MAAFISA UGANI WAHIMIZWA KUBADILISHANA UZOEFU ILI KUBORESHA HUDUMA KWA WANANCHI
Wataalamu wa ugani wa sekta za mifugo na uvuvi kutoka Kanda ya Ziwa wameanza mafunzo rejea katika Halmashauri ya Wilaya ya Chato mkoani Geita leo Machi 9, 2026, yaliyoandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma za ugani kwa wafugaji na wavuvi.
Akifungua mafunzo hayo, mgeni rasmi ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Chato, Mhe Lois Bura amewahimiza maafisa ugani kubadilishana uzoefu na kutumia ujuzi wao wa kitaalamu ili kuboresha huduma wanazozitoa kwa wananchi, hususan wafugaji na wavuvi wanaotegemea ushauri wao katika shughuli za uzalishaji.
"Maafisa ugani ni kiungo muhimu katika kufikisha sera, sheria na teknolojia bora za ufugaji na uvuvi ili kuongeza tija katika uzalishaji na kuendelea kuimarisha usalama wa chakula na kipato kwa wananchi." amesema Mhe. Bura
Aidha, Mhe. Bura amesema kuwa huduma za ugani zina mchango mkubwa katika kuleta mageuzi kwa kusaidia kupeleka mbinu na teknolojia mpya kwa wafugaji pamoja na kukabiliana na changamoto mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya tabianchi.
Kwa upande wake mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ndg. Joshua Elisha ambaye ni Afisa Tawala Mkuu amesema mafunzo hayo ni mwendelezo wa juhudi za wizara za kuwajengea uwezo wataalamu wa mifugo na uvuvi ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi katika utoaji wa huduma za lugani nchini.
Vilevile Ndg. Elisha ameongeza kuwa mafunzo hayo yanawakutanisha maafisa ugani kutoka ngazi mbalimbali ikiwemo mikoa, wilaya, kata, vijiji na mitaa ambapo washiriki wanapata fursa ya kujifunza mada mbalimbali zinazohusu uzalishaji wa mifugo, udhibiti wa magonjwa pamoja na usimamizi endelevu wa rasilimali za uvuvi.
Mafunzo hayo yanatarajiwa kuwasaidia wataalamu kubadilishana uzoefu, kujadili changamoto zilizopo na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha utoaji wa huduma kwa wafugaji na wavuvi nchini.





Maoni
Chapisha Maoni