MAPINDUZI SEKTA YA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI KUKUZA UCHUMI WA KATI WA JUU
Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi iko tayari kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Mageuzi ya Shoroba za Kilimo, Mifugo na Uvuvi (AMP 2050) utakaosaidia kuchochea ukuaji wa uchumi wa kati wa juu kwa taifa.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano wa uhamasishaji wa ukuzaji na uendelezaji wa shoroba za kilimo uliofanyika Februari 12, 2026 mkoani Singida, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamwile, amesema lengo kuu la mkutano huo ni kujenga uelewa wa pamoja kuhusu mpango huo kwa wataalam wa mikoa na halmashauri, hususan kuhusu dhana ya shoroba za kilimo.
“Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka msisitizo mkubwa katika mageuzi ya sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi kama injini ya kukuza uchumi wa taifa, kuongeza ajira na kuinua maisha ya Watanzania kwa ujumla,” amesema Mhe. Senyamwile.
Aidha, ameongeza kuwa mpango huo unalenga kupunguza gharama za uzalishaji na usafirishaji ili kuongeza thamani ya mazao, kuongeza kipato cha wakulima, wafugaji na wavuvi, pamoja na kuvutia uwekezaji wa sekta binafsi kwa kuzingatia mabadiliko ya tabianchi na kuyaunganisha maeneo yenye uzalishaji mkubwa na miundombinu muhimu kama barabara, reli, bandari, masoko na viwanda vya kuchakata mazao.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ofisi ya Mageuzi ya Kilimo (ATO), Bi. Elizabeth Missokia, amesema kuwa dhana ya shoroba za kilimo ni moja ya miradi ndani ya mpango kabambe wa mageuzi ya sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi, unaounganisha uzalishaji, usindikaji, uchakataji, usafirishaji na uhifadhi pamoja na masoko ili kuharakisha mageuzi ya sekta hizo.





Maoni
Chapisha Maoni