Na Mbaraka Kambona, Singida. Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ipo katika mchakato wa kukamilisha Mpango kabambe wa miaka 15 ijayo kuanzia 2021 utakaosimamia sekta ya Uvuvi na kutoa dira ya kulinda rasilimali za uvuvi ili sekta hiyo iweze kutoa mchango mkubwa na endelevu katika pato la taifa. Hilo limefahamika wakati Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah akifungua Mkutano wa Wadau wa Sekta ya Uvuvi wa kupitia, kujadili na kuidhinisha masuala ya kipaumbele yanayopaswa kuingizwa katika Mpango huo Kabambe unaofanyika Mkoani Singida Novemba 26-28, 2020. Dkt. Tamatamah alisema kuwa lengo la Serikali ni kuona sekta ya Uvuvi inaendelea kutoa mchango mkubwa katika pato la taifa zaidi ya ilivyosasa na ndio maana inaanda Mpango huo ili usimamizi wa rasilimali za uvuvi uwe imara. “Ni mategemeo yetu kuwa mpango huu utatoa hamasa kwa sekta ya uvuvi katika kulinda usalama wa chakula kuanzia ngazi ya kaya na taifa, vi...