DKT. BASHIRU AZINDUA MWONGOZO WA KITAIFA KUSIMAMIA RASILIMALI ZA UVUVI
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amezindua Mwongozo wa Kitaifa wa Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi Nchini (BMUs) ili kulinda rasilimali hizo ambazo ni muhimu katika kukuza uchumi na kuimarisha usalama wa chakula.
Mhe. Dkt. Bashiru amezindua mwongozo huo leo Machi 25, 2026 wakati akifunga Mkutano wa Siku Mbili wa Ngazi ya Juu Kuhusu Mustakabali wa Uendelevu na Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi na Uchumi wa Buluu aliofanyika Jijini Dodoma, na kutoa rai kwa Wataalam, Viongozi na Wadau wa Sekta ya Uvuvi nchini kutafuta mbinu shirikishi katika kukabiliana na uvuvi usiofuata sheria.
“Nimefanya ziara Kanda ya Ziwa nimeona kuna watu wanafanya ubunifu wa uhalifu kwa kubadilisha nyavu halali kufanya uvuvi usiofuata sheria, utaratibu wa namna ile huwezi kudhibiti kwa Polisi, utakuwa na Polisi wangapi ?, njia pekee ya kufanikiwa ni kuwa na mbinu shirikishi na kuelimishana bila kuchoka, kwa hiyo huu mwongozo usiishie kwenye makaratasi” alisema Dkt. Bashiru.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Hifadhi ya Mazingira Duniani (TNC) Bi. Lucy Magembe amesema shirika hilo na wizara ya mifugo na uvuvi hufanya ushirikishwaji wa wavuvi katika uhifadhi na kusimamia rasilimali za uvuvi, kupitia BMUs katika kuimarisha uvuvi endelevu na uchumi wa buluu nchini.
“Tumekuwa tukitoa sayansi na elimu ya uvuvi bora, kushirikiana na wananchi kupunguza uvuvi haramu ili kudumisha uvuvi endelevu” alisema Bi. Magembe.
Awali Naibu Katibu Mkuu anayesimamia sekta ya uvuvi Prof. Mohamed Sheikh amesema ulinzi wa rasilimali uvuvi ni jukumu la kila mtu na kwamba vikundi takriban 700 vya BMUs nchini vimekuwa vikishirikiana na wananchi katika kusimamia na kulinda rasilimali za uvuvi.








Maoni
Chapisha Maoni