JAMII YATAKIWA KUONGEZA JUHUDI MAPAMBANO DHIDI YA MABADILIKO YA TABIA YA NCHI.
Wananchi wametakiwa kuongeza juhudi katika kupambana na athari zinazotokana na mabadiliko ya hali ya nchi yanayoikumba nchi na dunia kwa ujumla.
Wito huo umetolewa leo Juni 1, 2026 na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhe. Kwagilwa Reuben (MB) wakati akifungua maadhimisho ya wiki ya mazingira katika Viwanja vya Jakaya Kikwete Convention Centre jijini Dodoma.
Mhe. Kwagilwa amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha mazingira yanatunzwa ili kuwezesha nchi kutimiza mipango ya Dira 2050 kwani athari za mabadiliko ya tabia ya nchi yana athari hasi kwenye uchumi wananchi na dunia.
“Mazingira ni Uchumi pia mazingira ni afya, tunatakiwa kuyatunza mazingira yetu ili malengo yetu ya Dira ya Taifa 2050 yanatimia. Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi tutaendelea kutekeleza wajibu wetu katika kulinda mazingira.” Amesisitiza Mhe.Kwagilwa.
Kwa upande wake mratibu wa maonesho hayo kutoka Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Bw. Maxmilian Zitatu amesema kuwa TALIRI inazalisha na kusambaza aina 5 za mbegu za malisho amabazo zinasaidia katika kuzuia mmomonyoko wa udongo, zinazostahimili ukamae na zinazoongeza rutuba kwenye udongo.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kikundi cha Furaha Women Group na Katibu Msaidizi wa Tanzania Women Fish Workers Association (TAWFA), Bi. Fatuma Katulla ambaye ni mdau wa Maabara ya Uvuvi amesema, maabara ina jukumu muhimu la kufanya uchunguzi wa mabaki ya kemikali na viuatilifu kwenye mazao ya uvuvi pamoja na kutoa elimu kuhusu matumizi salama ya kemikali ili kulinda afya ya binadamu na mazingira.




Maoni
Chapisha Maoni