WAFUGAJI NA WAKULIMA WAASWA KUTOCHUKUA SHERIA MKONONI
Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa( OWM- TAMISEMI) zimetoa pole kwa wahanga wa migogoro ya wakulima na wafugaji Wilayani Tunduru mkoni Ruvuma iliyosabahisha vifo vya watu nane na wengine kadhaa kujeruhiwa tukio lililotokea mwishoni mwa mwezi septemba 2025.
Akizungumza na Wananchi wa Tarafa ya Nalasi Wilayani Tunduru Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amewaasa wafugaji na wakulima nchini kuacha kujichukulia sheria mkononi hasa pale inapotokea changamoto ya kuingilia matumizi ya ardhi.
“Nimekuja hapa na Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI kwanza kuwapa pole wote walifariki kutokana na migogoro huo uliotokea mwenyezi Mungu Awarehemu , lakini niwaase ndugu zangu wafugaji na wakulima mjishichukulie sheria mkononi , toeni taarifa mapema kwa mamlaka za kisheria” alisema Mhe. Balozi Dkt. Bashiru.
Aidha, Dkt. Bashiru amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Ardhi na Ofisi ya Waziri Mkuu Tamisemi zimeanza kupanga mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa kutenga maeneo ya malisho ya mifugo hatua itakayopunguza migogoro ya wakulima na wafugaji nchini.
Naye, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt. Jafari Rajabu Seif amewataka watendaji wa halmashauri nchini kutenda haki kwa wananchi na kutokuwa chanzo cha migogoro ya wafugaji na wakulima.
Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kusini Eng. Fadhili Chilombe amepongeza hatua za serikali za kutenga vitalu kwa ajili ya wafugaji na kuomba vitalu hivyo viwezeshwe miundombinu ili wafugaji waanze kuitumia kwa ajili ya shughuoi za ufugaji.





Maoni
Chapisha Maoni