DKT. BASHIRU AHIMIZA KAMPENI YA TUTUNZANE KUTATUA MIGOGORO YA WAFUGAJI NA WAKULIMA
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amewahimiza wafugaji na wakulima kote nchini kuzingatia Kampeni ya Tutunzane inayotekelezwa Wilayani Mvomero inayolenga kuimarisha mahusiano baina yao ili kuepukana na migogoro na uhasama unaotokana na matumizi ya ardhi kati ya Wafugaji na watumiaji wengine wa Ardhi.
Balozi Dkt. Bashiru ametoa wito huo leo Machi 06, 2026 wakati akizungumza na Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma ambako amefika kutekeleza maelekezo ya Waziri Mkuu yaliyomtaka kufika katika Wilaya hiyo kwa ajili ya kuimarisha uhusiano baina ya wakulima na wafugaji, hivyo amewahimiza kuiga na kuzingatia kampeni ya tutunzane .
“Mhe. Rais mara nyingi amekuwa akisema hafurahishwi na migogo kati ya wakulima na wafugaji hivyo niwasihi viongozi wenzangu na wakulima na wafugaji tujifunze kupitia kampeni ya tutunzane ya Mvomero ili kuondokana na uhasama huu ambao unaturudisha nyuma.” Alisema Dkt. Bashiru.
Pia, amesema Serikali haitakubali kuona uvunjifu wa sheria ukifanywa na wakulima na wafugaji huku akisisitiza kuwa mfugaji kutumia maeneo yasiyotengwa kwa ajili ya mifugo na wakulima kutumia maeneo ya mifugo kwa shughuli za kilimo ni ukiukaji wa sheria na kwamba serikali haitakubaliana na hilo.
Awali Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Mhe. Denis Masanja amesema migogoro ya wakulima na wafugaji katika wilaya hiyo imekuwa ikiathiri shughuli za kiuchumi na kupendekeza kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na halmashauri ya Wilaya ya Tunduru kuanzisha programu maalum za vitalu vyenye miundombinu muhimu kwa ajili ya wafugaji.
Katika ziara hiyo Balozi Dkt. Bashiru ameambatana na Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Dkt. Jafar Rajabu Seif pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi.





Maoni
Chapisha Maoni