Nav bar

Ijumaa, 28 Aprili 2023

MIL 1O KWA KILA KIJANA KUFUGA KIBIASHARA

Na. Edward Kondela


Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda amewaasa watanzania hususan vijana wanaopatiwa mafunzo ya unenepeshaji mifugo na Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambapo baada ya mafunzo hayo ya mwaka mmoja kila mmoja ataondoka na mtaji usiopungua Shilingi Milioni Kumi kufanya ufugaji kibiashara.


Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Pinda ambaye kwa sasa ni Mwenyekiti wa Baraza la Kumshauri Rais Kuhusu Utekelezaji wa Masuala ya Kilimo na Chakula amebainisha hayo (24.04.2023), wakati alipofanya ziara ya siku moja Mkoani Tanga, kutembelea vituo atamizi vya wizara hiyo vinavyotekelezwa kupitia Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA) na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) kwa ajili ya kutoa mafunzo ya vitendo ndani ya mwaka mmoja kwa vijana juu ya unenepeshaji ng’ombe katika kipindi cha miezi mitatu.


Akiwa katika vituo hivyo kwa nyakati tofauti amesema ni vyema baada ya mafunzo vijana hao waliopo kwenye vituo atamizi vinane (8) kwenye maeneo mbalimbali nchini kufahamika katika mikoa wanayotoka ili wakitafutwa watoe taarifa wametoa faida gani kwa wafugaji wengine, ambao watakuwa wamebadilika kibiashara.


Ameongeza kuwa ufugaji wa kibiashara ni muhimu kwa vijana hao kuzingatiwa kwa kutoa elimu waliyopata kwa wafugaji ya namna bora ya kuchagua mifugo minadani na kuipatia malisho bora vikiwemo vyakula vya ziada ili kuwanenepesha na kuuza kwa faida baada ya miezi mitatu.


“Kumbe kilimo hiki au ufugaji huu ni biashara kwa uhakika, ng’ombe uliyemnunua Laki Mbili (2) unakuja kumnenepesha kwa miezi mitatu baadaye unakuja kumuuza Milioni Mbili kwa nini usihangaike nalo hili?, Mwaka mzima unaniachia Milioni Kumi kwa nini nisifanye?”  amesema Mhe. Pinda


Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. David Silinde amesema kuanzishwa kwa programu ya vituo atamizi ni maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan lengo likiwa ni kuboresha Sekta ya Mifugo kuwa ya kisasa na kuleta tija zaidi.


Ameongeza kuwa kijana atayakayemaliza pogramu ya unenepeshaji mifugo hususan ng’ombe itakayodumu kwa mwaka mmoja atapatiwa na serikali Shilingi Milioni Kumi za mtaji na kwamba fedha hizo siyo mkopo bali aende kujiendeleza katika ufugaji kibiashara.


Ametoa rai kwa watanzania kumuunga mkono Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa anajihusisha na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja ili kuboresha maisha ya wananchi.


Naye Mwakilishi wa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Sekta ya Mifugo Dkt. Angello Mwilawa ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani amemwambia Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda namna wizara ya Mifugo na Uvuvi inavyoshirikiana na taasisi nyingine za serikali ili vijana kupata mafunzo hayo kupitia mikopo pamoja na uwekaji wa miundombinu pamoja na rasilimali chakula cha mifugo kwa gharama za chini huku mmoja wa vijana wanaopatiwa mafunzo ya unenepeshaji ng’ombe Bi. Happy Samson akisema mtaji atakaopata baada ya kumaliza mafunzo utamwezesha kuanza biashara ya mifugo kwa ufasaha kwa kufuata elimu ya vitendo aliyoipata.


Serikali tayari imetenga Shilingi Bilioni 4.4 katika programu ya vituo atamizi kwenye vituo vinane (8) kote nchini kupitia Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA) na Taasisi ya Utafiti wa Mifyugo Tanzania (TALIRI), ambapo hadi Mwezi Machi mwaka huu ng’ombe 865 kati ya 900 wamenunuliwa kwa ajili ya programu hiyo ambayo mpango wa mafunzo ni mwaka mmoja na kila kijana atapata fursa ya kunenepesha mifugo hususan ng’ombe katika mizunguko minne ya ng’ombe kumi (10) kwa kila mzunguko na faida itakayopatikana baada ya kuuza ng’ombe hao itatumika kama mtaji kwa ajili ya kijana mnufaika kwenda kuanzisha miradi kama hiyo.

Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda (kushoto) akiwa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. David Silinde, mara baada ya Waziri Mkuu Mstaafu Pinda kutembelea vituo atamizi katika Mkoa wa Tanga vilivyopo Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tazania (LITA) na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), ikiwa ni moja ya vituo vinane (8) ambavyo vinatoa mafunzo ya mwaka mmoja kwa vijana namna ya kunenepesha mifugo hususan ng’ombe katika kipindi cha miezi mitatu na kupatiwa na serikali mtaji usiopungua Shilingi Milioni 10 kwa kila mmoja baada ya mafunzo ili kuendeleza mradi huo. (24.04.2023)

Mwakilishi wa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Sekta ya Mifugo Dkt. Angello Mwilawa ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani amemwambia Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda (hayupo pichani) namna wizara ya Mifugo na Uvuvi inavyoshirikiana na taasisi nyingine za serikali ili vijana kupata mafunzo ya unenepeshaji mifugo hususan ng’ombe katika vituo atamizi kupitia mikopo, uwekaji wa miundombinu pamoja na uwepo wa rasilimali chakula cha mifugo kwa gharama za chini. (24.04.2023)

Muonekano wa baadhi ya ng’ombe 865 kati ya 900 walionunuliwa na serikali kufikia Mwezi Machi mwaka huu kwa ajili ya programu ya vituo atamizi kwa ajili ya vijana kujifunza juu ya unenepeshaji katika vituo vinane (8) nchini kupitia Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA) na Taasisi ya Utafiti wa Mifyugo Tanzania (TALIRI), mpango wa mafunzo ni mwaka mmoja na kila kijana atapata fursa ya kunenepesha mifugo hususan ng’ombe katika mizunguko minne ya ng’ombe kumi (10) kwa kila mzunguko na faida itakayopatikana baada ya kuuza ng’ombe hao itatumika kama mtaji kwa ajili ya kijana mnufaika kwenda kuanzisha miradi kama hiyo. (24.04.2023)

Baadhi ya wanafunzi wa unenepeshaji mifugo hususan ng’ombe katika vituo atamizi vya Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA) na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) katika Mkoa wa Tanga, wakimsikiliza Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda (hayupo pichani) alipofika katika vituo hivyo kujionea kwa vitendo namna wanafunzi hao wanavyofundishwa juu ya ufugaji bora. (24.04.2023)

Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda (katikati), Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Waziri Kindamba na Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Mhe. David Silinde (kulia), wakiwa kwenye mazungumzo juu ya Sekta ya Mifugo, mara baada ya Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Pinda kufanya ziara ya siku moja mkoani humo. (24.04.2023)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni