DKT. BASHIRU: NATAKA MTAMBO WA KUKAUSHIA DAGAA SOKO LA CHATO BEACH
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally amemtaka Mkandarasi anayesimamia ujenzi wa miundombinu ya Soko la Kimataifa Samaki la Chato Beach mkoani Geita kukamilisha ufungaji wa mtambo wa kukaushia dagaa pamoja na kumalizia kazi zingine zilizobaki kabla ya mwezi Machi Mwaka huu.
Dkt. Bashiru ametoa maagizo hayo leo Februari 28, 2026 baada ya kukagua mwenendo wa ujenzi wa miundombinu ya soko hilo ambapo ameonesha kutoridhishwa na kasi ya kazi zinazofanywa licha ya changamoto za mkandarasi pia ameagiza kufanyika tathmini mpya ya gharama za mtambo huo ili upatikane kwa haraka katika soko hilo
“Nataka kazi kwa kasi, maelekezo niliyopewa na mamlaka iliyioniteua , sasa nataka Jumatatu barua iwe imejibiwa mpaka jumatano(mkandarasi) awe ameipata na mimi nipate ‘copy’, mimi nataka mtambo hapa, kama mtambo huu ni wa kukausha dagaa lazima uwepo ndio tuzindue soko hili ” alisema Dkt. Bashiru.
Akitolea ufafanuzi baadhi ya hoja zilizoibuliwa na mjadala huo mbele ya Waziri, Mkurugenzi wa Miundombinu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Mhandisi George Kwandu alisema kuwa kulikuwa na changamoto mbalimbali zilizosababisha kumcheleshea malipo mkandarasi na kumsababishia kushindwa kununua mtambo huo lakini tayari wamepanga kujadiliana kwa pamoja ili kuharakisha ununuzi wa mtambo huo.
Maagizo mengine aliyotoa Mhe. Balozi Dkt. Bashiru ni pamoja na ufungaji wa miundombinu ya maji, umeme, barabara, ambapo amemtaka mkandarasi huyo kushirikiana na taasisi zingine zinazotoa huduma za kijamii kama Tanesco, TARURA, RUWASA katika kukamilisha miundombinu iliyobaki kabla ya kuisha wa mwezi Machi 2026 ili soko hilo lizinduliwe na kuanza kufanya kazi.


Maoni
Chapisha Maoni