Nav bar

Alhamisi, 30 Mei 2024

WAZIRI MKUU AZINDUA KITUO CHA UFUGAJI MBUZI, KONGWA


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa leo Mei 13, 2024 amezindua na kushuhudia makabidhiano ya Kituo Atamizi cha Ufugaji wa Kibiashara kwa Vijana, baina ya Taasisi ya PASS TRUST na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI)kilichopo Kongwa mkoani Dodoma.

Akizungumza baada ya makabidhiano ya kituo hicho, ambacho kinathamani ya shilingi bilioni 1.63 ikijumuisha uwekezaji wa vifaa na mindombinu, Mheshimiwa Majaliwa ameagiza uwekezaji utunzwe ili taifa liweze kunufaika kupitia uwezeshwaji wa vijana.

Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa lengo la mradi huo ni kuwapatia vijana ujuzi kwa vitendo ikiwemo elimu ya ujenzi wa mabanda, ulishaji, matibabu na usimamizi wa mbuzi lakini pia kutoa mafunzo ya biashara ili vijana waweze kuwa wajasiriamali na kuendeleza biashara ya unenepeshaji mbuzi.

Kwa upande wake, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amesema kuwa hadi kufikia Aprili 2024, ongezeko la mauzo ya nyama nje ya nchi limefikia takribani shilingi bilioni 100 ambapo nyama ya mbuzi imeendelea kuongoza kwa kuchangia asilimia 70.1 ya mauzo yote, hivyo kituo hicho cha unenepeshaji wa mbuzi kitaendelea kuchaguza kwenye biashara ya nyama kupitia shughuli ya unenepeshaji wa mbuzi utakaokuwa ukifanywa na vijana hao.

 Aliongeza kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi imepanga kukifanya  Kituo Atamizi cha Ufugaji kilichopo Kongwa kuwa kituo kikubwa kwa ajili ya ufugaji na unenepeshaji wa mbuzi nchini.

 Kituo hicho kilichokuwa kikisimamiwa na Taasisi isiyo ya kiserikali ya PASS kimekabidhiwa kwa Serikali na kitakuwa chini ya uangalizi wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI).





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni