Nav bar

Jumanne, 23 Januari 2024

WAZIRI ULEGA AKUTANA NA WAWEKEZAJI KUTOKA POLAND


Leo Januari 18, 2024, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amekutana na Wawekezaji kutoka Kampuni ya Uwekezaji ya Contractus ya nchini Poland ambao wameonesha nia ya kufanya uwekezaji kwenye tasnia ya Maziwa hapa nchini.

Wawekezaji hao ambao ni Makamu Mwenyekiti wa Kampuni Contractus, Bw. Witold Karczewski na Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara ya Poland ambaye pia ni Meneja Mauzo wa Kampuni, Bw. Adam Borawski wameonesha nia ya kuingia ubia na Serikali ya Tanzania Kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuleta telnolojia ya kisasa ya kupoza maziwa katika vituo mbalimbali vya kukusanyia maziwa nchini.

Nia yao kuanzia mwaka 2024/ 2025 kuanza uwekezaji huo ambapo wataanza na vituo 500 nchi nzima vyenye uwezo wa kukusanya kati ya lita 2000 hadi 6000 kwa siku. Uwekezaji huo unatarajiwa  kuongeza ukusanyaji wa lita takribani milioni moja za maziwa kwa siku hapa nchini.

Aidha, mpango huo unaotarajiwa kuwa wa miaka 2 unakadiriwa kugharimu TZS. Bilioni 175, na inakusudiwa kupata ufadhili kutoka kwa Wadau na Serikali ya Poland.

Kwa upande wake, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amewahakikishia wawekezaji hao ushirikiano wa kutosha ili mradi huo uweze kuanza haraka ili tasnia ya maziwa iweze kuwa na tija zaidi kwa taifa.

Kampuni hiyo ya Contractus inatengeneza na kuuza Machine/Vifaa vya Kukusanyia maziwa ambazo zinatumia umeme wa jua na wana uzoefu wa kufanya kazi katika Tasnia ya Maziwa hususan usambazaji wa mashine na vifaa vya kukusanyia na kusindika maziwa kwa miaka 35 katika nchi mbalimbali ikiwemo nchi za Ulaya, Asia, na Afrika.  Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe na Msajili wa Bodi ya Maziwa, Prof. George Msalya.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (katikati) akimsikiliza Makamu Mwenyekiti wa Kampuni ya Contractus, Bw. Witold Karczewski wakati wa mazungumzo yao kuhusu uwekezaji katika sekta ya maziwa yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya waziri huyo jijini Dar es Salaam mapema leo Januari 18, 2024. Kulia kwake ni Katibu Mkuu, Prof. Riziki Shemdoe na kushoto kwake ni Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara ya Poland ambaye pia ni Meneja Mauzo wa Kampuni, Bw. Adam Borawski.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Makamu Mwenyekiti wa Kampuni Contractus, Bw. Witold Karczewski (wapili kulia) muda mfupi baada ya kumaliza mazungumzo yao kuhusu uwekezaji katika tasnia ya maziwa yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya waziri huyo jijini Dar es Salaam mapema leo Januari 18, 2024. Wapili kushoto ni Katibu Mkuu, Prof. Riziki Shemdoe. Wa kwanza kushoto ni Msajili wa Bodi ya Maziwa, Prof. George Msalya na wa kwanza kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara ya Poland ambaye pia ni Meneja Mauzo wa Kampuni ya Contractus, Bw. Adam Borawski.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni