UVUVI HARAMU KUTAFUTIWA MWAROBAINI
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Ng'wasi Damas Kamani amewataka watendaji wa Wizara kuja na mwarobaini ambapo utakuwa ni tiba katika kudhibiti uvuvi haramu, na amewataka watendaji hao kuangalia mifumo yao kama inafanya kazi vizuri na kuboresha pale ambapo panahitaji kuboreshwa ili uvuvi haramu ufike kikomo.
Mhe. Kamani ameyasema hayo leo, Septemba 14, 2026, jijini Mwanza, wakati wa kupokea wasilisho la andiko dhana la kudhibiti Uvuvi haramu, andiko ambao litasaidia katika kutokomeza tatizo hilo sugu, andiko ambalo limeandaliwa na Mkufunzi wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) Mwanza, Bw. Jackson Bulili pamoja na Mtaalam wa mambo ya Teknolojia kutoka Kampuni ya Affordable Computes and Technology for Tanzania (ACTT) Mwanza, Bw. Amos Zacharia.
"Uandishi wa andiko hili linaonesha fika kuwa Wizara inaungwa mkono na wananchi katika kutokomeza Uvuvi haramu" amesema Mhe. Kamani
Aidha, Mhe. Kamani amesema hii inaonesha Wizara itapata namna nyingine ya kupambana na uvuvi haramu, na kupitia maoni ya wadau Wizara itaendelea kuboresha Mifugo ili kuja na Mfumo bora zaidi ambayo itasaidia kutokomeza tatizo hilo na Wizara itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kutatua changamoto hiyo, na amewataka wadau kuja na maandiko ambayo yataleta tija katika Sekta.
Vilevile, Mhe. Kamani amewapongeza wadau hao kwa kuandika andiko ambalo litasaidia kudhibiti uvuvi haramu na kuwataka wadau mbalimbali wa Sekta ya Uvuvi kusaidi kutafuta mbinu mbadala na hatimaye kutokomeza shughuli hizo.
Pia, Mhe. Kamani amebainisha kuwa utatuzi wa changamoto lazima uanzie kwenye utafiti na baadae kuandika maandiko ambayo yanaleta tija nchini, na ameitaka Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) kukaa na wadau wa Sekta ya Uvuvi ili kuona ni namna gani changamoto hizo zitatatuliwa.





Maoni
Chapisha Maoni