Nav bar

Jumamosi, 28 Novemba 2020

WAFUGAJI WASHAURIWA KUWEKEZA KATIKA KILIMO CHA MALISHO.

WAFUGAJI WASHAURIWA KUWEKEZA KATIKA KILIMO CHA MALISHO

 

Wafugaji wa Ng’ombe wameshauriwa kujikita katika kilimo cha Malisho ili wawe na uhakika wa malisho bora kwa ajili ya mifugo yao na kuachana na uchungaji wa kutafuta malisho.

 

Mtendaji Mkuu wa Shamba la Ndoto, Hartmut Rottcher aliyasema hayo kwa Wakurugenzi na Mameneja wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi waliotembelea shamba la mfano la Ndoto lililopo Mkoani Iringa Novemba 27, 2020.

 

Rottcher alisema kilimo cha malisho yaliyo bora kinasaidia kuwapatia mifugo uhakika wa chakula bora huku akieleza kuwa mifugo ni muhimu kupewa pumba kwa kiasi na sio kuzidisha kwani kufanya hivyo hupelekea ng’ombe kupata asidi tumboni na kuuwa bakteria ambao husaidia kukata kata majani tumboni kwa mnyama.

 

Alisema kuwa yeye anafanya kilimo cha malisho kwa kumwagilia na ametenga maeneo katika mashamba yake illi kusaidia kulisha mifugo kwa mzunguko na kuipatia mifugo  mahitaji  wanayotaka na sio kuletewa chakula kwenye maboma yao.

 

“Njia ya kulisha kwa mzunguko husaidia kupata muda wa kuondoa magugu na kufanya shamba kuwa safi na malisho kustawi vizuri kwa wakati na linakuwa na rutuba ya kutosha,” alisema Rottcher

 

“Kulisha chakula cha kutosha na cha aina tofauti husaidia mnyama kupata virutubisho vingi vinavyosaidia kujenga afya ya mifugo,” Aliongeza Rottcher

 

Aidha, aliwashauri Wakurugenzi na Mameneja wa mashamba ya Serikali kutoa mifugo kwenda kujitafutia chakula na sio kuwaletea katika maboma yao kwani kwa kufanya hivyo kutasaidia mifugo kupata kile wanachotaka na sio kuwapimia chakula jambo ambalo litawezesha kupata mifugo iliyo bora yenye nyama nyingi na maziwa ya kutosha yenye viwango.

 

Akieleza kuhusu ziara yao katika Shamba hilo, Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Ugani Dkt. Kejeri Gillah alisema lengo ni kujifunza na kubadilishana uzoefu katika kuboresha kosaafu na utunzaji wa mifugo, ustawishaji wa malisho bora kwa mifugo ya aina mbalimbali na namna ya uhifadhi wa malisho kwa matumizi ya kipindi cha kiangazi.

 

“Ni mategemeo yetu kwamba safari hii itakuwa ya mafanikio makubwa sana kwetu na tutaweza kuboresha mifugo yetu na kustawisha malisho ya mifugo kama tutafuata yale yote tutakayoelekezawa” alisema Dkt. Gillah

 

Ziara hiyo iliratibiwa na Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani, ikiongozwa na Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Ugani, Dkt. Kejeri Gillah, wengine walishiriki katika ziara hiyo ni Mameneja kutoka Shamba la kitulo, Sao hill, Langwira, Vikuge, Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo (TALIRI) Uyole na meneja wa Ranchi ya Kalambo.






Afisa Utafiti Mifugo Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Felista Kimario akitoa neno la shukrani kwa Mtendaji Mkuu wa shamba la Ndoto, Bw. Hartmut Rottcher (hayupo pichani) kwa kutumia muda wake kuwatembeza kwenye shamba hilo na kuwaelimisha mambo mbalimbali katika upandaji wa malisho, namna ya kutunza na kulisha Mifugo. (27.11.2020)

Mtendaji Mkuu wa shamba la Ndoto, Bw. Hartmut Rottcher (wa pili kutoka kulia) akiwatembeza watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi waliofika shambani hapo  kujionea na kujifunza namna ya ustawishaji wa malisho, uboreshaji wa kosaafu na utunzaji Mifugo. (27.11.2020)

Kaimu Mkurugenzi kutoka Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Uyole Mbeya, Dkt. Edwin Peter Chang'a (katikati) akiuliza swali kwa Mtendaji Mkuu wa shamba la Miombo, Bw. Rex Fey (wa pili kushoto) wakati wa safari yao ya Mafunzo Mkoani Iringa. (27.11.2020)

Mtendaji Mkuu wa shamba la Ndoto mkoani Iringa, Bw. Hartmut Rottcher akiwaeleza watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi aina ya nyasi za malisho zilizopo shambani hapo na namna anavyofanya kilimo cha malisho ya Mifugo. (27.11.2020)

Watumishi kutoka katika mashamba mbalimbali ya Mifugo yaliyopo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa shamba la Miombo, Bw. Rey Fey (kushoto) wakati akizungumzia kuhusu mbegu, malisho na namna bora ya kulisha Mifugo kwenye shamba la Ndoto lililopo mkoani Iringa. (27.11.2020)

Kaimu Mkurugenzi Ugani Mifugo kutoka WMUV, Dkt. Kejeri Gillah akieleza lengo la safari yao ya Mafunzo wakati walipotembelea shamba la Ndoto mkoani Iringa, kuwa ni kubadilishana uzoefu katika uboreshaji wa kosaafu, utunzaji Mifugo, uhifadhi bora wa malisho, Udhibiti wa Magonjwa na matumizi ya madawa. (27.11.2020)

Kaimu Mkurugenzi Ugani Mifugo kutoka WMUV, Dkt. Kejeri Gillah akieleza lengo la safari yao ya Mafunzo wakati walipotembelea shamba la Ndoto mkoani Iringa, kuwa ni kubadilishana uzoefu katika uboreshaji wa kosaafu, utunzaji Mifugo, uhifadhi bora wa malisho, Udhibiti wa Magonjwa na matumizi ya madawa. (27.11.2020)







 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni