BI. MEENA ATAKA UTAFITI KUWA CHACHU YA MAENDELEO YA SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agness Meena, amesema kuwa utafiti una nafasi kubwa katika kuleta mageuzi na maendeleo endelevu ya sekta za mifugo, uvuvi na ukuzaji viumbe maji nchini, hivyo ni muhimu kuhakikisha agenda za utafiti zinaendana na mahitaji ya sasa na ya baadaye ya Taifa.
Bi. Meena amesema hayo leo Juni 9, 2026, wakati akifungua Warsha ya Wadau ya Kupitia Ajenda za Taifa za Utafiti wa Mifugo pamoja na Uvuvi na Ukuzaji Viumbe Maji za mwaka 2026–2030 iliyofanyika katika Ukumbi wa Brand Hotel jijini Dodoma.
Amesema uwepo wa wadau mbalimbali kutoka taasisi za serikali, sekta binafsi, vyuo vikuu, taasisi za utafiti, mashirika ya maendeleo, mamlaka za serikali za mitaa na wadau wengine wa sekta hizo unaonesha dhamira ya pamoja ya kutambua mchango wa utafiti katika kukuza uchumi wa Taifa.
"Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea kuimarisha shughuli za utafiti kwa kuanzisha taasisi maalumu za utafiti ambazo ni Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) na Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI), zenye jukumu la kusimamia, kuratibu na kuendesha tafiti za kisayansi katika sekta hizo." Amesema Bi. Meena
Amesema vipaumbele vya utafiti katika sekta za mifugo na uvuvi vimelenga kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa mazao kupitia mbari bora za mifugo na samaki, kudhibiti magonjwa, kuongeza thamani ya mazao, kuimarisha matumizi endelevu ya rasilimali na kuongeza kipato cha wafugaji pamoja na wavuvi nchini.
Aidha, Bi. Meena amebainisha kuwa ajenda zilizokuwa zikitumika zilifikia mwisho wa utekelezaji mwaka 2025, hivyo kuna umuhimu wa kuzifanyia mapitio ili ziendane na mabadiliko ya kiteknolojia, kiuchumi na kimazingira yanayoendelea kutokea duniani.
Hata hivyo amezitaka timu za wataalamu kuhakikisha ajenda mpya zinazingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) na vipaumbele vya Serikali kwa lengo la kuondoa umaskini na kuongeza ajira kwa vijana na wanawake
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti Mafunzo na Ugani wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Samweli . Mdachi ameeleza mchakato wa kuandaa ajenda hizo ambazo zinalenga kuongoza utekelezaji wa tafiti zenye tija Kwa kipindi cha mwaka 2026 hadi 2030 kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya maendeleo 2050.





Maoni
Chapisha Maoni