NG’OMBE waliotaifishwa na serikali katika
wilaya ya Mwanga, mkoani Kilimanjaro, wanatarajiwa kupigwa mnada kufuatia uamuzi
wa mahakama.
Hayo
yameelezwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina, wakati alipokwenda
kukagua lindo la ng’ombe hao, jana eneo la Mgagao, wilayani Mwanga,
walikohifadhiwa.
“Kufuatia
uamuzi wa mahakama, ng’ombe hawa watauzwa kwa njia ya mnada siku ya Ijumaa,
Oktoba 20, mwaka huu, kutokana na hali za ng’ombe hawa kutokuwa nzuri”,
alisema.
Aliongeza,
“Tayari mahakama imeridhia ombi la serikali la kutaka kuuzwa kwa ng’ombe hawa na
ishamteua dalali wa kufanya mnada huo ambaye ni Marepelanto wa mjini Moshi na
kazi hii itafanywa haraka kutokana na ng’ombe wengine kuanza kufa, kama
mlivyosikia tayari sita wameshakufa”.
Aidha
alisema serikali itaanza operesheni maalum ya kuwakamata ng’ombe walioingizwa
nchini kinyume cha sehria kuanzia Jumatatu ijayo.
“Baada
ya operesheni ya hapa Kilimanjaro, nilitoa siku saba kwa Mikoa mingine kuiondoa
mifugo iliyoingizwa nchini kinyume cha sheria kupitia Mikoa hiyo, muda huo
umekwisha, Jumatatu tunaanza oparesheni nyingine itakayochukua siku 15 ili kuhakikisha
mifugo hiyo inaondolewa yote”, alisema.
Akijibu
maswali kutoka kwa baadhi ya viongozi wa eneo hilo, Bw. Mpina alisema kuwa
iwapo kuna mifugo ya wenyeji ilikamatwa wakati wa operesheni hiyo wapeleke
orodha ya ng’ombe hao kwa kupitia ngazi husika ili waweze kurudishiwa.
“Wenyeji
wenye ng’ombe waliokamatwa watumie taratibu zilizopo kwa kuanzia kwa
viongozi wa maeneo wanayotoka hadi ngazi ya kamati ya ulinzi na usalama ya
wilaya ikithibitishwa bila mashaka yoyote kuwa mifugo hiyo ni ya kwao zitatumika taratibu
zinazohitajika kisheria kwa kuwa ng’ombe hawa sasa ni mali ya serikali”,
alisema.
Aidha
alitoa onyo kwa viongozi hao kuhakikisha wanafanya zoezi hilo kwa weledi na
kwamba iwapo watafanya udanganyifu hatua kali za kisheria zitachuliwa dhidi yao
bila kujali nyadhifa zao.
Kwa
upande wake Katibu Mkuu wa wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Maria Mashingo,
aliyeiongoza operesheni hiyo, alisema kuwa mwendelezo wa operesheni hiyo imepelekea serikali kukamata ng’ome wengine takribani 2,000.
“Tunawashukuru
Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA) kwa kutupatia ndege ambayo ilitusaidia
sana katika zoezi hili tulilofanya kupitia vyombo vya ardhini na angani”,
alisema.
Alisema
kuwa amebaini kuwa wizara ya Mifugo na Uvuvi ina changamoto ya uhitaji wa
vifaa kama ndege kwani operesheni hiyo imebainisha wazi uhitaji huo.
Awali
akitoa rai yake kwa niaba ya wafugaji wenyeji ambao ng’ombe zao zimekamatwa
kufuatia operesheni hiyo, Diwani wa Kata ya Kirya, Bw. Nyange Laizer aliiomba
serikali kuangalia uwezekano wa ng’ombe hizo kurudishiwa wenyewe.
“Unajua
sisi malisho yetu tunafanya hapa hapa na ndiyo maana operesheni hii ikawakumba
na watu wetu na hii ni kutokana na ukweli kuwa huwezi kutofautisha ng’ombe za
hapa kwetu na zile zinazoingizwa kinyume cha sheria”, alisema.
Uamuzi
huu wa mahakama unakuja baada ya ng’ombe hao kutaifishwa na serikali hivi
karibuni baada ya kuingizwa hapa nchini kinyume cha sheria.
Ng’ombe walioamriwa na mahakama kupigwa mnada,
mnada utafanyika siku ya ijumaa Octoba 2017.
|
Duh!Sheria inauma kweli.
JibuFuta