Nav bar

Jumatatu, 19 Agosti 2024

RUKWA NAO WAREJESHA UVUVI WA ZIWA TANGANYIKA

 Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Charles Makongoro Nyerere amewaongoza wananchi wa mkoa huo kwenye hafla ya ufunguzi wa shughuli za Uvuvi wa Ziwa Tanganyika kwa upande wa mkoa huo iliyofanyika kwenye kata ya Kasanga Agosti 17, 2024.

Katika hotuba yake ya ufunguzi wa shughuli hizo Mhe. Nyerere ambaye alimwakilisha Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega mbali na kuwashukuru Wavuvi wa mkoa huo kwa uvumilivu wao wakati wote wa ufungaji wa ziwa hilo amewataka kuvua kwa kufuata sheria na taratibu ili kutunza rasilimali iliyopatikana.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede mbali na kuwaeleza wananchi wa mkoa huo umuhimu wa upumzishwaji wa Ziwa hilo, amewataka wavuvi hao kuendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali wakati wote inapokuwa na kampeni inayolenga kulinda rasilimali za Uvuvi.

Akitoa Ushuhuda wa mavuno aliyopata baada ya ufunguzi huo, Mmoja wa wavuvi kutoka kijiji cha Kilewani Bw. Adam Pesambili amesema kuwa kwa usiku mmoja tu amefanikiwa kuvuna kiasi cha ndoo 60 za dagaa zenye thamani ya zaidi ya shilingi Mil 4.5 tofauti na awali ambapo alikuwa hawezi kupata hata ndoo 2 kwa siku.

"Tunaomba Serikalo iendelee na mpango huu wa upumzishaji wa Ziwa kwa sababu tumeona manufaa yake" Ameongeza Bw. Pesambili.

Tukio hilo la Ufunguzi wa shughuli za Uvuvi wa Ziwa Tanganyika mkoa wa Rukwa liliambatana na ugawaji wa makasha 70 ya kuhifadhia Samaki ambapo Wilaya ya Kalambo ilipata makasha 40 na Nkasi ilipata makasha 30.

Ufunguzi huo umefanyika ikiwa ni baada ya takribani miezi mitatu ya upumzishwaji wa Ziwa hilo ulioanza Mei 15, 2024.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni