Nav bar

Jumanne, 3 Februari 2026

BBT IWEKEZE KATIKA KUZALISHA MALISHO YA MIFUGO – DKT. BASHIRU

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, amezitaka taasisi zinazotekeleza Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) kutumia maeneo yao kuzalisha malisho ya mifugo ili kuimarisha ufugaji wa kibiashara.

Ametoa kauli hiyo leo Januari 31, 2026 alipokagua Kituo cha BBT cha unenepeshaji wa mbuzi na kondoo Kongwa mkoani Dodoma, akizitaka Kampuni za Ranchi ya Taifa (NARCO), Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) na Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (LITA) kuweka kipaumbele katika uzalishaji wa malisho kibiashara, kutokana na kwamba taasisi hizo zina ardhi, utaalam na uzoefu wa kutosha kufanikisha azma hiyo.

“Vituo vyetu vyote vyenye ardhi kubwa kama hizi TALIRI, NARCO, LITA kwa sababu tunautaalam na uzoefu  mkubwa nguvu zote zipelekwe kwenye uzalishaji wa malisho, mimi ningefurahi kuona  kuwa hii ni BBT ya malisho” alisema Mhe. Balozi Dkt. Bashiru. 

Aidha, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru amehimiza wafugaji kupewa elimu ya uzalishaji wa malisho na kuagiza utekelezaji wa programu hiyo uishirikishe Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana ili kuwafikia vijana wengi zaidi.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa BBT kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mkurugenzi wa Tathmini na Ufuatiliaji Dkt. Daudi Mayeji amesema Wizara hiyo imetengewa dola za Marekani milioni 32.8 sawa na shilingi bilioni 81 kwa ajili ya utekelezaji wa programu hiyo, huku uwekezaji wa awali wa Kituo cha Kongwa ukiwa dola milioni 11.82.

Programu ya BBT ilianza mwaka 2018 kupitia TALIRI kwa kushirikiana na PASS Trust Tanzania, ikilenga kuwawezesha vijana kujiajiri kupitia mnyororo wa thamani wa mifugo na kuchangia uchumi wa taifa.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa  akitoa maelekezo kwa Mhandisi wa Wizara juu ya ulinzi wa miundombinu ya BBT ya Mifugo wakati wa ziara yake kwenye kituo cha  BBT Kongwa  mkoani Dodoma leo Januari 31, 2026.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wapili kulia) akifafanuliwa jambo na Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Prof. Eric Komba (wapili kushoto) wakati wa ziara ya kukagua miundombinu ya Programu ya BBT Mifugo kituo cha Kongwa  mkoani Dodoma leo Januari 31, 2026.

Mabanda ya Mbuzi na Kondoo yanayotakiwa kufanyiwa ukarabati kwa ajili Programu ya BBT ya Mifugo awamu ijayo

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wa pili kulia) akikagua machinjio ya mbuzi na kondoo katika Kituo cha BBT ya Mifugo cha Kongwa Mkoani Dodoma wakati wa ziara yake ya kukagua miundombinu ya pragramu hiyo leo 31, Januari, 2026

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa akitoa maelekezo kwa wataalam kuhusu uzalishaji wa malisho ya mifugo kupitia Programu ya BBT Mifugo machinjio ya mbuzi na kondoo katika Kituo cha BBT ya Mifugo  wakati wa ziara yake ya kukagua miundombinu ya pragramu  hiyo Kituo cha Kongwa mkoani Dodoma leo 31, Januari, 2026

FETA YATAKIWA KUONGEZA UZALISHAJI WA VIFARANGA VYA SAMAKI

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Edwin Mhede ameitaka Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kuongeza uzalishaji wa vifaranga vya samaki ili viweze kukidhi hitajio kubwa lililopo hapa nchini.

Dkt. Mhede ametoa kauli hiyo jana,  29 Januari 2026 alipotembelea FETA Kampasi Kuu ya Mbegani kwa lengo la kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na FETA pamoja na miundombinu ya kujifunzia na kufundishia.

"Niwapongeze kwa utotoleshaji huu wa vifaranga na ufugaji samaki kwa ujumla ila niwasihi muongeze zaidi kasi ya uzalishaji vifaranga ili viende maeneo yenye uhitaji na nyie kujipatia kipato" amesema Dkt. Mhede.

Aidha, ameishauri FETA kuwekeza katika ufugaji samaki (hasa kwenye vizimba) katika maeneo mbalimbali ikiwepo Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika kwa lengo la kutoa mafunzo zaidi kama mashamba darasa na pia uzalishaji wa biashara ili kuongeza mapato.

Awali Mtendaji Mkuu wa FETA, Dkt. Semvua Mzighani amesema kuwa kwasasa FETA inaendelea kutoa mafunzo ya muda mfupi na mrefu katika ufugaji wa samaki ili wananchi na Taifa kwa ujumla lifaidike zaidi na fursa zilizopo katika  Uchumi wa Buluu. Maeneo ya kipaumbele ni pamoja na: ufugaji samaki, ufugaji wa Tango (Jongoo) Bahari, unenepeshaji wa Kaa na kilimo cha Mwani.

Akiwa FETA Dkt. Mhede alipata fursa ya kujionea mazingira mbalimbali ya kufundishia na kujifunzia ikiwemo eneo la utotoleshaji wa vifaranga vya samaki, mabwawa ya kufugia samaki aina ya sato na kambale, eneo la kukaushia samaki na mwani, Zahanati na Idara ya Uvuvi na Ubaharia ambapo alipata fursa kuongea na wanafunzi wa Fani ya Uvuvi na Ubaharia.