SERIKALI KUTOA PIKIPIKI 200 KUIMARISHA HUDUMA ZA UGANI
Na. Stanley Brayton
Wizara ya Mifugo na Uvuvi imezamiria kuimarisha huduma za Ugani kwa kununua pikipiki 200 ambazo zitasaidia kuongeza ufanisi katika utendaji kazi wa maafisa Ugani wa Mifugo na Uvuvi katika kutekeleza majukumu ya kuwahudumia wananchi ili kuongeza uzalishaji katika sekta hizo.
Akizungumza Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Uchumi na Uzalishaji Mkoa wa Pwani, Ndg. Shangwe Twamala, wakati wa hafla ya ufunguzi wa mafunzo rejea kwa maafisa hao kutoka Kanda ya Kati Mashariki leo Machi 11, 2026, mkoani Pwani, Ndg. Twamala amesema pikipiki hizo 200 zitasambazwa kwa maafisa ugani wote nchini.
"Wote tunashuhudia utekelezaji huo na hatua za Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuwa miongoni mwenu wapo wataalam wa ugani ambao wameshapatiwa vifaa pamoja na mafunzo mbalimbali yakiwemo haya mafunzo ya leo ambayo nimepata nafasi ya kuyafungua kwa Kanda ya Kati Mashariki.” Amesema Ndg. Twamala
Aidha, Ndg. Twamala amebainisha kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi inaendelea kutekeleza majukumu mbalimbali ikiwemo kampeni ya chanjo na utambuzi wa mifugo, ukusanyaji wa mapato kwa sekta za mifugo na kutoa mafunzo kwa wanajamii katika Halmashauri zote nchini.
Vilevile, Ndg. Twamala amewataka maafisa ugani kuongeza kasi katika utekelezaji wa majukumu yao, na ametaka wajikite katika kuboresha utoaji wa taarifa sahihi na kwa wakati, kusambaza teknolojia bora na bunifu zinazoongeza tija, kuimarisha elimu kwa wafugaji na wavuvi, pamoja na kutoa ushauri wa kitaalamu unaozingatia viwango na miongozo iliyopo.
Akizungumza kwa Niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Naibu Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania (VCT), Dkt. Obed Nyasebwa ameweka wazi kuwa mafunzo hayo ni mwendelezo wa hatua zinazochukuliwa na wizara za kuwajengea uwezo wataalam wa mifugo na uvuvi katika kutekeleza majukumu ya utoaji wa huduma za ugani nchini kama ilivyoainishwa katika Sera, Sheria na Kanuni za Mifugo.
Pia, Dkt. Nyasebwa amesema kupitia mafunzo hayo wataalam watapata nafasi ya kujadiliana kwa kina juu ya changamoto na utatuzi wake ili kuweza kuboresha sekta zote na mifugo na uvuvi.
Kwa upande wake, Afisa Mifugo Mkuu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI, Ndg. Elisante Qadwe amewapongeza maafisa ugani wa mifugo na uvuvi kwa kuhudhuria kwa wingi katika mafunzo hayo yenye lengo la kufanya mapinduzi makubwa hasa utendaji kazi unaozingatia matumizi ya sayansi.
Naye, Mkuu wa Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, Bi. Anna Kiria ameiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuendelea kutoa mafunzo hayo kwani yatazidi kuimarisha sekta na kuinua hali ya utendaji kazi wa maafisa ugani.

Maoni
Chapisha Maoni