Nav bar

Jumamosi, 28 Novemba 2020

PROF. OLE GABRIEL AWAFUNDA WASOMI HOMBOLO

Na Mbaraka Kambona,

 

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel amewaeleza wanafunzi wa Chuo cha Serikali za Mitaa- Hombolo kuwa wao ni Viongozi watarajiwa hivyo wanawajibu wa kuhakikisha watakapokuwa viongozi wanakidhi matarajio ya wale watakaokuja kuwaongoza.

 

Prof. Gabriel aliyasema hayo wakati akiwasilisha mada iliyohusu nafasi ya viongozi wa kuchaguliwa katika kuleta maendeleo kwa jamii anayoiongoza kwenye hafla ya kuwatunuku zawadi wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo yao na wafanyakazi bora wa chuo cha Hombolo iliyofanyika katika chuo hicho kilichopo Dodoma Novemba 25, 2020.

 

Alisema kuwa katika kipindi hiki ambacho nchi ya Tanzania imeingia katika uchumi wa kati viongozi wanawajibu mkubwa wa kuhakikisha kwamba wanakidhi matarajio ya Watanzania.

 

Prof. Gabriel aliongeza kuwa nchi nyingi na taasisi zimekuwa zikikwama kufikia malengo tarajiwa kwa sababu ya kukosa usimamizi mzuri.

 

“Kuwa na rasilimali ni jambo moja, lakini kusimamia rasilimali hizo ni jambo la muhimu zaidi, taasisi nyingi zimekwama kwa kushindwa kusimamia rasilimali zake ikiwemo rasilimali watu, rasilimali fedha na rasilimali miundombinu,” alisema Prof. Gabriel

 

Kwa mantiki hiyo aliupongeza Uongozi wa Chuo cha Hombolo kwa kusimamia agenda ya uongozi huku akisema kuwa elimu hiyo wanayoitoa kwa wanafunzi wa chuo hicho itawasaidia wanafunzi hapo mbeleni watakapokuwa viongozi.

 

Aliendelea kusema kuwa kiongozi yeyote wa kuchaguliwa au kuteuliwa ili awe kiongozi bora ni muhimu kuzingatia mambo matatu ambayo ni kufahamu hasa anaowaongoza wanamahitaji gani? pia Kiongozi atambue kuwa hatakumbukwa kwa cheo chake bali kwa mchango wake kwa jamii ile anayoiongoza na tatu, awe mtu anayewashirikisha wale anaowaongoza katika kutatua changamoto zao.

“Washirikishe wale unaowaongoza na ndipo utakapoweza kutatua changamoto, kiongozi mzuri ni yule anayeziona changamoto na kuzibadilisha kuwa fursa, na kwa kufanya hivyo ndipo utaweza kukidhi matarajio ya wale unaowaongoza,”alisisitiza Prof. Gabriel

 

Katika hafla hiyo ya kumi na mbili (12) ya chuo hicho, Prof. Elisante Ole Gabriel alikuwa Mtoa mada maalum na aliwasilisha mada hiyo ya nafasi ya viongozi wa kuchaguliwa na wakuteuliwa katika kuleta maendeleo kwa jamii ili kuwakumbusha wajibu wao mkubwa kwa jamii.

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi(Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia), akifurahia jambo alipokuwa akisalimiana na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), anayeshughulikia Elimu, Gerald Mweli (kushoto)  walipokutana kwenye Hafla ya Kutunukiwa zawadi wafanyakazi na wanafunzi wa Chuo cha Serikali za Mitaa- Hombolo waliofanya vizuri katika masomo.  Prof. Elisante Ole Gabriel alikuwa Mtoa mada maalum katika hafla hiyo iliyofanyika katika chuo hicho kilichopo Dodoma. (25.11.2020)

Sehemu ya Wanafunzi na Wafanyakazi wa Chuo cha Serikali za Mitaa - Hombolo waliohudhuria hafla ya kutunukiwa zawadi wafanyakazi na wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo iliyofanyika katika chuo hicho kilichopo Dodoma. (25.11.2020)

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi(Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akiwasalimia Wanafunzi na Wafanyakazi wa Chuo cha Serikali za Mitaa- Hombolo (hawapo pichani) alipokuwa akitambulishwa katika hafla ya kutunukiwa zawadi wafanyakazi na wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo iliyofanyika katika chuo hicho kilichopo Dodoma. (25.11.2020)

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akiwasilisha mada katika hafla ya kutunukiwa zawadi Wafanyakazi na Wanafunzi waliofanya vizuri wa Chuo cha Serikali za Mitaa-Hombolo iliyofanyika katika chuo hicho kilichopo Dodoma. (25.11.2020)





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni