Nav bar

Ijumaa, 28 Oktoba 2022

MAUZO YA NYAMA NJE YA NCHI YAONGEZEKA - DKT. MUSHI

Mauzo ya nyama nje ya nchi yameongezeka kutoka tani 1,774.00 mwaka 2020/2021 hadi kufikia tani 10,415 katika mwaka 2020/2022.

Hayo yamesemwa na Msajili wa Bodi ya Nyama Tanzania (TMB) Dkt. Daniel Mushi Oktoba 28,2022 Jijini Dodoma wakati akieleza  utekelezaji wa majukumu ya bodi hiyo kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Amesema mwaka 2018/2019, waliuza tani za nyama 1,759 wakati mwaka 2019/2020 waliuza tani za nyama 692.46.

 “Kwa mwaka wa fedha uliopita tuliuza nyama nje ya nchi tani 10,415 ni kiasi ambacho hatujawahi kufikia kukiuza na hii imetupatia Sh96 bilioni...Kiasi kikubwa cha fedha kimepatikana kutokana na kuuza nyama nje ya nchi,”amesema.

Amesema katika robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2022/2023 wameuza tani 3,256.60 za nyama nje ya nchi.

Amesema mkakati wao kwa mwaka 2022/2023 ni kuongeza kiasi cha nyama kinachouzwa nje ya nchi ambapo hadi sasa wanauza kwa kiasi kikubwa katika nchi za Mashariki ya Kati.

Amezitaja nchi zinazouzwa nyama kutoka Tanzania ni Qatar, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Bahrain, Kuwait, Oman, Comoro, Hong Kong, Jordan na Saudi Arabia.

Dkt. Mushi amesema lengo la bodi hiyo ni kuhakikisha kuwa wanaongeza uuzaji wa nyama nje ya nchi hadi kufikia tani 16,000 kila mwaka ifikapo mwaka 2026.

Amesema kuwa takwimu zinaonyesha bado mtanzania mmoja anakula kilo 15 za nyama kwa mwaka badala ya kilo 50 zinazoshauriwa kitaalam.

“Watanzania wengi tunahitaji kuboresha afya zetu kwa kula nyama, kiasi ambacho kinachoruhusiwa na kupendekezwa,”amesema.


Msajili wa Bodi ya nyama Tanzania (TMB), Dkt. Daniel Mushi  akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani)  Oktoba 28,2022 alipokutana nao kuzungumzia lengo na majukumu ya Bodi ya nyama  Tanzania kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Idara ya Habari Maelezo (Dodoma).


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni