KILIMO, MIFUGO NA UVUVI KUIMARISHA USALAMA WA CHAKULA NCHINI
Baraza la Kumshauri Rais Masuala ya Kilimo na Chakula limekutana na Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa lengo la kujadiliana namna ya kuongeza uzalishaji katika sekta hizo ili kuimarisha usalama wa chakula nchini.
Mwenyekiti wa Baraza hilo na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda ameongoza kikao hicho leo Machi 24, 2026 katika Ukumbi wa Kilimo Four Jijini Dodoma ambapo amesema kuwa baraza hilo limekuwa likiimarisha ushirikiano wa wadau na sekta binafsi katika kuongeza uzalishaji na kuzihimiza Wizara za Kilimo, Mifugo na Uvuvi kufanya kazi kwa umoja ili kuyafikia malengo ya kuongeza uzalishaji ifikapo Mwaka 2030.
“Malengo haya yanatupeleka 2030 leo hii 2026 unaona kabisa muda sio rafiki kwa hiyo nguvu kubwa sana inahitajika lakini tukiwa wamoja hatutashindwa kuyafikia” amesema Mhe. Pinda.
Akisoma taarifa ya Mpango wa Kuongeza Uzalishaji wa Chakula Nchini Katibu Mtendaji wa Baraza hilo Dkt. Florence Turuka amesema dhamira ya serikali katika sekta ya mifugo ni kuongeza uzalishaji wa nyama ya ng’ombe kutoka tani 742,000 za Mwaka 2021/2022 hadi kufikia tani 1,000,000 ifikapo 2030 na uzalishaji wa maziwa kufikia lita bilioni 5 ifikapo 2030 kutoka lita bilioni 3.4 za Mwaka 2021/2022.
Akizungumza katika kikao hicho Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amesema Wizara yake imeendelea kusimamia sekta za mifugo na uvuvi katika kuimarisha usalama wa chakula na kumuomba mwenyekiti wa baraza hilo kuisaidia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuwa wasimamizi wa mfumo mzima wa afya ya mifugo ikiwemo udhibiti wa dawa za mifugo nchini.
“Kwa bahati mbaya sasa hivi shughuli za udhibiti wa dawa za mifugo uko chini ya TMDA, kidogo hili linakaukakasi na TMDA iko chini ya Wizara ya Afya, lakini dunia imebadilika sasa hivi mchakato ni zaidi ya kudhibiti dawa lakini TMDA inakuwa haifanyi usimamizi wa kisayansi wa afya ya mifugo” amesema Dkt. Bashiru.
Kwa upande wake, Waziri wa Kilimo Mhe. Daniel Chongolo amesema kuna umuhimu wa serikali kuifanya kwa ushirikiano Programu ya Vijana ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi ili kuleta ufanisi ambao utawanufaisha vijana kiuchumi.









Maoni
Chapisha Maoni