani Morogoro.

Dkt. Madalla alisema mafunzo hayo yamelenga   kuhamasisha,  kuendeleza , kusimamia tasnia ya ukuzaji viumbe maji nchini na kuzalisha kwa tija .

Aliendelea kusema kuwa vituo vinavyozalisha vifaranga wa samaki kwa Sasa ni vitatu ambavyo ni  Ruhila kilichopo  mkoa wa Ruvuma,  Mwamapuli  mkoani Tabora, na Kingolwira Morogoro.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo,  mwaka 2020/2021 vituo hivyo  vitatu viliwezakuzalisha jumla  ya vifaranga vya samaki 1,901,717.

“Uzalishaji wa vifaranga vya Samaki katika vituo hivyo ni kama ifuatavyo, Kituo cha Ruhila kilizalisha vifaranga 972,305, Mwamapuli vifaranga 457,812 na cha hapa Kingolwira vifaranga 471,600 ", alisema Dk Madalla.

Aliongeza kwa kusema kuwa wizara imejipanga kuhakikisha ufugaji wa samaki unakuwa endelevu na wenye tija kwa wafugaji.

“kuanzishwa kwa vituo hivyo vya ukuzaji viumbe maji unakwenda sambamba na utoaji elimu sahihi ya ufugaji wa samaki pamoja na uzalishaji vifaranga vya Samaki", alifafanua

Aidha, aliwahimiza Watanzania kujitokeza kufuga samaki na viumbe maji wengine ili kujiongezea kipato chao na Taifa kwa ujumla.

Pamoja na hayo alitumia fursa hiyo kuwahimiza wananchi kupenda kula samaki na dagaa kwa wingi akisema kuwa madini mengi yanayopatikana ndani yake yanasaidia katika kupambana na magonjwa kwenye mwili wa binadamu.

Naye  Katibu Tawala Msaidizi, Uchumi na Uzalishaji Mali Mkoa wa Morogoro, Dkt. Rozalia Rwegasira  akisoma hotuba ya  Katibu Tawala wa Mkoa  huo, Mariam Mtunguja alisema kuwa wizara inatarajia kufikia lengo la mpango wa tatu wa maendeleo wa Taifa wa miaka mitano  kwa kuzalisha tani 50,000 za mazao ya ukuzaji wa viumbe maji kwa mwaka ifikapo mwaka 2025/2026.

Hivyo aliwataka Watanzania kuchangamkia fursa zilizopo katika uchumi wa bluu kutokana na kuwepo rasilimali maji ikiwemo bahari, maziwa, mito na maeneo oevu ambayo yanatoa wigo mpana wa kufanya shughuli za ufugaji wa samaki na viumbe wengine wa majini.

Dkt. Rwegasira aliongeza kuwa pamoja na Serikali kuwekeza nguvu kubwa katika sekta ya mifugo na uvuvi, bado kuna uzalishaji mdogo  wa mazao ya viumbe maji ukilinganisha na fursa zilizopo nchini.

“Tasnia ya ukuzaji viumbe maji inakabiliwa na upungufu wa maofisa ugani 15,323 ambapo kwa sasa kuna maofisa ugani 677 ikilinganishwa na mahitaji ya maofisa ugani 16, 000” alisema Dk Rwegasira.

Dk Rwegasira aliwataka maofisa ugani waliopo kupeleka teknolojia walioipata kwa watanzania ili waweze kufuga samaki na viumbe maji wengine kwa njia ya kisasa zaidi ili kukidhi mahitaji ya  soko la kimataifa  kwani kwa sasa kuna uhitaji mkubwa wa kitoweo cha samaki.

Kwa upande wao  washiriki wa mafuzo hayo Lucia Balilemwa pamoja na Emmanuel Ntobi  kwa nyakati tofauti waliishukuru serikali kwa kuwapatia mafunzo rejea hayo  na kwamba watayatumia kubadirisha maisha ya wananchi katika maeneo  walikotoka  juu ya  ufugaji bora wa samaki  na hivyo itapunguza changamoto ya uvuvi haramu.


Picha ya Pamoja ya Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Uchumi na Uzalishaji (Morogoro), Dkt. Rozalia Rwegasila (katikati waliokaa) Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji, Dkt. Nazael Madalla (kushoto), Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji Baridi, Dkt. Imani Kapinga (kulia) na Washiriki wa Mafunzo Rejea ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Kilimanjaro na Pwani mara baada ya kufunguliwa kwa mafunzo hayo,yanayoendelea katika kituo cha Kingolwira Mkoani Morogoro. (01.02.2022).* 






 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni