Nav bar

Ijumaa, 12 Machi 2021

SOKO LA SAMAKI WAFUGWAO NA MAJI YA ASILI KUSHINDANISHWA

 Na. Edward Kondela

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema serikali imeweka lengo la kuhakikisha Sekta ya Uvuvi kupitia ufugaji samaki inazalisha idadi kubwa ya samaki sambamba na samaki wapatikanao kwenye maji ya asili.

 

Akizungumza jana (10.03.2021) alipokuwa akikagua shughuli zinazofanywa na Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji cha Kingolwira kilichopo Mkoani Morogoro, Waziri Ndaki amesema tasnia ya ufugaji samaki imekuwa na mwitikio mkubwa kwa sasa kutokana na mahitaji ya soko la samaki kuongezeka hivyo jitihada nyingi zinafanyika kuongeza uzalishaji wa vifaranga vya samaki.

 

“Kwa sasa tasnia ya ufugaji samaki imekuwa ikitoa faida kubwa kwa wanaojishulisha na ufugaji hivyo natoa wito kwa watu kujitokeza kwa wingi kufuga samaki  na pia na toa wito kwa vituo vyetu vya ukuzaji viumbe maji vilivyopo nchini kuhakikisha vinaongeza uzalishaji wa samaki kwa kuwa mahitaji ya vifaranga ni mengi.” Amesema Mhe. Ndaki

 

Aidha, amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi itahakikisha inaendelea kuviboresha vituo hivyo kwa kuboresha miundombinu ya uzalishaji vifaranga na kupanua uwezo wake ili viweze kwenda sambamba na mahitaji ya vifaranga kwa watu wanaofuga samaki.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Nazael Madalla amesema wizara ipo katika hatua mbalimbali ya kupata programu maalum ya simu ya mkononi itakayoweza kutumiwa na watu wanaotaka kufahamu mambo mbalimbali kuhusu ufugaji samaki na namna ya kupata vifaranga vya samaki kutoka katika vituo ambavyo vipo chini ya wizara.

 

Pia, Dkt. Madalla amemfahamisha Waziri Ndaki uboreshaji ambao unafanyika katika Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji cha Kingolwira kwa kupanua shughuli za uzalishaji wa vifaranga vya samaki aina ya sato na pia kituo kipo mbioni kuanza uzalishaji wa vifaranga vya samaki aina kambale.

 

Kuhusu bei ya vifaranga vya samaki amesema kwa sasa vituo vya ukuzaji viumbe maji vilivyo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi vinauza kifaranga kimoja cha samaki aina ya sangara kwa Shilingi 100 na vimekuwa vikiwarahisishia wahitaji wa vifaranga kuwafikishia popote walipo bila ya ulazima wa wao kufika katika vituo hivyo. 

 

Naye Kaimu Afisa Mfawidhi wa Kituo cha Ukuzaji Vumbe Maji Kingolwira Bw. Hamady Makorwa amesema mikakati ya kituo katika kuendeleza shughuli za uzalishaji ni kufikia uzalishaji wa vifaranga 600,000 kwa mwezi hivyo kituo kinahitaji mabwawa yasiyopungua 26 na sato wazazi wasiopungua 24,000 ambapo kwa sasa wapo 5,430.

 

Amefafanua kwa sasa vifaranga vya samaki vilivyopo katika kituo hicho ni 38,000 huku tayari wamepokea maombi ya vifaranga zaidi ya 180,000 kutoka maeneo mbalimbali nchini.

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amefika kwa mara ya kwanza katika Kituo cha Uzalishaji Viumbe Maji cha Kingolwira lengo likiwa ni kuhakikisha tasnia ya ufugaji samaki inakuwa kwa uwepo wa idadi kubwa ya upatikanaji wa vifaranga vya samaki nchini vitakavyouzwa kwa bei nafuu zaidi.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza kulia) akipewa maelezo na Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka katika wizara hiyo Dkt. Nazael Madalla juu ya vifaranga ambavyo viko tayari kusafirishwa kwa wahitaji ambavyo vinahifadhiwa katika matanki. Waziri Ndaki amefanya ziara ya kikazi ya siku moja katika Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji Kingolwira kilichopo Mkoani Morogoro. (10.03.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiangalia vifaranga vya samaki aina ya sato ambavyo vimezalishwa na Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji Kingolwira kilichopo Mkoani Morogoro, na viko tayari kwa ajili ya kusafirishwa na kuwekwa kwenye mabwawa ili kuendelea kukuzwa na hatimaye kufikia ukubwa wa samaki unaotakiwa sokoni. (10.03.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (katikati), akiwa na Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka katika wizara hiyo Dkt. Nazael Madalla (wa kwanza kulia) na Kaimu Afisa Mfawidhi wa Kituo cha Ukuzaji Vumbe Maji Kingolwira Bw. Hamady Makorwa (wa kwanza kushoto), wakati Waziri Ndaki akipatiwa maelezo ya namna vifaranga vya samaki vinavyozalishwa katika kituo hicho kilichopo Mkoani Morogoro. (10.03.2021)

Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Nazael Madalla akizungumza wakati wa ugeni wa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki na baadhi ya wafanyakazi wa Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji Kingolwira (hawapo pichani). (10.03.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza kulia) wakijadiliana jambo na Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka katika wizara hiyo Dkt. Nazael Madalla, wakati Waziri Ndaki alipokuwa akikagua maboresho ya miundombinu ya uzalishaji vifaranga vya samaki katika Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji Kingolwira kilichopo Mkoani Morogoro. (10.03.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji Kingolwira kilichopo Mkoani Morogoro, mara baada ya kufanya ziara ya kikazi ya siku moja katika kituo hicho na kuwataka wafanye kazi kwa bidii na kuongeza uzalishaji wa vifaranga vya samaki kulingana na mahitaji ya soko. (10.03.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza kulia) akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka katika wizara hiyo Dkt. Nazael Madalla (anayemfuata), namna samaki wazazi aina ya sato wanavyozalisha mayai na njia wanazotumia wataalamu kutoka mayai hayo kwenye midomo ya samaki na kuyaweka katika hatua mbalimbali ili kupata vifaranga. Waziri Ndaki amefanya ziara ya kikazi ya siku moja katika Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji Kingolwira kilichopo Mkoani Morogoro. (10.03.2021)




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni