Nav bar

Jumanne, 23 Januari 2024

WAFUGAJI JONGOO BAHARI MTWARA WAASWA KUFUATA TARATIBU

 

Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji upande wa mazao ya bahari Dkt. Hamis Nikuli amewataka wafugaji jongoo bahari mkoani Mtwara kufuata sheria na taratibu za ufugaji wa zao hilo.

Dkt. Nikuli ameyasema hayo wakati wa zoezi la ujazaji wa dodoso linalohusu taarifa za wavuvi na wakuzaji viumbe maji  lililofanyika Januari 12, 2024 kwenye kampasi ya Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) iliyopo eneo la Mikindani mkoani humo.

"Tunahamasisha sana ufugaji wa jongoo bahari kwa sababu wale waliopo kwenye maji ya asili kwa huku Tanzania bara hawaruhusiwi kuvuliwa kwa sasa lakini ni lazima kila mtu au kikundi kifuate taratibu zilizopo kwenye kibali chake na isitokee mmoja wenu akatumia kibali cha mwenzie kuvuna jongoo hao" Amesema Dkt. Nikuli.

Dkt. Nikuli ameongeza kuwa ni lazima wafugaji jongoo bahari wote waliopo mkoani humo kuhakikisha wanatoa taarifa sahihi za idadi ya jongoo bahari wanaowafuga na kuwa waaminifu pindi wanapopewa kibali cha kuvuna ili wavune idadi waliyoidhinishiwa kwenye vibali hivyo.

Akizungumzia kuhusu madodoso ya taarifa za wavuvi na wakuzaji viumbe maji waliopo mkoani humo, Dkt. Nikuli amesema kuwa hatua hiyo imetokana na kutopatikana kwa haraka na usahihi wa taarifa za mvuvi mmoja mmoja, kikundi au kampuni inayojihusisha na uvuvi au ukuzaji viumbe maji pindi zinapohitajika kwa ajili ya madhumuni mbalimbali ikiwemo mikopo inayotolewa na Taasisi za kifedha na wadau wa maendeleo.

" Hadi sasa Mkoa wa Mtwara una vikundi 97 vinavyofuga na vinavyotarajia kufuga jongoo bahari na kwa ujumla dodoso hili limegusia taarifa za watu binafsi, kikundi na kampuni zinazojishughulisha na Uvuvi au Ukuzaji viumbe maji na kwa kuwa nyie mnajishughulisha na ufugaji jongoo bahari, taarifa mnazojaza zitaturahisishia kuelekeza rasilimali tunazopata kutoka kwa wadau wetu wa sekta kwa mujibu wa mahitaji mliyonayo" Amesisitiza Dkt. Nikuli.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Vikundi vya wafugaji wa jongoo bahari eneo la Mtwara Mikindani Bw. Ramadhan Banda amefurahishwa na hatua hiyo ya Wizara kukusanya taarifa zao huku akiweka wazi kuwa wamepata somo kubwa la namna bora ya kudhibiti soko la jongoo bahari ikiwa ni pamoja na kuwadhibiti wauzaji wa zao hilo kiholela.

"Nimefurahi pia kusikia hakuna mtu anayeruhusiwa kuvuna jongoo bahari bila kibali kutoka kwenu (wizarani) kwa sababu hatua hiyo itamaliza changamoto ya wizi wa zao hilo ambapo wengi wamekuwa wakiibuka sokoni na jongoo waliyowaiba kwenye vizimba vya wenzao" Ameongeza Bw. Banda.

Timu ya Wataalam kutoka Wizara ya mifugo na Uvuvi inaendesha zoezi la ujazaji madodoso ya Taarifa za Wavuvi na wakuzaji viumbe maji Mkoani kwenye mikoa ya Mtwara na Lindi kwa lengo la kuwa na taarifa sahihi za makundi hayo pindi wanapohitaji  kuwawezesha nyenzo mbalimbali za uendeshaji wa shughuli zao.


Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji (Bahari) Dkt. Hamis Nikuli akizungumza na vikundi vya Ufugaji jongoo bahari wa eneo la Mtwara Mikindani (hawapo pichani)  wakati wa zoezi la Ujazaji wa dodoso linalohusu taarifa za Wavuvi na wakuzaji viumbe maji waliopo mkoani Mtwara lililofanyika Januari 12, 2024, Kulia kwake ni Mwenyekiti wa vikundi hivyo Bw. Ramadhan Banda na kushoto kwake ni Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Janeth Rukanda.

Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi  Kresensia Mtweve (kulia) akiweka taarifa za mmoja wa wafugaji jongoo bahari  kwenye dodoso wakati wa zoezi la ujazaji wa taarifa hilo lililofanyika Januari 12, 2024,  Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya  Mikindani mkoani Mtwara.

Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi Janeth Rukanda (kushoto) akifafanua jambo wakati wa zoezi la ujazaji wa dodoso la wavuvi na wakuzaji viumbe maji lililofanyika Januari 12, 2024,  Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya  Mikindani mkoani Mtwara.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni