MABALOZI WATEULE WAHIMIZWA KUZINADI FURSA ZA MIFUGO NA UVUVI KIMATAIFA
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amekutana na Mabalozi Wateule wa Tanzania kwa lengo la kuwafahamisha fursa zilizopo katika sekta za mifugo na uvuvi ili kwenda kuzinadi kwenye Nchi walizopangiwa kuiwakilisha Tanzania ikiwa ni sehemu ya kuimarisha diplomasia ya uchumi kimataifa.
Mhe. Dkt. Bashiru amekutana na Mabalozi hao katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Jijini Dodoma leo Aprili 13, 2026 na kuwaeleza kuwa sekta za mifugo na uvuvi zinahitaji kupanua wigo wa masoko ya kimataifa yatakayochochea uzalishaji na ukuaji wa uchumi wa wananchi.
“Kama ambavyo mtakavyokuwa makini na sekta zingine za kiuchumi kama maliasili na utalii, pia sekta za mifugo na uvuvi ni eneo muhimu, nchi yetu bado tuna nafasi ya kujikomboa kiuchumi kutokana na Kilimo, Mifugo na Uvuvi, kwa hiyo uwakilishi wenu unakuwa na mchango mkubwa katika diplomasia ya uchumi” alisema Mhe. Dkt. Bashiru.
Aidha, Mhe. Dkt. Bashiru ameongeza kuwa Wizara bado inahitaji mashirikiano na mataifa mengine katika maeneo ya teknolojia na miundombinu ya uzalishaji, mitaji, uwekezaji katika uzalishaji wa vyakula vya mifugo na samaki, afya ya mifugo, kuimarisha mbari (mbegu bora) za mifugo, masoko ya mazao ya mifugo na uvuvi pamoja na mafunzo na utaalam katika sekta hizo, mambo ambayo yatavutia uwekezaji.
Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania Nchini Saudi Arabia Mhe. Eng. Zena Ahmed Saidi akizungumza katika kikao hicho ameiomba serikali kupitia wizara ya mifugo na uvuvi kushirikiana kwa karibu na balozi hizo ikiwa ni pamoja na kuwapatia vielelezo vyote vinavyohusiana na sekta ya mifugo na uvuvi ili kupata nguvu ya kuzitangaza sekta hizo kwa wawekezaji wa kimataifa.





Maoni
Chapisha Maoni