Nav bar

Jumamosi, 21 Novemba 2020

USHIRIKIANO WA BODI YA MAZIWA NA SEKTA BINAFSI KUONGEZA USINDIKAJI WA MAZIWA HAPA NCHINI

Bodi ya Maziwa yasisitiza ushirikiano na sekta binafsi katika kuongeza usindikaji wa maziwa nchini.

 

Hayo yamesemwa na Kaimu Msajili wa Bodi ya Maziwa, Bw. Noely Byamungu wakati wa kikao kazi cha kubainisha maeneo ya ushirikishwaji na Sekta Binafsi kilichofanyika jana (20.11.2020) jijini Dar es Salaam.

 

Kikao kazi hicho kililenga kupitia Mpango Mkakati wa miaka mitano 2020/21-2025/26 wa Bodi ya Maziwa na kubainisha namna ya bora ya ushirikishwaji wa sekta binafsi katika utekelezaji wa majukumu ya Bodi.

 

Kikao hicho kilihudhuriwa na Wakurugenzi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda na Makampuni ya Wasindikaji Maziwa ya UHT nchini kutoka kampuni ya Asas Dairies, Tanga Fresh, Milkcom na Azam Dairies, Wabia wa maendeleo kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) na Mradi wa Wasindikaji wa Maziwa Tanzania (TMPP).

 

Bw. Byamungu alisema kuwa lengo la Bodi ya Maziwa ni kuwezesha viwanda kuongeza uwezo wa kusindika maziwa ambao kwa sasa usindikaji wa maziwa katika viwanda hivyo ni asilimia 23.52.

 

Aidha, Msajili amesema kuwa Bodi ya Maziwa ipo tayari kuunga mkono jitihada za wadau wa Tasnia ya Maziwa kufikia malengo yao ya kuzalisha maziwa kwa kiwango kilichosimikwa.

 

Bw. Byamungu alisema kuwa kikao hicho kitaleta mtazamo wa muda mrefu wa Tasnia ya maziwa katika usindikaji na kutoa ramani ya kuongezeka kwa ushirikishwaji wa wadau, mawasiliano na ushirikiano miongoni mwa sekta binafsi, wabia wa maendeleo na wadau wengine kwenye sekta.

 

"Bodi ya Maziwa iko tayari na ina nia njema ya kufanya kazi pamoja nanyi kufikia malengo ya kuwa sekta endelevu katika uzalishaji, usindikaji na masoko ya maziwa na bidhaa zake nchini" Alisema Bw. Byamungu.

 

Nae Mkurugenzi wa Mradi wa Wasindikaji Tanzania, Bw. Mark Tsoxo amesema wapo tayari kuisaidia Bodi ya Maziwa kutekeleza majukumu yake ya kuongeza usindikaji wa maziwa nchini ili kuimarisha mnyororo mzima wa thamani. Pia ameiomba Bodi ya Maziwa kuendelea kushirikiana na Sekta Binafsi kwa Ukaribu ili kufikia azma iyo.

 

Tasnia ya Maziwa ina mchango mkubwa katika kuhakikisha usalama wa chakula na kupunguza umaskini.

Washiriki wa kikao cha "Stakeholder Engagement Towards Sustainable Dairy Industry in Tanzania" wakiwa kwenye picha ya pamoja katika kikao kilichofanyika jijini Dar es Salaam. (20.11.2020)

Kaimu Msajili wa Bodi ya Maziwa, Bw. Noel Byamungu (wa kwanza kushoto) akisikiliza kwa makini mada zinazowasilishwa na mdau (hayupo pichani) wakati wa kikao kazi cha kuimarisha mahusiano kati ya Sekta Binafsi na Serikali kilichofanyika jijini Dar. Es Salaam. Kulia ni mwakilishi kutoka Azam Dairies, Bw. Yunus Ibrahim. (20.11.2020)

Mhandisi kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara, Bw. Emmanuel Zakayo (kushoto) akifuatiwa na Mchumi Mkuu kutoka Wizara ya Viwanda, Bi. Genoveva Kilabuko na Mchumi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Francis Makusaro wakati wa kikao kazi cha kuimarisha mahusiano kati ya Sekta Binafsi na Serikali kilichofanyika jijini Dar. Es Salaam. (20.11.2020)

Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo na Usalama wa Chakula na Lishe (WMUV), Bw. Gabriel Bura akisikiliza kwa makini mada zinazowasilishwa wakati wa kikao kazi cha kuimarisha mahusiano kati ya Sekta Binafsi na Serikali kilichofanyika jijini Dar es Salaam. (20.11.2020)

Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Tanga Fresh, Bw. Innocent Mushi akisikiliza mada zinazowasilishwa wakati wa kikao cha kuimarisha mahusiano kati ya Sekta Binafsi na Serikali kilichofanyika jijini Dar. Es Salaam. (20.11.2020)

Baadhi ya Wasindikaji wa Maziwa wakiwa kwenye kikao cha kuimarisha mahusiano kati ya Sekta Binafsi na Serikali kilichofanyika jijini Dar es Salaam. Wa kwanza kushoto ni Mwakilishi kutoka Milkcom Dairies, Bw. Abubakar Faraji, akifuatiwa na Abdul Ally kutoka ASAS Dairies na wa kwanza kulia ni Mkurugenzi mtendaji kutoka Tangafresh, Innocent Mushi. (20.11.2020)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni