Nav bar

Alhamisi, 30 Mei 2024

VIJANA WATENGEWA BIL. 10.5 KWA AJILI YA MIRADI


Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetenga zaidi ya Shilingi Bilioni 10.5 kwa ajili ya mitaji ya miradi ya vijana ili kuwainua kiuchumi.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Patrobas Katambi amebainisha hayo (24.05.2024) jijini Mwanza, wakati wa kuhitimisha mafunzo kwa vitendo ya uvuvi na ukuzaji viumbe maji awamu ya pili kupitia Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT – LIFE) ambayo imewejenga katika kujiajiri kupitia Sekta ya Uvuvi.

Mhe. Katambi amempongeza Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) pamoja na viongozi wengine wa wizara kwa kusimamia vyema maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kukuza ajira kwa vijana kupitia sekta za mifugo na uvuvi.

Ameongeza kuwa ni wakati sasa kwa vijana kutumia vyema fursa zitokanazo na sekta hizo ili kujipatia ajira na utajiri pamoja na kufuga kisasa na kuuza mazao ya mifugo na uvuvi yakiwa katika ubora unaotakiwa.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe amesema zaidi ya vijana 300 wamenufaika kupitia mafunzo hayo ya miezi mitatu kupitia vituo mbalimbali.

Prof. Shemdoe ameongeza kuwa lango la mafunzo hayo ni kuwezesha vijana kuwa wajisiriamali na wawekezaji kwenye shughuli za uvuvi na ukuzaji viumbe maji kwa kuwajengea ujuzi utakaowawezesha kubuni miradi na kuanzisha vikundi au kampuni ili waweze kujiajiri na kutoa fursa za ajira kwa wenzao.

Amebainisha kuwa awamu ya pili ya wigo wa mafunzo hayo imeongezeka tofauti ya awamu ya kwanza ambapo yalipokelewa maombi zaidi ya 1,200 ambapo inaashiria vijana wana ari ya kujiunga katika mafunzo hayo ya vitendo ambapo Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Wizara ya Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu) zinahitaji kuweka nguvu zaidi katika kuwawezesha vijana kujiajiri.

Kwa upande wake mmoja wa wanufaika wa BBT – LIFE akisoma risala kwa niaba ya vijana wenzake Bw. Muhsin Mussa amesema katika mafunzo hayo wamejifunza namna ya utunzaji wa fedha, kuunda na kusajili vikundi, maandiko ya miradi na namna ya kuiendesha pamoja na mafunzo ya vitendo kwa vijana wa Tanzania Bara na Visiwani.

Aidha, amesema mafunzo hayo wanaamini yataenda kupunguza wingi wa vijana wasio na ajira ambapo sasa wataweza kujishughulisha na uvuvi pamoja na ukuzaji viumbe maji kibiashara.


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Patrobas Katambi (mwenye tai nyekundu) akiwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe (kulia kwake) wakiangalia moja ya vizimba vya kufugia samaki, wakati wa kuhitimisha mafunzo kwa vitendo ya uvuvi na ukuzaji viumbe maji awamu ya pili jijini Mwanza kupitia Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT – LIFE). (24.05.2024)

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Patrobas Katambi (mwenye tai nyekundu) akiwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe (kulia kwake) wakiangalia moja ya vizimba vyenye uwezo wa kufuga samaki takriban 100 na kisichogharimu zaidi ya Shilingi Laki Moja kwa ajili ya matengenezo yake, wakati wa kuhitimisha mafunzo kwa vitendo ya uvuvi na ukuzaji viumbe maji awamu ya pili jijini Mwanza kupitia Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT – LIFE). (24.05.2024)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni