Nav bar

Alhamisi, 22 Septemba 2022

NZUNDA AWATAKA WASIMAMIZI WA VITUO ATAMIZI KUWA WABUNIFU

Katibu Mkuu anayesimamia Sekta ya Mifugo, Bw. Tixon Nzunda amewataka wasimamizi wa Vituo Atamizi vya Ufugaji Mifugo Kibiashara kwa Vijana kuwa wabunifu na kuhakikisha wanasimami utekelezaji wa mwongozo uliotolewa kuhusu vituo hivyo.

 

Nzunda ameyasema hayo leo (21.09.2022) wakati akifunga mafunzo ya siku mbili ya wasimamizi wa vituo atamizi vya ufugaji mifugo kibiashara kwa vijana yaliyofanyika kwenye Chuo cha Mafunzo ya Mifugo Kampasi ya Morogoro.

 

Wasimamizi hao wa vituo wametakiwa kuwa wabunifu hasa katika kukabiliana na changamoto watakazo kutana nazo, huku wakitakiwa kuwajenga vijana hao uwezo wa kuweza kufuga kisasa kwa vitendo, kuwa na mahusiano na mawasiliano mazuri ambayo yatawasaidia katika masoko ya mifugo pamoja na mazao ya mifugo watakayokuwa wanazalisha.

 

Lakini pia amewataka wasimamizi hao kuwapatia vijana elimu ya utunzaji wa malisho na upandaji wa malisho mapya ili hata watakapotoka katika vituo hivyo waweze kwenda kuanzisha mashamba ya malisho kwa ajili ya mifugo yao.

 

Nzunda amesema serikali kwa sasa imeamua kufungua milango kwa vijana kupitia Sekta ya Mifugo ambapo vituo hivyo vitasaidia kuwabadilisha vijana kifikra kuhusu ufugaji, kupunguza tatizo la ajira, na kuongeza uzalishaji wa mifugo na mazao yake kwa kuzingatia viwango na kuongeza kipato cha vijana na taifa kwa ujumla.

 

Serikali katika kuhakikisha vituo hivi vinaanza kazi kwa mwaka wa fedha 2022/2023 imatenga kiasi cha shilingi bilioni 4 kwa ajili ya kuwawezesha vijana kuanza kupata mafunzo ya ufugaji wa kisasa kwenye vituo 8 vilivyopo LITA na TALIRI ambapo usahili wa vijana hao tayari ulishakamilika.

 

“Vijana hawa wanakwenda kupatiwa ujuzi kuhusu maisha, ujuzi kuhusu uzalishaji wa kazi, ujuzi wa uzalishaji fedha, ujuzi wa kupata mitaji, na ujuzi wa kwenda kujenga uchumi wa nchi kupitia Sekta ya Mifugo,” alisema Katibu Mkuu Nzunda

 

Vijana waliochaguliwa kujiunga na vituo atamizi wametakiwa kuwa na moyo wa kujituma na kujitambua kwamba wao ni wawekezaji ambao wameingia kuwekeza kwenye Sekta ya Mifugo.

 

Nzunda ameitaka LITA na TALIRI kuhakikisha kazi hii inaanza kutekelezwa Septemba 26, 2022 na kwamba fedha zilizotolewa kwa kazi hii zisitumike kwa ajili ya kuendeshea ofisi wala kazi nyingine yoyote nje ya kazi iliyokusudiwa na serikali.

 

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA), Dkt. Pius Mwambene amesema kuwa LITA inakwenda kuanzisha vituo 6 katika kampasi za Kikulula (Kagera), Mabuki (Mwanza) na Buhuri (Tanga) ambapo kila kituo kitachukua vijana 30 ambao watafundishwa namna ya kufuga kibiashara kwa muda wa miezi 12.

 

Dkt. Moses Olenesele, Mtumishi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) amewasihi vijana waliopata nafasi ya kujiunga na mafunzo hayo kuhakikisha wanaitumia fursa hiyo vizuri kwa kuwa serikali imeweka matumaini kwa vijana hao kuja kuwa wafanyabiashara wakubwa wa mifugo iliyo bora.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Tixon Nzunda akifunga mafunzo ya wasimamizi wa Vituo Atamizi vya Ufugaji Mifugo Kibiashara kwa Vijana yaliyofanyika kwenye Chuo cha Mafunzo ya Mifugo Kampasi ya Morogoro ambapo amewataka wasimamizi hao kuhakikisha wanakwenda kusimamia utekelezaji wa mwongozo na kuwa wabunifu katika kuhakikisha malengo ya serikali ya kuwa na vijana wenye uwezo wa kufuga mifugo kisasa na kwa tija yanatimia. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA), Dkt. Pius Mwambene na kushoto ni Dkt. Moses Olenesele, Mtumishi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO). (21.09.2022)


Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA), Dkt. Pius Mwambene (kulia) akichangia mada wakati wa mafunzo ya wasimamizi wa Vituo Atamizi vya Ufugaji Mifugo Kibiashara kwa Vijana yaliyofanyika kwenye Chuo cha Mafunzo ya Mifugo Kampasi ya Morogoro. Dkt. Mwambene amesema kuwa LITA kupitia kampasi zake imejipanga kuhakikisha malengo ya serikali yanatimizwa. (21.09.2022)


Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya wasimamizi wa Vituo Atamizi vya Ufugaji Mifugo Kibiashara kwa Vijana yaliyofanyika kwenye Chuo cha Mafunzo ya Mifugo Kampasi ya Morogoro wakifuatilia mada zilizokuwa zinawasilishwa wakati wa mafunzo hayo. (21.09.2022)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Tixon Nzunda akisikiliza maelezo kutoka kwa Meneja wa Shamba katika Chama cha Ushirika cha Wahitimu wa Chuo Kikuu cha Sokoine (SUGECO), Marcelina Lubuva (kushoto) wakati alipokuwa akikagua shamba la alizeti kwenye kituo chao. (21.09.2022)

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Tixon Nzunda akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Chama cha Ushirika cha Wahitimu wa Chuo Kikuu cha Sokoine (SUGECO), Joseph Massimba (wa pili kutoka kulia) wakati alipokuwa akikagua shughuli wanazozifanya katika kituo chao ambapo amewasihi kuanza kujikita kwenye ufugaji kwa kuwa zipo fursa nyingi kupitia Sekta ya Mifugo. (21.09.2022)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni