Nav bar

Alhamisi, 17 Novemba 2022

MAAFISA UGANI WATAKIWA KUTUMIA MIFUMO YA TEHAMA

Na. Elieda Euzebius


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amewataka Maafisa Ugani wote nchini kuhakikisha wanajisajili katika mfumo ya M- Kilimo ili waweze kuwafikia wafugaji wengi zaidi na kutatua changamoto mbalimbali wanazo kumbana nazo.


Mhe. Ndaki aliyasema hayo wakati akifungua Mafunzo Rejea kwa Maafisa Ugani wa Kata na Vijiji kwa Mikoa ya kanda ya kati ya Dodoma na Singida yaliyofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya chamwino, Dodoma Novemba 14, 2022.


 Alisema kuwa mpaka sasa jumla ya Maafisa Ugani 3,018 kati ya 3,201 ndiyo wamesajiliwa katika Mfumo wa M- Kilimo huku akiwahimiza maafisa ugani ambao bado hawajajisajili wafanye hivyo haraka.


 “Vilevile, niwahimize kuwahamasisha wafugaji katika maeneo yenu kuweza kujisajili katika Mfumo wa M-Kilimo ili tuweze kufikia lengo la kusajili wafugaji 1,000,000 nchini ifikapo Juni, 2023”, alisema Mhe. Ndaki


Halikadhalika, Waziri Ndaki alisema kuwa Wizara imeanza matumizi ya mifumo ya TEHAMA (Ugani Kiganjani) kwa lengo la kuwafikia wafugaji wengi na kutoa mrejesho wa kila kazi ambayo Afisa Ugani atakuwa ametekeleza katika eneo lake. 


Aliongeza kwa kusema katika kutatua changamoto ya ukosefu wa vitendea kazi vya kutolea huduma za Ugani, Wizara imepanga kununua pikipiki 1,200 na magari 13 ambayo yatagawiwa katika Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa.


Naye, Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Mifugo) Bw. Tixon Nzunda alisema Serikali imejipanga kufanya mabadiliko katika sekta ya mifugo na kuainisha maeneo kadhaa kama dira ya utekelezaji wa mabadiliko hayo.Baadhi ya vipaumbele alivyovitaja ni pamoja na kuboresha upatikanaji wa uhakika wa malisho na maji, ufugaji wenye tija, kuanzisha mashamba darasa ya malisho, kubadilisha Ranchi za Taifa pamoja na kuimarisha masoko na minada.


Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Gift Msuya aliiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuongeza Wataalam wa mifugo na vitendea kazi vya kutosha kulingana na mifugo iliyomo wilayani Chamwino kwani Wilaya hiyo Asilimia 60 ya pato lake linatokana na shughuli za sekta ya mifugo.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akiongea na washiriki wa Mafunzo Rejea kwa Maafisa Ugani wa Kata na Vijiji kwa Mikoa ya Kanda ya Kati ya Dodoma na Singida wakati akifungua Mafunzo hayo yanayofanyika Wilayani Chamwino, jijini Dodoma Novemba 14, 2022.


Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Tixon Nzunda akitoa neno la utangulizi  kabla ya ufunguzi wa  Mafunzo Rejea kwa Maafisa Ugani wa Kata na Vijiji kwa Mikoa ya Kanda ya Kati ya Dodoma na Singida  Mafunzo hayo yanayofanyika Wilayani Chamwino, jijini Dodoma Novemba 14, 2022.


Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu(Mifugo), Dkt. Charles Mhina akiongea na washiriki wa Mafunzo Rejea kwa Maafisa Ugani wa Kata na Vijiji kwa Mikoa ya Kanda ya Kati ya Dodoma na Singida yanayofanyika Wilayani Chamwino, jijini Dodoma Novemba 14, 2022.


Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na  Huduma za Ugani, Dkt. Angello Mwilawa akieleza lengo la  Mafunzo Rejea kwa Maafisa Ugani wa Kata na Vijiji kwa Mikoa ya Kanda ya Kati ya Dodoma na Singida wakati wa Mafunzo hayo yanayofanyika Wilayani Chamwino, jijini Dodoma Novemba 14, 2022.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki(katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa Mafunzo Rejea kwa Maafisa Ugani wa Kata na Vijiji kwa Mikoa ya Kanda ya Kati ya Dodoma na Singida yanayofanyika Wilayani Chamwino, jijini Dodoma Novemba 14, 2022. Wa pili kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Gift Msuya. Wa pili kushoto ni Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Tixon Nzunda.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akiagana na Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Gift Msuya(kulia) muda mfupi baada ya kufungua Mafunzo Rejea kwa Maafisa Ugani wa Kata na Vijiji kwa Mikoa ya Kanda ya Kati ya Dodoma na Singida yanayofanyika Wilayani Chamwino, jijini Dodoma Novemba 14, 2022.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni