Nav bar

Jumanne, 23 Januari 2024

DC NGUBIAGAI ASISITIZA MAPAMBANO DHIDI YA UVUVI HARAMU


Aipa Kongole Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia zoezi la Uhakiki wa Vikundi vya Wavuvi, Wakuzaji viumbe maji.

Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Mhe. Christopher Ngubiagai ameiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuziongezea nguvu timu za Doria baharini zilizopo wilayani humo ili ziweze kuendelea kupambana na Uvuvi haramu.

Mhe. Ngubiagai amesema hayo baada ya kupokea timu ya wataalam kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi iliyofika Wilayani hapo kwa ajili ya zoezi la uhakiki wa taarifa za vikundi vya Wavuvi na wakuzaji viumbe maji Januari 17, 2023.

" Jitihada hizi kubwa za kuwawezesha Wavuvi zitakuwa na maana kubwa zaidi kama tutahakikisha rasilimali za bahari zinapatikana kwa wingi na hili litawezekana kama tuweka mkazo na nguvu kwenye kupambana na uvuvi haramu ukanda huu wa bahari" Amesema Mhe. Ngubiagai.

Mhe. Ngubiagai amedokeza kuwa licha ya Wilaya yake kuendelea na doria ya kupambana na changamoto hiyo ikiwa ni pamoja na kukagua nyenzo zinazotumiwa na wavuvi hao bado nguvu waliyonayo haitoshi kupambana na eneo kubwa la bahari linaloizunguka Wilaya hiyo.

"Tunazo jumuiya za Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU) ambazo kwa kweli zinatusaidia sana kwenye hili ila bahati mbaya hata wenyewe hawana vifaa vya kisasa vya kuweza kudhibiti hali hiyo kwa hiyo bado nguvu kubwa inahitajika" Amesisitiza Mhe. Ngubiagai.

Aidha Mhe. Ngubiagai ameipongeza Wizara kwa utekelezaji wa programu ya "Jenga Kesho iliyo bora kwa wajasiriamali wanawake na vijana" (BBT-LIFE) ambapo amesema kuwa tayari wilaya yake imeshatenga maeneo ambayo yanaweza kutumika kwa ajili ya shughuli za ufugaji wa samaki na kilimo cha zao la Mwani.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe maji baharini Dkt. Hamis Nikuli amesema kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi inatarajia kutekeleza miradi mbalimbali Wilayani Kilwa ikiwa ni pamoja na Kujenga chanja za kisasa za kukaushia Mwani na Ghala kubwa la kuhifadhi zao hilo.

"Lakini pia tayari kuna hatua za kudhibiti uvuvi haramu zimeshaanza kuchukuliwa upande wa Dar-es-salaam ambapo zinatarajiwa kufika kwenye maeneo yote yanayopitiwa na bahari" Ameongeza Dkt. Nikuli.

Timu ya Wataalam kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi inaendelea na zoezi la uhakiki wa vikundi vya Wavuvi na Wakuzaji Viumbe Maji kupitia ujazwaji wa dodoso maalum lenye taarifa zote za Msingi lengo likiwa ni kuiwezesha Serikali kuelekeza rasilimali kwa mujibu wa mahitaji ya vikundi hivyo.


Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji baharini Dkt. Hamis Nikuli (kulia) akimueleza Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Mhe. Christopher Ngubiagai (katikati) namna yeye na timu yake watakavyoendesha zoezi la Uhakiki wa vikundi vya Wavuvi na Wakuzaji viumbe maji waliopo Wilayani humo Januari 17, 2024. Kushoto ni Katibu Tawala wa Wilaya hiyo Bw. Yusuph Mwinyi.

Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji baharini Dkt. Hamis Nikuli (kulia mbele) akimueleza Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilwa Bw. Shija Lyela (katikati) namna yeye na timu yake watakavyoendesha zoezi la Uhakiki wa vikundi vya Wavuvi na Wakuzaji viumbe maji waliopo Wilayani humo Januari 17, 2024.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni