Nav bar

Jumatano, 17 Julai 2019

ZIARA YA JPM NAMIBIA, YAWAIBUA WAWEKEZAJI KATIKA SEKTA YA MIFUGO NCHINI




Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel amemshukuru Rais Dkt. John Magufuli kufuatia ziara yake ya kikazi ya siku mbili aliyofanya nchini Namibia kuanzia Mei 27 hadi 28 Mwaka 2019, kuanza kuonesha mafanikio baada ya kupokea ugeni kutoka Kampuni ya Burmeister and Partners (PTY) Ltd inayomikili kiwanda cha kuchakata nyama nchini Namibia iliyoonesha nia ya kuwekeza hapa nchini.

Akizungumza (09.07.2019) ofisini kwake katika mji wa serikali eneo la Mtumba Jijini Dodoma na mmoja wa wakurugenzi katika kampuni hiyo Bw. Hendrick Boshoff, Prof. Gabriel amesema lengo la ziara yake ni kupata taarifa za awali, kutoka kwa wataalam wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili waweze kuwa na njia sahihi ya uwekezaji ambao utakuwa na tija kwa watanzania kupitia Sekta ya Mifugo.

“Mheshimiwa rais alifanya ziara ya kikazi ya siku mbili nchini Namibia akiambatana na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Luhaga Mpina na viongozi wengine, nichukue fursa hii kwa niaba ya wizara kumshukuru mheshimiwa rais kutuanzishia suala la soko la mazao ya mifugo hususan nyama, tumetembelewa na mmoja wa wakurugenzi wa Kampuni ya Burmeister and Partners (PTY) Ltd inayomiliki kiwanda cha kuchakata nyama nchini Namibia ili kukutana na wataalam baada ya rais kuonesha muelekeo na wao wakaitikia.” Amesema Prof. Gabriel

Katika mazungumzo hayo Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo, amesema wameuhakikishia ugeni huo kutoka Namibia kuwa wizara iko tayari kupitia Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Luhaga Mpina kwa kuhakikisha nia ya kampuni hiyo kuanzisha kiwanda kingine cha kuchakata nyama hapa nchini inafikia katika utekelezaji kufuatia ziara ya mheshimiwa rais nchini Namibia.

Prof. Gabriel amefafanua kuwa ujio wa ugeni huo unaratibiwa na wizara nne zikiwemo za Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Viwanda na Biashara, Ofisi ya Waziri Mkuu eneo la Uwekezaji na Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika Sekta ya Mifugo ambapo Prof. Elisante Ole Gabriel ndiye Katibu Mkuu anayeshughulikia sekta hiyo na kwamba ameupokea ugeni wa mkurugenzi wa kampuni hiyo kutoka Namibia kwa niaba ya makatibu wakuu kutoka katika wizara nyingine tatu.

Aidha, ametoa wito kwa watanzania kuunga mkono juhudi mbalimbali zinazofanywa na serikali hususan zinazolenga kuongeza masoko ya kutengeneza na kuuza bidhaa zinazozalishwa hapa nchini.

“Viwanda kama hivi vikija ajira nyingi zitaongezeka na pia pato la taifa litaongezeka, bado tuko chini katika ulaji wa nyama takwimu zilizotolewa na Shirika la Chakula Duniani (FAO) zinaonesha walau mtu wa kawaida anatakiwa kula kilogramu 50 kwa mwaka, bado kwa watanzania tunakula kilogram 15 kwa mwaka mzima, tunaleta wenzetu waongeze bidii katika hilo ili wazalishe na soko la ndani liwepo tuuze na nje ya nchi.” Alifafanua Prof. Gabriel

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Burmeister and Partners (PTY) Ltd inayomikili kiwanda cha kuchakata nyama nchini Namibia Bw. Hendrick Boshoff amwemambia Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel kuwa, kampuni hiyo ilianza kuendesha shughuli zake miaka 40 iliyopita na wamekuja nchini Tanzania wakilenga zaidi uwekezaji wa kuyaongezea thamani mazao ya mifugo hususan nyama.

Akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara katika kikao hicho, Mkurugenzi wa Viwanda Vidogo na Kati (DSME) Dkt. Consolata Ishebabi, amesema ugeni huo utafahamishwa pia fursa mbalimbali zilizopo hapa nchini kwa kushirikiana na Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC) ili kufahamu mazingira mbalimbali ya uwekezaji yakiwemo ya sekta binafsi.

Aidha, Dkt. Ishebabi amefafanua kuwa ugeni huo utafikishwa pia katika Kampuni ya Ranchi ya Taifa (NARCO) ambapo watafikishwa katika Ranchi ya Kongwa ambayo ipo chini ya NARCO kuweza kuona aina ya mifugo iliyopo nchini na waweze kupata taarifa za jumla ambazo zitawapatia mwanzo mzuri wa kuwekeza hapa nchini katika Sekta ya Mifugo.

Kikao hicho kiliwahusisha wataalam kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.



Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akiagana na kupiga picha ya pamoja na mmoja wa wakurugenzi katika Kampuni ya Burmeister na Partners (PTY) Ltd inayomiliki kiwanda cha kuchakata nyama nchini humo Bw. Hendrick Boshoff pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda na Biashara, Ofisi ya Waziri Mkuu eneo la Uwekezaji pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
 



Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa katika mazungumzo ofisini kwake jijini Dodoma (09.07.2019) na mmoja wa wakurugenzi katika Kampuni ya Burmeister and Partners (PTY) Ltd ya nchini Naimibia inayolimiki kiwanda cha kuchakata nyama nchini humo Bw. Hendrick Boshoff (Picha ya kwanza juu kushoto) ambaye yupo nchini kwa ajili ya nia ya kampuni hiyo kuwekeza kufuatia ziara ya Mhe. Rais Dkt. John Magufuli nchini Namibia. Bw. Boshoff alisindikizwa na Dkt. Consolata Ishebabi Mkurugenzi wa Viwanda Vidogo na Kati (DSME) (Picha ya chini kushoto) kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni