DKT. BASHIRU AAGIZA KUFANYIKA TATHMINI MIUNDOMBINU YA KUFUGIA SAMAKI - NANE NANE

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amemwagiza Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kufanya tathmini ya miundombinu ya kufugia samaki kutoka kwa Mwekezaji Hawa Fish Farm ili eneo hilo litumike kwa ajili ya Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT Uvuvi).

Balozi Dkt. Bashiru ametoa agizo hilo leo Mei 21, 2026 wakati alipotembelea na kukagua Mabwawa ya Kufugia Samaki ya  Mwekezaji Hawa Fish Farm yaliyopo Viwanja vya Nane Nane vya John Malecela jijini Dodoma, ambapo mwekezaji huyo amesema anaondoka na kwenda kuwekeza sehemu nyingine.

"Hatuwezi kuendesha shughuli za kiserikali zinazohusu watu bila kuwa karibu nao na kurahisisha mawasiliano, Nataka maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Viumbe maji kwa nini tumechelewa kumpa majibu mwekezaji huyu kutokana na mapendekezo yake?, Pia ifanyike tathmini ya miundombinu  hii kama inafaa kwa shughuli gani? amesema Balozi Dkt. Bashiru.

Aidha, Balozi Dkt. Bashiru ameongeza kwa kuitaka idara hiyo kuja na wazo mbadala la kuyatumia mabwawa hayo baada ya mwekezaji kuondoka eneo hilo, akisisitiza kuwa kwa sasa kuna Mradi wa BBT unaotekelezwa na Wizara yake, hivyo ifanyike tathmini ya jinsi miundombinu hiyo inavyoweza kutumia kwa ajili ya Programu hiyo.

Kwa mujibu wa Bi. Hawa Gondwe ambaye ni Mwekezaji na Mkurugenzi wa Hawa Fish Farm alimweleza Balozi Dkt. Bashiru kuwa aliwasilisha andiko la kupewa fidia ya miundombinu hiyo ili eneo hilo lichukuliwe na serikali kwa ajili kujenga Kituo cha Kuzalisha Vifaranga vya Samaki Kanda ya Kati ambapo hadi sasa takriban Samaki 30,000 wamepandikizwa kwenye mabwawa hayo.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wapili kushoto) akikagua mabwawa ya kufugia ya samaki yaliyopo kwennye Viwanja vya Nane Nane Jijini Dodoma Mei 21, 2026

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kushoto) akisalimiana na Mkurungeni wa Hawa Fish Farm Bi. Hawa Gondwe (wa nne kulia) mara baada ya kuwasili kwenye eneo la Mradi wa Ufugaji wa Samaki kwenye Mabwawa  lililopo Viwanja vya Nane Nane Jijini Dodoma Mei 21, 2026

Muonekano wa Bwawa la kufugia samaki lenye uwezo wa kubeba  samaki 10,000 ikiwa ni moja mabwawa manne ya mwekezaji Hawa Fish Farm ndani ya Viwanja vya Nane Nane Jijini Dodoma

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

LESENI, VIBALI VYA MAZAO YA MIFUGO NA VYAKULA VYA SAMAKI KUTOLEWA KWA NJIA YA KIELEKTRONIKI

DKT. MHEDE AONGOZA ZOEZI LA UCHANJAJI WA MIFUGO MKOANI IRINGA, WAFUGAJI WAPONGEZA HATUA YA SERIKALI

SERIKALI KURASIMISHA BIASHARA YA MABONDO