Nav bar

Ijumaa, 6 Agosti 2021

SERIKALI YAOMBWA KUSITISHA UCHINJAJI WA PUNDA SHINYANGA.

Serikali imeombwa kusitisha uchinjaji na uuzaji wa ngozi na malighafi zitokanazo na punda katika machinjio ya Shinyanga na kuwachukulia hatua watu wote waliobainika kukiuka haki za wanyama.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Shirika la Ulinzi na Utetezi wa haki na Ustawi wa Wanyama Arusha (ASPA) Bw. Livingstone Masija leo Agosti 6, 2021 Jijini Dodoma mbele ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel baada ya ukaguzi uliofanyika juni 20 mwaka huu na kubaini ukiukwaji mkubwa wa haki za mnyama punda kwa kuwafanyiwa mateso makubwa.

Alisema, miongoni wa vitendo vinavyofanyika ni pamoja na kuwakosesha malisho kwa muda mrefu, kuchinja punda walio na mimba, kuchinja punda wakati wengine wanawaangalia na kuwapiga na vitu vizito kichwani pindi mashine zimeharibika na kukaa na majeraha bila ya kutibiwa.

“kwa sababu watu wako pale wameaminiwa na Serikali lakini namna ya utekelezaji wao wa majukumu ni shida, wameambiwa wasimamie punda wachinjwe 20 kwa siku  lakini wao wako pale sijajua wanakuwa hawaoni au hawako kazini basi unakuta punda wanachinjwa zaidi ya walioambiwa wasimamie, tunaomba pia wachukuliwa hatua za kinidhamu” alisema Masija

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel alisema kuwa serikali imepokea wasilisho hilo na italifanyia kazi haraka iwezekanavyo kwa mujibu wa sheria kwa sababu lengo la Wizara ni kuona kuwa wanyama kazi wanaendelea kulindwa.

Alisema mpaka juni 30, 2020 idadi ya punda ilikuwa  ni 657,380 kwa hiyo endapo wangefata utaratibu wa kuchinja punda 20 kwa siku kama maelekezo ya Serikali yalivyo Punda hao  wangeishi kwa miaka 50 kama wazaliaji. 

“nimesema tuna taratibu zetu sasa za kisheria ambazo ndani ya Wizara  tutazitumia ili kuhakikisha tunasonga mbele nanyi mtaendelea kupewa taarifa kupitia Ofisi ya Mkurugenzi wa  huduma za Mifugo kwamba nini kinaendelea”. Alisema.

Aliongeza kuwa lengo la serikali si kufanya punda waishe bali kuongezeka lakini pia swala la punda kutoka nje ya nchi ni jambo lingine ambalo ni kosa kisheria kwa sababu serikali inapoteza mapato, kwa hiyo suala hilo litaangaliwa kwa umakini.

Naye Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania, Dkt. Bedan Masuruli amemshukuru Katibu Mkuu kwa kutenga muda wake na kuja kuwasikiliza wadau wa ustawi wa wanyama na wamekusikia vizuri na kwamba Wizara imelichukua.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akiongea na wadau (hawapo pichani) kwenye kikao cha mapendekezo ya usitishaji wa shughuli za uchinjaji punda uuzaji wa ngozi na malighafi nyinginezo zinazotokana na punda leo Agosti 6, 2021 Jijini Dodoma.* 

 


Mkurugenzi wa Shirika la Ulinzi na Utetezi wa Haki na Ustawi wa Wanyama Arusha (ASPA), Bw. Livingstone Masija akionyesha nyundo kama moja ya dhana inayotumiwa katika kupiga punda kichwani pale mashine zinapoharibika ambacho ni ukiukwaji wa haki za wanyama kwenye ukumbi wa Ofisi za Tume ya vyama vya ushirika makao makuu Jijini Dodoma leo Agosti 6, 2021.*
 


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto), akiangalia video pamoja na wadau  ya namna haki za punda zinavyokiukwa kwenye kampuni ya Fang Huo Investment Co. Ltd leo Agosti 6, 2021  Jijini Dodoma. 


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (Waliokaa katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wawakilishi kutoka Shirika la Ulinzi na Utetezi wa Haki na Ustawi wa Wanyama Arusha (ASPA) pamoja na watumishi wa Wizara hiyo mara baada ya kikao cha mapendekezo ya usitishaji wa shughuli za uchinjaji punda, uuzaji wa ngozi na malighafi nyinginezo zinazotokana na punda katika machinjio ya Shinyanga leo Agosti 6, 2021 Jijini Dodoma.* 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni