SERIKALI KUSHIRIKIANA NA CHUO CHA MINNESOTA KUWAJENGEA UWEZO WATAALAM WA MIFUGO
Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Minnesota cha Nchini Marekani, imeendelea kujadiliana na kuimarisha mahusiano yenye lengo la kuwajengea uwezo wataalam wa sekta ya mifugo kupitia mradi wa CAHFS ProgRESSVet ili kuhakikisha wataalam hao wanatoa huduma za afya ya wanyama zinazokidhi viwango vya kimataifa.
Hatua hiyo inafuatia ujio wa wataalam kutoka Kituo cha Afya ya Wanyama na Usalama wa Chakula cha Minnesota kwa ajili ya kujadili mashirikiano mapya ya mafunzo katika eneo la usalama wa chakula, Majadiliano yaliyo fanyika leo, Februari 25, 2026, katika Makao Makuu ya Wizara yaliyopo Mji wa Serikali Mtumba, Dodoma.
Ujumbe huo uliongozwa na Naibu Mkurugenzi wa CAHFS, Dkt. Maria Perez, na kupokelewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agnes Meena, ambaye alisisitiza dhamira ya serikali katika kuendeleza ushirikiano huo.
“Serikali itaendelea kushirikiana na Chuo Kikuu cha Minnesota kuhakikisha wataalam wetu wa mifugo wanapata mafunzo stahiki yatakayowawezesha kutoa huduma bora na zinazokidhi viwango vya kimataifa,”amesema Bi. Meena.
Kwa upande wake, Dkt. Perez amepongeza ushirikiano uliopo na kubainisha umuhimu wa programu hiyo katika kuimarisha sekta ya mifugo nchini Tanzania.
“Kupitia ProgRESSVet, tunalenga kujenga uwezo wa wataalam wa mifugo ili kuimarisha afya ya wanyama, usalama wa chakula na uchumi wa mifugo kwa ujumla,” amesema Dkt. Perez.
Hadi sasa, jumla ya wataalam 15 wa mifugo wamepata mafunzo katika awamu ya kwanza ya programu hiyo, huku awamu ya pili ikitarajiwa kuwahusisha wataalam 25 zaidi wanaotoa huduma za afya ya wanyama nchini.






Maoni
Chapisha Maoni