Nav bar

Jumanne, 23 Januari 2024

ZIWA TANGANYIKA KUPUMZISHWA, SERIKALI YAPIGIA CHAPUO UVUVI WA VIZIMBA

 

Na. Edward Kondela

Serikali yaazimia kupumzisha shughuli za uvuvi katika Ziwa Tanganyika kwa kipindi cha miezi mitatu kwa miaka mitatu mfululizo ili kuongeza mazalia ya samaki na kuhamasisha ufugaji samaki kwa njia ya vizimba katika ziwa hilo.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti amebainisha hayo (10.01.2024) kwa nyakati tofauti wakati alipokuwa akiongea na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Katavi na wadau wa uvuvi katika mkoa huo wakiwemo wanaojishughulisha na shughuli za uvuvi katika Mwalo wa Ikola uliopo katika Wilaya ya Tanganyika.

Naibu Waziri Mnyeti amesema serikali imeazimia kupumzisha shughuli za uvuvi katika Ziwa Tanganyika kuanzia tarehe 15 Mei hadi tarehe 15 Agosti Mwaka 2024 ikiwa ni utekelezaji wa Mkataba wa Kikanda wa Usimamizi wa Uvuvi endelevu katika ziwa hilo na bonde lake ambapo nchi wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika kwa maana ya Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Tanzania  na Zambia zilitia saini mkataba huo Tarehe 9 Mwezi Desemba Mwaka 2021 kwenye mkutano wa 9 wa mawaziri wa nchi hizo.

Mhe. Mnyeti amebainisha kuwa lengo la mkataba huo kwa nchi hizo ni kutoa muda kwa samaki kuzaliana ambapo kutokana na tafiti zilizofanywa na Tasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) katika kipindi cha Mwezi Mei na Agosti samaki huwa wanazaliana kwa wingi.

“Tunapumzisha ziwa hili kwa sababu samaki wanaenda kuisha ziwani ili tupishe wazaliane baada ya muda wa miezi mitatu tutaendelea na shughuli za uvuvi na jambo hili litakuwa la kila mwaka ili kuruhusu mazalia ya samaki ni mkataba wa nchi zinazozunguka Ziwa Tanganyika.” Amesema Mhe. Mnyeti

Aidha, ametaka wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi katika ziwa hilo kupatiwa elimu ya kutosha na pia serikali itaweka nguvu kwa wananchi hao kujikita katika ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba kwenye ziwa hilo huku wakiacha samaki wa asili waliopo ziwani kuzaliana.

Ameongeza kuwa serikali itafanya tathmini ya kupumzisha shughuli za uvuvi katika maziwa mengine kila baada ya muda kwa kipindi ambacho itaona inafaa ili samaki waweze kuzaliana kwa wingi ambapo kwa sasa inaanza na Ziwa Tanganyika.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko amesema uongozi wa mkoa huo uko tayari kusimamia utekelezaji huo ambao tayari umeanza kutekelezwa kwa mara ya kwanza Mwaka 2023 na nchi wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika ambapo Tanzania itatekeleza kwa mara ya kwanza mwaka huu. 

Mhe. Mrindoko amewataka wakazi wa mkoa huo kutoa ushirikiano kwa kuwa ni kwa manufaa yao na kwamba matarajio ni baada ya kufungwa Ziwa Tanganyika kwa miezi mitatu kutakuwa na ongezeko la samaki na katika kipindi cha miaka mitatu serikali itaweza kupata tathmini ya ongezeko la samaki.

Nao baadhi ya wananchi katika Mwalo wa Ikola Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi wamepokea taarifa hiyo na kuahidi kushirikiana na serikali wakati wote wa miezi mitatu ambapo shughuli za uvuvi zitakapokuwa hazifanywi katika Ziwa Tanganyika ili kupisha samaki kuzaliana kwa wingi.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kiwango cha samaki katika Ziwa Tanganyika kimekuwa kikipungua kila mwaka huku baadhi ya wavuvi wakitoa ushuhuda wa kupotea kabisa baadhi ya samaki katika ziwa hilo.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti akizungumza na wananchi wanaojishughulisha na uvuvi katika Mwalo wa Ikola uliopo Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi juu ya maamuzi ya serikali kulipumzisha Ziwa Tanganyika kwa shughuli za uvuvi kwa miezi mitatu kuanzia tarehe 15 Mwezi Mei hadi tarehe 15 Mwezi Agosti Mwaka 2024. (10.01.2024)

Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Ambakisye Simtoe akifafanua hoja mbalimbali kwa wananchi wa Mwalo wa Ikola uliopo Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi, baada ya wananchi hao kupatiwa taarifa juu ya upumzishwaji wa Ziwa Tanganyika kwa shughuli za uvuvi ili kuacha samaki wazaliane. (10.01.2024)


Mkurugenzi Msaidizi wa Undelezaji Rasilimali za Uvuvi Bi. Merisia Mparazo akizungumza na wananchi wakati akimwakilisha Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kwenye mkutano wa hadhara katika Mwalo wa Ikola juu ya upumzishaji wa shughuli za uvuvi katika Ziwa Tanganyika kwa miezi mitatu. (10.01.2024)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni