MHE. MACHA AWATAKA VIJANA KUTUMIA MIKOPO KWA USAHIHI ILI KUJENGA UCHUMI IMARA
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringa Macha, leo Agosti 5, 2026, amefungua mafunzo ya Programu ya Uwezeshaji Vijana Kiuchumi na kuwataka vijana walionufaika na mikopo ya Serikali kuitumia kwa malengo yaliyokusudiwa ili iwe chachu ya kujikwamua kiuchumi na kuchochea maendeleo ya Taifa.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Macha amesema kuwa mafanikio ya vijana katika miradi ya mifugo na uvuvi yanategemea utayari wao wa kujifunza, kufanya kazi kwa bidii na kuzingatia ushauri wa wataalamu. Amesema vijana wanapaswa kujifunza kutoka kwa wataalamu wa mifugo pamoja na wafugaji wenye uzoefu wa ufugaji wa kisasa ili wapate maarifa na mbinu bora zitakazowawezesha kuongeza uzalishaji na kuendesha miradi yao kwa ufanisi.
"Ninawasihi mtumie mikopo hii kwa malengo yaliyokusudiwa na mjifunze kutoka kwa wataalamu wa mifugo pamoja na wafugaji wenye uzoefu ili muweze kuendesha miradi yenu kwa ufanisi. Msiwe na haraka ya kutafuta mafanikio, kwani yanahitaji uvumilivu, nidhamu na usimamizi mzuri. Pia, hakikisheni mnarejesha mikopo kwa wakati ili vijana wengine nao wanufaike na fursa hii iliyotolewa na Serikali chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan," amesema Mhe. Macha.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Prisca Kayombo, amewataka vijana kuhakikisha mikopo waliyopewa inatumika kikamilifu katika shughuli zilizokusudiwa, huku akisisitiza umuhimu wa usimamizi mzuri wa miradi ili kufikia malengo ya Programu ya Uwezeshaji Vijana Kiuchumi.
Mafunzo hayo yanawawezesha wanufaika kupata ujuzi wa usimamizi wa miradi, matumizi sahihi ya mikopo pamoja na mbinu bora za uzalishaji katika sekta za mifugo na uvuvi. Mafunzo hayo yanatolewa na wataalamu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), yakilenga kuwawezesha vijana kujenga uchumi endelevu kupitia miradi yenye tija.





Maoni
Chapisha Maoni