SERIKALI KUONGEZA UWEKEZAJI KATIKA MIUNDOMBINU YA ELIMU NA MAFUNZO YA AMALI
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuwekeza katika uboreshaji wa miundombinu ya elimu na mafunzo ya ufundi ustadi ili kuendelea kujenga taifa la kujitegemea kupitia elimu ya amali.
Amesema hayo Wakati wa ziara yake mkoani Mara leo Agosti 12, 2026 baada Kukagua na kuweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Amali na Ufundi Musuguri iliyopo Wilayani Butiama inayogharimu shilingi bilioni 1.6.
" Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika uboreshaji wa miundombinu ya elimu na mafunzo ya amali ili kutengeneza taifa linaloweza kujitegemea kupitia vijana kama alivyoasisi Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, hivyo ujenzi wa shule za amali kama hii ya Musuguri utatusaidia kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira nchini" alisema Dkt. Bashiru.
Akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Butiama amewataka wananchi hao kuwa wa mfano katika kuilinda na kuitetea misingi iliyoachwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ikiwa ni pamoja kuendeleza elimu ya mafunzo na kujitegemea.
Aidha, katika hatua nyingine, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru ametoa rai kwa wananchi, wanasiasa, watendaji wa umma pamoja na sekta binafsi kumuenzi Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa kutekeleza kwa vitendo Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akiwa Wilayani Butiama Mhe. Balozi Dkt. Bashiru amezindua Nyumba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Butiama.
Baada ya kukagua, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi ya Wilaya ya Butiama, msafara wake unaekelea Wilayani Bunda kwa ajili ya kukagua na kuzindua miradi pamoja kuongea na wananchi.





Maoni
Chapisha Maoni