Nav bar

Jumatatu, 21 Oktoba 2024

TANZANIA NA IRAN ZA SAINI HATI SABA ZA MAKUBALIANO ILI KUKUZA DIPLOMASIA YA UCHUMI

Na. Stanley Brayton

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Kiislam ya Iran zimesaini hati saba  za makubaliano ili kukuza diplomasia ya uchumi baina ya mataifa hayo mawili.

Hafla ya kusaini hati hizo za makubaliano imefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam, tarehe 19 Oktoba, 2024, katika mkutano wa tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano baina ya Tanzania na Iran.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo na Waziri wa Kilimo wa   Jamhuri ya Kiislaam ya  Iran, Mhe. Golamreza Nouri Ghezelcheh walishuhudia zoezi hilo la uwekaji saini hati hizo lililohusisha Wizara za Kisekta, baadhi ya Taasisi za Umma na Taasisi binafsi. 

Akizungumza wakati akifungua mkutano huo uliohusisha Viongozi wa ngazi za juu za Serikali za nchi hizo, wakiwemo Mawaziri, Mhe. Balozi Kombo amemshukuru Mhe. Golamreza Nouri kwa jitihada zake za kuimarisha ushirikiano wa uwili na azma yake katika kuongeza maeneo ya ushirikiano yakiwemo Mifugo na Uvuvi,  biashara na  uwekezaji,   kilimo, nishati, ulinzi   na   usalama na elimu. Maeneo mengine ya ushirikiano baina ya Tanzania na Iran yatahusisha sekta ya afya, sayansi na teknolojia, na utamaduni. 

Hati hizo za makubaliano zilihusisha hati ya makubaliano kati ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania   na Wizara ya Kilimo ya   Jamhuri ya Kiislam ya   Iran, kuhusu ushirikiano katika sekta ya Mifugo na Uvuvi; Wizara ya Mifugo na Uvuvi  ya Tanzania na Wizara ya Kilimo ya Iran kuhusu ushirikiano katika sekta ya afya ya wanyama; na hati ya makubaliano baina ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na Wizara ya Michezo na Vijana ya Iran. 

Hati nyingine za Makubaliano zilisainiwa baina ya Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana, Ajira, na Watu wenye ulemavu ya Tanzania na Wizara ya Ushirika, Kazi na Maendeleo ya Jamii ya Iran kuhusu ushirikiano katika kazi, ajira na usalama wa raia.Taasisi   za Serikali zilizotia saini   hati za makubaliano ni pamoja   na Kikosi cha Uokozi  na Zimamoto, chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Tanzania, na Kitengo kinachoshughulikia masuala ya moto cha Iran, kuhusu ushirikiano katika huduma za zima moto na uokozi. 

Aidha katika hafla hiyo, Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) ilitia saini hati  ya makubaliano na Taasisi ya Uendelezaji  Biashara ya Iran kuhusu ushirikiano  katika kukuza na kutangaza biashara kwa manufaa ya pande zote mbili. 

Kwa upande wa sekta   binafsi, Taasisi ya Biashara, Viwanda  na   Kilimo ya Tanzania ilisaini hati ya  makubaliano na Taasisi  ya Biashara,  Viwanda  na  Kiimo ya Iran kuhusu   ushirikiano katika uanzishwaji wa Kamati ya Pamoja ya Biashara baina ya nchi hizo mbili. 

Akitoa neno la shukrani   wakati wa kuhitimisha   kikao hicho, Naibu   Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano  wa Afrika Mashariki   anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Mhe. Dennis Londo (Mb) amewashukuru Mawaziri, Viongozi wa Serikali na Sekta Binafsi pamoja na wadau wote kwa mchango wao katika kufanikisha mkutano huo wa tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano baina ya Tanzania na Iran, kwani umeziwezesha pande zote mbili kufikia malengo ili  kukuza  diplomasia na ushirikiano  wa kimataifa.

Mkutano wa Tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano baina ya Tanzania na Iran, ulianza rasmi tarehe 16 Oktoba 2024, na ulitanguliwa na kongamano la biashara, kikao cha ngazi ya  Wataalam   na   Maafisa   Waandamizi   kutoka   Tanzania   na   Iran   kilichoandaa   agenda   za kuiamarisha ushirikiano wa kidiplomasia baina ya nchi hizo pamoja na Kikao cha ngazi ya juu ya Viongozi wa nchi hizo wakiwemo Mawaziri, ambacho kiliidhinisha  na kutia saini Hati za Makubaliano ya pamoja kwa manufaa ya nchi hizo.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Pastory Mnyeti (kulia aliyesimama), na Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Kiislaam ya  Iran, Mhe. Golamreza Nouri Ghezelcheh (kushoto aliyesimama) wakionesha hati za makubaliano ya ushirikiano baada ya kuzisaini, ni katika Mkutano wa tano wa Tume ya pamoja ya kudumu ya Ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Kiislam ya Iran, ambayo umefanyika katika Ukumbi wa JNICC, Oktoba 19, 2024. Dar es Salaam


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Pastory Mnyeti (kulia aliyekaa na kusaini), akisaini hati za makubaliano ya ushirikiano na Iran, ambazo hati hizo zimehusisha Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, pamoja na Wizara ya Elimu, Sayansi, na Teknolojia, ni katika Hafla ya utiaji saini hati za makubaliano ya ushirikiano wakati wa Mkutano wa tano wa Tume ya pamoja ya kudumu ya Ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Kiislam ya Iran, ambayo yamefanyika katika Ukumbi wa JNICC, Oktoba 19, 2024. Dar es Salaam. Kushoto ni Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Kiislaam ya  Iran, Mhe. Golamreza Nouri Ghezelcheh


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni